SOMO LA 81
Mahubiri ya Mlimani
Baada ya kuwachagua mitume wake 12, Yesu alishuka kutoka mlimani na kukuta umati wa watu ukiwa umekusanyika. Watu hao walitoka Galilaya, Yudea, Tiro, Sidoni, Siria, na ng’ambo ya Yordani. Waliwaleta wagonjwa na watu waliokuwa wakiteswa na roho waovu. Yesu akawaponya wote, kisha akaketi kando ya mlima, na kuanza kufundisha. Alieleza mambo tunayopaswa kufanya ikiwa tunataka kuwa rafiki za Mungu. Ni lazima tujifunze kumpenda Yehova na kutambua kwamba yeye ni muhimu katika maisha yetu. Lakini hatuwezi kumpenda Mungu ikiwa hatuwapendi wanadamu wenzetu. Tunapaswa kuwa wema na wenye fadhili kwa kila mtu kutia ndani adui zetu.
Yesu alisema: ‘Haitoshi tu kuwapenda rafiki zako. Unapaswa pia kuwapenda adui zako na kuwasamehe wengine kutoka moyoni. Ikiwa umekosana na mtu fulani, nenda umwombe msamaha. Watendee wengine katika njia ambayo wewe ungependa kutendewa.’
Pia, Yesu aliwapa watu ushauri mzuri kuhusu vitu vya kimwili. Alisema hivi: ‘Ni muhimu zaidi kuwa rafiki ya Yehova kuliko kuwa na pesa nyingi. Mwizi anaweza kukuibia pesa, lakini hakuna mtu anayeweza kuiba urafiki wako pamoja na Yehova. Usihangaike kuhusu kile utakachokula, utakachokunywa, au kile utakachovaa. Waangalie ndege wa angani. Wakati wote Mungu anahakikisha kwamba wanapata chakula cha kutosha. Kuhangaika hakutakusaidia kuongeza siku za kuishi. Kumbuka kwamba Yehova anajua vitu unavyohitaji.’
Umati haukuwahi kumsikia mtu mwingine akifundisha kama Yesu. Viongozi wao wa kidini hawakuwa wamewafundisha mambo hayo. Ni nini kilimchofanya Yesu awe mwalimu mkuu? Kwa sababu yale aliyofundisha yalitoka kwa Yehova.
“Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu.”—Mathayo 11:29