Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • g 6/15 uku. 10-11
  • Galileo

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Galileo
  • Amuka!—2015
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • SAYANSI NA DINI
  • Habari Zilizo Ndani
    Amuka!—2015
Amuka!—2015
g 6/15 uku. 10-11
Galileo

MAMBO YENYE HISTORIA INATUFUNDISHA

Galileo

Kati ya mwaka wa 1301 na 1700, wanasayansi na wanafilozofia wa Ulaya walianza kuelewa ulimwengu kwa njia yenye ilipingana na mafundisho ya Kanisa Katoliki. Mwanaume mumoja mwenye alichunguza tena anga ni Galileo Galilei.

MBELE ya wakati wa Galileo, watu wengi waliamini kuwa jua, sayari, na nyota, vyote vilikuwa vinazunguka dunia. Imani hiyo ilikuwa kati ya mafundisho makubwa ya Kanisa Katoliki.

Lakini, kupitia teleskope yake, Galileo aliona mambo yenye yalipingana na mafundisho ya wanasayansi yenye yalikubaliwa na watu wengi. Kwa mufano, wakati aliona kama madoa yenye kuwa kwenye jua yalionekana kuwa hayakubakia mahali palepale, alitambua kama jua linajizunguka lenyewe. Mawazo kama hayo yalisaidia sana watu kujua ulimwengu, lakini pia yalifanya Kanisa Katoliki limupinge sana Galileo.

SAYANSI NA DINI

Galileo anatangaza waziwazi mambo alivumbua

Makumi ya miaka mbele ya hapo, Nicolas Copernic, mwanaume mumoja wa inchi ya Polandi (Pologne) mwenye elimu ya nyota alianzisha fundisho lenye kuonyesha kuwa dunia inazunguka jua. Galileo alijifunza maandishi ya Copernic juu ya mizunguko ya vitu vyenye kuwa katika anga, na alipata mambo yenye kuhakikisha fundisho la Copernic. Kwanza, Galileo alisita kutangaza waziwazi mambo yenye alikuwa amevumbua kwa sababu aliogopa kuwa watu watazarau mambo hayo na hawatayakubali. Galileo hakuweza kujizuia kusema mambo aliona kupitia teleskope, kwa sababu alipendezwa sana na mambo hayo. Kwa hiyo, alitangaza waziwazi mambo alivumbua. Wanasayansi fulani walipinga mawazo ya Galileo, na bila kukawia viongozi wa dini walianza kumuchambua katika kanisa.

Katika mwaka wa 1616, Kardinali Bellarmine, “mwanateolojia mukubwa wa wakati huo,” alimujulisha Galileo sheria mupya yenye Kanisa Katoliki lilitoa ili kupinga mafundisho ya Copernic. Alimuomba Galileo atii sheria hiyo, na kwa miaka mingi kisha hapo, Galileo hakupinga tena waziwazi kuwa dunia haizunguke jua.

Katika mwaka wa 1623, Papa Urbain wa 8, rafiki ya Galileo, akaanza kutawala. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1624, Galileo alimuomba papa aondoe sheria iliyotolewa mwaka wa 1616. Papa hakuondoa sheria hiyo, lakini alimuomba Galileo afasirie mafundisho yenye kupingana ya Copernic na Aristote bila kuunga mukono upande wowote.

Kisha, Galileo aliandika kitabu chenye kuzungumuzia maajabu ya ulimwengu (Dialogue on the Great World Systems). Hata ikiwa papa alimuomba asiunge mukono upande wowote, kitabu hicho kilionekana kuwa kilipendelea mawazo ya Copernic. Bila kukawia, maadui wa Galileo walisema kuwa kitabu chake kilimuzarau papa. Kwa sababu Galileo aliteswa na alishitakiwa kuwa muasi-imani, alilazimika kukataa mafundisho ya Copernic. Katika mwaka wa 1633, Tribinali ya Roma ya Kuwahukumu Waasi wa Dini ilimuhukumia kifungo cha nyumbani maisha yake yote, na ilikataza maandishi yake. Tarehe 8 Mwezi wa 1, 1642 Galileo alikufa nyumbani kwake katika kijiji chenye kuitwa Arcetri, karibu na muji wa Florence.

Papa Jean-Paul wa 2 alionyesha kuwa Kanisa Katoliki lilimuhukumu Galileo bila sababu

Kwa miaka mingi, maandishi fulani ya Galileo yalitiwa kati ya vitabu vyenye Wakatoliki walikatazwa kusoma. Lakini katika mwaka wa 1979, Kanisa Katoliki lilichunguza tena uamuzi wenye Tribinali ya Roma ya Kuwahukumu Waasi wa Dini ilikamata miaka 300 mbele ya hapo. Mwishowe, katika mwaka wa 1992, Papa Jean-Paul wa 2 alionyesha kuwa Kanisa Katoliki lilimuhukumu Galileo bila sababu.

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

  • Galileo Galilei alizaliwa katika mwaka wa 1564 huko Pisa, Italia, muji wenye kujulikana kwa sababu ya munara wake wenye kuegemea upande mumoja. Alifundisha kwenye Masomo ya Juu ya Padua na kisha aliishi na kutumika katika muji wa Florence.

  • Galileo hakuunda teleskope, lakini aliongeza uwezo wake wa kunenepesha vitu na aliifanya ikuwe yenye faida zaidi.

  • Kwa sababu ya mambo yenye alivumbua juu ya ulimwengu, Galileo alifikishwa mara mbili mbele ya Tribinali ya Roma ya Kuwahukumu Waasi wa Dini. Tribinali hiyo ya Kanisa Katoliki ilikuwa inatoa malipizi kwa watu wenye hawakufuata mafundisho ya dini hiyo.

Tribinali ya Kuhukumu Waasi wa Dini Ilimutesa Galileo?

Wanahistoria fulani wanasema kuwa inawezekana Tribinali ya Roma ya Kuhukumu Waasi wa Dini ilimutesa Galileo kimwili. Hukumu yenye ilitolewa juu ya Galileo inaonyesha kama, ilikuwa lazima apitishwe katika “uchunguzi mukali,” ili kujua nia yake ilikuwa nini kabisa. Katika usemi wenye ulitumiwa na tribinali hiyo, mara nyingi maneno hayo yalimaanisha “mateso.” Inawezekana “mateso” hayo yalikuwa “kumuogopesha mutu kwa maneno kuwa atatendewa vibaya kimwili.”

Watu wenye elimu wanaonyesha kama mateso yalikuwa na vipindi mbalimbali na yalikuwa na ukali tofauti-tofauti. Mateso hayo yangeweza kuwa kumuonyesha mutu vyombo vyenye kutumiwa kutesa watu, kumuvua nguo, ao kumufunga, ao hata kumutesa vikali kimwili. Haijajulikana ikiwa “uchunguzi mukali” wenye Galileo alifanyiwa ulikuwa wa namna gani.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine