Maumivu ya Kuwaacha Waende
“Mume wangu alikuwa amenionya siku ambayo mtoto wetu wa kwanza alizaliwa—‘Kulea watoto, mpenzi, ni utaratibu mrefu wa kuwaacha waende.’”—Ourselves and Our Children—A Book by and for Parents.
WAZAZI wengi wanafurahi—hata wanasisimka—mtoto wao wa kwanza anapozaliwa. Yajapokuwa magumu yote, mabishano, maumivu, kukatishwa tamaa, na mahangaiko yaletwayo na uzazi, watoto waweza kuwa chanzo cha shangwe kubwa. Kama miaka elfu tatu hivi iliyopita, Biblia ilijulisha wazi hivi: “Watoto ni zawadi kutoka kwa BWANA; wao ni baraka kwelikweli.”—Zaburi 127:3, Today’s English Version.
Hata hivyo, Biblia hutoa utabiri huu wenye kufanya mtu afikiri: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Kwa sababu tofauti-tofauti watoto walio watu wazima kwa kawaida huondoka nyumbani—kuendeleza masomo au kazi-maisha, kupanua huduma yao ya Kikristo, kuoa au kuolewa. Lakini kwa wazazi fulani, uhalisi huu ni wenye kuumiza sana. Wanaruhusu kushindania uhuru kwa watoto wao kwa asili kuwafanye—kama mwandikaji moja alivyosema—“wahisi kutukanwa, kutendwa kwa njia mbaya, kuaibishwa, kutishwa au kukataliwa.” Hii kwa kawaida huongoza kwenye zogo na uvutano wa kifamilia usiokwisha. Kukataa kuikabili siku ambayo watoto wao wataondoka nyumbani, wazazi fulani hukosa kuwatayarisha kwa ajili ya utu mzima. Matokeo ya kupuuza kama huko yaweza kuwa yenye kuogofya: kwaweza kutokeza watu wazima ambao hawako tayari kusimamia nyumba, kutunza familia, au hata kupata na kubaki katika kazi ya kuajiriwa.
Maumivu ya kutengana yaweza kuwa mabaya zaidi katika familia za mzazi aliye pekee. Mmoja aliye mzazi pekee aitwaye Karen asema: “Binti yangu nami tuna ukaribu sana; tumesitawisha muungano halisi wa urafiki. Kila nilikokwenda, nilienda naye.” Uhusiano wa karibu kati ya mzazi na mtoto ni wa kawaida katika nyumba zenye mzazi aliye pekee. Kwa kueleweka, wazo la kupoteza ukaribu huo laweza kuwa lenye kuangamiza kabisa.
Hata hivyo, kitabu Traits of a Healthy Family chawakumbusha wazazi hivi: “Hili ndilo lahusika katika maisha ya familia: kumtunza mtoto mchanga mwenye kuwategemea kabisa hadi awapo mtu mzima anayejitegemea.” Kisha chaonya: “Matatizo mengi katika familia hutokea kwa sababu wazazi hawawaachi watoto waende.”
Namna gani wewe? Je, wewe ni mzazi? Ikiwa ndivyo, je, umejitayarisha kwa ajili ya siku ambayo utawaacha watoto wako waende? Na namna gani watoto wako? Je, unawatayarisha ili waweze kujitegemea?