Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • Anasafisha Tena Hekalu
    Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
    • Yesu anapindua meza ya mubadilisha-feza

      SURA 103

      Anasafisha Tena Hekalu

      MATAYO 21:12, 13, 18, 19 MARKO 11:12-18 LUKA 19:45-48 YOHANA 12:20-27

      • YESU ANALAANI MUTI WA TINI NA ANASAFISHA HEKALU

      • YESU ANAPASWA KUFA ILI KUTOLEA WATU WENGI UZIMA

      Yesu na wanafunzi wake wamepitisha usiku tatu katika Betania tangu watoke Yeriko. Sasa Siku ya Kwanza asubui sana, tarehe 10 Mwezi wa Nisani, wanaenda Yerusalemu. Yesu anasikia njaa. Kwa hiyo, wakati anaona muti wa tini, anaenda kwenye muti huo. Je, muti huo uko na matunda?

      Sasa ni mwisho-mwisho wa Mwezi wa 3, lakini kipindi cha matunda ya tini kitaanza tu katika Mwezi wa 6. Lakini, ule muti umekwisha kuwa na majani, ni kusema yamechipuka mbele ya wakati. Kwa hiyo Yesu anawaza kama atapata matunda ya kwanza-kwanza. Lakini hapate kitu. Majani hayo yalifanya ionekane kama ule muti uko na matunda. Kwa hiyo Yesu anauambia: “Mutu yeyote asikule tena matunda kutoka kwako hata siku moja.” (Marko 11:14) Mara moja ule muti unaanza kukauka. Wanafunzi wataelewa maana ya jambo hilo asubui yenye kufuata.

      Kisha muda mufupi, Yesu na wanafunzi wake wanafika Yerusalemu. Anaenda kwenye hekalu lenye alikuwa amechunguza siku yenye ilipita kisha midi. Leo hachunguze hekalu tu, lakini anafanya mambo fulani kama yale yenye alifanya miaka tatu mbele ya hapo, wakati wa Pasaka ya mwaka wa 30 wakati wetu. (Yohana 2:14-16) Wakati huu Yesu anafukuza “wale wenye walikuwa wanauzisha na kununua katika hekalu.” Tena, ‘anapindua meza za wale wenye walikuwa wanabadilisha feza na viti vya wale wenye walikuwa wanauzisha njiwa.’ (Marko 11:15) Haruhusu mutu hata mumoja kubeba vitu mahali pengine katika muji kwa kupitia katika hekalu.

      Sababu gani Yesu anatendea kwa ukali wale wenye kubadilisha feza na kuuzisha wanyama katika hekalu? Anasema hivi: “Je, haikuandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa ajili ya mataifa yote’? Lakini ninyi mumeifanya kuwa pango la wanyanganyi.” (Marko 11:17) Anaita wanaume hao kuwa wanyanganyi kwa sababu wanauzisha kwa bei ya juu sana wanyama wenye watu wanauza kwa ajili ya kutoa zabihu. Yesu anaona matendo hayo kuwa wizi, ao unyanganyi.

      Bila shaka, wakubwa wa makuhani, waandishi, na viongozi wa watu wanasikia yale yenye amefanya, wanaanza kutafuta namna ya kumuua. Lakini wanajikuta mbele ya tatizo fulani. Hawajue watafanya nini ili kumuua Yesu, kwa sababu watu wengi wanakuja ili kumusikiliza.

      Haiko Wayahudi wa asili tu ndio wamekuja kwenye Pasaka, kuko pia wageuzwa-imani, ni kusema, watu wenye walianza kufuata dini ya Wayahudi. Kati yao muko Wagiriki wenye wamekuja kuabudu kwenye sherehe hiyo. Wanamukaribia Filipo, pengine wanavutiwa na jina lake la Kigiriki, na wanaomba kumuona Yesu. Pengine Filipo haiko hakika kama jambo hilo linafaa, kwa hiyo anamuelezea Andrea. Wote wawili wanaenda kumuelezea Yesu. Inaonekana kama angali kwenye hekalu.

      Yesu anajua kama atakufa kisha siku kidogo, hii haiko wakati wa kupenda kutimiza tamaa ya watu ao kutafuta kujulikana na watu. Anajibu mitume wake wawili kwa kutumia mufano; anawaambia hivi: “Saa imekuja ili Mwana wa binadamu atukuzwe. Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, kama mbegu ya ngano haianguke kwenye udongo na kufa, inabakia mbegu moja tu; lakini kama inakufa, basi inazaa matunda mengi.”—Yohana 12:23, 24.

