Abadoni
KWENYE Ufunuo 9:11 neno hili la Kiebrania limetoholewa katika maandishi ya Kiswahili. Hapo twasoma kuhusu lile pigo la ufananisho la nzige kwamba wana “mfalme juu yao, yule malaika wa abiso. Katika Kiebrania jina lake ni Abadoni, lakini katika Kigiriki ana jina Apolioni.”
Katika Kiebrania neno ʼavad·dohnʹ lamaanisha “uharibifu” na pia laweza kurejezea “mahali pa uharibifu.” Laonekana katika maandishi ya awali ya Kiebrania mara tano kwa jumla, na katika sehemu nne latumiwa kufananisha “mahali pa maziko,” “Sheoli,” na “kifo.” (Zaburi 88:11; Ayubu 26:6; 28:22; Mithali 15:11) Neno ʼavad·dohnʹ katika maandishi hayo hurejezea kwa wazi zile hatua mbalimbali za uharibifu zinazoanza na kifo cha kibinadamu, na maandiko haya yaonyesha kwamba kuoza au uharibifu hufanyika Sheoli, kaburi la ujumla la wanadamu. Kwenye Ayubu 31:12 ʼavad·dohnʹ hudokeza matokeo yenye kudhuru ya mwenendo wa uzinzi. Ayubu alitangaza hivi: “Kwa kuwa [mwenendo wa uzinzi] ni moto uteketezao hata Uharibifu [ʽadh-ʼavad·dohnʹ], nao ungeyang’oa maongeo yangu yote.”—Linganisha Mithali 6:26-28, 32; 7:26, 27.
Jina la Kigiriki lililotumiwa na mtume Yohana kutafsiri jina “Abadoni” la Kiebrania kwenye Ufunuo 9:11 ni Apolioni. Jina Apolioni lamaanisha “Mharabu,” nalo ndilo jina alilopewa “malaika wa abiso.” Ingawa vitabu vingi vya marejezo hutumia jina hilo kurejezea mtu fulani mwovu au kani fulani ovu, mastakimu yote ya hilo ono la kiapokalipsi ni kinyume cha marejezo hayo, kwa kuwa hurejezea tena na tena malaika wanaotumiwa na Mungu kuleta ole juu ya adui za Mungu.
Matumizi ya kitenzi kinachohusiana na jina hilo, a·polʹly·mi, yatolea kielezi jambo hilo, kama vile kwenye andiko la Yakobo 4:12, lisemalo hivi juu ya Mungu: “Mmoja yuko ambaye ni mpaji-sheria na hakimu, yeye awezaye kuokoa na kuangamiza.” (Linganisha Mathayo 10:28.) Roho isiyo safi ambayo Yesu alitoa ndani ya mtu katika sinagogi huko Kapernaumu ilimkiri Yesu kuwa wakili wa Mungu na kusema hivi: “Tuna jambo gani nawe, Yesu wewe Mnazareti? Je, ulikuja kutuangamiza sisi?” (Marko 1:24; Luka 4:34) Yesu aliwaonya wapinzani wasiotubu miongoni mwa wasikilizaji wake juu ya hatari ya kuangamizwa. (Luka 13:3-5; 20:16) Maandiko haya na mengine humwonyesha Kristo Yesu aliyetukuzwa kuwa yule arejezewaye kwa jina hilo la cheo.—Linganisha Ufunuo 19:11-16; Luka 8:31.
Abadoni, Malaika wa Abiso—Yeye Ni Nani?
Hata hivyo, kwenye Ufunuo 9:11, neno “Abadoni” latumiwa kuwa jina la “yule malaika wa abiso.” Jina la Kigiriki Apolioni linalolingana nalo lamaanisha “Mharabu.” Katika karne iliyopita kulikuwa na jitihada zilizofanywa ili kuonyesha kwamba maandishi hayo yalihusu kiunabii watu mmoja-mmoja kama vile Maliki Vespasiani, Muhamadi, na hata Napoleoni, naye malaika huyo alionwa kwa ujumla kuwa “wa kishetani.” Hata hivyo, lazima itambuliwe kwamba kwenye Ufunuo 20:1-3 malaika aliye na “ufunguo wa abiso” anaonyeshwa kuwa mwakilishi wa Mungu kutoka mbinguni, na badala ya kuwa “wa kishetani,” yeye anamfunga na kumtupa Shetani ndani ya abiso. Ikitoa maelezo juu ya Ufunuo 9:11, The Interpreter’s Bible yasema hivi: “Hata hivyo, Abadoni si malaika wa Shetani bali wa Mungu, akifanya kazi yake ya kuharibu kwa amri ya Mungu.”
Katika maandiko ya Kiebrania yaliyotoka kuchunguzwa, ni wazi kwamba ʼavad·dohnʹ linafananishwa na Sheoli na kifo. Kwenye Ufunuo 1:18 twakuta Kristo Yesu akitaarifu hivi: “Mimi niko hai milele na milele, nami nina funguo za kifo na za Hadesi.” Nguvu zake kuhusiana na abiso zaonyeshwa kwenye Luka 8:31. Jambo la kwamba ana nguvu za kuharibu, kutia na nguvu za kuharibu dhidi ya Shetani, laonekana kutoka Waebrania 2:14, ambalo lasema kwamba Yesu alishiriki damu na mwili ili “kupitia kifo chake apate kumfanya kuwa si kitu yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi.” Kwenye Ufunuo 19:11-16 anaonyeshwa waziwazi kuwa Mharabu au Mfishaji aliyewekwa rasmi wa Mungu.