Machinjo Matika Port Arthur—Kwa Nini Yalitokea?
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA AUSTRALIA
JUMAPILI alasiri, Aprili 28, 1996, halihewa ilikuwa yenye kupendeza katika Port Arthur Historical Site, ambapo ni mahali papendwapo na watalii katika Tasmania, Australia. Mkahawa uitwao Broad Arrow Café ulijaa watu waliokuwa wakila chakula cha mchana. Karibu saa 7:30 mchana, kijana mmoja mwenye nywele nyeupe ya kimanjano aliye na umri wa miaka 28 ambaye alikuwa ametoka tu kumaliza kula katika ua wa nje wa mkahawa huo akaingia ndani ya jengo na kuanza kufyatua risasi.
Wateja wakafa kwenye viti vyao, vyakula vikiwa vingali vinywani mwao. Polisi walisema hayo yalikuwa “kama mauaji katika uwanja wa vita.” Mtu huyo mwenye bunduki alipofikiri kwamba wote wamekufa—alikuwa ameua 20—akatoka nje kwa utulivu. Kwa sekunde chache, alikuwa ameua kimakusudi watu wengi zaidi kuliko watu waliopata kuuawa kimakusudi katika miaka minne iliyopita katika kisiwa-jimbo kizima cha Tasmania!
Lakini, mtu huyo akaendelea kuua watu kiholela, mmoja baada ya mwingine. Kwa mfano, alipokuwa akielekea kwenye malango ya mahali hapo pa kihistoria, alimwona Nanett Mikac akiwa na binti zake wachanga. Akamwua Nanett na binti yake mwenye umri wa miaka mitatu. Kisha, yule mwenye umri wa miaka sita alipojaribu kutoroka, alimnyemelea alipojificha nyuma ya mti akampiga risasi akafa.
Baadaye, katika mahali pa kutoza kodi kwenye malango ya kuondoka mahali hapo pa kihistoria, mtu huyo akaua watu watatu waliokuwa katika gari aina ya BMW na kuchukua gari lao. Kisha, mbele kidogo, akakutana na mwanamume na mwanamke katika gari jingine. Mwuaji huyo akamlazimisha mtu huyo aingie katika buti ya ile BMW na kuua mwanamke ambaye alikuwa ameandamana na mtu huyo. Kisha akaendesha gari kwa umbali mfupi akafika hoteli ya kulala ya Seascape Cottage—akifika karibu saa 8:00 alasiri. Hapo, akachoma ile BMW na kuwashika mateka yule mtu aliyekuwa amemweka katika buti na wale wenzi wa ndoa wazee-wazee ambao ni wenye hiyo hoteli. Alikuwa ameua watu 12 tangu aondoke kwenye ule mkahawa, na kufanya watu waliokuwa wameuawa kufikia 32. Wengine wengi walikuwa wamejeruhiwa.
Mahubiri ya Jumapili Alasiri
Kwa wakati uo huo, Jenny Ziegler na familia yake, ambao ni washiriki wa Kutaniko la Port Arthur la Mashahidi wa Yehova, walikutana saa 7:30 mchana kwa matayarisho ya kushiriki katika huduma. Kisha familia hiyo ikaelekea Port Arthur Historical Site. Jenny alitaka kumzuru David Martin mwenye urafiki ambaye ni mwenye ile hoteli ya kulala ya Seascape Cottage. Mapema, Jenny pamoja na dada mwingine Mkristo walikuwa wamefurahia mazungumzo ya Biblia pamoja na mtu huyo.
Muda mfupi baada ya saa 8:00 alasiri, Jenny, mume wake, na watoto wao walipokaribia ile hoteli, waliona moshi ukitoka kwenye gari lililokuwa likichomeka kwenye ua. Polisi waliwasimamisha na kuwaambia warudi walikotoka. “Mambo yalionekana kuwa mabaya,” Jenny akasema. “Barabara zilionekana kuwa bila watu isivyo kawaida.”
Hata hivyo, wakiwa wangali hawajui yaliyotokea, familia hiyo ikaondoka kwenye barabara kuu na kuelekea ufuo mdogo ili waendelee na utendaji wao wa kuhubiri waliokuwa wamepanga. Huko, hali ilionekana kuwa kawaida: Watoto walikuwa wakiogelea, watu walikuwa wakitembea-tembea kwenye mwisho mwingine wa ufuo, na wenzi wa ndoa wazee-wazee walikuwa wameketi ndani ya gari lao wakisoma. “Mume wangu akawaendea, na mazungumzo mazuri yakafuata,” Jenny akasema. “Akawaambia kwamba inaonekana kuna tatizo katika barabara kuu na akawadokezea watumie njia nyingine wanapoondoka kwenye ufuo. Nikazungumza kifupi na kijana mmoja, na muda mfupi baadaye tukaondoka.”
Akina Ziegler waliendelea kufuata barabara ielekeayo Port Arthur Historical Site. “Hapo, palikuwa na magari kadhaa,” Jenny akaeleza, “yakiziba malango ya kuingia mahali hapo. Baadaye tuligundua kwamba yalizuia miili ya watu waliokuwa wamepigwa risasi ili isionekane. Mtu mmoja akatuambia: ‘Kuna mtu mwenye bunduki ambaye amerukwa akili; labda watu 15 wamekufa!’ Tukashauriwa tuondoke mara hiyo.”
Mwisho Wenye Kuogofya wa Kisa Hicho
Masaibu hayo hayakuwa yamekwisha kamwe, kama alivyosema Jenny: “Kwenda nyumbani kuliogofya sana kwa sababu hatukujua mtu huyo alikuwa wapi. Kila wakati tulipokutana na gari jingine barabarani, tulijiuliza kama yumo ndani. Hata tulipofika nyumbani salama, hatukuhisi usalama, kwa kuwa tuliishi mahali penye upweke ambapo mtu anayejua eneo hilo angeweza kujificha kwa urahisi. Kwa kuwa ndugu na dada zetu wa Kikristo walijua mahali tulipoenda alasiri hiyo, mara moja tukaanza kupokea simu za kuhakikisha kwamba tulikuwa salama.
“Tulipokuwa tukifikiria kile ambacho kilikuwa kimetendeka, tulitambua kwamba kama tungalifika kwenye ile hoteli ya kulala dakika chache tu mapema, tungalikuwa miongoni mwa wale waliouawa. Tuliogopa sana tulipofikiria kwamba huenda hata muuaji huyo alikuwa ametulenga kwa bunduki tulipokuwa tukizungumza na polisi hapo!”
Hatimaye zaidi ya polisi 200 wakaizingira hoteli hiyo usiku huo wa Jumapili, wakienda chini-chini ili kuepuka risasi za mara kwa mara za huyo mtu. Yaonekana alidai apewe helikopta ya kutorokea, lakini usiku huo majadiliano hayakufaulu. Karibu saa 2:00 ya asubuhi ya Jumatatu, moshi ulionekana ukitoka kwenye nyumba hiyo. Mtu huyo akapona, ingawa alikuwa amechomeka. Wale mateka watatu, kutia ndani mwenye hoteli ambaye akina Ziegler walikuwa wamejaribu kumzuru, baadaye walipatikana wamekufa katika mabaki ya nyumba hiyo iliyochomeka, ikifanya waliokufa kufikia 35.
Kwa Nini Yalitokea?
Karibu majuma saba yaliyotangulia, mnamo Machi 13, mtu mmoja mwenye bunduki katika Dunblane, Scotland, alikuwa ameingia katika jumba la kufanya mazoezi ya mwili la shule na kuua kwa risasi watoto wadogo 16 pamoja na mwalimu wao. Kwa kupatana na usemi mmoja wa kale wa televisheni, “kama kuna umwagikaji wa damu, hiyo ni habari kubwa,” hilo likawa habari za kimataifa. Wastadi fulani wa tabia walidokeza kwamba mtu huyo wa Australia huenda alikuwa akijaribu kuua watu wengi zaidi kuliko wale waliouawa kimakusudi katika Dunblane. Na katika Marekani, yule aliyeitwa muuaji wa Zodiac, ambaye alihofisha New York City kwa miaka mingi, alisema kwamba yeye alikuwa amejaribu kuua watu wengi zaidi kuliko wauaji wengine wote ambao alikuwa amesoma juu yao.
Jambo jingine ambalo wengi husema huchangia mauaji mengi ni ngono na ujeuri unaoonyeshwa katika sinema na vidio. Gazeti la Australia Herald Sun liliripoti hivi: “Jumla ya vidio 2000 zenye jeuri na ponografia zilikuwa zimechukuliwa kutoka nyumba ya yule aliyesemekana kuwa muuaji mkubwa wa kimakusudi wa Port Arthur, Martin Bryant. . . . Vidio hizo zilipatikana wakati ambapo uangalifu ulikuwa unaelekezwa kwenye fungu la sinema zenye jeuri katika machinjo hayo ya Port Arthur.” Vivyo hivyo, Daily News la New York liliripoti kwamba “masanduku mawili ya vidio za kiponografia yalikuwa kwenye kitanda” cha mtu aliyeungama kuwa yule muuaji wa Zodiac.
Machinjo ya Port Arthur yalipojulikana, vituo fulani vya televisheni mara moja vilibadili programu zao zilizokuwa zimepangwa. Baadaye, mwandikaji wa magazeti Penelope Layland aliandika makala “Unafiki wa Televisheni juu ya Jeuri na Huzuni” na kutaja kwamba: “Kwa njia fulani, kutoonyesha vipindi hivyo vyenye jeuri ni kama lile ombolezo la dakika moja tu. Kesho, juma lijalo, mwezi ujao, hali itakuwa kawaida.”
Hata hivyo, ili kupata ufahamu wa ndani kwa jambo linalofanya ujeuri uenee sana sasa, twahitaji kuendea Biblia. Zamani za kale ilitabiri kwamba “siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema.” (2 Timotheo 3:1-5) Hivyo, ongezeko la leo la ujeuri laongezea tu uthibitisho wa kwamba tunaishi katika siku za mwisho na kwamba mwisho wa huu mfumo wa mambo umekaribia.—Mathayo 24:3-14.
Kama ambavyo huenda wengi wameshuku, roho waovu—ambao hawaonekani—wamehusika katika mweneo huu mkubwa wa mwenendo mkatili usio wa asili ya kibinadamu. (Waefeso 6:12) Baada ya kufafanua kuondoshwa kwa Shetani Ibilisi na roho wake waovu kutoka mbinguni, Biblia yasema: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:7-9, 12) Tumo katika kipindi hicho cha ole sasa hivi, na Shetani na roho wake waovu wanatumia njia yoyote ile wawezavyo ili kuhimiza wanadamu wazidi kutenda maovu.
Lakini, karibuni Shetani, roho wake waovu, na ulimwengu wao mwovu hawatakuwapo, na utawala wa Ufalme wa Mungu utaleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10; 2 Petro 3:13; 1 Yohana 2:17; Ufunuo 21:3, 4) Jenny alisema: “Kwa wakati huu, sisi ‘tunalia pamoja na waliao,’ lakini ni tamaa yetu kushiriki tumaini letu la Ufalme pamoja na wale katika jumuiya ambao wameshtuliwa sana na msiba huu.”—Warumi 12:15.
[Picha katika ukurasa wa 17]
The Broad Arrow Café, ambako machinjo yalianza
[Habari kuhusu chanzo cha ramani katika ukurasa wa 16]
Mountain High Maps® Copyright © 1995 Digital Wisdom, Inc.