Maisha na Huduma ya Yesu
Mahubiri Yenye Sifa Zaidi Ambayo Yamepata Kutolewa
TAMASHA yenyewe ni moja ya zile zinazokumbukika zaidi katika historia ya Biblia: Yesu ameketi kando ya mlima, akitoa Mahubiri ya Mlimani yake yaliyo na sifa sana. Mahali penyewe ni karibu na Bahari ya Galilaya, labda hapo pakiwa ni karibu na Kapernaumu. Yesu alikuwa ametumia usiku mzima akipelekea Mungu sala, na asubuhi iliyofuata akawa amechagua 12 wa wanafunzi wake wawe mitume. Halafu, akiwa pamoja nao wote, akawa ameteremka kuja mahali hapa pa chini milimani.
Umefikiri kwamba kufikia sasa,Yesu alikuwa amechoka sana na angetaka kulala kidogo. Lakini makundi makubwa ya watu wamekuja, wengine umbali mkubwa wa kutoka Yudea na Yerusalemu, umbali wa kilometa 100 mpaka 110. Wengine wametoka pwani ya Tiro na Sidoni upande wa kaskazini. Wamekuja kumsikia Yesu na kuponywa magonjwa yao Hao ni kutia hata na watu wanaosumbuliwa na mashetani.
Yesu anapoteremka, wagonjwa wanamkaribia wamguse, naye anawaponya wote. Baadaye, inaonekana Yesu anapanda kwenda mahali pa juu sana mlimani. Akiwa hapo anaketi chini na kuanza kufundisha makutano waliotapakaa mahali pale penye usawa mbele yake. Na ebu wazia! Sasa hakuna hata mtu mmoja kati ya wasikilizaji wote anayesumbuliwa na ugonjwa mkubwa!
Watu wana hamu nyingi ya kumsikia mwalimu huyu anayeweza kufanya miujiza hiyo ya kustaajabisha. Lakini, Yesu anatoa mahubiri yake hasa kwa faida ya wanafunzi wake, ambao labda ndiyo walio karibu naye wakiwa wanamzunguka. Lakini ili sisi pia tuweze kufaidika, Mathayo na Luka pia wameyaandika mahubiri hayo.
Masimulizi ya Mathayo ya mahubiri hayo yana urefu ulio karibu mara nne ya yale ya Luka. Zaidi ya hilo, Luka anaonyesha visehemu fulani vya mambo yaliyoandikwa na Mathayo kuwa vilisemwa na Yesu katika wakati mwingine wa huduma yake, kama inavyoweza kuonekana kwa kulinganisha Mathayo 6:9-13 na Luka 11.1-4, na Mathayo 6:25-34 na Luka 12:22-31. Hata hivyo jambo hilo halipasi kushangaza Ni wazi kwamba Yesu alifundisha mambo yale yale zaidi ya mara moja, na Luka akachagua kuyaandika mengine ya mafundisho hayo katika kikao tofauti
Kinachofanya mahubiri ya Yesu yawe ya thamani kubwa sana si kina tu cha mambo ya kiroho yaliyomo, bali pia ni urahisi na uwazi aliyoutumia kueleza kweli hizo. Yeye alitumia vituko vya kawaida na mambo yaliyojulikana sana na watu, hivyo akafanya mawazo yake yaeleweke kwa urahisi na wote wanaotafuta maisha bora katika njia ya Mungu. Katika matoleo yanayofuata tutachunguza mengine ya mambo aliyosema. Luka 6:12-20; Mathayo 5:1, 2.
◆ Mahubiri ya Yesu yanayokumbukia zaidi yalitolewa wapi, ni nani waliokuwapo, na ni jambo gani lililokuwa limetoka tu kutukia kabla hajayatoa?
◆ Kwa sababu gani haishangazi kwamba Luka anaandika mengine ya mafundisho yaliyotolewa katika mahubiri hayo yakiwa katika kikao kingine?
◆ Ni jambo gani linalofanya mahubiri ya Yesu yawe yenye thamani kubwa sana?