1 Timotheo
Ya Kwanza kwa Timotheo
1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu kwa amri ya Mungu Mwokozi wetu na ya Kristo Yesu, aliye tumaini letu, 2 kwa Timotheo, mtoto halisi katika imani:
Na kuwe fadhili isiyostahiliwa, rehema, amani kutoka kwa Mungu Baba na Kristo Yesu Bwana wetu.
3 Kama vile nilivyokutia moyo kukaa Efeso nilipokuwa karibu kushika njia yangu kwenda kuingia Makedonia, ndivyo nafanya sasa, ili upate kuwaamuru watu fulani kutofundisha fundisho tofauti, 4 wala kukazia uangalifu hadithi zisizo za kweli na nasaba, ambazo hazifanikiwi, lakini ambazo hutokeza maswali ya utafiti badala ya usimamizi wa kugawiwa kitu chochote na Mungu kuhusiana na imani. 5 Kwa kweli lengo la amri hii ni upendo kutokana na moyo safi na kutokana na dhamiri njema na kutokana na imani bila unafiki. 6 Kwa kukengeuka kutoka kwa mambo hayo watu fulani wamegeuzwa kando kuingia katika maongezi ya kipuuzi, 7 wakitaka kuwa walimu wa sheria, lakini wakiwa hawafahamu ama mambo wanayosema ama mambo ambayo wanasisitiza kwa nguvu juu yayo.
8 Basi twajua kwamba Sheria ni bora mradi mtu aitumia kisheria 9 katika ujuzi wa jambo hili, kwamba sheria hutangazwa hadharani, si kwa ajili ya mtu mwadilifu, bali kwa ajili ya watu wenye kuasi sheria na wasiotawalika, wasiomwogopa Mungu na watenda-dhambi, wenye kukosa fadhili-upendo, na wachafuaji, wauaji-kimakusudi wa akina baba na wauaji-kimakusudi wa akina mama, waua-binadamu kikatili, 10 waasherati, wanaume walalao na wa kiume, wateka-watu, waongo, waapaji wasio wa kweli, na jambo jingine lolote lile lililo katika upinzani na fundisho lenye afya 11 kulingana na habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha, ambayo mimi nilikabidhiwa.
12 Mimi ni mwenye shukrani kwa Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenipa nguvu, kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu kwa kunigawia huduma, 13 ijapokuwa hapo zamani nilikuwa mkufuru na mnyanyasaji na mtu fidhuli. Hata hivyo, nilionyeshwa rehema, kwa sababu nilikuwa asiye na ujuzi na nilitenda kwa ukosefu wa imani. 14 Lakini fadhili isiyostahiliwa ya Bwana wetu ikazidi sana pamoja na imani na upendo ambao ni kwa kuhusiana na Kristo Yesu. 15 Wa uaminifu na wenye kustahili ukubalifu kamili ni usemi wa kwamba Kristo Yesu alikuja katika ulimwengu ili kuokoa watenda-dhambi. Kati ya hao mimi ni wa kwanza kabisa. 16 Hata hivyo, sababu kwa nini nilionyeshwa rehema ilikuwa ili kwa njia ya mimi nikiwa kisa cha kwanza kabisa Kristo Yesu apate kuonyesha wote ustahimilivu wake wote kuwa mfano wa wale watakaoweka imani yao juu yake kwa ajili ya uhai udumuo milele.
17 Sasa kwa Mfalme wa umilele, asiyefisidika, asiyeonekana, Mungu pekee, kuwe heshima na utukufu milele na milele. Ameni.
18 Amri hii nakukabidhi wewe, mtoto, Timotheo, kwa kupatana na matabiri yaliyoongoza moja kwa moja hadi kwako, ili kwa hayo upate kuendelea kufanya shughuli ya vita bora; 19 ukishika imani na dhamiri njema, ambayo wengine wameisukuma kando na wamevunjikiwa imani kama vile kuvunjikiwa meli. 20 Himenayo na Aleksanda ni wa hao, nami nimewakabidhi kwa Shetani ili wapate kufundishwa kwa nidhamu kutokufuru.