Habari Fulani za Ulimwengu
Uswisi (Suisse)
Uchunguzi ambao ulifanywa katika inchi ya Uswisi unaonyesha kuwa kuna uwezekano mukubwa zaidi wa kwamba watu 14 juu ya mia moja ambao wana miaka zaidi ya 60 watakufa siku ya tarehe yao ya kuzaliwa kuliko siku zingine. Kwa ujumla, watu 18 juu ya mia moja wanakufa kwa sababu ya mushituko wa moyo siku ya tarehe yao ya kuzaliwa, kwa ukawaida wanawake 21 juu ya mia moja wanakufa kwa sababu ya ugonjwa wa kupooza, na kwa ukawaida wanaume 35 juu ya mia moja wanakufa kwa kujiua wao wenyewe. Wanasayansi wanawazia kwamba kuwa na wasiwasi mwingi kwa sababu ya mahangaiko ya maisha na pombe, ndiyo mambo ambayo yanafanya hesabu ya watu wanaojiua iongezeke na pia aksidenti. Hata hivyo, watu fulani wenye elimu wanapinga uchunguzi huo ambao ulifanywa huko Uswisi, na wanaamini kwamba hesabu hizo zilizotolewa kuhusu watu wanaokufa tarehe ya siku yao ya kuzaliwa ni zenye makosa.
Israeli
Wanaume wenye sura nzuri walikuwa na nafasi kubwa kuitwa ili kuulizwa maulizo ya kupata kazi wakati walibandika picha zao kwenye karatasi ya maelezo kuhusu elimu yao na kazi ambazo wamekwisha kufanya; wanawake wenye kuvutia walikuwa na nafasi ndogo za kuitwa. Sababu gani? Wachunguzi Waisraeli wanasema kwamba jambo hilo linaweza kuwa hivyo kwa sababu katika biro zinazohusika na kazi ya kuamua ni nani ambaye ataulizwa maulizo, kuna wanawake wengi zaidi kuliko wanaume. Gazeti fulani (The Economist) linasema kwamba “maelezo yasiyopendeza yanaonyesha kuwa wivu usiofaa unawafanya wanawake hao wafanyakazi wakatae maombi ya wanawake wenye sura nzuri ambao wanatafuta kazi.”
Amerika
Watu watatu wa chama cha wapinga-vita, mutawa mumoja mwanamuke aliye na miaka 82 pamoja na wenzake wawili, mumoja aliye na miaka 63 na mwengine aliye na miaka 57, walivunja hivi karibuni milango ya makao fulani huko Oak Ridge, Tennessee, ambamo mulikuwa toni 100 za vifaa vya nyukilia, na waliandika maneno ya kupinga vita kwenye nyumba moja kati ya nyumba hizo. Steven Chu, waziri wa mambo ya nyukilia, alieleza kwamba kukosekana kwa usalama mahali “panapowaziwa kuwa penye usalama zaidi ulimwenguni ni jambo lenye kusumbua sana.”
Australia
Mahakama kubwa zaidi katika taifa inaomba mashirika ya biashara ambayo yanatengeneza tumbaku yaondoe rangi mbalimbali na alama kwenye paketi za sigareti. Sasa, sigareti zote zinapaswa kuuzishwa zikiwa ndani ya paketi nyepesi za rangi ya kahawa isiyovutia ambazo zina picha zinazoonyesha hatari za kuvuta tumbaku.