Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha
TAREHE 4-10/06
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | MARKO 15-16
“Yesu Alitimiza Unabii”
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Mk 15:24, 29
kugawa nguo zake za inje: Habari yenye kupatikana kwenye Yohana 19:23, 24 inatoa maelezo mengine yenye Matayo, Marko, na Luka hawakutaja: Askari Waroma walifikia kupigia kura nguo ya inje na ya ndani; askari waligawanya nguo za inje “katika sehemu ine, sehemu moja kwa kila askari;” hawakutaka kugawanya nguo ya ndani; kwa hiyo waliipigia kura; na kupigia kura nguo hiyo kulitimiza Zab 22:18. Ilionekana wazi kwamba, wale wenye walikuwa wanaua watu walizoea kunyanganya nguo za watu wenye walipaswa kuuawa; kwa hiyo watu wenye walihukumiwa kifo walinyanganywa nguo zao na vitu vyao vingine mbele wauawe, na kwa hiyo walifanya mateso yao ikuwe ya haya zaidi.
wakitikisa vichwa vyao: Kwa kawaida alama hiyo ya kutikisa vichwa ilisindikizwa na maneno, na ilionyesha zarau, ao zihaka. Bila kujua, wapita-njia walitimiza unabii wenye kupatikana katika Zab 22:7.
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Mk 15:43
Yosefu: Hali tofauti ya waandikaji wa Injili inaonekana wazi katika habari zenye wanatoa juu ya Yosefu. Mukusanya-kodi Matayo anasema kama alikuwa ‘mutu tajiri’; Marko, mwenye aliandikia kwanza Waroma, anasema kama alikuwa “mushiriki wa Baraza mwenye kuheshimiwa” mwenye alikuwa anangojea Ufalme wa Mungu; Luka, munganga mwenye huruma, anasema kama ‘alikuwa mutu mwema na mwadilifu [mwenye haki]’ mwenye hakupiga kura ili kuunga mukono tendo la Baraza kumuhusu Yesu; ni Yohana tu anaandika kama alikuwa “mwanafunzi wa Yesu lakini kwa siri kwa sababu alikuwa akiwaogopa Wayahudi.”—Mt 27:57-60; Mk 15:43-46; Lu 23:50-53; Yoh 19:38-42.
Chimba ili Kupata Mali ya Kiroho
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Mk 15:25
saa ya tatu: Ni kusema, karibu saa tatu (9H00). Watu fulani wanasema kama habari hii inapingana na ile yenye kupatikana katika Yohana 19:14-16, yenye inasema kama ilikuwa “karibu saa sita” wakati Pilato alimutoa Yesu ili auawe. Hata kama Maandiko haieleze wazi-wazi tofauti, kuko mambo fulani ya kufikiria: Kwa kawaida habari zenye kupatikana katika Injili zinapatana wakati zinazungumuzia wakati wa matukio ya siku za mwisho-mwisho za Yesu katika dunia. Injili zote ine zinaonyesha kama makuhani na wazee wote walikutana kisha asubui, na walimupeleka Yesu kwa Pontio Pilato, Gavana wa Roma. (Mt 27:1, 2; Mk 15:1; Lu 22:66–23:1; Yoh 18:28) Matayo, Marko, na Luka wote waliandika kama, wakati Yesu alikuwa tayari kwenye muti wa mateso, kukakuwa giza juu ya inchi yote kuanzia ‘saa sita . . . mupaka saa kenda.’ (Mt 27:45, 46; Mk 15:33, 34; Lu 23:44) Jambo lenye linaweza kutusaidia kujua saa yenye Yesu aliuawa ni hili: Watu fulani waliona kama kuteswa ao kupigwa ilikuwa sehemu ya hatua zenye ziliongoza kwenye kuuawa. Wakati fulani mutu aliteswa sana mupaka alifikia kufa. Kuhusu Yesu, mateso ilikuwa makali sana, ndiyo sababu wakati Yesu alijaribu kubeba muti wa mateso yeye mwenyewe, mwanaume mwingine alikuja kumusaidia. (Lu 23:26; Yoh 19:17) Kama mateso ilionwa kuwa sehemu ya hatua zenye kuongoza kwenye kuuawa, wakati fulani ulikuwa umepita mbele Yesu atundikwe kabisa-kabisa kwenye muti wa mateso. Kwa hiyo, Matayo 27:26 na Marko 15:15 inataja pamoja mateso na kuuawa kwenye muti wa mateso. Kwa hiyo, watu tofauti wangetaja saa tofauti kuhusu kuuawa, kulingana na mawazo yenye walikuwa nayo kuhusu wakati mateso hayo ilianza. Hilo linaweza kufasiria sababu gani Pilato alishangaa kusikia kama Yesu alikufa mbio kisha tu kutundikwa kwenye muti wa mateso. (Mk 15:44) Tena, mara nyingi waandishi wa Biblia walikuwa na zoezi la kugawanya siku katika sehemu ine za saa tatu-tatu, kama vile usiku uligawanywa. Kugawanya siku kwa njia hiyo kunafasiria sababu gani mara nyingi saa tatu, saa sita, na saa kenda zinatumiwa, kuanzia saa 12 (6H00) hivi wakati jua inalamuka. (Mt 20:1-5; Yoh 4:6; Mdo 2:15; 3:1; 10:3, 9, 30) Pia, kwa ujumla watu hawakukuwa na vyombo vya kuwasaidia kujua saa ya kweli kabisa; kwa hiyo, kwa kawaida ili kutaja saa waliongeza neno “karibu,” kama vile inaonyeshwa katika Yoh 19:14. (Mt 27:46; Lu 23:44; Yoh 4:6; Mdo 10:3, 9) Kwa kifupi: Pengine Marko alianza kuhesabia saa kuanzia wakati Yesu alianza kuteswa mupaka wakati alitundikwa kwenye muti wa mateso; lakini Yohana anataja mara moja wakati Yesu alitundikwa kwenye muti wa mateso. Pengine waandishi wote wa Injili walikadiria saa yenye ilikuwa karibu sana na kipindi cha saa tatu, na Yohana alitumia neno “karibu” wakati anaeleza habari yake. Pengine mambo hayo inafasiria sababu gani waandikaji wa Injili wanatumia saa tofauti. Mwishowe, kwa sababu Yohana, mwenye aliandika Injili yake kisha makumi ya miaka, anataja saa tofauti na ile ya Marko, hilo linaonyesha kama Yohana hakurudilia tu habari ya Marko.
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Mk 16:8
kwa sababu walikuwa na woga: Kulingana na maandishi ya kwanza-kwanza ya sehemu ya mwisho ya Injili ya Marko yenye kupatikana sasa, Injili ya Marko inamalizika na maneno yenye kupatikana kwenye mustari wa 8. Watu fulani wanasema kama umalizio huo unamalizika kwa kushitukia, na kama haiko umalizio wa kweli-kweli wa Injili ya Marko. Lakini, hatupaswe kufikiri hivyo, kwa sababu kwa kawaida Marko alizoea kuandika mambo kwa kifupi. Pia, Jérôme na Eusèbe, wenye elimu ya Biblia wa miaka ya kati ya 301-400, wanakubaliana kama maandishi ya kwanza-kwanza inamalizika na maneno “kwa sababu walikuwa na woga.”
Kuko maandishi na tafsiri nyingi za Kigiriki katika luga zingine zenye zinaongeza umalizio murefu ao umalizio mufupi kisha mustari wa 8. Umalizio murefu (uko na mistari 12 ya kuongeza) unapatikana katika Codex Alexandrinus, katika Codex Ephraemi Syri rescriptus, na katika Codex Bezae Cantabrigiensis, yote ni ya miaka kati ya 401-500. Umalizio huo unapatikana pia katika Latin Vulgate, katika Curetonian Syriac, na katika Syriac Peshitta. Hata hivyo, haupatikane katika maandishi mbili ya Kigiriki ya mwanzo-mwanzo ya miaka ya 301-400, ni kusema Codex Sinaiticus na Codex Vaticanus, ao katika Codex Sinaiticus Syriacus ya miaka kati ya 301-400, ao 401-500, ao katika maandishi ya kwanza-kwanza ya Marko yenye kuitwa Sahidic Coptic ya miaka kati ya 401-500. Vilevile, maandishi ya zamani ya Marko katika Kiarmenia na Kigeorgia inaishia kwenye mustari wa 8.
Tafsiri na maandishi fulani ya Kigiriki katika luga zingine yenye ilitokea kisha, ziko na umalizio mufupi (wenye kuwa tu na misemwa fulani). Codex Regius ya miaka kati ya 701-800 iko na umalizio wote mbili; inaanza na umalizio mufupi. Kwenye mwanzo wa kila umalizio, kuko maneno yenye kuonyesha kama maandiko hayo inakubaliwa katika maeneo fulani, lakini Codex hiyo haikubali umalizio wote huo mbili.
UMALIZIO MUFUPI
Umalizio mufupi kisha Marko 16:8 haiko sehemu ya Maandiko yenye iliongozwa na roho. Unasema hivi:
Lakini mambo yote yaliyokuwa yameamriwa wakayasimulia kwa ufupi kwa wale waliomzunguka Petro. Tena, baada ya mambo hayo, Yesu mwenyewe akapeleka kupitia wao tangazo takatifu na lisiloweza kuharibika la wokovu wa milele kutoka mashariki mpaka magharibi.
UMALIZIO MUREFU
Umalizio murefu kisha Marko 16:8 haiko sehemu ya Maandiko yenye iliongozwa na roho. Unasema hivi:
Baada ya kufufuka mapema siku ya kwanza ya juma akamtokea kwanza Maria Magdalene, ambaye alikuwa amefukuza roho waovu saba kutoka kwake. Maria Magdalene akaenda, akawaambia wale waliokuwa wamekuwa pamoja na Yesu, kwa maana walikuwa wakiomboleza na kulia. Lakini wao, waliposikia alikuwa amefufuka na Maria Magdalene alikuwa amemwona, hawakuamini. Tena, baada ya mambo hayo aliwatokea katika umbo lingine wawili kati yao wakitembea, walipokuwa wakienda mashambani; nao wakarudi wakawaambia wale wengine. Wala hawakuwaamini. Lakini baadaye akawatokea wale kumi na mmoja wenyewe walipokuwa wameketi mezani, naye akaushutumu ukosefu wao wa imani na ugumu wa moyo, kwa sababu hawakuwaamini wale waliokuwa wamemwona sasa akiwa amefufuka kutoka kwa wafu. Naye akawaambia: “Nendeni, mkaingie katika ulimwengu wote na kuhubiri habari njema kwa uumbaji wote. Yeye anayeamini na kubatizwa ataokolewa, lakini yule ambaye hataamini atahukumiwa adhabu. Zaidi ya hayo, ishara hizi zitafuatana na wale wanaoamini: Kwa kutumia jina langu watatoa roho waovu, watasema kwa lugha, nao watainua nyoka kwa mikono yao, na wakinywa kitu chochote chenye kuua hakitawaumiza hata kidogo. Wataweka mikono yao juu ya watu wagonjwa, nao watapona.”
Kwa hiyo, basi, Bwana Yesu, alipokuwa amekwisha kusema nao, akachukuliwa juu mpaka mbinguni na kuketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu. Basi, wakatoka kwenda na kuhubiri kila mahali, huku Bwana akifanya kazi pamoja nao na kuutegemeza ujumbe huo kupitia ishara zenye kufuatana nao.
TAREHE 11-17/06
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | LUKA 1
“Iga Unyenyekevu wa Maria”
Tazama! Mimi Ni “Kijakazi wa Yehova!”
Maneno aliyomuambia Gabrieli, maneno yenye kuonyesha unyenyekevu na utii, hata leo yanakumbukwa na watu wengi wenye imani. Anamuambia hivi: “Tazama! [Mimi ni] kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo [ao neno] lako.” (Luka 1:38) Kijakazi alikuwa mutumishi wa chini sana kati ya watumishi wote kwa sababu maisha yake yalikuwa mikononi mwa bwana wake. Hivyo ndivyo Maria anavyojiona mbele ya Bwana wake, Yehova. Anajua kwamba Yehova ni mushikamanifu kwa wale walio washikamanifu kwake, kwa hiyo anajisikia salama mikononi mwake, na kwamba atamubariki ikiwa anafanya yake yote ili kutimiza mugao huo mugumu.—Zab. 18:25.
Tazama! Mimi Ni “Kijakazi wa Yehova!”
Kisha Maria naye anasema. Maneno aliyosema yamechungwa vizuri katika Neno la Mungu. (Soma Luka 1:46-55.) Maneno hayo ndiyo mazungumuzo marefu ya Maria katika Biblia, na yanafunua mengi juu yake. Maneno yake yanaonyesha namna anavyomusifu Yehova ili kuonyesha shukrani yake na kuonyesha kwamba anasamini pendeleo analomutolea la kuwa mama ya Masiya. Yanaonyesha kwamba Maria ana imani kubwa: anasema kwamba Yehova anawashusha wenye majivuno na wenye nguvu na kuwasaidia watu wa hali ya chini na masikini wanaotaka kumutumikia. Pia, yanaonyesha kwamba Maria ana ujuzi sana wa maandiko. Inakadiriwa kwamba alitaja Maandiko ya Kiebrania zaidi ya mara 20!
Ni wazi kwamba Maria ni mwanamuke mwenye kutafakari sana juu ya Neno la Mungu. Hata hivyo, yeye anabaki tu munyenyekevu, anaacha Maandiko yaseme kuliko kujitungia mambo ya kusema. Mutoto aliyekuwa katika tumbo lake alipokomaa, alionyesha pia unyenyekevu huohuo, alisema hivi: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Kwa hiyo, ni vizuri kujiuliza: “Je, ninaliogopa na kuliheshimu Neno la Mungu hivyo? Ao je, ninapendelea kufundisha mawazo yangu mwenyewe?” Maria kwa upande wake alikuwa na maoni yanayofaa.
Chimba ili Kupata Mali ya Kiroho
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Lu 1:69
pembe ya wokovu: Ao “mukombozi mwenye nguvu.” Katika Biblia, mara nyingi pembe za wanyama zinamaanisha nguvu na ushindi. (1Sam 2:1; Zab 75:4, 5, 10; 148:14.) Pia, falme na watawala, wazuri na wabaya, wanafananishwa na pembe, na matendo yao ya kupata ushindi ililinganishwa na kusukuma kwa kutumia pembe. (Kum 33:17; Dan 7:24; 8:2-10, 20-24) Hapa, maneno “pembe ya wokovu” inamuhusu Masiya, mwenye kuwa na uwezo wa kuokoa, mukombozi mwenye nguvu.
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Lu 1:76
utaenda mbele ya Yehova: Yohana Mubatizaji angeenda “mbele ya Yehova” katika maana ya kwamba angemutayarishia Yesu njia, mwenye angemuwakilisha Baba yake, na mwenye angekuja katika jina la Baba yake.—Yoh 5:43; 8:29; ona kwa ajili ya funzo kuhusu Yehova katika andiko hilo.
TAREHE 18-24/06
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | LUKA 2-3
“Vijana, Urafiki Wenu na Yehova Unaendelea Kuwa Nguvu?”
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Lu 2:41
wazazi wake walizoea: Sheria haikuruhusu wanamuke waende kwenye sikukuu ya Pasaka. Lakini, kila mwaka Maria alizoea kumusindikiza Yosefu katika safari ya kuenda Yerusalemu kwa ajili ya sikukuu hiyo. (Kut 23:17; 34:23) Kila mwaka, walikuwa wanafanya safari ya kilometre 300 hivi ya kuenda na kurudia pamoja na familia yao yenye iliendelea kuongezeka.
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Lu 2:46, 47
kuwauliza maulizo: Kushangaa kwa wale wenye walikuwa wanamusikiliza kulionyesha kama maulizo yake haikukuwa tu kama ile ya kijana mwenye kuuliza-uliza ili tu ajue. (Lu 2:47) Maneno ya Kigiriki yenye kutafsiriwa “kuwauliza maulizo” inaweza wakati fulani kumaanisha namna ya kuuliza maulizo yenye kutumiwa kwenye tribinali. (Mt 27:11; Mk 14:60, 61; 15:2, 4; Mdo 5:27) Wanahistoria wanasema kwamba viongozi fulani wa dini walizoea kubakia kwenye hekalu kisha sikukuu na kufundisha katika muingilio moja mukubwa. Watu walikuwa wanakaa kwenye miguu ya wanaume hao ili kuwasikiliza na kuwauliza maulizo.
waliendelea kushangazwa: Hapa tendo la Kigiriki lenye kutafsiriwa “kushangazwa” linaweza kumaanisha kuendelea kushangaa ao kushangaa tena na tena.
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Lu 2:51, 52
akaendelea kujitiisha: Ao “aliendelea kutii; alibakia mutiifu.” Kutumia tendo hilo la Kigiriki kwa njia yenye kuendelea kunaonyesha kama kisha kushangaza walimu kwenye hekalu kwa ujuzi wake wa Neno la Mungu, Yesu alirudia kwao na alijitiisha kwa unyenyekevu kwa wazazi wake. Utii huo ulikuwa na maana ingine ya pekee kuliko ule wa mutoto mwingine yeyote; ulikuwa pia kati ya mambo yenye alitimiza kuhusiana na Sheria ya Musa.—Kut 20:12; Gal 4:4.
Chimba ili Kupata Mali ya Kiroho
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Lu 2:14
na amani katika dunia kati ya watu wa nia njema: Maandishi fulani iko na maneno yenye inaweza kutafsiriwa “na katika dunia amani, nia njema kwa watu,” na maneno hayo inapatikana katika tafsiri fulani za Biblia. Lakini maneno yenye Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia inategemezwa kabisa na maandishi. Tangazo hili la malaika halimaanishe nia njema ya Mungu kwa wanadamu wote bila kufuata maoni na matendo tofauti. Lakini, inahusu wale wenye watapokea nia njema yake kwa sababu wanaoyesha imani kubwa kwake na wanakuwa wafuasi wa Mwana wake.—Ona kwa ajili ya funzo kuhusu watu wa nia njema katika andiko hilo.
watu wa nia njema: Maneno “nia njema” yenye kutumiwa katika tangazo hili la malaika ni nia njema ya Yehova Mungu, hapana ya wanadamu. Neno la Kigiriki eu·do·kiʹa linaweza pia kutafsiriwa “wema; upendezi mwema; kukubaliwa.” Tendo eu·do·keʹo lenye kufanana eu·do·kiʹa linatumiwa kwenye Matayo 3:17; Marko 1:11; na Luka 3:22 (ona kwa ajili ya funzo kuhusu Mt 3:17; Mk 1:11), kwenye Mungu anaongea na Mwana wake kisha tu yeye kubatizwa. Maana ya kwanza ya tendo hilo ni, “kukubali; kupendezwa sana na; kuangalia kwa kukubali; kufurahia.” Kulingana na matumizi haya, maneno “watu wa nia njema” (an·throʹpois eu·do·kiʹas) inahusu watu wenye Mungu anakubali na kuonyesha nia njema, na inaweza pia kutafsiriwa “watu wenye anakubali; watu wenye anapendezwa nao sana.” Kwa hiyo, tangazo hilo la malaika linahusu nia njema ya Mungu, hapana kwa wanadamu kwa ujumla, lakini kwa wale wenye wanamupendeza kwa kuonyesha imani kubwa kwake na kwa kumufuata Mwana wake. Hata kama wakati fulani neno la Kigiriki eu·do·kiʹa linaweza kumaanisha nia njema ya wanadamu (Rom 10:1; Flp 1:15), Mara nyingi linatumiwa kuhusu nia njema ya Mungu, ao upendezi mwema, ao kwa njia yenye anakubali (Mt 11:26; Lu 10:21; Efe 1:5, 9; Flp 2:13; 2Tes 1:11). Katika tafsiri ya Septante kwenye Zaburi 51:18 [50:20, LXX], neno hilo linatumiwa ili kumaanisha “nia njema” ya Mungu.
Ulijua?
Baba ya Yosefu alikuwa nani?
Yosefu, seremala (mwenye kufanya kazi ya mbao) wa Nazareti, alikuwa baba mwenye alikomalisha Yesu. Baba ya Yosefu alikuwa nani? Kizazi cha Yesu chenye kuwa katika Injili ya Mathayo kinataja mwanaume mumoja mwenye kuitwa Yakobo, lakini kizazi chenye kuwa katika Injili ya Luka kinasema kama Yosefu alikuwa “mwana wa Heli.” Sababu gani inaonekana kuwa zinapingana?—Luka 3:23; Matayo 1:16.
Habari ya Mathayo inasema hivi: ‘Yakobo akamuzaa Yosefu.’ Inatumia neno la Kigiriki lenye kuonyesha waziwazi kama Yakobo alikuwa baba muzazi wa Yosefu. Kwa hiyo, Mathayo alionyesha kizazi cha Yosefu, ni kusema, utawala wa kifalme, wenye ungemupitishia Yesu, mwana mwenye Yosefu alikomalisha, haki ya kisheria ya kukaa kwenye kiti cha Ufalme.
Lakini, Injili ya Luka inasema hivi: “Yosefu, mwana wa Heli.” Maneno hayo, “mwana wa,” yanaweza kueleweka ‘mwana-mukwe wa.’ Maneno kama hayo yanapatikana katika andiko la Luka 3:27, kwenye Shealtieli, mwenye baba yake muzazi alikuwa Yekonia, anatajwa kuwa “mwana wa Neri.” (1 Mambo ya Nyakati 3:17; Mathayo 1:12) Inawezekana Shealtieli alioa mutoto wa Neri mwenye hatajwe jina, katika njia hiyo akakuwa mwana-mukwe wake. Ndiyo maana Yosefu anatajwa kuwa “mwana” wa Heli, kwa sababu alioa Maria, mutoto wa Heli. Kwa hiyo, Luka anataja kizazi cha Yesu “kulingana na mwili,” kupitia Maria, mama yake muzazi. (Waroma 1:3) Ndiyo sababu Biblia inatupatia vizazi viwili vya maana vya Yesu vyenye kuwa tofauti.
TAREHE 25/06–1/07
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | LUKA 4-5
“Umuige Yesu kwa Kupambana na Majaribu”
Tunapaswa Kuwa Watu wa Namna Gani?
Shetani alitumia ufundi huo-huo wakati alijaribu kumushawishi Yesu katika jangwa. Kisha Yesu kufanya siku 40 muchana na usiku bila kula, Shetani alimujaribu kwa kuchochea tamaa yake kwa ajili ya chakula. Shetani alimuambia hivi: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mukate.” (Luka 4:1-3) Yesu alikuwa na maamuzi mawili: Kutumia uwezo wake wa kufanya miujiza ili apate chakula, ao kukataa kutumia uwezo huo. Yesu alijua kwamba hapaswe kutumia uwezo huo kwa ajili ya faida zake mwenyewe. Hata kama alisikia njaa, jambo lenye alitia pa nafasi ya kwanza lilikuwa kuendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova kuliko kutosheleza tamaa ya chakula. Yesu alimujibia Shetani hivi: “Imeandikwa, ‘mwanadamu ataishi, si kwa mukate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’”—Luka 4:4.
Tunapaswa Kuwa Watu wa Namna Gani?
Tuseme nini kuhusu Yesu? Shetani “alimuonyesha [Yesu] mara moja falme zote za dunia inayokaliwa; naye alimwambia: ‘Hakika nitakupa mamlaka yote hii na utukufu wake.’” (Luka 4:5, 6) Yesu hangeona mara moja falme zote hizo kwa macho yake ya kibinadamu, lakini inawezekana Shetani alifikiri kwamba utukufu wa falme hizo, zenye alimuonyesha katika maono, ungemuvutia Yesu. Bila kusikia haya, Shetani alimuambia hivi: “Ukifanya tendo la ibada mbele yangu, yote itakuwa yako.” (Luka 4:7) Yesu hakutaka hata kidogo kumupendeza Shetani. Alimujibia mara moja hivi: “Imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumuabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumutolea utumishi mutakatifu.’”—Luka 4:8.
nwtsty picha na video
Munara wa Hekalu
Pengine Shetani alimusimamisha Yesu moja kwa moja “juu ya munara [ao “sehemu ya juu sana”] wa hekalu” na kumuambia ajitupe chini kutoka hapo; lakini pengine mahali kabisa kwenye Yesu alisimama hapajulikane. Kwa sababu neno lenye kutafsiriwa “hekalu” lenye kutumiwa hapa linaweza kumaanisha eneo lote la hekalu, Pengine Yesu alisimamishwa juu ya pembe ya kusini-mashariki (1) ya hekalu. Ao pengine alisimamishwa juu ya pembe ingine ya hekalu. Bila musaada wa Yehova, kujitupa chini kutoka moja kati ya pembe hizo kungetokeza kifo hakika.
Tunapaswa Kuwa Watu wa Namna Gani?
Tofauti na Eva, Yesu alituachia mufano muzuri sana wa unyenyekevu! Shetani alijaribu kumushawishi katika njia nyingine, lakini Yesu alitupilia mbali wazo lolote la kufanya jambo la kushangaza lenye lingemujaribu Mungu. Hilo lingekuwa tendo la kiburi! Lakini jibu la Yesu lilikuwa wazi na la moja kwa moja: “Imesemwa, ‘Usimujaribu Yehova Mungu wako.’”—Soma Luka 4:9-12.
Chimba ili Kupata Mali ya Kiroho
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Lu 4:17
kitabu cha kukunjwa cha nabii Isaya: Kitabu cha Kukunjwa cha Bahari ya Chumvi cha Isaya kilikuwa na kurasa 17 zenye ziliunganishwa, na zenye urefu wa metre 7 hivi, na kilikuwa na safu (colonnes) 54. Pengine kitabu cha kukunjwa cha Isaya chenye Yesu alitumia katika sinagogi kule Nazareti kilikuwa na urefu kama huo. Wakati wa mitume Maandiko haikukuwa imegawanywa katika sura na mistari; kwa hiyo, Yesu alipaswa kutafuta andiko lenye alipenda kusoma. Lakini, kwa sababu alipata mahali kwenye maneno ya unabii ilikuwa imeandikwa, hilo linaonyesha kama alijua Neno la Mungu muzuri sana.
nwtsty kwa ajili ya funzo kuhusu Lu 4:25
kwa miaka tatu na miezi sita: Kulingana na 1Fal 18:1, Eliya alitangaza kama kipwa kingemalizika “katika mwaka wa tatu.” Kwa hiyo, watu fulani wamesema kama Yesu anapinga habari yenye kupatikana katika 1 Wafalme. Lakini, habari zenye kupatikana katika Maandiko ya Kiebrania hazionyeshe kama kipwa kilifanya chini ya miaka tatu. Ni wazi kama maneno “katika mwaka wa tatu” inahusu kipindi cha wakati kuanzia wakati Eliya alimujulisha Ahabu kuhusu kipwa hicho. (1Fal 17:1) Inawezekana tangazo hilo lilitolewa wakati majira ya baridi, yenye kwa kawaida inafanya miezi sita lakini yenye pengine ilichukua wakati murefu zaidi, ilikuwa imeanza. Zaidi ya hilo, kipwa hakikumalizika mara moja wakati Eliya alikutana tena na Ahabu, “katika mwaka wa tatu,” lakini kisha tu jaribu la moto kwenye Mulima Karmeli. (1Fal 18:18-45) Kwa hiyo, maneno haya ya Yesu, na pia maneno ya ndugu ya Yesu yenye kufanana na hiyo, yenye kupatikana kwenye Yakobo 5:17, inapatana kabisa na mambo yenye kutajwa katika 1Wafalme 18:1.