“Madaktari Wafikiria Upya Utiaji-Damu Mishipani”
“Programu Iliyokusudiwa Kusaidia Mashahidi wa Yehova Ina Manufaa kwa Kila Mtu”
Chini ya vichwa hivyo vya habari katika gazeti Rocky Mountain News, mwandikaji wa habari ya kitiba Kris Newcomer aripoti hivi: “Zaidi ya madaktari 100 wa Denver wameungana pamoja wahudumie kanisa la Mashahidi wa Yehova, ambalo huiona damu kuwa kitu kitakatifu kisichopasa kutolewa kuwa upaji au kutiwa mishipani wakati wa upasuaji na taratibu nyingine za kitiba.” Dakt. Greg Van Stiegmann wa Programu ya Upasuaji na Tiba Isiyotumia Damu kwenye Hospitali ya Chuo Kikuu katika Denver, Colorado, United States, alisema hivi: “Lililotukia ni [kwamba] tumepanga pamoja watu wa kitivo walio na nia ya kupanga upya njia watumiayo kufanya mambo.”
Van Stiegmann alisema kwamba ingawa programu hiyo itawahudumia Mashahidi wa Yehova, si wao pekee yao wanaokataa damu. Kuna idadi inayokua ya watu ambao wangekuwa afadhali zaidi kama hawangepokea damu. “Sisi hujaribu sana kadiri iwezekanavyo tusimtie damu mishipani mtu yeyote. . . . Kuna habari bora sana zinazotokana uchunguzi mwingi zidokezazo [kwamba] jaribio lako la kwanza la kusahihisha tatizo la kiafya la kansa ni afadhali zaidi ikiwa hujapata kutiwa damu mishipani ama kabla ama baada ya upasuaji wako,” akasema Van Stiegmann.
Makala hiyo iliendelea hivi: “Badiliko katika maoni ya tiba ya ki-siku-hizi ni habari njema kwa Mashahidi wa Yehova wanaokadiriwa kuwa 10,000 katika Colorado. Kitabu cha Agano la Kale cha Mwanzo kina fungu hili la maneno: ‘Nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile,’ ambalo kwa Mashahidi humaanisha hakuna damu ipaswayo kuingizwa ndani ya mwili kwa njia yoyote, kutia na utiaji-damu mishipani.”