Maoni ya Biblia
Je, Yehova Alikuwa Mungu wa Kikabila?
KATIKA nchi nyingi leo, jina Yehova huhusianishwa na tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, jina hilo linapatikana pia katika tafsiri fulani za Biblia zinazotumiwa na dini nyinginezo mbali na Mashahidi wa Yehova. Kwelikweli, jina Yehova kama linavyowakilishwa na Tetragramatoni, limetumiwa kwa maelfu ya miaka.
Nyakati nyingine, Yehova huitwa “Mungu wa Israeli.” (1 Mambo ya Nyakati 17:24) Usemi huo umefanya wengine waamini kuwa alikuwa mungu wa kikabila tu ambaye Waebrania walibuni au kuiga kutoka kwenye utamaduni mwingine. Karen Armstrong, mwandishi wa kitabu kinachoitwa A History of God, adai hivi, ‘Hapo mwanzoni [Yehova] alikuwa mungu mjeuri wa kikabila aliyewapendelea Waisraeli. Baadaye, katika karne ya saba na ya sita K.W.K., manabii wa Israeli . . . , walimfanya huyo Mungu wa kikabila kuwa mtu wa kiroho ambaye mwanzo wake haujulikani wala yeye hajulikani.’
Baadhi ya wanahistoria wa kidini wamedokeza kwamba jina Yehova lilianzia Kanaani au Misri. Wengine husisitiza kwamba ni “jina la kale la kikabila” na halirejezei yule Mungu anayefafanuliwa katika “Agano Jipya.” Je, ni kweli? Usomaji makini wa Biblia unafunua nini?
Yehova—Mungu wa Watu Wote
Biblia huonyesha uhusiano wa karibu uliokuwepo kati ya Yehova na taifa la Israeli. Lakini hiyo si sababu ya kumwona kuwa mungu wa kikabila tu. Paulo, yule mtume Mkristo aliuliza hivi: “Je, yeye ndiye Mungu wa Wayahudi tu? Je, yeye si wa watu wa mataifa pia?” Paulo alijibuje waziwazi? “Ndiyo, wa watu wa mataifa pia.” (Waroma 3:29) Paulo alirejezea Mungu yupi? Katika barua hiyo kwa Waroma, jina Yehova lapatikana mara 19. Akimnukuu nabii Mwebrania wa kale Yoeli, mtume asema kwamba “kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa” wala si Wayahudi tu.—Waroma 10:13; Yoeli 2:32.
Si Waisraeli waliomchagua Yehova kuwa Mungu wao. Badala yake, Yehova ndiye aliyewachagua kutimiza kusudi lake la kumtayarishia Mesiya njia. Zaidi ya hayo, wakati ujao wa mungu wa kikabila hutegemea yanayowapata waabudu wake. Kabila linaposhindwa, mungu wa kabila hilo huwa ameshindwa. Katu haijawa hivyo kwa habari ya Yehova.
Karne nyingi kabla ya Ukristo, Yehova aliwaahidi watu wa mataifa yote baraka kupitia agano alilofanya pamoja na Abrahamu. Jambo hilo lilionyesha kwamba Mungu anapendezwa na wanadamu wote. (Mwanzo 12:1-3; Matendo 10:34, 35; 11:18) Mfalme Mwisraeli Daudi, alionyesha kwamba Yehova hakumiliki nchi ya Israeli tu aliposema hivi: “Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya BWANA, dunia na wote wakaao ndani yake.”—Zaburi 24:1.
Baadaye, Solomoni mwana wa Daudi alipokuwa akiliweka wakfu hekalu kwa ajili ya ibada ya Yehova, alionyesha kuwa kuna njia ambayo watu wanyenyekevu wa taifa lolote wangeweza kumfikia Yehova. Alipokuwa akitoa sala ya kuliweka wakfu hekalu, Solomoni alisema: “Hata na mgeni naye, asiyekuwa mmoja wa watu wako Israeli, atakapokuja kutoka nchi iliyo mbali sana . . . na kuomba kuielekea nyumba hii; basi, usikie huko mbinguni, makao yako, ukatende kwa kadiri ya yote atakayokuomba mgeni huyo; ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako, na kukucha wewe kama watu wako Israeli.”—1 Wafalme 8:41-43.
Israeli Lakataliwa
Profesa C. J. Labuschagne aliandika hivi kuhusu uhusiano wa Israeli pamoja na Yehova: “Katika historia yote ya taifa la Israeli, yule Mungu wa ‘taifa’ angetenda tena na tena bila ya kupendelea taifa hilo na hata dhidi ya taifa hilo.” Israeli lilipomkataa Mesiya katika karne ya kwanza, Yehova alilikataa taifa hilo.
Hata hivyo, jina la Yehova lingeendelea kutumiwa na Wakristo. Kutaniko la Kikristo lilipoendelea kukua, watu wa mataifa yote walijiunga nalo. Akiongoza kusanyiko la Kikristo huko Yerusalemu, yule mwanafunzi Myahudi Yakobo alisema jinsi Mungu “alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa [wasio-Wayahudi] ili achukue kutoka kwayo watu kwa ajili ya jina lake.” Kisha Yakobo akanukuu unabii fulani katika kitabu cha Amosi unaolitaja jina la Yehova, ili kuthibitisha kwamba hilo lilikuwa limetabiriwa.—Matendo 15:2, 12-18; Amosi 9:11, 12.
Huwajali Wote, Huwabariki Wote
Akithibitisha hata zaidi kwamba Yehova ni Mungu wa watu wote, Paulo aliandika hivi: “Hakuna tofauti yoyote kati ya Myahudi na Mgiriki, kwa maana kuna Bwana yuleyule juu ya wote, aliye tajiri kwa wote wale wanaomwita.” (Waroma 10:12) Naam, wanadamu wote watiifu wanaweza kubarikiwa na Yehova.
Haidhuru taifa au jamii yao, Yehova awaahidi watoto wake wote waaminifu na watiifu wakati ujao mtukufu. Neno lake lafafanua watu wa aina hiyo kuwa “vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote.” (Hagai 2:7) Watu hawa hupata kumjua Yehova na kumpenda. Kitabu cha mwisho cha Biblia husema hivi kuwahusu: “Mataifa yote yatakuja na kuabudu mbele yako [Yehova], kwa sababu maagizo yako ya uadilifu yamefanywa kuwa dhahiri.”—Ufunuo 15:4.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Musa akiwa na zile Amri Kumi