Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • Dunia hii Itaokoka ao Hapana?
    Amuka!—2017 | No. 6
    • Saa ya Mwisho wa Dunia

      HABARI KUBWA | DUNIA HII ITAOKOKA AO HAPANA?

      Dunia Hii Itaokoka Ao Hapana?

      MWAKA wa 2017 ulianza na tangazo la mubaya la wanasayansi. Katika Mwezi wa 1, kikundi kimoja cha wanasayansi kilitangaza kwamba dunia inakaribia sana musiba mubaya zaidi wenye haujatokeaka. Kwa kutumia Saa ya Mwisho wa Dunia ili kuonyesha namna dunia inakaribia mwisho, wanasayansi walipeleka mbele, kwa segonde 30, mukuki wa kuonyesha dakika. Kwa sasa, Saa ya Mwisho wa Dunia iko kwenye saa 6 ya usiku kosa dakika mbili na nusu (23:57:30), ni kusema, karibu zaidi na musiba wa ulimwengu muzima kuliko wakati wowote katika kipindi cha miaka 60!

      Katika mwaka wa 2018, wanasayansi wanapanga kupima tena kadiri gani tuko karibu na mwisho wa dunia. Saa ya Mwisho wa Dunia itaendelea kuonyesha kwamba musiba mukubwa kuliko yote unakaribia sana? Unawaza namna gani? Dunia hii itaokoka? Pengine unaona kwamba iko nguvu kupata majibu ya maulizo haya. Hata wanasayansi wako na mawazo tofauti kuhusu jambo hilo. Haiko kila mutu ndiye anaamini hatari hiyo yenye haiwezi kuepukwa.

      Kwa kweli, mamilioni ya watu wanatumainia wakati muzuri wenye kuja. Wanaamini kwamba wako na mambo yenye kuhakikisha kwamba wanadamu na dunia wataokoka milele na maisha yetu yatakuwa muzuri. Unaweza kuamini mambo hayo? Dunia hii itaokoka ao hapana?

      “Saa ya Mwisho wa Dunia ni saa ya mufano yenye kukubaliwa katika dunia yote yenye inaonyesha namna ulimwengu wetu unakaribia kuharibiwa kupitia teknolojia hatari zenye sisi wenyewe tunafanya. Hatari ya kwanza na kubwa kati ya teknolojia hizo ni silaha za kinyuklia, lakini hatari hizo zinatia ndani teknolojia zenye kutokeza kubadilika kwa hali ya hewa, kuongezeka kwa bioteknolojia, na teknolojia ya Internete yenye inaweza kutokeza hatari kubwa sana katika namna yetu ya kuishi na kwa dunia, ikuwe kimakusudi, kwa kukosea, ao kwa aksidenti.”​—Bulletin of the Atomic Scientists.

  • Kutafuta Majibu
    Amuka!—2017 | No. 6
    • HABARI KUBWA | DUNIA HII ITAOKOKA?

      Kutafuta Majibu

      KAMA unahangaika ao kuogopa sana kwa sababu ya habari nyingi za mubaya zenye unasikia, ujue kwamba hauko peke yako. Katika mwaka wa 2014, Barack Obama, mwenye wakati huo alikuwa raisi wa Amerika, alisema kwamba kwa sababu ya mambo ya mubaya yenye kuonyeshwa katika vyombo vya habari, watu wengi wanasema “kwamba dunia inazunguka kwa mwendo mukubwa sana na hakuna mutu mwenye anaweza kuizuia.”

      Lakini, kisha tu kusema maneno hayo, alisema kwa shauku kuhusu mipango yenye inakamatwa sasa ili kumaliza matatizo ya dunia. Alisema kwamba mipango ya serikali fulani ni “habari njema” na alisema pia kwamba alikuwa na “tumaini kabisa” na mwenye “kutazamia kabisa mambo ya muzuri.” Katika maneno mengine, alisema kwamba mambo yenye watu wanajikaza kufanya wakiwa na nia nzuri yanaweza kupunguza matatizo na kuzuia musiba wa ulimwengu wote.

      Watu wengi wanatazamia mambo ya muzuri kama yeye. Kwa mufano, watu fulani wanatia tumaini lao katika sayansi, wakitabiri kwamba maendeleo ya haraka katika teknolojia yanatoa ahadi ya kumaliza magumu ya ulimwengu. Mutu mumoja wa elimu katika vifaa vya kielektroniki na teknolojia mupya alitabiri akiwa na tumaini kwamba katika mwaka wa 2030, “teknolojia yetu itakuwa na uwezo mukubwa zaidi mara elfu moja, na katika mwaka wa 2045, itakuwa na uwezo mukubwa zaidi mara milioni moja.” Aliongeza hivi: “Tunafanya maendeleo kabisa. Hata kama magumu yanaendelea kuwa mubaya zaidi kuliko zamani, tuko na uwezo wa kumaliza magumu mbele yatokee.”

      Kwa kweli, hali za dunia ziko mubaya kiasi gani? Tunakaribia kabisa musiba mukubwa wa dunia? Hata kama wanasayansi na viongozi fulani wa inchi wanatoa ujumbe wenye tumaini, watu wengi wanaendelea kuwa na wasiwasi kuhusu wakati wenye kuja. Sababu gani?

      Mulipuko wa kinyuklia

      SILAHA ZA UHARIBIFU MUKUBWA. Hata kama Umoja wa Mataifa na mashirika mengine yamejikaza sana, yameshindwa kumaliza ao kupunguza silaha za kinyuklia. Tofauti na hilo, viongozi wenye kiburi wanazarau sheria kuhusu matumizi ya silaha. Inchi zenye tangu zamani zimekuwa na silaha za kinyuklia, zinajikaza sana ili kufanya mabomu zao za zamani zikuwe muzuri zaidi, na zinatengeneza zingine za mupya zenye kuua zaidi. Inchi zenye zamani hazikuwa na uwezo wa kufanya uharibifu mukubwa, ziko sasa na uwezo wa kuharibu hesabu kubwa ya watu.

      Kwa kuwa mataifa yako tayari zaidi kuliko zamani kuingia katika vita vya kinyuklia, hilo linafanya dunia ikuwe eneo hatari, hata katika vipindi vya “amani.” Gazeti Bulletin of the Atomic Scientists inaonya kwamba “mifumo ya silaha roboti hatari zenye kujiongoza zenyewe, na kuuwa bila kuongozwa na mutu, kwa mufano, zinaweza kuwa zenye kuogopesha katika njia ya pekee.”

      Mwanaume fulani analala kwenye kitanda ndani ya hospitali

      AFYA YETU IKO KATIKA HATARI. Sayansi iko na mipaka juu ya mambo yenye inaweza kufanya ili afya yetu ikuwe muzuri. Tatizo la damu kutembea haraka katika mwili, kunenepa kupita kiasi, kuchafuliwa kwa hewa, matumizi mabaya ya dawa za kulewesha vinaongezeka sana. Mambo yote hayo yanaweza kutokeza magonjwa. Watu wengi wako wanakufa kwa sababu ya hesabu kubwa ya magonjwa yenye hayaambukize, kama vile kansere, magonjwa ya moyo, na magonjwa ya sukari (diabète). Hesabu ya watu wenye wanakuwa wazaifu kwa sababu ya magonjwa mengine, kutia ndani magonjwa ya akili, inaendelea kuongezeka. Katika miaka ya hivi karibuni, tumejionea sisi wenyewe hali fulani zenye hazikuwaziwa kama vile magonjwa hatari ya virusi vya Ebola na virusi vya Zika. Kwa kifupi: Ni vigumu kwa wanadamu kuzuia magonjwa, na inaonekana kama hakuna tumaini lolote la kumaliza magonjwa!

      Kuharibika kwa mazingira kunachafua hewa na maji

      WANADAMU WANAHARIBU MAZINGIRA. Izine mbalimbali zinaendelea kuharibu anga-hewa ya dunia. Mamilioni ya watu wanakufa kila mwaka kwa sababu ya kupumua hewa yenye kuharibika.

      Mashirika za kipekee, za mataifa, na za serikali zinaendelea kumwanga katika bahari maji machafu, uchafu wa dawa na wa mashamba, plastiki, na vitu vingine vyenye kuchafua mazingira. Kitabu Encyclopedia of Marine Science kinasema hivi: “Uchafu huo wenye sumu unaambukiza wanyama na mimea ya bahari, na pia wanadamu wenye kuvikula.”

      Na tumeanza kukosa maji safi. Robin McKie, mwanasayansi Mwingereza, iko na haki ya kusema hivi: “Dunia iko na matatizo ya maji yenye itagusa kila sehemu.” Viongozi wa inchi wanakubali kwamba tatizo la kupata maji ni tatizo lenye kutokezwa na wanadamu na linaleta hatari kubwa sana.

      Upepo mukubwa

      NGUVU ZA ASILI ZINASHAMBULIA WANADAMU. Upepo mukubwa, kimbunga, na matetemeko ya dunia vinaleta mafuriko makubwa sana, kuporomoka kwa udongo, na maharibifu mengine. Leo kuliko zamani, watu wengi wanakufa ao wanaguswa mubaya sana na nguvu hizo za asili. Uchunguzi mumoja wenye ulitolewa na shirika la NASA ulionyesha hatari kubwa zaidi ya kutokea kwa “upepo mukubwa zaidi, joto kali sana, na muzunguko wa ukame na mafuriko.” Nguvu za asili zitafutilia mbali wanadamu?

      Bila shaka, unawazia mambo mengine yenye yanaweza kutia uzima wetu katika hatari. Lakini, hautapata majibu yenye kufurahisha kuhusu wakati wenye kuja kwa kuchunguza mambo yote ya mubaya yenye kufanyika leo. Wengine wanaweza kusema hivyo pia kuhusu mambo yenye viongozi wa inchi na wanasayansi wanasema. Lakini, kama vile ilionyeshwa katika habari yenye kutangulia, watu wengi wamepata majibu ya kweli kuhusu hali za ulimwengu na wakati wenye kuja. Majibu ya maulizo hayo yanaweza kupatikana wapi?

