Sura 35
Mahubiri Yenye Sifa Zaidi ya Yote Yaliyopata Kutolewa
MANDHARI yenyewe ni moja ya zile zinazokumbukika zaidi katika historia ya Biblia: Yesu ameketi kando ya mlima, akitoa Mahubiri yake ya Mlimani yaliyo na sifa sana. Mahali penyewe ni karibu na Bahari ya Galilaya, labda karibu na Kapernaumu. Baada ya kutumia usiku kucha akisali, ndipo tu Yesu amechagua 12 wa wanafunzi wake wawe mitume. Kisha, akiwa pamoja nao wote, aja chini kwenye mahali hapa penye usawa mlimani.
Kufikia sasa, ungefikiri, Yesu angekuwa amechoka sana na angetaka kupata usingizi kiasi fulani. Lakini umati mkubwa umekuja, baadhi yao kutoka mbali sana Yudea na Yerusalemu, zapata kilometa 100 hadi 110. Wengine wametoka pwani ya Tiro na Sidoni yaliyoko kaskazini. Wamekuja ili wamsikie Yesu na waponywe magonjwa yao. Hata kuna watu wanaosumbuliwa na roho waovu, wale malaika waovu wa Shetani.
Yesu anapoteremka, wagonjwa wanamkaribia wamguse, naye anawaponya wote. Baadaye, inaonekana Yesu anapanda kwenda mahali pa juu zaidi mlimani. Akiwa hapo aketi chini na kuanza kufundisha umati uliotapakaa mahali pale penye usawa mbele yake. Na ebu wazia! Sasa hakuna hata mtu mmoja kati ya wasikilizaji wote anayesumbuliwa na udhaifu mkubwa!
Watu wana hamu nyingi ya kumsikia mwalimu huyu anayeweza kufanya miujiza hiyo ya kustaajabisha. Lakini, Yesu anatoa mahubiri yake hasa kwa manufaa ya wanafunzi wake, ambao labda ndio walio karibu zaidi naye wakiwa wanamzunguka. Lakini ili sisi tuweze kunufaika pia, Mathayo na Luka pia wameyaandika mahubiri hayo.
Masimulizi ya Mathayo ya mahubiri hayo yana urefu ulio karibu mara nne ya yale ya Luka. Zaidi ya hilo, Luka anaonyesha visehemu fulani vya mambo yaliyoandikwa na Mathayo kuwa vilisemwa na Yesu katika wakati mwingine wa huduma yake, kama inavyoweza kuonekana kwa kulinganisha Mathayo 6:9-13 na Luka 11:1-4, na Mathayo 6:25-34 na Luka 12:22-31. Hata hivyo jambo hilo halipasi kushangaza. Ni wazi kwamba Yesu alifundisha mambo yale yale zaidi ya mara moja, na Luka alichagua kuyaandika mengine ya mafundisho hayo katika kikao tofauti.
Kinachofanya mahubiri ya Yesu yawe ya thamani sana si kina tu cha mambo ya kiroho yaliyomo, bali pia ni urahisi na uwazi aliyoutumia kueleza kweli hizo. Yeye atumia maono ya kawaida na mambo yaliyojulikana sana na watu, hivyo akifanya mawazo yake yaeleweke kwa urahisi na wote wanaotafuta maisha bora katika njia ya Mungu.
Ni Nani Wenye Furaha Kikweli?
Kila mtu hutaka kuwa na furaha. Akitambua hivyo, Yesu aanza Mahubiri yake ya Mlimani kwa kueleza wale ambao ni wenye furaha kikweli. Kama tuwezavyo kuwazia, jambo hilo lanasa mara hiyo usikivu wa wasikilizaji wake wengi sana. Na bado maneno yake ya kufungua lazima yaonekane kwa wengi kuwa yenye kupinganisha.
Akielekeza maelezo yake kwa wanafunzi wake, Yesu aanza hivi: ‘Wenye furaha ni nyinyi maskini, kwa sababu ufalme wa Mungu ni wenu. Wenye furaha ni nyinyi mnaoona njaa sasa, kwa sababu mtajazwa. Wenye furaha ni nyinyi mnaolia sasa, kwa sababu mtacheka. Wenye furaha ni nyinyi wakati wowote watu wanapowachukia . . . Furahini siku hiyo na kuruka-ruka, kwa maana, tazameni! Thawabu yenu ni kuu katika mbingu.’
Hayo ni masimulizi ya Luka ya utangulizi wa mahubiri ya Yesu. Lakini kulingana na maandishi ya Mathayo tu, Yesu asema pia kwamba wapole, wenye rehema, walio safi moyoni, na wenye kuamanika ni wenye furaha. Yesu asema kwamba wao ni wenye furaha kwa sababu watairithi dunia, wataonyeshwa rehema, watamwona Mungu, na wataitwa wana wa Mungu.
Lakini analomaanisha Yesu juu ya kuwa wenye furaha si kufanya shangwe wala kucheka-cheka, kama wakati mtu anapokuwa na mambo ya kumfurahisha. Furaha ya kweli ina kina kirefu zaidi, ina wazo la kuridhika, mtu kujisikia ametosheka na anatimiza mambo maishani.
Hivyo Yesu aonyesha kwamba wale wenye furaha kweli kweli ni watu wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, wanaosikitishwa na hali yao yenye dhambi, na wanaopata kumjua Mungu na kumtumikia. Basi, hata kama wakichukiwa au kunyanyaswa kwa kufanya mapenzi ya Mungu, wao ni wenye furaha kwa sababu wanajua wanapendeza Mungu na watapokea thawabu yake ya uhai wa milele.
Lakini, wengi wa wasikilizaji wa Yesu sawa na watu fulani leo wanaamini kwamba kuwa tajiri, mwenye ufanisi, na kufurahia anasa ndiyo mambo yanayomfanya mtu awe mwenye furaha. Yesu ajua jambo tofauti na hilo. Akionyesha tofauti ambayo lazima iwe yashangaza wengi wa wasikilizaji wake, yeye anasema:
“Ole wenu ninyi mlio na mali, kwa kuwa faraja yenu mmekwisha kuipata. Ole wenu ninyi ambao mmeshiba sasa, kwa kuwa mtaona njaa. Ole ninyi mnaocheka sasa, kwa kuwa mtaomboleza na kulia. Ole, wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo.”
Yesu amaanisha nini? Kwa sababu gani kuwa na mali, kufuatia anasa kwa kucheka, na kufurahia sifa za wanadamu kunaleta ole? Ni kwa sababu wakati mtu anapokuwa na vitu hivyo na kuvithamini sana, utumishi kwa Mungu, ambao ndio pekee unaoleta furaha ya kweli, unaondolewa katika maisha yake. Wakati ule ule, Yesu hakumaanisha kwamba kuwa tu maskini, mwenye njaa, na mwenye kuomboleza ndiko kunafanya mtu awe mwenye furaha. Lakini, mara nyingi watu hawa wenye hali za shida wanaweza kuitikia mafundisho ya Yesu, na kwa njia hiyo wao wanabarikiwa kupata furaha ya kweli.
Ndipo, akiambia wanafunzi wake, Yesu anasema: “Ninyi ni chumvi ya dunia.” Bila shaka, yeye hamaanishi kwamba wao kwa halisi ni chumvi. Bali chumvi inahifadhi vitu. Rundo kubwa la chumvi liliwekwa karibu na madhabahu kwenye hekalu la Yehova, na makuhani wenye kusimamia shughuli zilizoendeshwa humo waliitumia kuyakoleza matoleo.
Wanafunzi wa Yesu ni “chumvi ya dunia” katika maana ya kwamba wao wanakuwa na matokeo yenye hifadhi juu ya watu. Kwa kweli, ujumbe wanaochukua utahifadhi maisha za wote watakaouitikia! Utaingiza katika maisha za watu hawa sifa za udumifu, ushikamanifu na uaminifu, uzuie kuoza kokote kwa kiroho na kiadili ndani yao.
“Nyinyi ni nuru ya ulimwengu,” Yesu awaambia wanafunzi wake. Taa haiwekwi chini ya kikapu bali inawekwa juu ya kinara cha taa, kwa hiyo Yesu anasema: “Vivyo hivyo nuru yenu na ingaze mbele ya watu.” Wanafunzi wa Yesu wanafanya hivyo kwa ushahidi wao wa peupe, pia kwa kutumikia wakiwa vielelezo vyenye kung’aa vya mwenendo unaopatana na kanuni za Biblia.
Kiwango cha Juu kwa Wafuasi Wake
Viongozi wa kidini wamwona Yesu kuwa mvunjaji wa Sheria ya Mungu na hivi majuzi hata wametunga hila ya kumwua. Kwa hiyo Yesu anapoendelea na Mahubiri yake ya Mlimani, yeye aeleza hivi? “Msidhani yakuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza.”
Yesu aiheshimu sana Sheria ya Mungu na awatia wengine moyo wawe na heshima hiyo pia. Kwa kweli, yeye asema: “Mtu ye yote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni,” ikimaanisha kwamba mtu kama huyo hangeingia katika Ufalme huo hata kidogo.
Badala ya kupuuza Sheria ya Mungu, Yesu alaumu sana hata mielekeo inayofanya mtu aivunje. Baada ya kutaja kwamba Sheria inasema, “usiue,” Yesu aongeza hivi: “Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu.”
Kwa kuwa kuendelea kuonea hasira mtu aliye mshirika ni jambo zito sana hivyo, labda hata likiongoza kwenye uuaji, Yesu atoa kielezi cha kuonyesha ni kwa kadiri gani mtu apaswa kujitahidi ili apate amani. Yeye aagiza: “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.”
Akigeuza fikira zake kuelekea ile ya saba kati ya zile Amri Kumi, Yesu aendelea kusema: “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini.” Lakini, Yesu alaumu sana hata ule mwelekeo wenye kuendelea kuelekea uzinzi. “Mimi nawaambia Kila mtu atazamaye [anayeendelea kutazama] mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.”
Hapa Yesu hasemi juu ya wazo la ukosefu wa adili la kitambo tu, bali juu ya ‘kuendelea kutazama.’ Kuendelea kutazama hivyo kunaamsha nyege, ambazo zinaweza kufikia upeo wa kufanya uzinzi ikiwa nafasi inatokea. Mtu aweza kuzuiaje jambo hilo lisitokee? Yesu aonyesha jinsi kuchukua hatua zaidi huenda kukahitajiwa, akisema: “Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe . . . Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe.”
Mara nyingi watu wanakuwa na nia ya kujinyima mkono au mguu halisi ulio na ugonjwa ili waokoe maisha zao. Lakini kulingana na Yesu, ni jambo la maana hata zaidi ‘kutupa’ kitu chochote, hata kitu kilicho cha thamani kubwa sana kama jicho au mkono, ili kuepuka mawazo na matendo ya ukosefu wa adili. Ama sivyo, Yesu aeleza kwamba, watu kama hao watatupwa ndani ya Gehena (rundo la takataka zenye kuchomeka karibu na Yerusalemu), ambayo inafananisha uharibifu wa milele.
Yesu azungumzia pia jinsi ya kushughulika na watu wanaoumiza na kuudhi wengine. “Msishindane na mtu mwovu,” ndilo shauri lake. “Lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili.” Yesu hamaanishi kwamba mtu hapaswi kujikinga yeye mwenyewe au jamaa yake ikiwa wanashambuliwa. Kofi halitupwi ili kuumiza mwingine kimwili, bali, ili kuchokoza. Kwa hiyo, analosema Yesu ni kwamba mtu yeyote akijaribu kuchochea pigano au ubishi, ama kwa kupiga kofi halisi kwa mkono uliofumbuliwa ama kwa kuchoma sana mtu kwa maneno yenye kuumiza, lingekuwa kosa kulipa kisasi.
Baada ya kuelekeza fikira kwenye sheria ya Mungu juu ya kupenda jirani, Yesu ataarifu hivi: “Lakini, mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi.” Akitoa sababu yenye nguvu ya kufanya hivyo, yeye anaongeza hivi: “[Hivyo] mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema.”
Yesu anamalizia kisehemu hicho cha mahubiri yake kwa kutoa onyo hili la upole: “Ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” Yesu hamaanishi kwamba watu wanaweza kuwa wakamilifu katika maana ya kabisa kabisa. Bali, kwa kuiga Mungu wanaweza kupanua upendo wao utie ndani hata adui zao. Masimulizi ya Luka yanayolingana na hayo yana kumbukumbu hili la maneno ya Yesu: “Iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma.”
Sala, na Kumtumaini Mungu
Yesu anapoendelea na mahubiri yake, alaumu vikali unafiki wa watu wanaojionyesha kuwa wanatii Mungu. “Utoapo sadaka,” yeye asema, “usipige pande mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo.”
“Tena,” Yesu anaendelea kusema, “msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu.” Bali, yeye aagiza: “Wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini.” Yesu mwenyewe alitoa sala peupe, kwa hiyo kwa kusema hivyo halaumu hizo. Yeye alaumu vikali sala zinazosemwa ili kuvutia wasikilizaji na kuwafanya wasifu mtu.
Yesu anaendelea kushauri hivi: “Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa.” Yesu hamaanishi kwamba kurudia pekee ni kubaya. Wakati mmoja yeye mwenyewe alirudia-rudia kutumia “neno lile lile” alipokuwa akisali. Lakini jambo ambalo yeye anakataa ni kusema vifungu vya maneno yaliyokaririwa moyoni ‘tena na tena,’ kama wanavyofanya wale wenye kuhesabu-hesabu shanga kwa vidole vyao wanaporudia-rudia sala zao walizokariri.
