Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • mwbr21 Mwezi wa 1 uku. 1-15
  • Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha (1/2021)

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha (1/2021)
  • Vichapo Vyenye Kutajwa mu Buku la Mukutano Utumishi na Maisha—2021
  • Vichwa Vidogo
  • TAREHE 4-10/01
  • TAREHE 11-17/01
  • TAREHE 18-24/01
  • TAREHE 25-31/01
  • TAREHE 1-7/02
  • TAREHE 8-14/02
  • TAREHE 15-21/02
  • TAREHE 22-28/02
Vichapo Vyenye Kutajwa mu Buku la Mukutano Utumishi na Maisha—2021
mwbr21 Mwezi wa 1 uku. 1-15

Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha

TAREHE 4-10/01

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 18-19

“Endelea Kuwa na Mwenendo Safi”

w19.06 uku. 28 fu. 1

Namna ya Kujilinda Kabisa na Mutego Fulani wa Shetani

Yehova alitaja mambo machafu yenye mataifa yenye ilizunguka Waisraeli ilikuwa inafanya na aliwaambia hivi: “Hamupaswe kufanya mambo yenye wanafanya katika inchi ya Kanaani, kwenye ninawapeleka. . . . Inchi hiyo haiko safi, na nitaleta azabu juu ya inchi hiyo kwa sababu ya kosa lake.” Mungu mutakatifu wa Israeli aliona maisha ya Wakanaani kuwa machafu sana mupaka akaona inchi yao kuwa chafu.​—Law. 18:3, 25.

w17.02 uku. 20 fu. 13

Yehova Anaongoza Watu Wake

13 Viongozi wa mataifa mengine waliongozwa na hekima ya wanadamu yenye kuwa na mipaka. Kwa mufano, viongozi Wakanaani na watu wao walifanya mambo ya mubaya sana, kama vile ngono kati ya watu wa familia moja, mwanaume kulala na mwanaume ao mwanamuke kulala na mwanamuke, ngono kati ya mutu na munyama, kutoa watoto kuwa zabihu, na ibada ya sanamu. (Mambo ya Walawi 18:6, 21-25) Pia, viongozi Wababiloni na Wamisri hawakukuwa na sheria zilezile juu ya usafi zenye watu wa Mungu walikuwa nazo. (Hesabu 19:13) Lakini, watu wa Mungu wangeweza kuona namna viongozi wao waaminifu waliwatia moyo ili waendelee kufanya ibada yao ikuwe safi, wakuwe safi kimwili, na waepuke mambo machafu ya uasherati. Ni wazi kwamba Yehova alikuwa anawaongoza.

w14 1/7 uku. 7 fu. 2

Mambo Mungu Atafanya Juu ya Mabaya

Itakuwa namna gani juu ya wale wanaokataa kwa kiburi kubadilisha njia zao na wanaendelea kufanya mambo mabaya? Fikiria ahadi hii iliyo wazi: ‘Kwa maana wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila [ao wenye ujanja], watangolewa [ao kuondolewa] kutoka ndani yake.’ (Methali 2:21, 22) Ushawishi wa wanadamu waovu hautakuwa tena. Katika hali hizo zenye amani, wanadamu watiifu wataondolewa polepole katika hali ya kutokamilika yenye waliriti.​—Waroma 6:17, 18; 8:21.

Mali ya Kiroho

w06-SW 15/6 uku. 22 fu. 11

“Jinsi Ninavyoipenda Sheria Yako!”

11 Jambo la pili katika Sheria ya Musa ambalo linaonyesha jinsi Mungu alivyojali hali ya watu wake ni haki ya kuokota masalio. Yehova aliamuru kwamba wakati mkulima Mwisraeli alipovuna mazao ya shamba lake, watu wenye uhitaji walipaswa waruhusiwe kuokota masalio ambayo wavunaji waliacha. Wakulima hawakupaswa kuvuna kila kitu kwenye ukingo wa mashamba yao, wala hawakupaswa kukusanya zabibu au zeituni zilizobaki. Hawakupaswa kurudi kuchukua masuke ya nafaka yaliyosahauliwa mashambani. Huo ulikuwa mpango wa upendo wa kuwasaidia maskini, wakaaji wageni, mayatima, na wajane. Ni kweli kwamba kazi ya kuokota masalio ilikuwa ngumu, lakini kazi hiyo ingewazuia wasiombe-ombe.​—Mambo ya Walawi 19:9, 10; Kumbukumbu la Torati 24:19-22; Zaburi 37:25.

Hotuba

w02-SW 1/2 uku. 29

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Sheria ambayo Yehova alilipa taifa la Israeli haisemi mengi kuhusu utaratibu na sherehe za arusi. Hata hivyo, sheria hiyo ina vizuizi kuhusu ndoa fulani. Kwa mfano, katika andiko la Mambo ya Walawi 18:6-20, tunapata orodha ya uhusiano wa ngono uliokatazwa kati ya ‘mtu aliye wa jamaa ya karibu.’ Mistari hiyo inafafanua kinaganaga ni watu gani wa jamaa ya karibu wasiopaswa kuwa na uhusiano wa ngono. Bila shaka, Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa wala hawajafungwa na amri zake. (Waefeso 2:15; Wakolosai 2:14) Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba Wakristo wanaweza kupuuza tu sheria hiyo wanapochagua mwenzi wa ndoa. Kuna sababu nyingi za kutopuuza sheria hiyo.

Kwanza kabisa, nchi mbalimbali zina sheria zinazozuia ndoa kati ya watu wa jamaa ya karibu, nao Wakristo wanapaswa kutii sheria za nchi wanakoishi. (Mathayo 22:21; Waroma 13:1) Bila shaka, sheria hizo hutofautiana katika nchi mbalimbali. Sheria nyingi za kisasa kuhusu ndoa za namna hiyo, zimewekwa kwa kufikiria hasa kasoro za urithi zinazoweza kutokea. Ni jambo linalojulikana wazi kwamba ikiwa watu wa jamaa ya karibu wataoana yaelekea watazaa watoto wenye kasoro za urithi na magonjwa. Kwa sababu hiyo na kwa sababu ya ‘kujitiisha kwa mamlaka zilizo kubwa,’ Wakristo wanaofunga ndoa hutii sheria za kwao kuhusu ndoa.

Kisha kuna mambo yanayokubalika na yasiyokubalika katika jumuiya ambako mtu anaishi. Karibu kila utamaduni una sheria na desturi zinazokataza ndoa kati ya watu wa jamaa ya karibu, na mara nyingi ndoa hizo huonwa kuwa sawa na kufanya ngono na mtu wa familia na hivyo ni mwiko. Ijapokuwa tamaduni mbalimbali huenda zikatofautiana sana kuhusu vizuizi vya ndoa hususa, ‘kwa kawaida mwiko huo huzingatiwa hata zaidi ikiwa watu ni wa jamaa za karibu zaidi ili kuwakataza kuwa na uhusiano wa ngono,’ chasema kichapo The Encyclopædia Britannica. Kwa hiyo, hata kusipokuwa na uhusiano wa ngono kati ya watu wa jamaa ya karibu, Wakristo hawangependa kupuuza kabisa desturi au maoni ya jumuiya na kuleta suto kwa kutaniko la Kikristo au kwa jina la Mungu.​—2 Wakorintho 6:3.

Hatupaswi pia kupuuza dhamiri tuliyopewa na Mungu. Watu wote huzaliwa wakiwa na uwezo wa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa, mema na mabaya. (Waroma 2:15) Dhamiri yao huwaambia mambo yanayokubalika na yanayofaa na mambo yasiyokubalika na yanayoudhi, isipokuwa iwe imepotoshwa au imefanywa kuwa sugu na mazoea mapotovu. Yehova alidokeza jambo hilo alipowapa Waisraeli sheria yake inayokataza ndoa kati ya watu wa jamaa ya karibu. Twasoma hivi: “Nanyi msifanye matendo kama yale ya nchi ya Misri mliyokaa; wala msifanye matendo kama yale ya nchi ya Kanaani, nitakayowapeleka; wala msiende katika amri zao hao.” (Mambo ya Walawi 18:3) Wakristo huthamini sana dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia na hawairuhusu ipotoshwe na viwango vya mataifa vilivyopotoka vya kuamua mema na mabaya.​—Waefeso 4:17-19.

Kwa hiyo, tunaweza kufikia mkataa gani? Ingawa Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, dhamiri yao huwaonyesha waziwazi kwamba ndoa kati ya watu wa jamaa ya karibu​—kama vile baba na binti, mama na mwana, ndugu na dada​—haikubaliki kabisa katika kutaniko la Kikristo. Kadiri ukoo unavyozidi kuwa wa mbali, Wakristo hutambua kwamba kuna sheria na amri kuhusu ndoa zilizofungwa kisheria na kwamba kuna viwango vinavyokubalika kijamii na kitamaduni. Mambo hayo yapasa kufikiriwa kwa makini ili tuweze kutii amri hii ya Kimaandiko: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote.”​—Waebrania 13:4.

TAREHE 11-17/01

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 20-21

“Yehova Anatenga Watu Wake na Mataifa Ingine”

w04-SW 15/10 uku. 11 fu. 12

Je, Una Sababu ya Kuamini Kwamba Kutakuwa na Paradiso?

12 Hata hivyo, kuna jambo fulani tusilopaswa kupuuza. Mungu aliwaambia Waisraeli hivi: “Mtashika amri yote ninayowaamuru leo, ili muwe na nguvu na mpate kuingia na kuimiliki nchi ambayo mnavuka ili kuimiliki.” (Kumbukumbu la Torati 11:8) Nchi hiyohiyo inatajwa katika Mambo ya Walawi 20:22, 24: “Nanyi mtazishika sheria zangu zote na maamuzi yangu yote ya hukumu na kuzifanya, ili nchi nitakayowaingiza mkae ndani yake isije ikawatapika ninyi. Ndipo nikawaambia ninyi: ‘Ninyi mtaimiliki nchi yao, nami nitawapa ninyi ili mwimiliki, nchi inayotiririka maziwa na asali.’” Naam, kumiliki Nchi ya Ahadi kulitegemea kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu. Mungu aliwaruhusu Wababiloni wawashinde Waisraeli na kuwatoa katika makao yao kwa sababu walikosa kumtii.

it-1-F uku. 1106

Uriti

Ni mali yenye, kisha mwenye nayo kufa, inapewa muriti ao inapewa wale wenye wanafuatia ule muriti; kitu chochote chenye mutu anapata kutoka kwa babu ao kutoka kwa wenye walimutangulia. Kitenzi (verbe) cha musingi cha Kiebrania chenye kinatumiwa ni na·chalʹ (jina, na·chalahʹ). Kinatia ndani kupata uriti ao kupatia mutu fulani uriti; mara mingi kulingana na vile watu wanafuatana. (Hes 26:55; Eze 46:18) Wakati fulani, kitenzi ya·rashʹ kinatumiwa ili kumaanisha ‘kuwa muriti’ wa mutu fulani, lakini mara mingi kinatumiwa ili kumaanisha ‘kuriti’ kwenye hakutegemee namna watu wanafuatana. (Mwa 15:3; Law 20:24) Tena, kinatumiwa ili kumaanisha ‘kukamata ao kufukuza,’ zaidi sana mu mambo ya kijeshi. (Kum 2:12; 31:3) Maneno ya Kigiriki yenye inapatana na neno uriti iko na uhusiano na neno kleʹros, lenye maana yake ya kwanza ni “kura” lakini lilifikia kuwa na maana ya “kuchangia” na ku mwisho likafikia kuwa na maana ya “uriti.”​—Mt 27:35; Mdo 1:17; 26:18.

it-2-F uku. 438 fu. 5

Ndege

Kisha Garika, Noa alimutolea Yehova ‘viumbe vyenye kuruka vyenye kuwa safi’ pamoja na zabihu zingine za wanyama. (Mwa 8:18-20) Kuanzia pale, Mungu aliruhusu watu waanze kula ndege, lakini hakuwaruhusu kula damu. (Mwa 9:1-4; linganisha na Law 7:26; 17:13.) Kama ndege fulani waliitwa kuwa ‘safi’ ni juu kwa njia fulani Yehova aliruhusu watolewe kuwa zabihu; Biblia inaonyesha kama, kuhusu mambo ya chakula, hakuna ndege mwenye aliitwa kuwa ‘haiko safi’ mbele Sheria ya Musa ianze kutumika. (Law 11:13-19, 46, 47; 20:25; Kum 14:11-20) Kuhusu mambo ya dini, Biblia haionyeshe sababu zenye zilifanya ndege fulani waitwe kuwa ‘hawako safi.’ Kwa mufano, ndege wengi walikuwa wenye kuwinda ao wenye kula mizoga, lakini haiko wote njo walikuwa vile. (ona HUDIHUDI) Wakati agano jipya lilianzishwa, mambo ya kusema kama huyu ndege iko safi ao hapana iliisha. Na mu maono yenye Petro aliona, Mungu alimusaidia aelewe vile.​—Mdo 10:9-15.

Mali ya Kiroho

it-1-F uku. 1180

Kujikata-kata

Sheria ya Mungu alikataza Waisraeli kujikata-kata mwili kwa ajili ya mutu mwenye kufa. (Law 19:28; 21:5; Kum 14:1) Juu ya nini? Juu Waisraeli walikuwa watu watakatifu kwa ajili ya Yehova, mali yake ya pekee. (Kum 14:2) Tena walipaswa kujilinda na mazoea yote ya kuabudu sanamu. Zaidi ya ile, kuomboleza kupita mipaka kwa kujikata-kata mwili ilikuwa kosa kwa Waisraeli, juu walijua muzuri hali ya wafu na walikuwa na tumaini ya ufufuo. (Da 12:13; Ebr 11:19) Pia, Mungu alikataza Waisraeli kujikata-kata juu ya kuwakumbusha kama walipaswa kuheshimia mwili wa mwanadmu wenye aliumba.

TAREHE 18-24/01

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 22-23

“Sikukuu za Vipindi Zinatufundisha Nini”

it-1-F uku. 884-885

Sikukuu ya Mikate Yenye Haina Chachu

Siku ya kwanza ya Sikukuu ya mikate yenye haina chachu, ilikuwa mukusanyiko mukubwa, na ilikuwa pia sabato. Siku ya pili, tarehe 16 Mwezi wa Nisani, waliletea kuhani fungu la matunda ya kwanza ya mavuno, nafaka yenye inakomaa haraka mu Palestine. Mbele ya ile sikukuu, haikuruhusiwa kula nafaka yoyote ya mupya, yenye kukaangwa, ao mukate wowote. Kwa njia ya mufano, kuhani alikuwa anatolea Yehova ile matunda ya kwanza kwa kutikisa ile fungu mbele na nyuma, wakati mwana-kondoo dume katika mwaka wake wa kwanza mwenye hana kasoro iko anatolewa, pamoja na toleo la nafaka lenye kuchanganywa na mafuta, na pia toleo la kinywaji. (Law 23:6-14) Ile wakati, haikuruhusiwa kuunguza ile nafaka ao unga wake ku mazabahu. Lakini, kisha wakati fulani makuhani waliruhusiwa kufanya vile. Wakati wa ile sikukuu, matunda ya kwanza ilitolewa kwa ajili ya taifa lote. Lakini haiko ile tu; ku ile sikukuu, kila familia ya Waisraeli na kila mutu mwenye alikuwa na vitu fulani, alipewa nafasi ya muzuri ya kuvitoa kama zabihu za shukrani.​—Kut 23:19; Kum 26:1, 2; ona MATUNDA YA KWANZA.

Maana. Ile wakati, kukula mikate yenye haina chachu kulipatana na maagizo yenye Yehova alipatia Musa, yenye kuwa mu Kutoka 12:14-20. Mu mustari wa 19, Yehova alisema: “Hakuna unga wenye kufinyangwa na wenye kuwa na chachu wenye unapaswa kupatikana katika nyumba zenu kwa muda wa siku saba.” Mu Kumbukumbu la Torati 16:3, mikate yenye haina chachu inaitwa “mikate ya mateso.” Kila mwaka, ile mikate ilikuwa inakumbusha Wayahudi namna walitoka haraka mu Misri (hali yenye ilifanya wasipate wakati wa kutia chachu mu mikate yao [Kut 12:34]). Kwa hiyo, ile ilifanya Waisraeli wakumbuke namna walikombolewa kutoka mu mateso na utumwa wa Misri. Njo maana Yehova alisema: “Fanya vile siku zote za maisha yako ili ukumbuke siku yenye ulitoka katika inchi ya Misri.” Waisraeli walifanya sikukuu ya kwanza kati ya sikukuu tatu kubwa zenye walikuwa nazo mu mwaka ili kukumbuka vile walikombolewa, na ili kumushukuru Yehova mwenye aliwakomboa.​—Kum 16:16.

it-2-F uku. 527 fu. 1

Pentekoste

Matunda ya kwanza ya mavumo ya ngano haikupaswa kutolewa namna moja na matunda ya kwanza ya shayiri. Ili kutengeneza mikate mbili, iliomba kutumia sehemu mbili za kumi (2/10) za efa (litre 4.4) ya unga ya ngano na pia chachu. Waisraeli walipaswa kutosha ile mikate ‘mahali kwenye wanaishi’, ni kusema ile mikate ilipaswa kuwa sawa na mikate ya kila siku yenye wanatengezaka na kula mu nyumba zao, hapana sawa mikate yenye ilitumiwa tu kwa ajili ya utumishi mutakatifu. (Law 23:17) Ile mikate mbili ilitolewa pamoja na toleo la kuteketezwa na toleo la zambi, na wana-kondoo dume wawili walitolewa ili wakuwe toleo la ushirika. Kuhani alitikisa mbele na nyuma ile mikate na wale wana-kondoo dume mbele ya Yehova; ile ilimaanisha kama walitolewa mbele ya Yehova. Alifanya vile kwa kutia mikono yake chini ya ile mikate na chini ya vipande vya wale wana-kondoo dume. Kuhani njo alikuwa anakula ile mikate na wale wana-kondo dume wawili kisha kutolewa. Aliikula sawa vile toleo la ushirika.​—Law 23:18-20.

w14 15/5 uku. 29 fu. 11

Unaendelea Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Yehova

11 Tengenezo la Yehova linatutia moyo tufuate shauri hili la mutume Paulo: ‘Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri munavyoona siku ile kuwa inakaribia.’ (Ebr. 10:24, 25) Sikukuu za kila mwaka na mikusanyiko mingine ya kumuabudu Yehova, iliwasaidia Waisraeli wawe na uhusiano muzuri pamoja na Mungu. Zaidi ya hilo, mikusanyiko hiyo kama vile Sikukuu ya pekee ya Vibanda iliyofanywa katika siku za Nehemia ilikuwa wakati wa kufurahi sana. (Kut. 23:15, 16; Neh. 8:9-18) Sisi pia tunapata furaha kama hiyo kwenye mikutano, na mikusanyiko yetu. Acheni tuhuzurie mikutano na mikusanyiko hiyo ili tuwe na hali nzuri ya kiroho na furaha.​—Tito 2:2.

Mali ya Kiroho

w19.02 uku. 3 fu. 3

Endelea Kuwa Muaminifu-Mushikamanifu!

3 Wakati neno uaminifu-mushikamanifu linatumiwa juu yetu sisi watumishi wa Mungu, linamaanisha kumupenda Yehova kwa moyo wote na kujitoa kwake kwa moyo wote, na hilo linatuchochea kutia mapenzi yake pa nafasi ya kwanza katika maamuzi yetu yote. Tuchunguze habari fulani juu ya namna neno uaminifu-mushikamanifu linatumiwa mu Biblia. Maana ya kwanza ya neno la Biblia lenye kutafsiriwa “uaminifu-mushikamanifu,” ni kuwa kamili, bila kasoro, ao muzima. Kwa mufano, Waisraeli walikuwa wanamutolea Yehova zabihu za wanyama, na Sheria ilisema kama wanyama hao walipaswa kuwa bila kasoro. (Law. 22:21, 22) Watu wa Mungu hawakuruhusiwa kutoa munyama mwenye alikuwa anakosa muguu, sikio, ao jicho; na hawangepaswa kutoa munyama mwenye kuwa mugonjwa. Yehova aliona kama ni jambo la maana munyama wa zabihu akuwe kamili, bila kasoro, ao muzima. (Mal. 1:6-9) Tunaweza kuelewa juu ya nini Yehova anapendezwa na kitu chenye hakina kasoro ao chenye kuwa kamili. Kwa mufano, wakati tunauza kitu fulani kama vile tunda, kitabu, ao kifaa fulani, hatupendi kile chenye kuwa na matundu ao chenye kukosa sehemu fulani. Tunapenda kitu chenye kuwa kamili, chenye hakina kasoro, ao chenye kuwa kizima. Yehova naye anataka upendo na ushikamanifu wenye tunamuonyesha ukuwe vile; unapaswa kuwa kamili, bila kasoro, ao muzima.

Hotuba

w07-SW 15/7 uku. 26

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Sheria ya Musa iliwaagiza hivi Waisraeli: “Mara tatu katika mwaka kila mwanamume wa kwako ataonekana mbele za Yehova Mungu wako katika mahali ambapo atapachagua: katika sherehe ya keki zisizo na chachu na katika sherehe ya majuma na katika sherehe ya vibanda.” (Kumbukumbu la Torati 16:16) Kuanzia wakati wa Mfalme Sulemani na kuendelea, hekalu la Yerusalemu lilikuwa mahali ambapo Mungu alichagua.

Sherehe ya kwanza kati ya sherehe hizo tatu ilifanywa mwanzoni mwa majira ya kuchipua. Sherehe hiyo iliitwa Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, nayo ilianza siku iliyofuata sherehe ya Pasaka mnamo Nisani 14 na ikaendelea kwa siku saba mpaka Nisani 21. Siku ya pili ya sherehe hiyo, Nisani 16, ilikuwa mwanzo wa mavuno ya kwanza ya mwaka kulingana na kalenda takatifu. Siku hiyo, kuhani mkuu alipaswa kuchukua “mganda wa matunda ya kwanza” ya mavuno ya shayiri na kuutikisa “huku na huku, mbele za Yehova” katika patakatifu. (Mambo ya Walawi 23:5-12) Kwa kuwa wanaume wote walipaswa kuhudhuria Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, ni nani aliyevuna matoleo hayo?

Amri ya kutoa matunda ya kwanza ya mavuno kwa Yehova wakati wa Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu ilitolewa kwa taifa lote. Kila mtu hakuhitajiwa kuanza kuvuna na kuleta matunda ya kwanza kwa ajili yake mwenyewe katika patakatifu. Badala yake, taifa hilo liliamriwa lifanye hivyo kupitia watu fulani walioliwakilisha taifa lote. Hivyo, mganda wa Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu ungekatwa na wajumbe waliotumwa katika shamba la karibu la shayiri. Kitabu kimoja (Encyclopaedia Judaica) kinasema hivi kuhusu jambo hilo: “Ikiwa shayiri ilikuwa imekomaa ilichukuliwa kutoka karibu na Yerusalemu; kama sivyo ingeletwa kutoka sehemu yoyote ya Israeli. Ilivunwa na wanaume watatu, kila mmoja wao alikuwa na mundu wake na kikapu.” Kisha, mganda wa shayiri uliletwa kwa kuhani mkuu, ambaye aliutoa kwa Yehova.

Takwa la kutoa matunda ya kwanza ya mavuno liliwapa Waisraeli nafasi nzuri sana ya kuonyesha kwamba walithamini jinsi ambavyo Mungu alibariki nchi yao na mavuno yao. (Kumbukumbu la Torati 8:6-10) Hata hivyo, kwa kuongezea, toleo hilo la sherehe lilikuwa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja.” (Waebrania 10:1) Kwa kweli, Yesu Kristo alifufuliwa mnamo Nisani 16 mwaka wa 33 W.K., siku ya kutoa matunda ya kwanza ya mavuno kwa Yehova. Mtume Paulo aliandika hivi kumhusu Yesu: “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo. . . . Lakini kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.” (1 Wakorintho 15:20-23) Mganda wa matunda ya kwanza ambao kuhani mkuu alitikisa huku na huku mbele za Yehova ulifananisha Yesu Kristo aliyefufuliwa, mtu wa kwanza kabisa kufufuliwa kutoka kwa wafu na kupata uzima wa milele. Hivyo, Yesu alifungua njia ya kuwakomboa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo.

TAREHE 25-31/01

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 24-25

“Mwaka wa Yubile na Kuwekwa Huru Wakati Wenye Kuja”

it-2-F uku. 137

Uhuru

Mungu wa Uhuru. Yehova ni Mungu wa uhuru. Alikomboa taifa la Israeli kutoka mu utumwa wa Misri. Na aliwaambia kama ikiwa wanatii amri zake atawabariki na kuwafanya kuwa huru. (Kum 15:4, 5) Daudi alisema kama kungekuwa “usalama” ndani ya minara ya Yerusalemu. (Zb 122:6, 7) Lakini kulingana na Sheria, kama mutu alikuwa maskini alipaswa kujiuzisha na kuwa mutumwa juu apate mambo yenye yeye na familia yake wako nayo lazima. Tena, Sheria ilisema kama ule mutumwa Muebrania alipaswa kuwekwa huru mu mwaka wa saba wa utumwa wake. (Kut 21:2) Wakati wa Yubile (yenye ilikuwa inafanyika kila mwaka wa 50), uhuru ulikuwa unatangazwa kwa wakaaji mu inchi yote. Kila mutumwa Muebrania aliwekwa huru, na kila mwanaume alikuwa anarudilia uriti wake.​—Law 25:10-19.

it-1-F uku. 1107 fu. 7

Uriti

Inchi haikupaswa kuuzishwa kwa muda wa kudumu kwa sababu ilikuwa mali ya familia, kutoka kizazi mupaka kizazi. Kwa kweli, kuuzisha inchi kulimaanisha kuikopesha kulingana na mazao yenye ile inchi ingetokeza. Bei ya kuuza inchi, iliwekwa kulingana na hesabu ya miaka yenye ilikuwa inabakia mbele Yubile ingine ianze. Iliomba kufanya vile, juu ni mu mwaka wa Yubile njo inchi ingerudia mu mikono ya mwenye nayo kama haikununuliwa tena mbele ya ile Yubile. (Law 25:13, 15, 23, 24) Ile sheria ilitumiwa pia kuhusu manyumba yenye ilikuwa mu miji yenye haikuzungukwa na ukuta. Ile manyumba ilionwa kuwa sehemu ya mashamba. Lakini, kuhusu manyumba yenye ilikuwa mu miji yenye ilizungukwa na ukuta, haki ya kuikomboa ilikuwa inafanya tu mwaka moja, kuanzia tarehe yenye mutu anainunua. Sasa kuhusu manyumba ya mu miji ya Walawi, haki ya kuikomboa ilikuwa ya kudumu juu hawakupewa uriti wa inchi.​—Law 25:29-34.

it-2-F uku. 70 fu. 2

Yubile

Kuheshimia sheria kuhusu Yubile kulilinda Waisraeli wasiangukie mu mambo yenye tuko tunaona mu inchi mingi leo; ni kusema, mwenye wengine ni maskini sana na wengine ni matajiri sana. Ile sheria ililetea Waisraeli wote faida, juu hakukuwa mutu mwenye alionwa kuwa wa bure sababu ya umaskini. Lakini, kila mutu alikuwa anasaidia taifa kupitia vipawa na uwezo mbalimbali wenye alikuwa nao. Yehova alikuwa anabariki udongo wa Waisraeli na kuwapatia maagizo. Wakati walikuwa wanatii ile maagizo, walikuwa wanafurahia uongozi wenye kukamilika wenye ni Yehova tu njo anaweza kupatia watu wake.​—Isa 33:22.

Mali ya Kiroho

w09-SW 1/9 uku. 22 fu. 4

Wakati Mtu Anapokuudhi

Ikiwa Mwisraeli angempiga Mwisraeli mwenzake na kumng’oa jicho, Sheria iliruhusu haki itendeke. Hata hivyo, halikuwa jukumu la mtu aliyeumizwa kumwadhibu yule aliyempiga au kumwadhibu mtu wa familia yake. Sheria ilitaka mtu yule aliyeumizwa alifikishe jambo hilo kwa wenye mamlaka, yaani, waamuzi waliowekwa, ili jambo hilo lishughulikiwe kwa njia inayofaa. Kujua kwamba mtu anayetenda uhalifu au ujeuri kwa kupenda dhidi ya mwenzake angeadhibiwa kwa njia hiyohiyo, kuliwasaidia watu wengine wasilipize kisasi. Hata hivyo, kulikuwa na mengi yanayohusika.

TAREHE 1-7/02

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | MAMBO YA WALAWI 26-27

“Mambo ya Kufanya ili Yehova Atubariki”

w08-SW 15/4 uku. 4 fu. 8

Kataa Kabisa “Vitu Visivyo na Thamani”

8 “Utajiri” unaweza kuwa kama mungu jinsi gani? Kwa mfano, fikiria jiwe likiwa kwenye uwanja fulani katika Israeli la kale. Jiwe kama hilo lingeweza kutumiwa kujenga nyumba au ukuta. Kwa upande mwingine, ikiwa lingewekwa kama “nguzo takatifu” au ‘jiwe ambalo ni sanamu,’ lingewakwaza watu wa Yehova. (Law. 26:1) Vivyo hivyo, pesa zina faida zake. Tunazihitaji ili kuishi, na tunaweza kuzitumia vizuri katika utumishi wa Yehova. (Mhu. 7:12; Luka 16:9) Lakini tukitanguliza pesa badala ya utumishi wetu wa Kikristo, pesa zinakuwa kama mungu kwetu. (Soma 1 Timotheo 6:9, 10.) Katika ulimwengu huu, ambamo watu wanathamini sana utajiri, ni lazima tuhakikishe kwamba tunadumisha maoni yenye usawaziko kuhusu pesa.​—1 Tim. 6:17-19.

it-2-F uku. 753 fu. 2

Kuogopa

Musa alionyesha mbele ya watu wa Mungu nguvu zenye kuogopesha (Kiebr.: môraʼ), kulingana na vile Mungu alikuwa anamutumia na kumutendea. (Kum 34:10, 12; Kut 19:9) Wale wenye walikuwa na imani waliogopa sana mamlaka yenye Musa alikuwa nayo. Walielewa kama Mungu alikuwa anasema kupitia Musa. Waisraeli walipaswa pia kuogopa patakatifu pa Yehova. (Law 19:30; 26:2) Ile ilimaanisha kama walipaswa kupaheshimia kwa kumuabudu Yehova kulingana na vile aliwaomba na kwa kufuata amri zake zote.

w91-SW 1/3 uku. 17 fu. 10

Acha “Amani Ya Mungu” Ilinde Moyo Wako

10 Yehova aliambia taifa hilo hivi: “Kama mkienda katika amri zangu, na kuyashika maagizo yangu, na kuyafanya; ndipo nitazinyesha mvua zenu kwa nyakati zake, na nchi itazaa maongeo yake, na miti ya mashambani itazaa matunda yake. Nami nitawapa amani katika nchi, tena mtalala wala hapana atakayewatia hofu; nami nitawakomesha wanyama wabaya katika nchi yenu, wala hautapita upanga katika nchi yenu. Nami nitakwenda kati yenu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mtakuwa watu wangu.” (Walawi 26:3, 4, 6, 12) Israeli wangeweza kuona shangwe wakiwa na amani kwa kuwa walikuwa na usalama kutokana na maadui wao, wingi wa mali, na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Lakini hayo yangetegemea kushikilia kwao sheria ya Yehova.​—Zaburi 119:165.

Mali ya Kiroho

it-2-F uku. 564

Ugonjwa wa Kuambukiza

Matokeo ya Mubaya ya Kuacha Sheria ya Yehova. Mungu aliambiaka Waisraeli mbele ya wakati kama wakivunja agano lenye alifanya pamoja nao, ‘atawatumia ugonjwa wa kuambukiza.’ (Law 26:14-16, 23-25; Kum 28:15, 21, 22). Maandiko yote inaonyesha kama kuwa na afya ya muzuri ya kiroho ao ya kimwili, ni baraka yenye inatoka kwa Mungu (Kum 7:12, 15; Zb 103:1-3; Mez 3:1, 2, 7, 8; 4:21, 22; Ufu 21:1-4), lakini magonjwa inatokana na zambi na hali ya kukosa kukamilika. (Kut 15:26; Kum 28:58-61; Isa 53:4, 5; Mt 9:2-6, 12; Yo 5:14) Kwa hiyo, ni kweli kama wakati fulani, Yehova alipiga moja kwa moja watu fulani kwa magonjwa. Kwa mufano, alipiga Miriamu, Uza na Gehazi kwa ugonjwa wa ukoma. (Hes 12:10; 2Ny 26:16-21; 2Fa 5:25-27) Lakini mara mingi, inaonekana kama magonjwa na magonjwa ya kuambukiza yenye mutu ao watu walipata ilikuwa ni kwa sababu ya zambi zenye walifanya. Wale watu walikuwa wanavuna tu kile chenye walipanda; mwenendo wao mubaya ulifanya mwili wao wenye haukamilke upatwe na ile magumu. (Gal 6:7, 8) Kuhusu wale wenye walikuwa wanafanya matendo machafu sana ya uasherati, mutume Paulo alisema kama Mungu “aliwaacha katika uchafu, ili miili yao ivunjiwe heshima kati yao . . . na kupokea ndani yao wenyewe azabu kamili, kwa sababu ya kosa lao.”​—Ro 1:24-27.

Hotuba

w09-SW 1/8 uku. 30

Wasomaji Wetu Wanauliza

“Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanajua maneno hayo. Hata hivyo, huenda watu fulani wanaoenda kanisani wakahisi kwamba wanalazimika kutoa zaidi ya uwezo wao. Kwa kweli, dini fulani zinawataka washiriki wao watoe kiasi fulani cha pesa. Zoea hilo linaitwa kutoa zaka, yaani, mtu kutoa asilimia 10 ya mapato yake kwa kanisa.

Je, kweli Biblia inatuamuru tutoe kiasi fulani hususa cha pesa kama mchango? Mimi binafsi, ninapaswa kuchanga kiasi gani cha pesa?

Matakwa na Michango ya Hiari Zamani

Biblia ina maagizo ya wazi kwa taifa la Israeli kuhusu kiasi ambacho Mungu alitaka watoe. (Mambo ya Walawi 27:30-32; Hesabu 18:21, 24; Kumbukumbu la Torati 12:4-7, 11, 17, 18; 14:22-27) Matakwa hayo hayakuzidi uwezo wao. Yehova aliahidi kwamba ikiwa wangetii sheria zake, angefanya taifa hilo ‘lifurike kwa ufanisi.’​—Kumbukumbu la Torati 28:1, 2, 11, 12.