      Mbegu moja ya ngano inaweza kuonekana kuwa haina faida. Lakini kama inatiwa katika udongo na “kufa” inaweza kuota na kufikia kuzaa mbegu nyingi. Vilevile Yesu, mutu mukamilifu, kwa kubaki muaminifu kwa Mungu mupaka kufa, atakuwa njia ya kutolea uzima wa milele watu wengi wenye kuwa na roho kama hiyo ya kujitoa. Kwa hiyo, Yesu anasema: “Kila mutu mwenye anapenda sana uzima wake anauharibu, lakini kila mutu mwenye anachukia uzima wake katika ulimwengu huu ataulinda kwa ajili ya uzima wa milele.”—Yohana 12:25.

      Yesu hajifikirie tu yeye mwenyewe, kwa sababu anasema hivi: “Kama mutu yeyote anataka kunitumikia, basi anifuate, na kwenye niko, ni pale mutumishi wangu pia atakuwa. Kama mutu yeyote anataka kunitumikia, Baba atamuheshimia.” (Yohana 12:26) Ni baraka kabisa! Wale wenye wataheshimiwa na Baba yake watatawala pamoja naye katika Ufalme.

      Yesu anakumbuka mateso na maumivu ya kifo yenye atapata; anasema hivi: “Sasa ninavurugika sana, na niseme nini? Baba, uniokoe kutoka katika saa hii.” Lakini Yesu hapendi kuepuka kufanya mapenzi ya Mungu. Anaongeza hivi: “Hata hivyo, ndiyo sababu nimekuja kwenye saa hii.” (Yohana 12:27) Yesu iko tayari kutenda kulingana na makusudi ya Mungu, kutia ndani kifo chake cha zabihu.

      • Sababu gani Yesu anatazamia kupata matunda ya tini, hata kama kipindi cha matunda ya tini hakijafika?

      • Juu ya nini Yesu iko na sababu ya kuita wale wenye wanauzisha katika hekalu kuwa “wanyanganyi”?

      • Ni katika njia gani Yesu anaweza kulinganishwa na mbegu ya ngano, na anajisikia namna gani kuhusu mateso na kifo chenye kinamungojea?

  • Wayahudi Wanasikia Sauti ya Mungu—Wataonyesha Imani?
    Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
    • Yesu anasema: “Baba, tukuza jina lako,” na Wayahudi wenye kusimama hapo wanasikia sauti ya Mungu

      SURA YA 104

      Wayahudi Wanasikia Sauti Ya Mungu​—Wataonyesha Imani?

      YOHANA 12:28-50

      • WATU WENGI WANASIKIA SAUTI YA MUNGU

      • WATU WATAHUKUMIWA KWA MUSINGI GANI?

      Kwenye hekalu, Siku ya Kwanza, tarehe 10 Mwezi wa Nisani, Yesu anazungumuzia kifo chake chenye kukaribia. Akiwa na hangaiko kuhusu matokeo yenye jambo hilo litakuwa nayo juu ya jina la Mungu, anasema: “Baba, tukuza jina lako.” Sauti kubwa kutoka mbinguni inasikilika: “Nimelitukuza na nitalitukuza tena.”—Yohana 12:27, 28.

      Watu wenye kuwa hapo wanavurugika. Wamoja wanawaza kama wanasikia ngurumo. Wengine wanasema: “Malaika amesema naye.” (Yohana 12:29) Lakini, sauti hiyo yenye wanasikia ni ya Yehova! Na haiko mara ya kwanza watu wanasikia sauti ya Mungu tangu Yesu aanze kazi yake.

      Miaka tatu na nusu mbele ya hapo, wakati Yesu alibatizwa, Yohana Mubatizaji alisikia Mungu akisema juu ya Yesu hivi: “Huyu ni Mwana wangu, mupendwa, mwenye nimekubali.” Muda fulani kisha Pasaka ya mwaka wa 32 wakati wetu, Yesu aligeuzwa sura mbele ya Yakobo, Yohana na Petro. Wanaume hao watatu walisikia Mungu akisema: “Huyu ni Mwana wangu, mupendwa, mwenye nimekubali. Mumusikilize.” (Matayo 3:17; 17:5) Lakini sasa, kwa mara hii ya tatu, Yehova anasema katika njia yenye watu wengi wanasikia!

      Yesu anasema hivi: “Sauti hii haikutokea kwa ajili yangu, lakini imetokea kwa ajili yenu.” (Yohana 12:30) Hilo linahakikisha kabisa kama yeye ni Mwana wa Mungu, Masiya mwenye aliahidiwa.

      Zaidi ya hayo, maisha ya Yesu yanaonyesha namna wanadamu wanapaswa kuishi na yanahakikisha kwamba Shetani Ibilisi, mutawala wa ulimwengu huu, anastahili kufa. Yesu anasema hivi: “Sasa ulimwengu huu unahukumiwa; sasa mutawala wa ulimwengu huu atatupwa inje.” Kuliko kuwa alama ya kushindwa, kifo cha Yesu chenye kukaribia kitakuwa ushindi. Namna gani? Yesu anaeleza hivi: “Lakini mimi, kama ninainuliwa kutoka duniani, nitavuta kwangu watu wa namna zote.” (Yohana 12:31, 32) Kupitia kifo chake kwenye muti, Yesu atavuta wengine kwake, na kufungulia watu njia ya uzima wa milele.

      Kuhusu maelezo ya Yesu juu ya “kuinuliwa,” watu wanasema hivi: “Tulisikia katika Sheria kwamba Kristo anadumu milele. Namna gani unasema kwamba Mwana wa binadamu anapaswa kuinuliwa? Ule Mwana wa binadamu ni nani?” (Yohana 12:34) Ijapokuwa ushuhuda wote, kutia ndani kusikia sauti ya Mungu mwenyewe, wengi wao hawakubali kama Yesu ni Mwana wa kweli wa binadamu, Masiya mwenye aliahidiwa.

      Kama vile alifanya hapo mbele, Yesu anasema kama yeye ni “mwangaza.” (Yohana 8:12; 9:5) Anashauria watu hivi: “Mwangaza utaendelea kuwa kati yenu kwa wakati kidogo. Mutembee wakati mungali na mwangaza, ili giza lisiwapite nguvu. . . . Wakati muko na mwangaza, mukuwe na imani katika mwangaza, ili mukuwe wana wa mwangaza.” (Yohana 12:35, 36) Kisha Yesu anatoka pale, kwa sababu tarehe 10 Mwezi wa Nisani haiko siku yenye anapaswa kufa. Pasaka ya tarehe 14 Mwezi wa Nisani ndio wakati anapaswa “kuinuliwa,” ni kusema, kupigiliwa misumari kwenye muti.—Wagalatia 3:13.

      Kuanzia mwanzo wa utumishi wa Yesu, Wayahudi walishindwa kumuamini. Ni wazi kwamba hali hiyo ilitimiza unabii fulani. Isaya alitabiri kama macho ya watu yangepofushwa na mioyo yao ingekuwa migumu ili wasiponyeshwe. (Isaya 6:10; Yohana 12:40) Ndiyo, Wayahudi wengi walikataa kwa kiburi ushuhuda wa kwamba Yesu ni Mukombozi wao mwenye aliahidiwa, njia ya uzima.

      Nikodemo, Yosefu wa Arimatea, na watawala wengine wengi “walimuamini” Yesu. Je, watatenda kwa imani, ao hapana, kwa sababu wanaogopa wasifukuzwe katika sinagogi ao kwa sababu ‘wanapenda utukufu wa wanadamu’?—Yohana 12:42, 43.

      Yesu mwenyewe anaeleza maana ya kumuamini: “Kila mutu mwenye ananiamini, haniamini mimi tu lakini anamuamini pia Ule mwenye alinituma; na kila mutu mwenye ananiona mimi, anaona pia Ule mwenye alinituma.” Kweli zenye Mungu alimuambia Yesu afundishe na zenye Yesu anaendelea kutangaza ni za maana sana, hivi kwamba anaweza kusema: “Kila mutu mwenye ananizarau na hapokee maneno yangu iko na mwenye atamuhukumu. Neno lenye nimesema ndilo litamuhukumu katika siku ya mwisho.”—Yohana 12:44, 45, 48.

      Yesu anamalizia hivi: “Kwa maana sikusema kwa uamuzi wangu mwenyewe, lakini Baba mwenye alinituma, yeye mwenyewe amenipatia amri juu ya jambo la kusema na la kufundisha. Na ninajua kwamba amri yake inamaanisha uzima wa milele.” (Yohana 12:49, 50) Yesu anajua kama hivi karibuni atamwanga damu yake kuwa zabihu kwa ajili ya wanadamu wenye kumuamini.—Waroma 5:8, 9.

      • Ni katika matukio gani tatu yenye kumuhusu Yesu watu walisikia sauti ya Mungu?

      • Ni watawala gani walimuamini Yesu, lakini pengine, ni sababu gani walishindwa kufanya hivyo waziwazi?

      • “Siku ya mwisho” watu watahukumiwa kwa musingi gani?

Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili (Congo)
  • Tumia Wengine
  • Préférences
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Kanuni za Matumizi
  • Kanuni za Kutunza Siri
  • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
  • JW.ORG
  • Ingia
Tumia Wengine