Kwa Nini Sisherehekei Halloween
MWAKA jana, majirani wake walipokuwa na shughuli nyingi za maandalio ya Halloween, ambayo katika nchi fulani ni sherehe ya kila mwaka yenye uhusiano mwingi na roho waovu, Michael kijana mwenye miaka 14 anayeishi Kanada alikuwa na shughuli tofauti. Michael alisema hivi katika insha aliyoandika kwa ajili ya shule yao:
‘Usiku wa leo ni mkesha wa Halloween. Ninapotazama nje dirishani, ninaona nyanja za majirani wetu zikiwa zimepambwa na mawe ya makaburi na viunzi vya mifupa huku taa zikiwa zimening’inizwa kwenye madirisha yao.a Wazazi wanarekebisha mavazi ya watoto wao; watoto nao wanawazia jinsi watakavyopewa peremende nyingi kesho.
‘Familia yetu ni tofauti. Uwanja wetu haujapambwa, nayo madirisha yetu hayajaning’iniziwa taa. Watu huniuliza kwa nini sisherehekei Halloween. Mashahidi wa Yehova hawaisherehekei hasa kwa sababu ya asili yake.b
‘Inashangaza kwamba ninayapenda majira ya Halloween. Huenda ukauliza, “Kwa nini?” Kwa sababu majira hayo hunifanya nitafakari. Hunifanya nifikirie sababu zilizonifanya niamue kutofanya mambo fulani. Kila mtu anapaswa kujichunguzia mwenyewe ikiwa ni muhimu kufikiria asili ya sherehe fulani. Ninafikiri ni muhimu kufikiria asili ya jambo. Kwa mfano, watu wengi wangeudhika ikiwa majirani wao wangevaa nguo kama za Wanazi. Kwa nini? Kwa sababu ya asili ya nguo hizo na kinachowakilishwa nazo, yaani, mambo yanayowaudhi wengi. Mambo yanayowakilishwa na ibilisi, roho waovu, na wachawi yananiudhi, nami sitaki kuhusianishwa nayo. Inafaa kufikiria mambo tunayochagua kufanya na sababu zinazofanya tuyachague, na pia kuhakikisha kwamba uamuzi wetu unategemea kanuni wala si maoni ya wengi. Hiyo ndiyo sababu inayonifanya nipende majira haya ya mwaka. Ninajivunia kuwa tofauti na kushikamana na mambo ninayoamini.’
[Maelezo ya Chini]
a Taa hizo huundwa kwa maboga yaliyokatwa, yakaondolewa sehemu yake ya ndani na kutiwa alama kama za uso wenye pua, mdomo, na macho. Mshumaa au chanzo kingine cha nuru hutiwa ndani ya maboga hayo.
b Ili upate habari zaidi, ona Amkeni! la Oktoba 8, 2001, ukurasa wa 5-10.