Nyakati nyingine, Waisraeli walitoa michango mingi au michache ya hiari kadiri walivyotaka. Kwa mfano, Mfalme Daudi alipopanga kumjengea Yehova hekalu, raia wake walitoa “dhahabu yenye thamani ya talanta elfu tano.” (1 Mambo ya Nyakati 29:7) Tofautisha hilo na yale ambayo Yesu aliona alipokuwa duniani. Alimwona “mjane fulani mwenye uhitaji akitumbukiza . . . sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana” ndani ya sanduku la hazina la hekalu. Mchango wake ulikuwa wa kiasi gani? Ulikuwa tu 1/64 ya mshahara wa siku moja. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba kiasi hicho kidogo kilikubalika.​—Luka 21:1-4.

Je, Wakristo Wanapaswa Kutoa Kiasi Fulani cha Pesa?

Wakristo hawako chini ya agano la Sheria ambalo Waisraeli walipewa. Hivyo, hawalazimishwi kumtolea Mungu kiasi fulani cha pesa. Hata hivyo, katika kutaniko la kweli la Kikristo, kutoa kunaleta shangwe kubwa sana. Yesu Kristo mwenyewe alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—Matendo 20:35.

Mashahidi wa Yehova wanategemeza kazi yao ya kuhubiri ulimwenguni pote kupitia michango ya hiari. Michango hiyo inatumiwa kuchapisha vichapo, kama vile gazeti hili unalosoma, na kujenga na kutunza majengo yao ya ibada ambayo yanaitwa Majumba ya Ufalme. Pesa zinazokusanywa hazitumiwi kamwe kulipa mishahara. Wengine wanaojitoa wakati wote katika kazi ya kufanya wanafunzi wanapewa msaada ili kulipia gharama zao za kusafiri na gharama nyingine za kibinafsi. Lakini hakuna mtu anayesisitiza apewe msaada huo. Kwa kweli, Mashahidi wengi wa Yehova hawapewi msaada wowote wa kifedha ili kutegemeza kazi yao ya kuhubiri. Badala yake, wengi wao wanafanya kazi za kimwili ili kujitegemeza wenyewe, kama tu Paulo alivyofanya kazi ya kutengeneza mahema.​—2 Wakorintho 11:9; 1 Wathesalonike 2:9.

Ikiwa mtu anataka kutoa mchango kwa ajili ya kazi inayotimizwa na Mashahidi wa Yehova, anapaswa kutoa kiasi gani? Mtume Paulo aliandika hivi: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”​—2 Wakorintho 8:12; 9:7.

TAREHE 8-14/02

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 1-2

“Yehova Anapanga Watu Wake”

w94-SW 1/12 uku. 9 fu. 4

Mahali Pafaapo pa Ibada ya Yehova Maishani Mwetu

4 Kama ungetazama kutoka angani Israeli iliyopiga kambi nyikani, je, ungeona nini? Mahema mengi sana, lakini yaliyopangwa kwa utaratibu, yenye watu wapatao milioni tatu au hata zaidi, wakiwa katika vikundi vya makabila matatu-matatu upande wa kaskazini, kusini, mashariki na magharibi. Kama ungechunguza kwa ukaribu zaidi, ungeona pia vikundi vingine karibu na katikati ya kambi. Vikundi hivyo vinne vidogo-vidogo vya mahema vilikuwa vya familia za kabila la Lawi. Katikati kabisa mwa kambi, katika eneo lililotenganishwa kwa pazia, kulikuwa na kitu cha kipekee sana. Hicho kilikuwa “hema ya kukutania,” au tabenakulo, ambayo Waisraeli ‘waliokuwa na moyo wa hekima’ walikuwa wamejenga kulingana na plani ya Yehova.​—Hesabu 1:52, 53; 2:3, 10, 17, 18, 25; Kutoka 35:10.

it-1-F uku. 385

Kambi

Kambi ya Israeli ilikuwa kubwa sana. Vile tumeona, hesabu yote ya wapiganaji-vita wenye kuandikishwa ilikuwa 603 550. Ku ile hesabu inaomba kuongeza wanamuke na watoto, wazee na vilema, Walawi 22 000 na “kikundi kikubwa cha watu wenye kuchangamana” cha wageni. Ni kusema, pengine wote walikuwa 3 000 000 ao zaidi. (Kut 12:38, 44; Hes 3:21-34, 39) Ukubwa wa eneo kwenye kulikuwa kambi haujulikane muzuri, na namna watu wanawaziaka ukubwa wenyewe haipatane hata kidogo. Kulingana na vile Biblia inaonyesha, wakati kambi iliwekwa mu maeneo tambarare ya Moabu, yenye kuangaliana na Yeriko, ilianzia “Bet-yeshimoti mupaka Abel-shitimu.”​—Hes 33:49.

Mali ya Kiroho

it-1-F uku. 767

Kuandikishwa

Ni kuandika majina ya watu, kwa kawaida kulingana na kizazi chao, kabila na vile wanafuatana mu nyumba yao. Kusudi haikukuwa tu kuhesabia watu. Sawa vile Biblia inaonyesha, kulikuwa sababu mingi zenye zilifanya watu waandikishwe. Kwa mufano, wamoja waliandikishwa juu ya mambo ya kodi, wengine ili kuwa maaskari, ao ili kutumikia mahali patakatifu (zaidi sana Walawi).

Hotuba

w08-SW 1/7 uku. 21

Makabila, au familia za Israeli zilitokana na wana wa Yakobo ambaye jina lake lilibadilishwa na kuwa Israeli. Mzee huyo wa ukoo alikuwa na wana 12​—Rubeni, Simeoni, Lawi, Yuda, Dani, Naftali, Gadi, Asheri, Isakari, Zebuloni, Yosefu, na Benyamini. (Mwanzo 29:32–30:24; 35:16-18) Hakuna kabila lililoitwa la Yosefu, lakini makabila kumi na moja yaliitwa majina ya ndugu zake. Makabila mawili yalipewa majina ya wana wa Yosefu, Efraimu na Manase, walioonwa kuwa wakuu wa makabila yao. Kwa hiyo, idadi ya makabila ya Israeli ikafikia 13. Kwa nini basi, Biblia inazungumzia makabila 12?

Miongoni mwa Waisraeli, wanaume wa kabila la Lawi waliwekwa kando ili watumikie katika maskani ya Yehova na baadaye hekaluni. Hivyo, hawakuandikishwa jeshini. Yehova alimwambia Musa hivi: “Ni kabila la Lawi tu ambalo hutaandikisha, na hesabu yao usiichukue kati ya wana wa Israeli. Na wewe mwenyewe uweke rasmi Walawi juu ya maskani ya Ushuhuda na juu ya vyombo vyake vyote na juu ya kila kitu kilicho chake.”​—Hesabu 1:49, 50.

Zaidi ya hilo, Walawi hawakupewa urithi katika Nchi ya Ahadi. Badala yake, walipewa majiji 48 kotekote katika eneo la Israeli.​—Hesabu 18:20-24; Yoshua 21:41.

Kwa sababu hizo mbili, kwa kawaida kabila la Lawi halikutiwa ndani makabila yalipoorodheshwa. Hivyo, kwa kawaida makabila ya Israeli yalisemwa kuwa 12.​—Hesabu 1:1-15.

TAREHE 15-21/02

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 3-4

“Kazi Yenye Walawi Walikuwa Wanafanya”

it-2-F uku. 655 fu. 1

Kuhani

Chini ya Agano la Sheria. Wakati Waisraeli walikuwa watumwa mu inchi ya Misri, Yehova alijitakasia wazaliwa wote wa kwanza wanaume wa Waisraeli wakati alitumia pigo la kumi, ili kuua kila muzaliwa wa kwanza mwanaume wa Wamisri. (Kut 12:29; Hes 3:13) Wale wazaliwa walikuwa wake na alipaswa kuwatumia tu mu kazi ya pekee yenye angewapatia. Yehova angetumiaka wale wazaliwa wa kwanza wanaume Waisraeli na kuwapatia kazi ya ukuhani na kazi ya kuhangaikia patakatifu. Lakini kulingana na kusudi lake, aliona kama ni muzuri kuchagua wanaume wa kabila la Lawi juu wafanye ile kazi. Njo maana aliruhusu taifa lichukue wanaume Walawi pa nafasi ya wazaliwa wa kwanza wanaume wa makabila ingine 12 (wazao wa Efraimu na wa Manase, watoto wa Yosefu, walihesabiwa kuwa makabili mbili). Kisha kuandikisha watu, ku hesabu ya wanaume Walawi, kuliongezeka wazaliwa wa kwanza wanaume 273 wenye hawakukuwa Walawi, wenye waliandikishwa kwa majina kuanzia mwezi mumoja na zaidi. Kwa hiyo, Mungu aliomba shekeli 5 (11 $) kwa ajili ya kila mumoja wa wale wazaliwa wa kwanza wanaume 273 ili kulipa bei yao ya ukombozi, na ile shekeli ilipewa Haruni na watoto wake wanaume. (Hes 3:11-16, 40-51) Mbele ya pale, Yehova alikuwa alishakachagua na kuweka pembeni wanaume wa familia ya Haruni, wa kabila la Lawi ili wakuwe wanafanya kazi ya ukuhani mu Israeli.​—Hes 1:1; 3:6-10.

it-2-F uku. 133 fu. 1

Walawi

Kazi Yenye Walikuwa Wanafanya. Walawi walifanyizwa na familia tatu za watoto wa Lawi: Gershoni (Gershomu), Kohati na Merari. (Mwa 46:11; 1Ny 6:1) Wakati walikuwa mu jangwa, kila familia ya Walawi ilipewa fasi karibu na tabenakulo. Familia ya Kohati ya Haruni ilikuwa mbele ya tabenakulo upande wa mashariki. Wakohati wengine walipiga kambi upande wa kusini, Wagershoni upande wa mangaribi, na Wamerari upande wa kaskazini. (Hes 3:23, 29, 35, 38) Kazi ya Walawi ilikuwa kubomoa, kusimamisha na kubeba tabenakulo. Wakati wa kuondoa kambi, Haruni na watoto wake wanaume walikuwa wanashusha pazia yenye ilitenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi, kisha walifunika sanduku la ushuhuda, mazabahu na vyombo vingine vitakatifu. Kisha Wakohati walikuwa wanabeba vile vitu. Kazi ya Wagershoni ilikuwa kubeba vitambaa vya hema, vifuniko, vitambaa vya kuficha, mapazia yenye kuninginia ya kiwanja, na kamba za hema (ni kusema kamba za tabenakulo). Kazi ya Wamerari ilikuwa kusimamia kadre za mbao za tabenakulo, nguzo zake, vikalio vyake, misumari na kamba zake (kamba za kiwanja chenye kinazunguka tabenakulo).​—Hes 1:50, 51; 3:25, 26, 30, 31, 36, 37; 4:4-33; 7:5-9.

it-2-F uku. 133 fu. 3

Walawi

Wakati wa Musa, iliomba Mulawi aeneze miaka 30 juu aanze kufanya kazi zake zote. Kwa mufano, kazi ya kubeba tabenakulo na vyombo vyake wakati ilikuwa inapelekwa fasi ingine. (Hes 4:46-49) Hata vile, kulikuwa kazi zingine zenye Mulawi alikuwa anafanya kuanzia miaka 25, lakini inawezekana haikukuwa kazi ya nguvu sawa vile kubeba tabenakulo. (Hes 8:24) Wakati wa Daudi, ile miaka ilishuka mupaka 20. Daudi alisema kama sababu ya kufanya vile ni juu tabenakulo haingekuwa inabebwa tena (hekalu njo ingetumiwa pa nafasi ya tabenakulo). Wakati mutu alifikia miaka 50 aliacha kazi ya kulazimishwa. (Hes 8:25, 26; 1Ny 23:24-26; ona UMRI) Walawi walipaswa kujua sana Sheria juu ni wao njo walipaswa kuisoma mbele ya watu na kuifundisha.​—1Ny 15:27; 2Ny 5:12; 17:7-9; Ne 8:7-9.

Mali ya Kiroho

w06-SW 1/8 uku. 23 fu. 13

Uwe Mwenye Hekima​—mwogope Mungu!

13 Daudi alipoona Yehova akimsaidia wakati wa taabu, hilo lilimfanya amwogope Yehova zaidi na kumwamini zaidi. (Zaburi 31:22-24) Hata hivyo, katika visa vitatu vya pekee, Daudi hakumwogopa Mungu, na hilo lilisababisha msiba. Kisa cha kwanza ni wakati ambapo alipanga sanduku la agano la Yehova lisafirishwe kwa gari la kukokotwa hadi Yerusalemu badala ya kuwatumia Walawi kulibeba juu ya mabega yao, kama Sheria ya Mungu ilivyoagiza. Uza ndiye aliyeliendesha gari hilo. Wakati alipolishika Sanduku ili kuzuia lisianguke, alikufa papo hapo kwa sababu ya “tendo [hilo] lisilo la heshima kwa Mungu.” Naam, Uza alitenda dhambi nzito, lakini msiba huo ulitukia hasa kwa sababu Daudi hakuiheshimu Sheria ya Mungu. Kumwogopa Mungu kunamaanisha kufanya mambo kwa njia yake.​—2 Samweli 6:2-9; Hesabu 4:15; 7:9.

TAREHE 22-28/02

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 5-6

“Namna Gani Unaweza Kuiga Wanaziri?”

it-2-F uku. 381-382

Munaziri

Kila mutu mwenye alifanya naziri ya kuwa Munaziri hakupaswa kufanya hii mambo tatu: 1) Kunywa vinywaji vya kulewesha; ile ilitia ndani kula kitu chochote chenye kilitengenezwa na muti wa muzabibu, ikuwe zabibu zenye hazijakomaa, za kukomaa ao za kukauka, ao kunywa maji yoyote yenye ilitengenezwa na zabibu, ikuwe yenye haijatiwa chachu, yenye ilishatiwa chachu ao ya siki; 2) Kukata nywele za kichwa chake; 3) Kugusa maiti, hata maiti ya mutu wa karibu sana: baba, mama, ndugu ao dada.​—Hes 6:1-7.