  • Biblia Inasema Nini?
    Amuka!—2017 | No. 6
    • Mwanaume mumoja katika dunia mupya yenye Mungu aliahidi

      Mambo yenye Saa ya Mwisho wa Dunia inatabiri hayatatimia kwa sababu Mungu anaahidi wakati wenye kuja wenye furaha kwa ajili ya wanadamu na dunia

      HABARI KUBWA | DUNIA HII ITAOKOKA?

      Biblia Inasema Nini?

      HALI ya mubaya yenye kuwa katika dunia ilitabiriwa na Biblia kumepita miaka mingi. Zaidi ya hilo, Biblia ilitabiri pia wakati wenye kuja wenye furaha kwa ajili ya wanadamu. Hatupaswe kukataa mara moja mambo yenye Biblia inasema, kwa sababu mambo yenye ilitabiri yanatimia hata katika mambo madogo-madogo.

      Kwa mufano, fikiria unabii mbalimbali wa Biblia wenye kufuata:

      • “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine.”​—Mathayo 24:7.

      • ‘Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushugulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumupenda Mungu.’​—2 Timotheo 3:1-4.

      Unabii huo unaonyesha hali ya dunia hivi kwamba watu fulani wanaweza kusema kwamba dunia inaendelea kuwa mubaya zaidi kwa njia yenye haiwezi kuzuiwa. Kwa njia fulani, wanadamu hawawezi tena kuongoza ulimwengu wetu. Kulingana na Biblia, wanadamu hawana hekima na uwezo wa kumaliza magumu hayo kwa njia yenye kudumu. Jambo hilo linaonyeshwa katika maandiko yenye kufuata:

      • “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.”​—Methali 14:12.

      • ‘Mwanadamu amemutawala mwanadamu kwa kumuumiza.’​—Mhubiri 8:9.

      • “Mwanadamu . . . hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”​—Yeremia 10:23.

      Kama wanadamu wanaendelea kufanya mambo yenye wanataka, dunia inaweza kabisa kupata musiba mukubwa. Lakini, hilo halitatokea! Sababu gani? Biblia inasema hivi:

      • Mungu ‘ameiwekea dunia musingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mupaka wakati usio na kipimo, au milele.’​—Zaburi 104:5.

      • ‘Kizazi kinaenda, kizazi kinakuja; lakini dunia inasimama mupaka wakati usio na kipimo.’​—Mhubiri 1:4.

      • “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”​—Zaburi 37:29.

      • “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”​—Zaburi 72:16.

      Mafundisho hayo ya Biblia yanaleta majibu yenye kuwa wazi. Wanadamu wote hawatakufa kwa sababu ya kuchafuliwa kwa mazingira, kukosekana kwa chakula ao maji, ao kwa sababu ya magonjwa yenye yataenea katika dunia yote. Dunia haitaangamizwa katika uharibifu mukubwa wa kinyuklia. Sababu gani? Wakati wenye kuja wa dunia yetu uko katika mikono ya Mungu. Ni kweli kwamba Mungu ameruhusu wanadamu watumie uhuru wao wa kuchagua. Lakini watavuna matokeo ya maamuzi yao. (Wagalatia 6:7) Dunia haiko kama treni yenye imeharibika katika mwendo, yenye haiwezi tena kuongozwa, na yenye kungojea tu musiba. Mungu ameweka mipaka kuhusu kiasi cha magumu yenye wanadamu wanaweza kujiletea.​—Zaburi 83:18; Waebrania 4:13.

      Lakini Mungu atafanya zaidi ya hilo. Ataleta “wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Mambo mazuri yenye kuonyeshwa katika habari hii ni mambo madogo tu kati ya mambo mengi yenye mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wamejifunza kupitia funzo la Biblia.

      Mashahidi wa Yehova wenye kuwa katika dunia yote ni wanaume na wanawake wa miaka yote na wenye walikomaa katika hali mbalimbali za maisha. Wanaabudu Mungu mumoja wa kweli ambaye jina lake ni Yehova, kama vile Biblia inaonyesha. Hawaogope wakati wenye kuja kwa sababu Biblia inasema: ‘Yehova, Muumba wa mbingu, Yeye Mungu wa kweli, Mufanyizaji wa dunia na Mutengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.’​—Isaya 45:18.

      Habari hii imezungumuzia mafundisho fulani ya Biblia kuhusu wakati wenye kuja wa dunia na wa wanadamu. Ili kupata habari zaidi, ona somo la 5 la broshua Habari Njema Inayotoka Kwa Mungu! yenye kuchapishwa na Mashahidi wa Yehova na yenye kupatikana kwenye www.jw.org

      Unaweza pia kuangalia video Sababu Gani Mungu Aliumba Dunia? yenye kupatikana kwenye www.jw.org. (Fungua kichwa VICHAPO > VIDEO)

Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili (Congo)
  • Tumia Wengine
  • Préférences
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Kanuni za Matumizi
  • Kanuni za Kutunza Siri
  • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
  • JW.ORG
  • Ingia
Tumia Wengine