Je! Katekisimu Mpya Itabadili Mambo?
Na mleta habari za Amkeni! katika Italia
“KATEKISIMU ya Mwaka 2000,” “Orodha ya Dhambi Mpya,” “Sura Mpya ya Kanisa”—hivi ni vichwa vya karibuni katika magazeti ya Italia juu ya hali mpya ya Catechism of the Catholic Church, kwa sasa imechapishwa katika Kifaransa, Kijerumani, Kiitaliano, na Kihispania. Katika Italia mauzo ya katekisimu yalipanda hadi nakala 110,000 katika majuma yanayopungua matatu. Bila shaka, katika nchi ya Kikatoliki yenye watu karibu milioni 58, hesabu hiyo si ya juu mno. Mwandikaji mmoja Mwitalia alisema kwamba yeyote anayeinunua ili “kutafuta tu orodha ya dhambi mpya” atapatwa na “mtamauko.”
Katika Desemba 7, 1992, Papa John Paul wa 2 alitoa rasmi kitabu chenye kurasa 450 ambacho alikiita “muhtasari wa imani ya Kikatoliki na maadili.” Ilikuwa imechukua zaidi ya miaka sita kukipiga mswada tena na tena, kutia ndani uchambuzi mwingi kutoka ulimwengu wa Katoliki, ili kutokeza buku hili. Hakuna budi kwamba, kinaeneza fumbo la Jumuiya ya Wakristo la “ule Utatu Mtakatifu Zaidi . . . , fumbo kuu la dini hiyo.” Pia kinasema kwamba “kila nafsi ya kiroho imeumbwa moja kwa moja na Mungu . . . , na haiwezi kufa.” (Linganisha 1 Wakorintho 15:28; Mathayo 24:36; ona pia Ezekieli 18:4, 20.) Lakini kwa nini katekisimu mpya ilifikiriwa kuwa ya lazima?
Mwanachuo mmoja Mkatoliki aliandika: “Katekisimu nyingi zinazochapishwa na vitovu vya dayosisi vya katekisimu ni za kijuu-juu sana, zilizojaa kanuni zenye makosa na zenye kupita kiasi.” Hata hivyo, hizo zimetumiwa kwa miaka mingi kuwafundisha Wakatoliki waaminifu. Kichapo cha Kikatoliki La Civiltà Cattolica kilisema kwamba kitabu hicho kipya kilipaswa kitoe “msaada wa maana katika kuhakikisha umoja wa imani,” ambao umetikiswa katika miongo ya miaka ya karibuni. Papa mwenyewe alisema: “Si rahisi kuona maendeleo ambayo katekisimu hii italeta. Hata hivyo, . . . kinaweza kuwa kifaa chenye thamani, chenye matokeo kwa ajili ya ujuzi wa kina kirefu na kufanywa upya kiroho na kimaadili ambako ni kwa asilia.”
Je! kweli itakuwa hivyo? Je! katekisimu hii itarudisha umoja kwa Wakatoliki? Migawanyiko hii imekuwa hasa dhahiri sana katika njia ambayo Wakatoliki ulimwenguni pote wanaitikia masuala kama vile utoaji-mimba, njia za upangaji uzazi, theolojia ya ukombozi, na kushiriki katika vile vinavyoitwa vita vya haki (hata kama vinatokeza Wakatoliki kuua Wakatoliki). Katika vyeo vya juu zaidi, maoni yanayotofautiana na mgawanyiko yamekuwa yakiendelea kati ya kikundi chenye nguvu sana kiitwacho Opus Dei, kikiungwa mkono na papa na washirika wengi mashuhuri wenye vyeo, na Wayesuiti, ambao kwa sasa hawapendelewi na papa.
Je! katekisimu hiyo itabadili mioyo na mwenendo wa maelfu ya viongozi wa Kiitalia wa kisiasa na wa kibiashara ambao hivi karibuni wamejiingiza katika ufisadi na mambo ya aibu? Hati hii itaathiri kwa kadiri gani mwenendo wa wenye mamlaka wa Italia? Ikishindwa kubadili maadili ya jamii yenye kutawala, kwa nini Mkatoliki wa kawaida abadilike? Kwa kuwa buku hilo lina kurasa 450—na kusoma si jambo linalopendwa na watu wengi—je, tutazamie badiliko lenye kudumu juu ya tabia?