Naziri za Pekee. Mutu mwenye alifanya naziri ya pekee alipaswa “kuishi akiwa Munaziri [kutengwa, kutolewa ao kuwekwa pembeni] kwa ajili ya Yehova,” hapana juu watu wamusifu juu alichagua maisha ya kujiima mambo mingi. Sheria ilisema kama “yeye ni mutakatifu kwa ajili ya Yehova siku zote za Unaziri wake.”​—Hes 6:2, 8; linganisha na Mwa 49:26, maelezo ya chini.

Mambo yenye wanaziri waliombwa kufanywa ilikuwa ya maana na ilikuwa na kusudi ya pekee mu ibada ya Yehova. Munaziri alikuwa sawa na kuhani mukubwa mwenye hakuruhusiwa kugusa maiti, hata maiti ya mutu wa karibu sana, kwa sababu kazi yake ilikuwa takatifu. Juu walikuwa na madaraka mazito, kuhani mukubwa na makuhani wengine hawakuruhusiwa kunywa divai ao kinywaji chochote cha kulewesha wakati walikuwa wanafanya kazi yao takatifu mbele ya Yehova.​—Law 10:8-11; 21:10, 11.

Zaidi ya ile, Munaziri (Kiebr.: nazir) ‘alipaswa kujionyesha kuwa mutakatifu kwa kuacha nywele za kichwa chake zikuwe za murefu,’ ile ilikuwa alama ya kusaidia watu wote watambue mara moja kama unaziri wake ulikuwa takatifu. (Hes 6:5) Ileile neno ya Kiebrania nazir, ilitumiwa pia kuhusu miti ya mizabibu “yenye matawi yake hayajakatwa” wakati wa miaka takatatifu ya Sabato na ya Yubile. (Law 25:5, 11) Inafurahisha kujua kama ku sehemu ya mbele ya kilemba cha bamba la zahabu la kuhani mukubwa, kwenye kuliandikwa maneno: “Utakatifu ni wa Yehova,” kuliitwa pia “alama takatifu ya kuwekwa pembeni kwa ajili ya kusudi la pekee [Kiebr.: nézèr, yenye kuwa na maana moja na neno nazir].” (Kut 39:30, 31) Taji lenye wafalme watiwa-mafuta Waisraeli walikuwa wanavaa liliitwa pia nézèr (2Sa 1:10; 2Fa 11:12; ona KUJITOA; TAJI). Mu kutaniko la Kikristo, mutume anasema kama ni muzuri mwanamuke kuwa na nywele za murefu kuliko kufunika kichwa chake; na ile inamukumbusha kama iko na daraka yenye kuwa tofauti na ya mwanaume. Kulingana na mupango wa Mungu wa ukichwa, anapaswa kukumbuka kama ni lazima ajitiishe. Kwa hiyo, kulingana na mambo yote yenye Munaziri aliombwa, sawa vile kuepuka kukata nywele (jambo lenye haliko la kawaida kwa mwanaume), kuepuka kabisa kunywa divai na kuepuka uchafu wowote, ilikuwa inakumbusha kila Munaziri ulazima wa kujitoa na kujiitisha kabisa ili kufanya mapenzi ya Yehova.​—1Ko 11:2-16; ona NYWELE; KUFUNIKA KICHWA; ASILI.

Mali ya Kiroho

w05-SW 15/1 uku. 30 fu. 2

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hata hivyo, Samsoni, alikuwa Mnadhiri katika maana tofauti. Kabla ya kuzaliwa kwa Samsoni, malaika wa Yehova alimwambia mama yake hivi: “Tazama! utachukua mimba, nawe utazaa mwana, na wembe wowote usipite juu ya kichwa chake, kwa maana mtoto huyo atakuwa Mnadhiri wa Mungu tangu atakapotoka tumboni; naye ndiye atakayeongoza katika kuokoa Israeli kutoka mkononi mwa Wafilisti.” (Waamuzi 13:5) Samsoni hakuweka nadhiri ya kuwa Mnadhiri. Mungu ndiye aliyemweka rasmi kuwa Mnadhiri, naye angekuwa Mnadhiri maisha yake yote. Katazo kuhusu kugusa maiti halikumhusu. Kama lingemhusu naye aguse maiti bila kukusudia, angewezaje kuanza tena Unadhiri wake ambao ulianza alipozaliwa? Basi, yaonekana kwamba kwa njia fulani, matakwa ya Wanadhiri wa maisha yalitofautiana na ya wale waliojitoa wenyewe kuwa Wanadhiri.

Hotuba

w06-SW 15/1 uku. 32

MIAKA 25 iliyopita, wanaakiolojia wa Israel waligundua jambo la kustaajabisha. Katika pango la kuzikia kwenye miteremko ya Bonde la Hinomu huko Yerusalemu, walipata hati mbili za kukunjwa zilizotengenezwa kwa fedha ambazo zilikuwa na maandiko ya Biblia. Hati hizo zilitengenezwa kabla ya Wababiloni kuharibu Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Hati hizo zilinukuu baadhi ya baraka zinazotajwa kwenye Hesabu 6:24-26. Jina la Mungu, Yehova, lilipatikana mara kadhaa katika hati hizo. Hati hizo zimetajwa kuwa “maandishi ya kale zaidi kuwahi kupatikana ambayo yanarekodi masimulizi ya Biblia ya Kiebrania.”

Hata hivyo, wasomi fulani walitilia shaka tarehe ya hati hizo na wakasema kwamba ziliandikwa katika karne ya pili K.W.K. Sababu moja ni kwamba picha za awali za hati hizo ndogo hazikuwawezesha kuzichunguza vizuri. Ili kutatua ubishi huo kuhusu tarehe za hati hizo, kikundi fulani cha wasomi kilifanya uchunguzi mwingine. Walitumia mashini na kompyuta za kisasa za kutokeza picha ili kupata picha nzuri zaidi za hati hizo. Matokeo ya uchunguzi huo yalichapishwa hivi karibuni. Wasomi hao waligundua nini?

Kwanza, wasomi hao wanasisitiza kwamba habari zilizopatikana mahali hati hizo zilipovumbuliwa zinaonyesha kwamba ziliandikwa kabla ya Wayahudi kupelekwa uhamishoni huko Babiloni. Uchunguzi wa hati hizo kwa kukagua herufi zilizoandikwa, yaani, umbo lake, mtindo wake, mkao wake, mfuatano wake, na upande ambao herufi hizo zilielekezwa, unaonyesha kwamba ziliandikwa katika kipindi hichohicho, yaani, karibu na mwisho wa karne ya saba K.W.K. Hatimaye, baada ya kuchunguza usahihi wa maneno, wasomi hao walisema: “Uchunguzi wa usahihi wa maneno yaliyo katika [hati] hizo unaonyesha kwamba ziliandikwa wakati uleule ambao umethibitishwa kupitia habari zilizopatikana mahali zilipovumbuliwa na kwa kuchunguza herufi.”

Jarida Bulletin of the American Schools of Oriental Research linakata kauli hii kuhusu uchunguzi huo wa hati hizo za fedha, ambazo pia huitwa maandishi ya Ketef Hinnom: “Hivyo, tunaweza kuunga mkono kauli iliyofikiwa na wasomi wengi kwamba maandishi yaliyo kwenye hati hizo ndiyo manukuu ya awali zaidi ya Biblia kuwahi kupatikana.”

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine