Mahubiri ya Mlimani—Msingi Wake na Kikao Chake
MAHUBIRI ya Mlimani ndiyo mahubiri yanayojulikana zaidi yaliyopata kuhubiriwa. Mitajo kutoka kwayo imo mioyoni na vinywani mwa mamia ya mamilioni ya watu duniani pote. Je! hotuba hii ya Yesu Kristo iliyotolewa karibu miaka 2,000 iliyopita, ina ujumbe fulani kwa watu leo?
Je! watu wangali wanajitahidi kupata furaha? Je! wanadamu wangali wanahitaji kanuni sahihi zipate kuongoza tabia za mtu na mwenzake? Je! leo kuna watu wanaotaka kujua anayotaka Mungu juu ya ibada inayokubalika?
Watu mmoja mmoja wanaotamani habari ya kweli juu ya mambo haya ni wengi zaidi kuliko walivyopata kuwa katika wakati mwingine wo wote uliopita. Kwa kuwa hayo ndiyo mambo yanayozungumzwa hasa katika Mahubiri ya Mlimani, yanafaa sana katika karne hii ya 20 kama vile yalivyokuwa siku ile yaliyosemwa. Kwa hiyo tutafaidika tukichunguza aliyosema Yesu katika mahubiri hayo yanayojulikana sana.
Lakini kabla ya kufanya hivyo, ebu na tuchunguze msingi na kikao cha hotuba hii kuu.
MASIMULIZI MAWILI YANAYOPATANA
Kwa wazi Mahubiri ya Mlimani yanaonekana katika masimulizi mawili ya Injili. (Mathayo, sura ya 5 mpka 7; Luka 6:20-49) Masimulizi ya Mathayo ya mahubiri haya ni marefu karibu mara nne ya yale ya Luka. Kuna mistari mitano tu katika masimulizi ya Luka isiyopatikana katika yale ya Mathayo. Mahali masimulizi haya mawili yanapolingana mara nyingi yanatofautiana sana kwa maneno yanayotumiwa. Je! hii inapaswa kuleta mashaka juu ya ukweli wa mahubiri haya namna yalivyo katika Biblia zetu?
Kwa habari ya kipingamizi kinachotokea kutokana na ukweli wa kwamba Luka anaacha sehemu kubwa za mahubiri hayo tofauti na yalivyo katika Mathayo, A. T. Robertson anaandika katika A History of the Gospels for Students of the Life of Christ: “Haya yanakosa kuangalia sehemu kadha za habari ile ile ambazo Luka ameweka kwingineko, au ambazo Yesu alirudia pindi nyingine ([linganisha] Mt. 6:9-13 na Luka 11:2-4; Mt. 6:25-34 na Luka 12:22-31). Yesu alirudia mara nyingi aliyosema katika pindi nyingi na ndivyo wanavyofanya na wanavyopaswa kufanya waalimu wote. . . . Wala hatupaswi kushangaa kwamba Luka, akiandikia Wakristo wote kwa ujumla, anaacha sehemu kubwa ya mahubiri hayo walizoandikiwa Wayahudi hasa (tazama Mt. 5:17-27; 6:1-18).” Halafu Robertson anaongeza hivi:
“Zaidi ya hayo, kuondoa tofauti hizi zinazoelezeka, inatupasa kukumbuka kwamba hotuba zote mbili zinaanza na kumalizika namna ile ile, kwamba zina ulinganifu wa ujumla kwa namna sehemu mbalimbali zilivyopangwa, na kwa ujumla zinaonyesha ulinganifu na misemo inayofanana kabisa.”
WAKATI GANI NA MAHALI GANI?
Mwana wa Mungu alitoa mahubiri haya wakati gani katika wakati wa utumishi wake wa kidunia? Maandiko yanaripoti kwamba Yesu alikatiza safari yake ya kwanza ya Galilaya ili apate kusherehekea “sikukuu ya Wayahudi” (inaelekea ni Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka 31 W.K.) huko Yerusalemu. (Yohana 4:46–5:1) Luka anaeleza kwamba baada ya Yesu kurudi Galilaya alikemewa na Mafarisayo kwa sababu ya kumponya mtu mwenye mkono uliopooza katika siku ya Sabato. (Luka 6:6-11) Muda mfupi baadaye “ali-ondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu. Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita mitume.”—Luka 6:12, 13.
Baada ya hayo, Yesu “akashuka pamoja nao, akasimama mahali tambarare, pamoja na wanafunzi wake wengi, na makutano makubwa ya watu waliotoka Uyahudi wote na Yerusalemu, na pwani ya Tiro na Sidoni; waliokuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao; na wale waliosumbuliwa na pepo wachafu; waliponywa. Na makutano yote walikuwa wakitaka kumgusa, kwa sababu uweza ulikuwa ukimtoka ukiwaponya wote. Akainua macho yake akawatazama wanafunzi wake” akasema yale Mahubiri ya Mlimani.—Luka 6:17-20.
Yesu alitoa hotuba yake akiwa mahali gani? Kumekuwako makisio mengi juu ya hili. Wengine wanasema kwamba alikuwa juu ya mlima mrefu katika Galilaya, kama vile Mlima Tabari. Wengine wanapendelea mahali paitwapo “pembe za Hatini, palipo kati ya Mlima Tabori na Kapernaumu. Hata hivyo, Maandiko, hayataji mahali penyewe yalipotolewa hayo Mahubiri ya Mlimani. Juu ya hili, kitabu A Dictionary of the Bible kilichotengenezwa na James Hastings chasema hivi:
“Mahubiri haya yalitolewa katika Galilaya, mahali ambapo sana sana Yesu alifanya huduma yake ([linganisha] Mt 4:23-25, Lk 6:17) Ikiwa kuna wonyesho katika Mt 8:5, Lk 7:1 kwamba mahali pa tukio hilo palikuwa karibu na Kapernaumu, hata hivyo mahali penyewe hapangeelezeka. . . . Mlima unaotajwa katika Mt 5:1 8:1, Lk 6:12 hautajwi wala hauwezi kujulikana. Hata hivyo, tunaweza kuwazia kwamba mahali penyewe pa Mahubiri hayo palikuwa katika sehemu iliyokuwa magharibi mwa ziwa hilo, karibu na sehemu ya pwani iliyokuwa na watu wengi.”
NJIA YA YESU YA KUFUNDISHA
Umepata kuona namna njia ya kufundisha ipatikanayo katika Mahubiri ya Mlimani inavyotofautiana na ile wenye elimu nyingi ya kilimwengu wanayotumia kutoa mashauri? Kitabu icho hicho cha Hastings kinasema hivi juu ya njia ya Yesu ya kufundisha:
“Alipokuwa akifundisha makutano, katika masinagogi yao, katika njia kuu, kandokando ya bahari, na katika pande za vilima vya Galilaya, Yeye alitumia kweli Zake za kidini na kanuni za tabia njema katika misemo inayojulikana na watu wote na yenye kufahamika wazi, Akitofautisha mawazo Yake ya maisha katika nja nyingi rahisi na mawazo na matendo yaliyokubalika pote, na kutoa mafundisho Yake kwa kutumia mifano ya hali ya kawaida ya maisha, maono, na mazingira ya wasikilizaji Wake. Pasipo hata kidogo hali ya wenye elimu nyingi na wenye akili nyingi, . . . Hakufundisha mambo haya kwa namna ya shule za kikale na za kisa-sa. Alitoa mawazo Yake katika njia ambayo yangefahamika ulimwenguni pote. Alizungumza kwa urahisi, kwa ufahamu, na kwa juhudi ambayo ingekubaliwa na wote wanaosikiliza kwa uzito.”
Unafahamianaje na kweli zinazopatikana katika Mahubiri ya Mlimani? Yawezekana ukawa unafahamiana na mengine ya maneno ya hekima, kama vile Sala ya Kielelezo, au “Baba Yetu,” na msemo una-ojulikana sana aliposema Yesu: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii.” (Mt. 6:9-13; 7:12) Lakini namna gani juu ya sehemu inayobaki ya hotuba ya Yesu? Je! ungefurahia kuichunguza zaidi?
Matoleo ya Mnara wa Mlinzi yanayokuja yatatoa mfuatano wa makala yakieleza Mahubiri ya Mlimani yote. Sababu gani usijitayarishe ili ufaidike kabisa kutokana na habari hii kwa kusoma mahubiri hayo yote kwa uangalifu sasa au mapema iwezekanavyo? Yasome kwa uangalifu. Yatafakari aliyoyasema Yesu. Nawe utaona kwamba kufanya hivyo ni jambo linalopendeza sana.