Ili kusaidia wasikilizaji wake kusali, Yesu atoa sala ya kielelezo inayotia ndani maombi saba. Yale matatu ya kwanza yanatoa kwa kufaa utambuzi kwa enzi kuu ya Mungu na makusudi yake. Hayo ni maombi ya kwamba jina la Mungu litakaswe, Ufalme wake uje, na mapenzi yake yafanywe. Yale manne yaliyobaki ni maombi ya mambo ya kibinafsi, yaani, chakula cha kila siku, kusamehewa dhambi, kutokushawishwa kupita kadiri ya uvumilivu wa mtu, na kuokolewa na mwovu.
Akiendela, Yesu ataja mtego wa kukazia isivyofaa mali za kimwili. Yeye ahimiza hivi: “Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba.” Si kwamba hazina hizo zinaweza kuharibika tu bali pia hazisitawishi ustahili mbele za Mungu.
Kwa sababu hiyo, Yesu asema: “Bali, jiwekeeni hazina mbinguni.” Jambo hilo linafanywa kwa kuweka utumishi wa Mungu kwanza katika maisha yako. Hakuna mtu anayeweza kuondoa ustahili uliokusanywa kwa wingi hivyo mbele za Mungu wala thawabu bora. Halafu Yesu anaongezea hivi: “Hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.”
Akiendelea kuutaja mtego wa kufuatia vitu vya kimwili, Yesu atoa kielezi hiki: “Taa ya mwili ni jicho; Basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru. Lakini jicho lako likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza.” Jicho linalofanya kazi kwa kufaa linakuwa kwa mwili kama taa iliyowashwa mahali penye giza. Lakini ili lione kwa usahihi, ni lazima jicho liwe rahisi, yaani, ni lazima litazame kitu kimoja. Jicho lisilotazama mahali pamoja linaongoza kwenye kukadiria mambo kimakosa, kwenye kutanguliza shughuli za kimwili mbele ya utumishi kwa Mungu, na matokeo ni “mwili” mzima kuwa na giza.
Yesu afikisha jambo hilo kwenye upeo kwa kielezi hiki chenye mkazo mwingi: “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kutumikia Mungu na Mali.”
Baada ya kutoa shauri hilo, Yesu ahakikishia wasikilizaji wake kwamba hawahitaji kuwa na wasiwasi juu ya mahitaji yao ya kimwili ikiwa wanaweka utumishi wa Mungu kwanza. “Waangalieni ndege wa angani,” yeye asema, “ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao.” Ndipo auliza: “Ninyi je! si bora kupita hao?”
Halafu Yesu aelekeza kwenye maua ya mashamba na kusema kwamba “hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. Basi,” yeye aendelea kusema, “ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, . . . je! hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba?” Basi Yesu amalizia hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, ‘Tule nini?’ au ‘Tunywe nini?’ au ‘Tuvae nini?’ . . . Kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na yote hayo mtazidishiwa.”
Njia ya Uhai
Njia ya uhai ni ile ya kufuata sana mafundisho ya Yesu. Lakini si jambo rahisi kufanya hivyo. Kwa kielelezo, Mafarisayo wana maelekeo ya kuhukumu wengine vikali, na inaonekana sana kwamba watu wengi wanawaiga. Kwa hiyo Yesu aendelezapo Mahubiri yake ya Mlimani, yeye aonya hivi: “Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi. Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa.”
Ni hatari kufuata uongozi wa Mafarisayo wenye kulaumu watu kupita kiasi. Kulingana na masimulizi ya Luka, Yesu atoa kielezi juu ya hatari hiyo kwa kusema: “Je! aliye kipofu aweza kuongoza kipofu? Hawatatumbukia shimoni wote waili?”
Kulaumu-laumu wengine mno, kukuza makosa yao na kuwaonea, ni kosa kubwa. Kwa hiyo Yesu auliza: “Utamwambiaje nduguyo, Niache nikitoe kibanzi katika jicho lako; na kumbe! mna boriti ndani ya jicho lako mwenyewe? Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako.”
Hilo halimaanishi kwamba wanafunzi wa Yesu hawapaswi kutumia utambuzi wowote kuhusiana na watu wengine, kwa maana yeye anasema: “Msiwapee mbwa kilicho kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe.” Kweli zinazotoka katika Neno la Mungu ni takatifu. Ziko kama lulu za mfano. Lakini ikiwa watu fulani mmoja mmoja, walio kama mbwa au nguruwe, hawaonyeshi uthamini wowote kwa kweli hizo zenye thamani kubwa, wanafunzi wa Yesu wanapaswa kuwaacha watu hao wakatafute wale wenye kuitikia zaidi.
Ingawa Yesu amezungumza juu ya sala mapema katika Mahubiri yake ya Mlimani, sasa akazia uhitaji wa kudumu katika sala. “Ombeni,” yeye ahimiza, “nanyi mtapewa.” Kutoa kielelezo cha utayari wa Mungu kujibu sala, Yesu auliza: “Kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akiomba mkate, atampa jiwe? . . . basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?”
Ndipo Yesu anapotoa ile ambayo imekuwa kanuni ya mwenendo inayojulikana na wengi kuwa Kanuni Bora. Yeye asema: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” Kuishi kulingana na kanuni hiyo kunatia ndani kuchukua hatua ya uhakika katika kufanyia wengine mema, kuwatendea kama vile unavyotaka utendewe.
Kwamba njia ya uhai si rahisi inafunuliwa na maagizo ya Yesu: “Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango i mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.”
Hatari ya kupotezwa ni kubwa, kwa hiyo Yesu aonya: “Jihadharini na manabii wa uwongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali.” Kama vile miti myema na mibaya inavyoweza kutambuliwa kwa matunda yayo, Yesu asema, manabii wa uwongo wanaweza pia kutambuliwa kwa mwenendo na mafundisho yao.
Akiendelea, Yesu aeleza kwamba si yale tu anayosema mtu yanayomfanya awe mwanafunzi Wake bali ni yale anayotenda. Watu fulani wanadai kwamba Yesu ndiye Bwana wao, lakini ikiwa wao hawatendi mapenzi ya Baba yake, yeye asema: “Nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.”
Mwishowe, Yesu autoa ule umalizio wa mahubiri yake wenye kukumbukika. Asema: “Kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba.”
Kwa upande ule mwingine, Yesu atangaza hivi: “Kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.”
Yesu anapomaliza mahubiri yake, umati unashangazwa sana na njia yake ya kufundisha, kwa maana yeye awafundisha kama mtu mwenye mamlaka wala si kama viongozi wao wa kidini. Luka 6:12-23, NW; Mathayo 5:1-12; Luka 6:24-26; Mathayo 5:13-48; 6:1-34; 26:36-45; 7:1-29; Luka 6:27-49.
▪ Yesu yuko wapi anapotoa mahubiri yake yenye kukumbukika zaidi, ni nani waliopo, na ni jambo gani ambalo ndipo tu limetukia kabla ya yeye kuyatoa?
▪ Kwa nini haishangazi kwamba Luka anaandika baadhi ya mafundisho ya mahubiri hayo katika kikao kingine?
▪ Ni jambo gani linalofanya mahubiri ya Yesu yawe yenye thamani sana?
▪ Ni nani walio wenye furaha kweli kweli, na kwa nini?
▪ Ni nani wanaopokea ole, na kwa nini?
▪ Ni kwa njia gani wanafunzi wa Yesu ni “chumvi ya dunia” na “nuru ya ulimwengu”?
▪ Yesu aonyeshaje kwamba aiheshimu sana Sheria ya Mungu?
▪ Yesu atoa mafundisho gani ili kung’oa visababishi vya uuaji na uzinzi?
▪ Yesu amaanisha nini anaposema juu ya kugeuza shavu lile jingine?
▪ Tunawezaje kuwa wakamilifu kama vile Mungu alivyo mkamilifu?
▪ Yesu atoa mafundisho gani juu ya sala?
▪ Kwa nini hazina za kimbingu ni bora, nazo zinapatikanaje?
▪ Ni vielezi gani vinavyotolewa kusaida mtu aepuke kufuatia vitu vya kimwili?
▪ Kwa nini Yesu asema hakuna uhitaji wa kuwa na wasiwasi?
▪ Yesu asema nini juu ya kuhukumu wengine, na hata hivyo alionyeshaje kwamba wanafunzi wake wahitaji kutumia utambuzi kuhusu watu?
▪ Yesu azidi kusema nini kuhusu sala, naye atoa kanuni gani ya mwenendo?
▪ Yesu aonyeshaje kwamba njia ya uhai haingekuwa rahisi na kwamba kuna hatari ya kupotezwa?
▪ Yesu amaliziaje mahubiri yake, nayo yawa na matokeo gani?