Kuutazama Ulimwengu
“Asilimia 60 ya watu ulimwenguni sasa wana simu za mkononi . . . Hilo ni badiliko kubwa tangu miaka sita iliyopita wakati chini ya asilimia 15 walikuwa na simu za mkononi.”—MACLEAN’S, KANADA.
Katika muda wa miaka kumi iliyopita, spishi mpya 1,068 zimegunduliwa katika eneo la Mekong huko Kusini-Mashariki mwa Asia.—HAZINA YA WANYAMAPORI ULIMWENGUNI, MAREKANI.
“Nchi ya Marekani ina asilimia 5 ya idadi ya watu ulimwenguni lakini ina asilimia 25 ya wafungwa wote ulimwenguni. Kati ya wakazi 100,000, watu 756 ni wafungwa, idadi ambayo ni zaidi ya mara tano ya wastani wa nchi nyingine zote.”—THE ECONOMIST, UINGEREZA.
“Kukengeushwa Sana Fikira”
Mifumo fulani ya mawasiliano inaweza kumzuia mtu asikazie fikira mambo mengine. Wataalamu ambao huchunguza jinsi mashini zinavyowasaidia wanadamu kuwasiliana na kuwakumbusha mambo—kama vile ujumbe wa haraka, vikumbusho vya kalenda ya kompyuta, barua-pepe, na habari zinazojitokeza kwenye kompyuta—wanasema kwamba watu wanaotumia programu kama hizo wanapata tatizo la “kukengeushwa sana fikira na hawawezi kukazia jambo moja fikira kwa kuendelea.” Matokeo ya kukatizwa-katizwa mara nyingi ni kwamba “unaweza kukosa kukazia fikira wazo lolote kwa muda mrefu na unaweza kushindwa kabisa kuanza na kumaliza kazi yoyote unayofanya bila kukengeushwa,” linasema gazeti Newsweek. Zaidi ya hilo, kukengeushwa kwa njia hiyo kunaweza kumfanya mtu awe na tatizo la “kupoteza kumbukumbu” na “kutokumbuka mambo kwa usahihi” kutia ndani kufanya makosa yanayoweza kusababisha madhara.
Watafsiri Wanahitajika
Mara nyingi mahakama, polisi, hospitali, na watu wengine wanaotoa huduma nchini Marekani wanahitaji kusaidiwa kuwasiliana na watu mbalimbali. Kama vile shirika la habari la Reuters lilivyosema, mashirika yanayowaajiri watafsiri yanashughulikia uhitaji wa kuwasiliana “katika ulimwengu wenye lugha nyingi tofauti-tofauti.” Kampuni moja huko California imewaajiri watafsiri 5,200 wanaozungumza lugha 176—kuanzia zile zinazojulikana sana kama vile, Kichina, Kihispania, Kirusi, na vilevile zile zisizojulikana sana kama vile lugha za sehemu fulani za Afrika na Mexico. Kwa muda usiozidi dakika moja, kampuni kama hizo zinaweza “kutambua ni lugha gani mtu anazungumza” na kumuunganisha mtafsiri kwenye simu awasaidie wanaohusika “kuzungumza,” inasema ripoti hiyo.
Dhahabu Kutoka Chanzo Kisichotarajiwa
Katika Wilaya ya Nagano, kaskazini-magharibi mwa Tokyo, “maji-taka yamegunduliwa kuwa chanzo kipya cha madini yenye thamani,” linasema shirika la habari la Reuters likiripoti kutoka Japani. Uchunguzi ulionyesha kwamba jivu lililookotwa baada ya kuchomwa kwa masalio ya maji-taka yanapochujwa kwenye mtambo wa kusafishia maji hayo huko Suwa, lilikuwa na dhahabu nyingi sana kuliko ile inayokusanywa katika migodi yenye dhahabu nyingi zaidi nchini Japani. Wilaya ya Nagano inatazamia kupata yen milioni 15, yaani, zaidi ya dola 167,000, kwa ajili ya dhahabu hiyo katika mwaka mmoja tu. Inafikiriwa kwamba dhahabu hiyo nyingi katika maji-taka “inatokana na viwanda vingi katika eneo hilo vinavyotengeneza vifaa kwa kutumia dhahabu,” inasema ripoti hiyo.