Biblia Huonyeshaje Maana ya Familia Katika Kutaniko la Kikristo?
KATIKA kutaniko la Kikristo familia hutambuliwa kuwa kiungo cha msingi cha jamii ya Kikristo. Nafasi kubwa imetolewa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo juu ya maagizo ya uhusiano wa familia. Tena mwanamume apewa heshima ya ukichwa wa familia, huku mke akiwa katika ujitiisho kwa mume wake, akisimamia nyumba chini ya uangalizi wa jumla wa mume. (1 Wakorintho 11:3; 1 Timotheo 2:11-15; 5:14) Akifananisha Yesu na mume na kichwa cha familia juu ya ‘mke’ wake aliye kutaniko, Paulo awashauri waume kwa upole watumie ukichwa kwa upendo, naye awashauri wake wawastahi waume zao na kujinyenyekeza kwao. (Waefeso 5:21-33) Watoto waamriwa watii wazazi wao, na akina baba hasa wamekabidhiwa daraka la kulea watoto katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.—Waefeso 6:1-4.
Mwanamume atumiwaye kama mwangalizi katika kutaniko la Kikristo, ikiwa ameoa, ni lazima aonyeshe viwango vya juu akiwa kichwa cha familia, akisimamia kwa njia ifaayo na kuweka watoto wake katika ujitiisho, hawa wakiwa si watukutu wala wenye kushtakiwa ufasiki, kwa maana, Paulo auliza hivi: “Mtu asiyejua kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje Kanisa [“kutaniko,” NW] la Mungu?” kwa kuwa kutaniko ni kama familia. (1 Timotheo 3:2-5; Tito 1:6) Wake wahimizwa wawapende waume na watoto wao, wawe wafanya-kazi nyumbani, na kujitiisha kwa waume zao wenyewe.—Tito 2:4, 5.
Yesu alitabiri kwamba upinzani kwa kweli ya Mungu ungezigawanya familia. (Mathayo 10:32-37; Luka 12:51-53) Lakini mtume Paulo aliwashauri waamini kwa upole thabiti dhidi ya kuvunja uhusiano wa ndoa, akisihi kwa msingi wa hali-njema ya mwenzi asiyeamini na pia ya watoto. Alikazia thamani kubwa ya uhusiano wa familia alipoonyesha wazi kwamba Mungu huwaona watoto wachanga kuwa watakatifu, hata ingawa mwenzi asiyeamini hajasafishwa kutoka dhambi zake kwa imani katika Kristo. Kwa kweli, huenda huyo asiyeamini akawa anazoea baadhi ya mambo ambayo Paulo asema Wakristo fulani walikuwa wamezoea kabla ya kukubali ile habari njema juu ya Kristo. (1 Wakorintho 7:10-16; 6:9-11) Pia mtume alinda muungamano wa familia ya Kikristo kwa kuwapa maagizo waume na wake kuhusu kutoleana haki za ndoa.—1 Wakorintho 7:3-5.
Ushirika katika mahusiano ya familia ulithibitika kuwa baraka kwa wengi kuhusu Ukristo, “kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo?” (1 Wakorintho 7:16) Hili lathibitishwa pia na yaliyomo katika salamu za mtume Paulo kwa nyumba kadhaa. Waamini fulani walipendelewa kutumia kao la familia kama mahali pa kutaniko kukutania. (Warumi 16:1-15) Filipo mishonari Mkristo alikuwa mwanamume wa familia, akiwa na binti waaminifu wanne Wakristo. Alibarikiwa kwa kuweza kukaribisha mtume Paulo na wafanya-kazi wenzake kwa muda fulani katika nyumba yake katika Kaisaria. (Matendo 21:8-10) Kutaniko la Kikristo lenyewe latajwa kuwa “nyumba ya Mungu.” Mshirika wayo mkuu na kichwa ni Yesu Kristo, na “nyumba” hii humtambua kuwa ndiye Mbegu ambayo kwayo familia zote za dunia zitajibariki.—1 Timotheo 3:15; Waefeso 2:19; Wakolosai 1:17, 18; Mwanzo 22:18; 28:14.
Maandiko yaliyopuliziwa yametabiri shambulio kali juu ya kianzilisho cha familia kukiwa na matokeo ya kuvunja maadili na jamii ya kibinadamu nje ya kutaniko la Kikristo. Paulo huainisha lile fundisho la ‘kuwazuia watu wasioe’ miongoni mwa mafundisho yaliyopuliziwa na roho waovu katika “nyakati za mwisho.” Yeye atabiri kwamba “siku za mwisho” hali ya kutotii wazazi, kukosa uaminifu-mshikamanifu, na watu ‘kutopenda wa kwao’ ingeenea sana, hata miongoni mwa wale “wenye mfano wa utauwa.” Awaonya Wakristo wajiepushe na watu kama hao.—1 Timotheo 4:1-3; 2 Timotheo 3:1-5, linganisha NW.
Babiloni Mkubwa, adui ya “mwanamke” wa Mungu (Mwanzo 3:15; Wagalatia 4:27) na ya “bibi-arusi” wa Kristo (Ufunuo 21:9), ni tengenezo kubwa “kahaba,” linalofanya uasherati na wafalme wa dunia. Kuwa ‘mama wa makahaba na machukizo ya nchi’ kwaonyesha kwamba “binti” zake ni makahaba, pia kwamba yeye husababisha kupuuzwa kwa kadiri kubwa kwa vianzilisho na amri za Yehova Mungu, kutia na matakwa yake yachangiayo uaminifu-maadili wa familia. (Ufunuo 17:1-6) Yeye amefanya jitihada za kuvuta wengine kwenye ukahaba na amefaulu kutokeza binti wengi ‘makahaba,’ huku majaribio yakifanywa ya kuzuia Kristo asiwe na “bibi-arusi” safi. Hata hivyo, “bibi-arusi” wake hutokea akiwa mwenye ushindi, aliye safi, mwadilifu, astahiliye kuwa katika “familia” ya Yehova akiwa ‘mke’ wa Yesu Kristo, kwa baraka na shangilio la ulimwengu wote mzima.—2 Wakorintho 11:2, 3; Ufunuo 19:2, 6-8.