Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • fu kur. 3-32
  • Wakati Ujao Salama—Jinsi Unavyoweza Kuuona

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakati Ujao Salama—Jinsi Unavyoweza Kuuona
  • Wakati Ujao Salama—Jinsi Unavyoweza Kuuona
  • Vichwa vidogo
  • Mahali Msaada wa Kweli Waweza Kupatikana
  • Sababu Kukosa Usalama Kunaharibu Uhai wa Kibinadamu
  • Mipango Inayowezesha Kuwe Wakati Ujao Salama
  • Usalama Unaoweza Kufurahiwa Sasa
  • Unaloweza Kufanya
Wakati Ujao Salama—Jinsi Unavyoweza Kuuona
fu kur. 3-32

Wakati Ujao Salama—Jinsi Unavyoweza Kuuona

1. Ni usalama wa namna gani ambao wewe mwenyewe na wapendwa wako mngetaka?

WATU wa namna zote wanatamani sana usalama. Bila shaka huo ndio wewe na wapendwa wako mnataka. Watu wengi wanataka zaidi kuliko ahadi tu ya hali bora zitakazotokea wakati fulani ujao, usiojulikana. Kuna matatizo ya haraka ya maisha yanayotuelekea sasa hivi. Linalotakiwa ni jambo fulani linalotoa usalama wa kweli sasa na litakaloendelea kufanya hivyo katika miaka itakayokuja. Je! usalama huo wawezekana?

2. (a) Biblia yasema nini juu ya usalama, katika Isaya 32:17, 18,? (b) Je! hali hizo zakuvutia?

2 Kuna watu wa mataifa yote, wanaoishi katika sehemu zote za dunia, wanaosadiki kwamba wawezekana. Usalama unaowapendeza ulisimuliwa zamani na nabii aliyeongozwa na Mungu aliyeandika hivi: “Kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima. Na watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.” (Isaya 32:17, 18)a Mamia ya maelfu ya watu katika sehemu zote za dunia wamekwisha kuanza kufurahia usalama wenye amani ijapokuwa msukosuko uliopo wa ulimwengu, nao wana sababu ya kutazamia wakati ujao wenye tumaini zuri hata zaidi. Wewe pia unaweza kushiriki pamoja nao faida hizo.

3. Je! kuna jambo jingine lo lote ambalo Biblia inaahidi kwamba litatokeza usalama kwa mwanadamu? (Ufunuo 21:4, 5)

3 Watu hawa wanautazamia wakati ujao, ulio karibu sana sasa, wakati ‘hakutakuwako na mtu wa kuwatia watu hofu’—wakati kutakapokuwako mwisho wa uvunjaji wa sheria, mwisho wa hatari ya mali ya mtu na yeye mwenyewe. (Mika 4:4) Wana sababu nzuri ya kusadiki kwamba watu wengi wanaoishi sasa watauona wakati kutakapokuwa hakuna njaa tena, kwa sababu kutakuwako “wingi wa nafaka katika ardhi.” (Zaburi 72:16) Tena wanatazamia kujionea wenyewe utimizo wa ahadi ya kwamba ‘Mungu atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.’ (Ufunuo 21:3, 4) Wanawezaje kuwa na hakika hiyo kwamba mambo hayo kweli yatatukia? Kwa sababu ahadi hizi zapatikana katika Neno la Mungu mwenyewe, Biblia.

4. Ijapokuwa wanadamu walitumiwa kuandika, sababu gani mambo yaliyoandikwa katika Biblia yalitoka kweli kwa Mungu? (2 Timotheo 3:16, 17)

4 Yale ambayo Biblia inasema juu ya wakati wetu ujao si matokeo tu ya jitihada za kibinadamu kutafsiri maelekeo ya historia. Wanadamu walitumiwa waandike, lakini akili zao ziliongozwa na roho ya Mungu. Hivyo ule ujumbe unatoka kwa Mungu. Kwa habari ya chanzo cha mambo yaliyomo, Biblia yenyewe yasema: “Hakuna unabii katika maandiko unafasiriwa kama mutu fulani tu anavyopenda. Maana unabii wo wote haukuletwa kwa mapenzi ya muntu, lakini watu walisema yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na [roho takatifu].” (2 Petro 1:20, 21) Si vigumu kwetu leo kufahamu namna Mungu alivyoweza kufanya hivi. Hata wanadamu wanaosafiri katika anga ya juu wamerudisha ujumbe duniani, na huu umepokewa waziwazi sana. Je! Mungu mbinguni hangaliweza kupelekea wanadamu waaminifu waliopatana naye ujumbe katika njia bora zaidi? Bila shaka! Basi, kwa sababu nzuri, twakukaribisha uchunguze ambayo Biblia inasema juu ya jinsi unavyoweza kuona wakati ujao salama

Mahali Msaada wa Kweli Waweza Kupatikana

5. Ni maoni gani yanayofaa ambayo Biblia inatutia moyo tuwe nayo juu ya fedha na mali nyingine za kimwili? (Mhubiri 7:12)

5 Biblia inatusaidia tutazame maisha kwa maoni yanayofaa. Inatusihi tutie tumaini letu hakika katika yale yatakayodumu, ikifanya hivyo ili tuwe na hali njema milele. Leo mamilioni ya watu wanazitumaini mali za kimwili. Ijapokuwa yakubali faida za fedha na mali nyingini za kimwili, Biblia yaonyesha kwamba hizi silo jambo la maana katika maisha. Inasema kweli isiyokanikana kwamba ”uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” (Luka 12:15) Mali zaweza kupoteza thamani yazo. Zaweza kuibwa au kuharibiwa. Huenda hata uhai wa mwenye mali ukatiwa katika hatari na mtu fulani anayetaka kuiba fedha zake. Bila shaka usalama wa kweli uko kwingineko. Lakini wapi?

6. Sababu gani ni upumbavu kuweka matumaini yetu yote ya wakati ujao juu ya mambo ambayo viongozi wa kibinadamu wanaahidi?

6 Kuna watu wanaoweka matumaini yao yote ya wakati ujao juu ya yale ambayo viongozi wa kibinadamu huahidi. Je! wewe? Bila hata kutokeza ulizo juu ya kama viongozi mmoja mmoja ni waaminifu au ni wenye uwezo, Biblia inakwenda kwenye kiini cha shauri hili kwa kutukumbusha kwamba wote wanakufa. Inaonya kwa hekima hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake. [Roho] yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:3, 4) Hivyo, viongozi wa kibinadamu wanaongoza mambo ya sehemu ndogo ya wanadamu kwa miaka michache tu. Kwa habari ya usalama wa kudumu, hawawezi kuutoa kwako kama wasivyoweza kujipatia wenyewe.

7. (a) Ni nani hasa awezaye kutupatia usalama wenye kudumu, na kwa sababu gani? (Matendo 17:28) (b) Ikiwa twataka kufurahia usalama huo, twahitaji nini?

7 Lakini kuna Mmoja awezaye kuutoa. Yeye ndiye Muumba wa mbingu na dunia. Kabla ya kuafnyizwa dunia hii, yeye alikuwako; na ataendelea kuwako wakati wote baada ya kupita karne hii ya 20. Kama Zaburi 90:2 imwambiavyo: “Tangu milele hata milele ndiwe Mungu.” Yeye ndiye Chanzo cha uzima na Ndiye ameipa Dunia uwezo wa kutegemeza vitu vilivyo hai. Hivyo, hali njema yetu ya sasa na matumaini yetu ya wakati ujao yamtegemea yeye. Ndiyo sababu tunahitaji uhusiano mzuri na yeye ikiwa tutafurahia usalama wo wote wa kweli

8. (a) Mungu anatafuta watu wa namna gani? (b) Basi, ili tutimize takwa hilo yatupasa tuwe na nia ya kufanya nini mmoja mmoja? (Mathayo 7:21-23)

8 Je! hii maana yake ni kwamba lazima mtu awe na dini fulani katika maisha yake? Kungekuwa kukosea kukata shauri hivyo. Wale ambao Mungu anatoa kwao uhusiano mzuri pamoja naye ni namna fulani ya watu. Namna gani? Biblia yawasimulia katika njia hii: “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kweli, Baba anatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu yeye. Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yawapasa kuabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24, NW) Je! wewe ni mtu anayemwabudu Mungu ‘kwa kweli’? Je! umechunguza imani zako kwa msaada wa Neno la Mungu, uone kama zinapatana kabisa na yaliyoandikwa humo na “Mungu wa kweli”? (Zaburi 31:5) Je! una nia ya kufanya hivyo? Mafundisho na mazoea yasiyopatana na kweli hayana faida ya kudumu kwa ye yote. Yanafanya watu wasiangalie namna mambo yalivyo hasa; yanapoteza watu. Uradhi unaotokana na usalama wa kweli waweza kupatikana ikiwa mtu anataka sana kuijua kweli tu, na ana nia ya kurekebisha mambo inapokuwa lazima ili apatanishe maisha yake na kweli hiyo. Mojawapo ya kweli za maana kuliko zote inahusu Mungu mwenyewe alivyo.

9, 10. (a) Jina la Mungu mwenyewe ni jina gani? (b) Ungetumia andiko gani kumwonyesha rafiki jina la Mungu ni nini? (c) Watafsiri fulani wamejaribuje kuficha jina hilo? (Zaburi 110:1)

9 Je! unajua jina lake mwenyewe? Si “Mungu” wala “Bwana.” Hayo ni majina ya cheo au heshima, kama “Mister” (“Bwana”) na “Mfalme.” Walakini, kulingana na Biblia, Zaburi 83:18 yasema hivi: “Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” Hili si jina ambalo wanadamu wamempa Mungu. Kama inavyoonyeshwa katika Biblia ya Revised Version (American Standard Edition, iliyochapswa mwaka wa 1901 W.K.), Mungu anajitaja mwenyewe anaposema hivi: “Mimi ni Yehova, hilo ndilo jina langu.” (Isaya 42:8) Tafsiri fulani za Maandiko ya Kiebrania ya kwanza zinatafsiri jina hilo kama “Yahweh.” Nyingine zinatumia neno hili “BWANA” tu, lakini kama kawaida zinachapa kama ilivyoonyeshwa hapa katika sehemu hizi, kwa herufi kubwa “B” ikifuatana na herufi kubwa zenye chapa ndogo, kwa njia hiyo kuonyesha kwamba kuna zaidi katika maandishi ya lugha ya kwanza kuliko vile wanavyosema katika tafsiri yao.

10 Kwa mfano, sababu gani usitazame Zaburi 8:9 katika Biblia yako mwenyewe. Kulingana na Common Bible (iliyochapwa mwaka wa 1973 kwa idhini ya waalimu wa Kikatoliki na wa Kiprotestanti), inasema hivi: “Ee BWANA, Bwana wetu, jinsi lilivyo tukufu jina lako katika dunia yote!” Ebu angalia tofauti ya herufi mahali pote pawili ambapo neno hili “Bwana” linaonekana katika mstari huu mmoja. Mara ya kwanza, herufi kubwa zenye chapa ndogo zatumiwa baada ya herufi kubwa “B”; lakini mara ya pili neno lile lile laonekana limechapswa kwa herufi kubwa ya kwanza kisha zinazobaki katika herufi ndogo. (Katika New American Bible ya Katoliki hili lapatikana katika Zaburi 8:10.)b Walakini, tafsiri nyingine zinatafsiri mstari huu bila kujaribu kuficha jambo lo lote hivi: “Ee Yehova Bwana wetu, jinsi lilivyo tukufu jina lako katika dunia yote!”

11. (a) Je! ni jambo la maana kweli kujua na kutumia jina la Mungu? (Matendo 15:14) (b) Ikiwa twampenda Yehova, imetupasa sisi wenyewe tutumieje jina hilo? (Isaya 43:10)

11 Labda watafsiri fulani wanafikiri kwamba wanaifanya Biblia ikubalike kwa watu wengi zaidi kwa kutotumia jina la pekee la Mungu, lakini wanapojaribu kulificha jina linaloonekana mara nyingi zaidi kuliko jina jingine lo lote katika maandishi ya lugha ya kwanza, je! ni watafsiri waaminifu? Mungu wa kweli ataka watu wajue jina lake. Alijulisha hili wakati alipomwambia mtumishi wake Musa apashe habari mtawala wa Misri ya kale sababu gani Mungu alikuwa amemruhusu awepo mpaka wakati huo. Sababu gani ilikuwa hivyo? “Kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote,” akasema Mungu. (Kutoka 9:16) Ni jambo la maana kwetu kutumia jina la Mungu, tukifanya hivyo kwa heshima. Na kama twaipenda kweli, hatutasita kujijulisha wenyewe kama waabudu wa Yehova, Mungu wa pekee wa kweli.

12. Mungu anaonaje matumizi ya sanamu (mifano) katika ibada? (Zaburi 115:3-8; Kumbukumbu la Torati 7:25)

12 Walakini, yatupasa tuangalie tusije tukashirikisha jina la Mungu na kitu fulani asichokubali. Kumbuka, “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yawapasa kuabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24, NW) Ikiwa tunafahamu uhakika wa kwamba “Mungu ni Roho,” na tukimwabudu “kwa roho,” yaani, katika njia za kiroho, hatutatumia vitu vinavyoonekana viwe badala viwe badala ya Mungu. ‘Hakuna Mtu ambaye amemwona Mungu wakati wo wote,’ kulingana na Yohana 1:18, basi haiwezekani kufanya mfano wo wote au kitu kilichochongwa kiwe badala yake. Mfano usioweza kuona au kusikia au kusema, usioweza kuinua hata kidole ili kusaidia wale wanaoabudu mbele yake, haungeweza kamwe kumwakilisha sawasawa Mungu aliye hai. Ndiyo, mifano mingine haikusudiwi kuwa badala ya Mungu mwenyewe, lakini ulizo ndilo hili, Je! ni vitu vinavyotumiwa katika ibada ya kidini? Mungu alipotoa Amri Kumi, alisema waziwazi kwamba hakuna sanamu ambazo zingeruhusiwa kufanywa kwa kusudi hilo. Aliamuru hivi: “Hutajifanyia mwenyewe sanamu ya kuchongwa au mfano wo wote wa kitu cho chote . . . hutavipigia magoti wala kuvitumikia.” (Kutoka 20:4, 5, Jerusalem Bible ya Katoliki) Badala ya kutumia vitu ambavyoYehova hakubali, kuipenda kweli kutatusaidia tumjue Mungu kama alivyo sasa.

13. (a) Yehova ni Mungu wa namna gani? (b) Ni ipi kati ya sifa zake inayokuvutia zaidi?

13 Sifa zake ni njema sana hata zinavuta tumaini hakika la kila mtu anayependa haki. Kati ya sifa hizi, kama nguvu za uweza na hekima inayopita ile ya mwanadamu ye yote, zaonekana kutokana na kazi zake za uumbaji unaoonekana. Na wewe hukubali kwamba uzuri wa machweo (magharibi), sauti tamu za mlio wa ndege, hafuru nzuri ya maua, na ladha (mionjo) nyingi unazofurahia zote zaonyesha upendo wa Mungu kwa wanadamu? Lakini Biblia inasimulia zaidi ikituambia mengi zaidi juu ya Mungu. Inafunua kwamba Yehova anategemeza kilicho haki, lakini kwamba yeye pia ni mwenye huruma na fadhili. Inamsimulia katika njia hii: “[Yehova, Yehova], Mungu anayejaa rehema na mwenye neema, si mwepesi kwa hasira, mwenye rehema na kweli nyingi; akiwa na rehema kwa elfu za watu, akisamehe uovu na makosa na zambi; wala si mwenye kuhesabia mwovu kuwa kama hana zambi.” (Kutoka 34:6, 7, ZSB) Tena Biblia inasimulia juu ya matendo ya Mungu kwa karne nyingi na taifa la Israeli wa kale, matendo yanayoonyesha sifa hizo waziwazi sana. Pia maandishi hayo yanathibitisha kwamba “Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Matendo 10:34, 35) Yeye anataka namna zote za watu wafurahie uhusiano mzuri pamoja naye, na kwa fadhili amefanya mpango ili jambo hilo liwezekane.

14. Maisha ya mtu yanageuzwaje wakati anapomtumainia Yehova sana? (Mithali 3:5, 6)

14 Wakati mtu anapostawisha kuthamini sifa nyingi bora za Mungu wa kweli, kunatukia nini? Lile “jina” la Mungu linakuwa na maana sana kwake. Anaweka tumaini lake katika Yehova, akifanya mambo katika njia ya Mungu na, matokeo yake, anapata ujuzi. Ni kama Mithali 18:10 isemavyo: “Jina la [Yehova] ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.”

15. (a) Sababu gani wati wetu ujao wamtegemea Yehova? (b) Ni uamuzi gani mzito ambao kila mtu anapaswa kufanya? (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20)

15 Usalama huo unatia ndani matumaini ya mtu ya wakati ujao. Kwa kweli, wakati ujao wa wanadamu wote wategemea Yehova. Kwa sababu gani? Kwa sababu dunia hii ni kuumba kwake na wote wanaoishi juu yake wanategemea mipango yange ya kuendeleza uhai. Katika Biblia ameeleza kusudi lake kupatia watu wake hali za maisha zilizo salama na zenye furaha. Hakuna kitu mbinguni au duniani kiwezacho kumzuia Mungu Mwenye Nguvu Zote asitimize kusudi lake. Walakini, kusudi hilo halituzuii kutumia hiari. Halimhukumu mapema kila mmoja wetu kupata mauti hata tusiwe na uamuzi wo wote katika shauri hili. Lakini linatutolea uamuzi mzito: Je! kuthamini yote ambayo Yehova ametufanyia, na yale atakayotufanyia wakati ujao, kunatuongoza tupatanishe maisha zetu na mapenzi yake? Kutosadiki kwa mtu hakutabadili uhakika wa kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli, wala hakutageuza kusudi Lake. Lakini kunaweza kuonyesha kama mtu mwenyewe anafaidika na kusudi hilo la upendo. Kwa hakika uchaguzi huo ni wa lazima kama vile unahusu uzima au mauti

Sababu Kukosa Usalama Kunaharibu Uhai wa Kibinadamu

16. Ni baadhi ya mambo gani yanayofanya maisha yakose usalama?

16 Ili kufahamu namna kusudi la Yehova linavyotokeza usalama wa kweli, labda inafaa tujikumbushe kwanza mambo fulani kati ya yale yanayofanya maisha yasiwe yenye usalama leo. Kati ya haya ni kukosa upendo, kutojali sheria, kutoheshimu mali za wengine, na kutumia uongo na jeuri ili mtu apate anachotaka. Kwa kuongeza, hatuwezi kusahau ugonjwa na kujua kwamba lazima watu wafe. Kutokana na yanayotupata na pia yale tunayoona, twajua namna mambo haya yanavyohusu uhai wa kibinadamu. Lakini ilitukiaje? Jibu lapatikana katika Biblia.

17. Mwanzoni, ni nini kilicholeta usalama uliofurahiwa na Adamu na Hawa? (Mwanzo 1:31; 2:8, 15)

17 Kitabu chenyewe cha kwanza cha Biblia kinatupasha habari kwamba wakati Yehova alipoumba wazazi wetu wa kwanza wa kibinadamu, Adamu na Hawa, kazi yake ilikuwa njema sana. Kulikuwa hakuna kosa katika miili yao ambalo lingetokeza ugonjwa; walikuwa na tumaini la kuishi milele. Kwa upendo, Mungu aliwapa bustani (shamba lenye kupendeza), paradiso katika Edeni, iwe makao yao. Kwa ukarimu mwingi alitia ndani ya makao yao ya bustani wingi wa mimea yenye kuzaa mbegu na miti yenye kuzaa matunda ili kuwapatia chakula. Alijaza pia maisha zao kusudi kwa kuwaagiza watawale samaki, ndege na wanyama wote, na kuilima dunia na kuijaza watoto wao mpaka yote iwe kama paradiso ambamo alikuwa amewaweka. Hali ya usalama ilikuwa ya asili katika mazingira hayo. Lakini ikiwa walitaka waendelee kufurahia usalama huo, jambo fulani lilitakiwa kwao.

18. (a) Ni nini lililotakiwa kwa Adamu na Hawa ikiwa wangetaka kuendelea kuwa salama? (b) Yehova alijaribuje utii wao, na kwa sababu gani hili lilikuwa jambo kubwa? (Luka 16:10)

18 Ilikuwa lazima wakubali cheo chao kuhusiana na Mungu. Dunia na vitu vyote ndani yake vilikuwa mali ya Muumba wao, basi alikuwa na haki ya kuamua namna hivi vingetumiwa. Uzima wenyewe ulikuwa zawadi yenye masharti; yaani, Adamu na Hawa wangeweza kuendelea kulitimiza takwa la utii wenye upendo kwa Baba yao wa kimbinguni tu. Ili kukazia uzito wa takwa hili, Yehova alimwamuru mwanadamu hivi: “Wa kila muti wa shamba unaweza kula; lakini wa muti wa kujua uzuri na ubaya usile kwa maana siku unapokula, hakika utakufa.” (Mwanzo 2:16, 17, ZSB) Utii ungeonyesha kwamba mwanadamu anamkubali Mungu kama Mtawala; kutokutii kungemaanisha kukataa mapenzi makamilifu ya Mungu. Sheria hii haikuwa ngumu; haikumnyima mwanadamu cho chote alichohitaji, lakini iliweka jaribu jepesi lakini lenye matokeo, lililofaa hali ambazo katika hizo aliishi. Ilimpa Adamu na mke wake Hawa nafasi ya kuonyesha upendo wao kwa Baba yao wa kimbingu.

19. (a) Ni mambo gani yanayokosesha usalama yalionekana kwanza kuhusiana na dhambi ya Adamu na Hawa na tokea hapo? (b) Kama inavyoelezwa katika Warumi 5:12, watoto wote wa Adamu wamepatwaje?

19 Habari ya Biblia katika Mwanzo sura ya tatu yaonyesha kwamba walishindwa. Walikula kwa makusudi kutokana na mti ambao Mungu alikuwa amewakataza kula. Ule usalama uliofurahiwa mwanzoni na wanadamu wawili uliharibiwa. Mambo yale yale yanayokosesha usalama leo yakatokea mara ya kwanza wakati huo. Kukawa kukosa kumpenda Mungu, kutojali sheria yake, kutoheshimu mali yake. Wakiisha kukataliwa na Mungu, Adamu na Hawa wakafukuzwa katika Edeni. Kule nje ya paradiso, wengi wa watoto wao, kutia na mtoto wao wenyewe wa kiume Kaini, walizidi kuharibika walipotumia jeuri. Hata wale wasiopuza sheria ya Mungu kwa makusudi wameona katika miili yao wenyewe matokeo ya dhambi iliyorithiwa. Kama Warumi 5:12 inavyoeleza: “Kwa mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauiti ikawafikia watu wote kwa sababu woet wamefanya dhambi.”

20. (a) Uasi katika Edeni ulitokana na nani? (Ufunuo 12:9) (b) Aligeukaje akawa Shetani Ibilisi? (Yakobo 1:14, 15)

20 Walakini, na ifahamike kwamba hatua ya kwanza kuelekea uasi haikutokana na Adamu wala mke wake. Biblia inataja “nyoka” akisema kwa Hawa, akimshawishi kwa udanganyifu avunje sheria ya Mungu. Bila shaka, nyoka halisi hawezi kusema; na mwishowe Biblia inajulisha aliyemtumia nyoka huyo kuwa mtu wa kiroho asiyeonekana. Mtu huyu wa kiroho hakuwa ameumbwa awe mbaya. Lakini, kama wale wanadamu, mwana huyu wa kiroho wa Mungu pia alikuwa na hiari, uwezo wa kuchagua namna angetumia akili zake. Kwa kukubali tamaa mbaya, alisitawisha kiburi; alitaka viumbe wengine wamwabudu kama Mungu. Kwa njia hiyo alifuatia ili atimize miradi wake alijifanya mwenyewe mpinzani wa Mungu, Shetani, na mchongezi, Ibilisi.

21. (a) Alipokuwa akisema na Hawa, Shetani alifanya madai gani? (b) Sababu gani Hawa hakufanya hali yake iwe bora kwa kutii aliyosema Shetani?

21 Alimkaribia Hawa, kwanza akiuliza maulizo kisha akampinganisha Mungu moja kwa moja kwa kumwambia Hawa hivi: “Hakika hamtakufa [mkila kutokana na mti uliokatazwa], kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:1-5) Kwa yule mwanamke, jambo hili lilionekana kuwa bora zaidi ya lile alilokuwa nalo. Lakini kwa kulisadiki, je! kweli alipata usalama mkubwa zaidi? Je! hali ya mume wake ikawa bora kwa kujiunga naye katika kosa? Hapana; ulikuwa uongo mtupu. Jambo hili lilithibitishwa sana wakati walipokufa, na mpaka leo hii wanadamu wanaendelea kufa.

22. (a) Ni maulizo gani ya maana yaliyotokezwa katika Edeni, na haya yanahusuje usalama wa kuumba kote? (b) Katika siku za Ayubu, ni shtaka gani zaidi lililofanywa, na lilionyesha nini? (Ayubu 1:7-12; 2:1-5)

22 Maulizo ya maana yalitokezwa huko katika Edeni, na haya yauhusu usalama wa kuumba kote. Ukweli wa Mungu ulipingwa, na hili likatilia shaka uhalali na haki ya utawala wake. Ilishauriwa kwamba wanadamu wangekuwa na uwezo wa kujifanyia maamuzi yao wenyewe juu ya mema na mabaya, wakijiwekea kanuni zao wenyewe, wakijitawala wenyewe. Kuasi kwa Shetani na kushindwa kwa wanadamu wa kwanza wawili kushikamana na Mungu kulitokeza ulizo juu ya jambo ambalo wengine wa viumbe vya Mungu vyenye akili wangefanya. Je! ye yote angeshikamana na Mungu? Wakati uliofuata, katika ziku za mwanadamu Ayubu, Shetani alishtaki kwamba wale waliomtumikia Mungu walimtumikia kwa sababu za kichoyo tu, si kwa sababu ya upendo. Je! “Yobu anaogopa Mungu bule?” Shetani akapinga. (Yobu 1:9, ZSB) Alionyesha kwamba hakuna mtu ambaye angeshika ukamilifu kwa utawala wa Yehova ikiwa yeye, adui ya Mungu, angeruhusiwa amjaribu. Wanadamu hawangefurahia tena usalama kamili wakati wo wote mpaka mauliyo haya yajibiwe. Walakini, Yehova alijua kwamba maulizo hayo yangejibiwa hata wote wanaopenda haki wafurahi kabisa, naye alifanya mipango kwa kusudi hilo.

Mipango Inayowezesha Kuwe Wakati Ujao Salama

23. (a) Wakati wa kutoa hukumu juu ya wazazi wetu wa kwanza, Yehova alifanya jambo gani liwezekane kwetu? (2 Petro 3:9) (b) Mpango wa Yehova wa wakati ujao wa wanadamu unategemea nani?

23 Wakati hukumu ilipotolewa juu ya wazazi wetu wa kwanza kwa sababu ya uasi wao juu ya Mungu, Yehova hakusahau watoto wao walikuwa bado kuzaliwa. Kwa upendo alifanyiza kusudi lililomwezesha kila mmoja wetu achague mwenyewe kama ataka kuishi chini ya utawala wa kimungu. Kusudi hilo lategemea Yesu Kristo Mwana wa Mungu.

24. (a) Ni maisha ya namna gani ambayo Yesu alikuwa nayo kabla hajawa mwanadamu? (b) Sababu gani tusimseme kuwa Mungu au anayelingana na Mungu? (Yohana 17:3)

24 Mwana huyu alikuwa ndiye wa kwanza kabisa kuumbwa na Yehova katika makao ya kimbinguni. “Katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi,” Biblia yatupasha habari. (Wakolosai 1:15-17) Lakini katika wakati uliowekwa na Mungu, Mwana wake aliacha utukufu wake wa kimbinguni akazaliwa kwa mwujiza kama mwanadamu duniani. Malaika Gabrieli, aliyetangulia kutumwa ili atangaze kuzaliwa huko, hakusema yule mtoto atakayezaliwa angekuwa Mungu. Badala yake, alikutangaza kama kuzaliwa kwa “Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Yesu mwenyewe hakujidai kuwa Mungu. Yeye hakufanya kama Shetani, aliyetafuta kuabudiwa. Yeye alisema kweli hivi: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Kwa hiyo, ili kufurahia uhusiano mzuri na Mungu wa kweli, haitupasi tuhesabie Mwana wake cheo tofauti, tukimsema kuwa Mungu au anayelingana na Mungu.

25. Ni nini lililotimizwa kwa kuonyesha kwa Yesu ukamilifu wake chini ya mkazo mkubwa kama mwanadamu duniani?

25 Hapa duniani Yesu alipatwa na mambo ambayo hakuwa amepatwa nayo zamani hata kidogo. Alikuwa amefanya mapenzi ya Baba yake mbinguni bila makosa. Lakini je! angeendelea kuwa mshikamanifu (loyal) kama mwanadamu duniani, hasa kama angeumizwa na kutwezwa asivyostahili? Shetani alikuwa ameazimia kuhakikisha kwamba hakuna mtu, hata huyu Mwana mkuu wa Mungu, ambaye angekuwa mwaminifu anapojaribiwa. Lakini Yesu alishikamana sana na Neno la Mungu, akilitegemea kama uongozi wake, akilitumia katika kupinga vishawishi. Alipinga kwa nguvu mkazo wa kufanya mabaya, akisema: “Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie [Yehova] Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” (Mathayo 4:10) Yesu alishika ushikamanifu wake kwa Yehova kama Mtawala mpaka mauti, na alifanya hivi kwa majaribu makali zaidi sana kuliko yo yote ambayo Adamu alikuwa amepata. Katika njia hii Yesu aliondolea jina la Baba yake mashtaka ya uongo ya Shetani. Kwa mfano wake Yesu alituonyesha jinsi ya kushinda vishawishi, na jinsi ya kuonyesha kwamba sisi pia ni wategemezaji washikamanifu wa utawala wa Yehova.

26. Ni nini jinginelo lililotokana na mauti ya Yesu kama mwanadamu mkamilifu, nalo lilituwezeshea nini? (1 Timotheo 2:3-6)

26 Walakini, Mwana wa Mungu alitutolea mengi zaidi kuliko mfano mzuri tu. Yesu mwenyewe alieleza kwamba alikuja “kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Marko 10:45) Hili lilikuwa la lazima ikiwa wanadamu wangeondolewa dhambi, na magonjwa na mauti yanayotokana na dhambi. Kulingana na sheria ya Mungu, bei ya ukombozi yapaswa iwe uhai mkamilifu wa kibinadamu, ulingane na ule uhai mkamilifu wa kibinadamu uliopotezwa na Adamu. Hakuna mzao asiyekamilika wa Adamu ambaye angeweza kuitoa. Kwa upendo Yehova mwenyewe alifanya mpang huo. Alimtuma Mwana wake mwenyewe duniani. Kisha, baada ya mauti ya Yesu, Mungu alimfufua, akiwa sasa kama mtu wa kiroho, akaikubali thamani ya uhai wake wa kibinadamu kama ukombozi kwa ajili ya wanadamu. Hii ilitufungulia nafasi ya kupata tena kile ambacho Adamu alipoteza. Kama Biblia inavyoeleza: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminifye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Lo! ni matumaini mazuri sana kama nini yanayotuwezesha tupate uzima tukimwamini Mwana wa Mungu, kwa kujifunza alivyofundisha na kuyafuata sana!

27. (a) Sababu gani Yesu hakujitia katika mambo ya kisiasa? (Yohana 18:36) (b) Yesu alifundisha wafuasi wake kuwa na maoni gani juu ya serikali? (Mathayo 22:17-21)

27 Imani hiyo inatia kulithamini daraka ambalo Yehova amempa Mwana wake katika serikali. Yes hakujitia katika mambo ya kisiasa ya wakati wake; alijua kwamba hakuna serikali ya kibinadamu iliyotegemeza utawala wa Yehova. Hata watawala hao waseme juu ya kumwamini Mungu, wote walikuwa wakijiwekea kanuni zao wenyewe juu ya mema na mabaya. Basi, kama walikubali au hawakukubali, wote walikuwa wakifuata uongozi wa adui ya Mungu, Shetani Ibilisi, ambaye Biblia inajulisha kama “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30, NW) Yesu alifundisha wanafunzi wake walipe kodi zao, wawe wenye kutii sheria, kwa muda wote ambao Mungu aliruhusu serikali za wanadamu ziweko. Lakini alionyesha wazi kwamba tumaini peke yake la kuwa na wakati ujao salama ni kupitia kwa ufalme wa Mungu, serikali ya haki kweli kweli yenye kutenda kutoka mbinguni kwenyewe na kutumia mamlaka juu ya wanadamu wote. Kwa hiyo, aliwafundisha wasali kwa Mungu hivi: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” Yesu aliwatia moyo wafuate sheria za ufalme huo kama zilivyoandikwa katika Biblia. Tena aliwaagiza kuhubiri “habari njema ya ufalme” kwa watu kila mahali.—Mathayo 6:10; 24:14.

28. Ufalme wa Mungu ni nini, na twawezaje kuonyesha tunauthamini? (Mathayo 6:33)

28 Ufalme huo ni njia ya Yehova ya kutimizia mapenzi yake. Utaunganisha tena viumbe vyote vyenye akili chini ya utawala wa Yehova. Watakaotiwa katika ushiriki wa serikali hiyo ya kimbinguni ni watu waliochaguliwa katika dunia hii wakaonekana kuwa wenye kuunga mkono kwa ushikamanifu enzi kuu ya Yehova, utawala wake. Hawa wanasemekana kuwa “kundi dogo.” (Luka 12:32) Kitabu cha mwisho cha Biblia kinaonyesha kwamba wana kikomo cha hesabu ya watu “elfu mia moja makumi ine na ine [144,000], walionunuliwa katika dunia.” (Ufunuo 14:1, 3, ZSB) Walakini, yule mkubwa aliyepewa mamlaka ya ufalme ni Mwana wa Mungu mwenyewe Yesu Kristo. Katika utimizo wa unabii wa kimungu, yeye ndiye anayepewa na Yehova “mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na zugha zote, wamtumikie.” (Danieli 7:13, 14) Ni jambo la lazima kila mmoja wetu aishi kupatana kabisa na mpango huo wa kimungu. Wale wanaokataa kufanya hivyo hawataruhusiwa milele wazuie usalama wa wengine.

29. (a) Utawala wa kibinadamu umekuwako kwa muda gani na kwa sababu gani sasa hautaendelea kwa muda mrefu zaidi? (Yeremia 17:5) (b) Hili litakuwa na maana gani kwa Shetani? (c) Ni nini litakalozipata serikali za kibinadamu? (d) Itakuwaje kwa watu waovu? (e) Ni nini litakalopata wale wasiotaka utawala wa Yehova? (2 Wathesalonike 1:6-9)

29 Tangu ule uasi katika Edeni, wanadamu wamekuwa na miaka karibu elfu sita ya kuonja matunda ya utawala wa kibinadamu. Umekuwa msiba. Kwa kufaa, Biblia inaelekeza kwenye kizazi hiki kuwa ndicho katika hicho Mungu atafikiliza hukumu zake. Hili litakuwa na maana gani kwa adui mkuu zaidi wa wanadamu, Shetani Ibilisi? Yeye na mashetani zake watazuiwa kabisa wasiweze kutenda kazi, ‘watavurumishwa katika shimo refu lisilo na mwisho,’ wasiweze kupoteza wanadamu. (Ufunuo 20:1-3, NW) Kufikilizwa kwa hukumu za Mungu kutakuwa na maana gani kwa serikali za wanadamu? Biblia inatabiri hivi, “Ufalme . . . utavunja falme hizi zote [za wanadamu] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele.” (Danieli 2:44) Itakuwa na maana gani kwa waongo, wevi, na wale wanaozoea jeuri? “Asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo.” (Zaburi 37:10) Itakuwa na maaga gani kwa wale wasiotaka kufanya lo lote na utawala wa Yehova? Katika siku za Nuhu, “hawakujua hata garika ilipokuja na kuwaondosha wote,” na itakuwa vile vile sasa wakati Mungu atakapomtumia Mwana wake afikilize hukumu.—Mathayo 24:39, ZSB.

30. Yote haya yatakuwa na maana gani kwa waunga mkono washikamanifu wa utawala wa Yehova? (Ufunuo 7:9, 10, 13, 14)

30 Lakini yote haya yatakuwa na maana gani kwa wale ambao wameonyesha kwamba wao ni waunga mkono washikamanifu wa utawala wa Yehova? Yatamaanisha kukombolewa kuingia katika taratibu mpya yenye haki ya Mungu. Katika matendo ya Mungu na taifa la kale la Israeli, mfano ulitolewa ili kuonyesha namna haya yatakavyotokea juu ya maisha. Yalitukia sawasawa kama Mungu alivyokuwa amemwagiza Musa aseme: ‘Mtakaa katika nchi anayowarithisha [Yehova], Mungu wenu, naye atawapeni raha, akiwaokoa na adui zenu pande zote, nanyi mtakaa salama.’ (Kumbukumbu la Torari 12:10) Kwa habari ya hali wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani, iliandikwa hivi: “Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani [kuelekea kaskazini ya mbali] mpaka Beer-sheba [kusini].” (1 Wafalme 4:25) Kulingana na sheria ya Mungu, kila jamaa ilikuwa na shamba lake yenyewe la kulima na kuishi humo. Kumtii Mungu kulitokeza baraka yake, na, kama alivyokuwa ameahidi, hii ilitia ndani ‘mvua ya nchi kwa wakati wake.’ (Kumbukumbu la Torati 11:13-15) Kulikuwako usalama wa kiuchumi.

31. Kama inavyosimuliwa katika Zaburi 72, ni hali gani zinazosaidia kuleta usalama zitakazoenea dunia yote chini ya ufalme wa Mungu?

31 Hayo yaliandikwa katika Biblia, si kama maandishi ya historia tu, bali yatutie moyo. Bwana Yesu Kristo, yeye ambaye Yehova ameweka kuwa mfalme juu ya dunia yote, anasemekana katika Maandiko kama aliye “mkubwa kuliko Sulemani.” (Luka 11:31) Chini ya utawala wa Kristo, hali bora hata kushinda zile zilizokuwako katika Yuda na Israeli wakati wa siku za Sulemani zitaenea dunia yote. Zaburi 72 inasimulia kwa uzuri baraka hizo katika njia hii: “Katika siku zake mwenye haki atasitawi; na wingi wa salama, hata mwezi utakapokoma. Naye atatawala vilevile toka bahari hata bahari, na toka Muto [Frati] hata miisho ya dunia. Atakomboa nafsi yao na jeuri na ukali; na damu yao itakuwa ya damani machoni mwake. Na nafaka zitakuwa nyingi juu ya kichwa cha milima.” (Zaburi 72:7, 8, 14, 16, ZSB) Hali zitakazokuwako wakati huo zitakuwa zile ambazo Yesu Kristo alimsimulia mwanadamu aliyekuwa ameomba akumbukwe wakati Yesu angeingia katika ufalme wake. Yesu alimwambia hivi: “Utakuwa pamoja nami katika paradiso.”—Luka 23:43, ZSB.

32. (a) Itawezekanaje hata kwa wafu kufaidia na mipango hii ya ajabu? (b) Wale watakaofufuliwa watakuwa wakirudi kutoka wapi? (Ezekieli 18:4; Ayubu 14:13)

32 Wale ambao wamekwisha kufa kwa sababu ya kurithi dhambi kutoka kwa Adamu hawatasahauliwa wakati huo. Wao pia watafaidika na dhabihu ya ukombozi ya Mwana wa Mungu. Biblia inatabiri kwa kutia moyo hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Hili lina maana gani? Biblia inasema kwamba “walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Hawana uhai katika kaburi. Basi, ufufuo unamaanisha kurudia uhai. Kuondoa wale wa lile “kundi dogo” watakaoshiriki uzima wa kimbinguni pamoja na Yesu Kristo, wote wale watakaofufuliwa watakuwa katika umbo la kibinadamu, wakiwa na tumaini mbele yao la kuishi milele apa hapa duniani.

33. (a) Magonjwa na mauti yataondolewa kwa njia gani? (Marko 2:1-12) (b) Je! wewe mwenyewe wataka ufaidike na mipango hii ambayo Yehova amefanya kwa wakati ujao salama?

33 Huu utakuwa wakati wa jamaa ya kinadamu kuungana tena. Kwa usimamizi wa ufalme wa kimbinguni kila alama ya dhambi na matokeo yake itaondolewa kwa kuitumia thamani ya dhabihu ya Yesu kwa wote wenye imani. Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha hili lingekuwa na maana gani kwa wanadamu. Aliponya kila namna ya ugonjwa, hata kuponya macho ya vipofu na kuponya vilema. Katika taratibu mpya ya Mungu dunia itajawa na watu watakaopokea baraka hizo. Ahadi ya kimungu ni: “Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” (Ufunuo 21:4) Ndiyo, mambo yote ambayo yamefanya maisha yasiwe na usalama yatatoweka. Lo! hilo ni taraja ajabu!

34. Je! kuna usalama wa kweli wo wote unaoweza kufurahiwa sasa hivi?

34 Lakini si kila jambo linalotokeza usalama litafurahiwa wakati ujao tu. Mengi yaweza kufurahiwa sasa hivi.

Usalama Unaoweza Kufurahiwa Sasa

35. Ni mambo gani yanayotajwa hapa yangetokeza usalama mkubwa wa kipekee?

35 Bila kujali hali nyingine ambazo mtu anapata katika maisha, watu wengi wangekubali kwamba ye yote anayehakikishiwa kupatiwa chakula cha kila siku na mavazi ya kutosha ana usalama sana. Kwa kuongezea, ikiwa watu ambao anashirikiana nao sana wanapendana kweli kweli, hili pia lingeongezea usalama huo. Na kama angejua yaliyoko wakati ujao, hili, pia, lingesaidia kupunguza hali yo yote ya kuona mashaka. Lakini wingi wa watu haufurahii hali hiyo ya usalama. Je! hilo lina maana ya kwamba zile ahadi za usalama zinazotolewa katika Neno la Mungu zitatimizwa wakati ujao tu? Au je! watu wanaweza kuona usalama hata sasa kwa kuziamini ahadi hizo na kwa kutenda kupatana nazo? Je! kuna watu wanaofanya hivyo sasa kwa umoja?

36. (a) Ni chini ya gali gani Mungu anasema atatoa chakula cha kila siku na mavazi sasa hivi? (b) Nani wanaofurahia usalama huo, na wanapataje riziki hizi? (Waefeso 4:28)

36 Wakristo wale wanaojulikana kama Mashahidi wa Yehova wameona Neno la Mungu kuwa la kweli na wamepata kuona kwamba kulitumia katika maisha zao kunaleta faida bora sasa hivi. Faida hizo zinatokana na kuthamini kwa kuafa mambo ya kiroho katika maisha ya mtu ya kila siku. Bila shaka, kila mtu duniani, kama ni mtu anayefikiria mambo ya kiroho au sivyo, aweza kufaidika na mazao ya dunia. Lakini Biblia inaonyesha kwamba Mungu anapendezwa kwa njia ya pekee ili wale wanaotanguliza utumishi wake wawe na hali njema. Ili kutia nguvu imani ya wanafunzi wake Yesu alisema hivi: “Musisumbuke mukisema: Tutakula nini? ao: Tutakunywa nini? ao: Tutavikwa nini? Kwa maana Mataifa wanatafuta maneno haya yote; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kama munahitaji vitu hivi vyote. Lakini ninyi tafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na vitu hivi [vingine] vyote vitaongezwa kwenu.” (Mathayo 6:31-33) Lakini wanapataje ‘vitu hivi vingine,’ vitu vinavyohitajiwa ili kumsaidia mtu katika njia ya kimwili? Si kwamba kundi la Kikristo linawasaidia na fedha. Badala yake, wote ni wafanya kazi wenye nia. Na, wakati watu wanapofanya ufalme wa Yehova na haki yake kuwa ndiyo mambo ya maana sana katika maisha zao, Mungu anabariki jitihada zao za kupata riziki za maisha. Anajibu sala yao “utupe leo riziki yetu.” (Mathayo 6:11) Yehova hawaahidi watumishi wake wingi wa vitu vya kimwili wakati ulimwengu wa sasa ungali upo, lakini anawahakikishia kwamba watapata wanachohitaji hasa. Na hakuna mwingineyo awezaye kama yeye kuona kwamba wanakipata.

37. (a) Ni namna gani za mwenendo na maoni zinazoleta ukosefu wa usalama? (b) Hasa, ni sifa gani inayokosekana miongoni mwa watu wa namna hiyo? (c) Ni wapi Yesu alisema upendo huo ungepatikana?

37 Pia Mpaji mkuu wa mahitaji ya kimwili anafanya jambo jinginelo lipatikane ambalo ni la maana kwa usalama sasa. Kama unavyoweza kufahamu, kuwa na riziki za kimwili hakutamfanya mtu ajione kuridhika na kuwa salama ikiwa washiriki wake ni watu wasiopendezwa naye. Ukosefu wa usalama unatokeo wakati watu wanaposema uongo na kupunja; wakati wanapotumia ulimi wao bila kufikiria sana maoni ya wengine; wakati wanapoamua ubora wa wengine kwa kadiri ya mali za kimwili, rangi ya ngozi au taifa la mtu; na wakati mara nyingi “fadhili” inapoongozwa na kusudi la siri, la kichoyo. Jambo linalokosekana sana kati ya watu wa namna hiyo ni upendo—kufikiria kweli kweli watu wengine bila choyo. Je! kweli upendo huo waweza kupatikana—si kati ya watu wachache tu, bali kama tabia yenye kuonekana wazi sana ya jamii nzima ya watu? Yesu Kristo anatuhakikishia kwamba upendo huo waweza kupatikana. Alisema: “Hivi watu wote watajua ya kama ninyi ni wanafunzi wangu, kama ninyi mukiwa na mapendo ninyi kwa ninyi.” Naye alijua kwamba wangekuwako watu hao wakati wetu, kwa sababu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka mwisho wa taratibu ya mambo.”—Yohana 13:35, ZSB; Mathayo 28:20, NW.

38. Biblia inatusaidiaje kuwajua watu walio na upendo huo? (1 Yohana 4:20, 21)

38 Ikiwa umeona upendo huu haumo miongoni mwa washiriki wako, basi ni lazima utafute kwingineko. Katika 1 Yohana 4:8, Biblia inatoa uongozi unaohitajiwa, ikisema: “Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo.” Basi, upendo huo waweza kupatikana kati ya watu ‘wamjuao Mungu.’ Bila shaka hili halina maana ya kwamba utauona kwa watu wote ambao ni wenye dini; wewe wajua kwamba sivyo. Lakini utauona kati ya wale wanaomjua Yehova, Mungu wa pekee wa kweli, wanaoheshimu jina lake na wanaojaribu kupatanisha maisha zao kweli kweli na mapenzi yake. Faida zinazotokana na ushirika huo ni wazi.

39. Zaidi ya kuwa tu miongoni mwa watu hao, ni jambo gani jinginelo mtu aweza kufanya litakalomletea usalama na kufurahia maisha?

39 Ndiyo, katika njia hii mtu hakosi kupatwa na mwenendo usio wa sheria na wengine katika ulimwengu. Walakini, yeye mwenyewe anapomtegemea Mungu na kkubali sana kanuni ya Mungu ya wema na ubaya kama ilivyoandikwa katika Biblia, anafaidika sana. Analindwa asijiingize katika matendo ambayo yangetokeza uchungu na huzuni. Kama mithali 1:33 isemavyo: “Kila anisikilizaye [yaani, hekima ya kimungu] atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya.” maisha yake yaweza kujaa maana ya kweli ikiwa anayatumia kupatana na mapenzi ya Muumba. Badala ya kupingwa kama watu wengi sana, yeye aweza kuishiriki furaha inayotokana na kusaidia wengine wajifunze njia ya pekee ya kweli ya kuondolea matatizo ya wanadamu—ule ufalme wa Mungu. Yesu Kristo alitabiri kazi hiyo, akisema: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14, NW.

40. Mashahidi wa Yehova wanaonaje juu ya wakati ujao, na kwa sababu gani? (Luka 21:28-32)

40 Wakati wale wanaoshiriki utendaji huu wa kuhubiri wanapoutazamia wakati ujao, hawajawi na hofu. Wakiisha kujifunza Biblia, na kusadiki inayosema, wanajua mambo yaliyoko wakati ujao. Badala ya kujiona kupingwa na kila tukio baya katika mambo ya ulimwengu, wanaona mambo haya kuwa utimizo wa unabii wa Biblia juu ya mwisho wa taratibu hii ya mambo. Wanajua kwamba karibuni sasa, katika kizazi hiki, Mungu ataharibu wote wanaoendelea kutojali utawala wake halali na wanaoendelea kuharibia wanadamu wenzao furaha ya maisha. Wakiwa na tumaini hakika wanatazamia utimizo wa lile tumaini lililoandikwa katika 2 Petro 3:13, NW, linalosema hivi: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizi haki itakaa.”

41, 42. (a) Basi, ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanafurahia sana usalama sasa hivi, ijapo waishi katikati ya ulimwengu wenye matata? (b) Je! ule usalama unaofurahiwa na Mashahidi wa Yehova ndio wewe unataka?

41 Huo ndio usalama unaofurahiwa sasa hivi na waabudu wa Kikristo wa Yehova Mungu, na wale ‘wanaomwabudu Baba kwa roho na kweli.’ Unatokana na kufuata kwao kanuni za haki za Yehova na kwa kuzitumia katika maisha zao. Kama ilivyotabiriwa katika Isaya 32:17, 18: “Kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima. Na watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.” Wao ni waunga mkono washikamanifu wa enzi kuu ya Yehova. Hawajiwekei kanuni zao wenyewe za wema na ubaya. Hawajaribu kutatua matatizo ya ulimwengu kwa uwezo wao wenyewe. Wanakubali kwa kushukuru na kuutegemeza mpango wa upendo ambao Yehova amefanya, yaani, ufalme wake kupitia kwa Yesu Kristo.

42 Je! wewe ungependa ushiriki usalama ule ambao wanafurahia? Unaweza.

Unaloweza Kufanya

43. Ukienda kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, utaweza kujionea nini?

43 Mojawapo ya hatua za kwanza ni kushirikiana na watu wanaofurahia usalama huo. Katika njia hii unaweza kujionea mwenyewe kama hili ndilo kweli umekuwa ukitafuta. Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha kwa furaha sana uhudhurie mikutano yao kwenye Jumba la Ufalme lililo katika eneo lako. Utaona kwamba mikutano yao si yenye kujaa sherehe za dini tu, na sadaka za fedha hazitozwi. Badala yake, kuna mazungumzo yenye maana ya Neno la Mungu na namna linavyogeuza maisha zetu. Biblia inatushauri hivi: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane.” (Waebrania 10:24, 25) Roho hii ndiyo utaona katika Jumba la Ufalme.

44. (a) Ili wewe mwenyewe uufurahie usalama unaouona katika maisha za wengine katika Jumba la Ufalme, wahitaji nini? (b) Ni kwa sababu gani hakuna ye yote wa sisi anaweza kudai kuwa na uhusiano huo, lakini unaweza kupatikanaje?

44 Kuhudhuria mikutano hiyo kutakuwezesha uuone usalama ambao wengine wanafurahia, nawe bila shaka utaufurahia ushirika huo. Lakini jambo fulani zaidi latakiwa kama wewe mwenyewe wataka uwe na usalama huo. Unalohitaji zaidi kuliko yote ni uhusiano wenye kukubaliwa na Yehova Mungu. Yeye Ndiye juu yake hali njema yako ya sasa na matumaini yako yote ya wakati ujao yategemea. Uhusiano huo si jambo fulani ambalo ye yote wa sisi aweza kudai kuwa nalo. Hatukuzaliwa nao. Sisi sote ni wazao wa Adamu mwenye dhambi, hivyo tulizaliwa katika jamaa ya kibinadamu iliyotengana na Mungu. Ili tupate ukubali wa Yehova, ni lazima tupatanishwe naye, na hili lawezekana kwa kuuamini mpango ambao amefanya kupitia kwa dhabihu ya Mwana wake tu. Kama Yesu mwenyewe alivyosema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”—Yohana 14:6.

45. (a) Kwa ni lazima tufahamu nini juu ya maisha na namna maisha zetu zipaswavyo kutumiwa? (Ufunuo 4:11) (b) Ili tumpendeze Yehova, yatupasa sisi wenyewe tuoneje juu yake? (c) Sababu gani uzamisho wa maji ni wa maana sana, na ni jambo gani la lazima kabla ya mtu kuwa tayari kubatizwa? (Mathayo 28:19, 20)

45 Ni lazima tufahamu kwamba tuna deni na Mungu juu ya maisha zetu na kwamba kushindwa ko kote kutumia maisha zetu katika kumtii Mungu ni kosa. Tukisikitikia kwa unyofu wa moyo kushindwa ko kote kwa zamani kutumia maisha zetu kupatana na mapenzi ya Muntu tutakataa mwendo huo mbaya na kugeuka, tukipatanisha maisha zetu na mapenzi ya Mungu. Huku kunatia ndani kufanya lile ambalo Yesu aliwaambia wanafunzi wake yawapasa kufanya, yaani, ‘wajikane wenyewe.’ (Mathayo 16:24) Mtu anyefanya hivi hadai tena kwamba anayo “haki” ya kuishi ili afurahishe tamaa zake mwenyewe tu, bila kufikiria mapenzi ya Mungu. Badala yake, anajitoa kabisa afanye mapenzi ya Mungu kama ilivyoagizwa na Mwana wake. Naye anafanya hivi kwa sababu inafaa na kwa sababu amesadikishwa kwamba kila jambo analofanya Yehova lina kusudi zuri na lenye haki, na kwamba jambo ambalo Mungu anafanya litatokeza baraka kwetu ikiwa twapenda haki. Anampenda Yehova kweli kweli ‘kwa moyo wake wote, akili, nafsi na nguvu.’ (Marko 12:29, 30) Akiisha kufanya ahadi hiyo katika moyo wake mwenyewe, yuko tayari kujitoa kwa uzamisho wa maji waziwazi, kwa kufuata mfano wa Yesu Kristo na kwa kutii maagizo aliyowapa wanafunzi wake. Katika njia hii peke yake, kama ilivyoandikwa katika Neno la Mungu, ndipo mtu aweza kuingia katika uhusiano wenye kukubaliwa na Mungu wa kweli na kushiriki usalama ambao watumishi wake wanafurahia.

46. Tunaonyeshaje kwamba kweli twataka Yehova awe Mtawala wetu?

46 Tangu hapo, ni lazima kuendelea kuonyesha kwamba umeukataa kabisa mwendo wa kujitegemea unaoendelezwa na Shetani; kwamba hujiwekei kanuni yako mwenyewe ya mema na mabaya; kwamba unataka sana Yehova awe Mtawala wako. Utahitaji ufanye kama inavyosemwa katika Mithali 3:5, 6, ZSB: “Tumainia [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usitegemee ufahamu wako mwenyewe: katika njia zako zote umukiri yeye, naye ataongoza mapito yako.” Ndiyo, yeye ataongoza mapito yako katika njia ya usalama wa kweli wenye kudumu.

47. Ni usalama gani unaowajia wale wanaoikubali kweli kweli mipango yenye upendo ya Yehova?

47 Lo! ni baraka za ajabu kama nini zinazowajia wote wanaoikubali kweli kweli mipango yenye upendo ambayo Yehova amewafanyia wanadamu! Wakisimama imara chini ya utawala wake, wanalindwa sasa, na wana matumaini hakika ya wakati ujao. Kwa sababu ya fadhili za upendo za Yehova na ukweli wake, wataushiriki usalama wenye kufurahisha sana utakaowajia wanadamu chini ya ufalme wa Mungu kupitia kwa Mwana wake Yesu Kristo.

[Maelezo ya Chini]

a Mitajo ya Maandiko iliyotumiwa katika kijitabu hiki inatokana na Biblia ya Union Version na Biblia ya Kiswahili ya Zaïre (ZSB), chapa ya mwaka wa 1975, isipokuwa imeonyeshwa vingine.

b Katika New English Bible na Union Version njia hii iliyotumiwa na watafsiri yaweza kuonwa vizuri zaidi katika Zaburi 135:5 na katika Nehemia 10:29.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Watu waishio sasa watauona wakati njaa haitakuwapo tena

[Picha katika ukurasa wa 7]

Matumaini yetu ya wakati ujao yamtegema Yeye aliyeziumba mbingu na dunia

[Picha katika ukurasa wa 13]

Maandishi ya Biblia juu ya wazazi wetu wa kwanza yaonyesha sababu gani kukosa usalama kunaharibu uhai wa kibinadamu leo

[Picha katika ukurasa wa 22]

Chini ya ufalme wa Mungu kutakuwako mwisho wa uvunjaji wa sheria, na mwisho wa hatari ya mali ya mtu na kuumizwa mwili wake

[Picha katika ukurasa wa 24]

Neno la Mungu laahidi kwamba magonjwa na mauti yataondolewa—ndiyo, hata wapendwa waliokufa watafufuliwa waishi tena

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki