Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 11/1 kur. 7-11
  • Mathayo Atangaza: ‘Masihi Amekuja!’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mathayo Atangaza: ‘Masihi Amekuja!’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SEHEMU ZENYE KUTOKEZA
  • MAHUBIRI YA MATHAYO JUU YA MASIHI
  • SIKU ZA KUMALIZIA ZA HUDUMA YA YESU
  • Kitabu Cha Biblia Namba 40—Mathayo
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Kitabu Cha Biblia 42—Luka
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Yesu Kristo—Ufunguo Uongozao Kwenye Ujuzi Juu ya Mungu
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 11/1 kur. 7-11

Mathayo Atangaza: ‘Masihi Amekuja!’

NI NINI yaliyokuwa matukio ya maana zaidi kutokea katika historia ya wanadamu? Bila shaka lo lote, yalikuwa ni kuzaliwa, huduma, kifo, ufufuo na kupaa mbinguni kwa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu.

Kwa kupatana na kanuni ya kimungu kwamba “kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno litathibitishwa,” Yehova Mungu alihakikisha kwamba masimulizi manne ya maisha ya Yesu Kristo yaliandikwa ili kuthibitisha ukweli wa matukio hayo. (Kumbukumbu la Torati 17:6; 2 Wakorintho 13:1) Hao watu wanne ambao Yeye alitumia walikuwa ni Mathayo, Marko, Luka na Yohana. Imeonekana kwamba kati ya waandikaji hao wanne kila mmoja wao ana kichwa chake mwenyewe cha habari, kusudi lake mwenyewe, anaonyesha utu wake mwenyewe na anawakumbuka wasomaji wake wa karibu.

Juu ya Mathayo, wa kwanza wa waandikaji hao, tunajua machache. Lakini, tunaweza kukata maneno kwamba yeye alikuwa mtu mnyenyekevu, kwa maana ni kutokana na masimulizi yake tu tunajifunza kwamba yeye alikuwa mtoza kodi aliyedharauliwa. (Mathayo 9:9) Na haishangazi kwamba watoza ushuru walidharauliwa! Sababu moja ni kwamba, wao waliwakilisha kongwa la Waroma ambalo lilitoza kodi nyingi sana! Zaidi ya hilo, walikuwa na sifa mbaya sana ya kutumia vibaya madaraka yao, walikuwa wanyang’anyi. Maneno ya mtoza ushuru Zakayo yanaonyesha hilo. Baada ya Yesu kuja nyumbani mwake, Zakayo alifanya badiliko la moyoni, na kusema: “Ikiwa nimenyang’anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne.” (Luka 19:8) Lakini inaonekana hakuna shaka kwamba Mathayo alikuwa mtoza kodi mwenye moyo mnyofu; ama sivyo Yesu hangemwalika toka pale pale kazini pake awe mfuasi Wake.

Tangu huk-o-o nyuma wakati wa kutokutii kwa Adamu katika Edeni, Yehova Mungu, katika usemi wa fumbo, alikuwa ametabiri kuja kwa Masihi, kwa kumtaja kuwa “uzao” wa mwanamke. Na mapema sana wakati wa Mfalme Daudi huyo alitajwa kuwa ni “masihi” (mpakwa mafuta, NW) wa Mungu. Nabii Danieli hasa alitabiri juu ya kuja kwa Masihi. (Mwanzo 3:15; 22:17, 18; Zaburi 2:2; Danieli 9:24-27) Zilikuwa habari zenye kusisimua kwamba yule Masihi aliyekuwa ametazamiwa kwa muda mrefu alikuwa amefika hata kwamba Mathayo hakupoteza wakati kutangaza jambo hilo kupitia Injili yake. Kutokana na ushuhuda bora zaidi uliopo, inaonekana sana huenda akawa aliandika masimulizi yake mapema kama mwaka 41 W.K.

SEHEMU ZENYE KUTOKEZA

Ni wazi sana kwamba Mathayo alikusudia masimulizi yake ya Injili yaunganishe matukio yaliyoandikwa katika Maandiko ya Kiebrania na yale yanayohusu maisha ya Masihi. Kulingana na ushahidi wa wanahistoria wa kanisa wa kwanza, Mathayo, kwanza aliiandika katika Kiebrania na baadaye akafanya nakala ya Injili yake katika Kigiriki. Wenye kuunga mkono jambo hilo ni uhakika wa kwamba mitajo yake yote kutoka katika Maandiko ya mapema zaidi si kutoka Septuagint Version ya Kigiriki, kama ilivyo kawaida ya wale waandikaji wengine wa Injili, bali ni kutoka maandiko ya Kiebrania. Na kupatana na kichwa chake cha habari kwamba Yesu Kristo alikuwa ndiye Masihi aliyetabiriwa kweli kweli, Mathayo kuwapita wengine, anaonyesha jinsi maisha ya Yesu na matendo yake yalivyotimiza unabii wa Biblia. (Linganisha Mathayo 8:16, 17 na Marko 1:34 na Luka 4:40.) Vilevile, zaidi ya waandikaji wengine wa Injili, Mathayo alikazia kichwa cha habari ya “ufalme wa mbinguni,” na kwa sababu hiyo, yake imeitwa “Injili ya Ufalme.”​—Mathayo 4:17; 5:3; 11:12; 22:2.

Kazi ya awali (kwanza) ya Mathayo akiwa mtoza kodi inajionyesha kote katika uandikaji wake. Kwanza, yeye alithamini sana fadhili zisizostahilika nyingi sana alizoonyeshwa akiwa mtoza kodi ili awe mtume wa Masihi. Kwa hiyo yeye tofauti na wengine tunaona ameandika mkazo wa Yesu wa uhakika wa kwamba rehema inahitajiwa wala si dhabihu peke yake. Inavutia kwamba ni Mathayo peke yake anayetupa yale maneno ya Yesu yenye kufariji yanayoanza na mwaliko, “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.”​—Mathayo 9:9-13; 11:28-30; 12:7; 18:21-35.

Kukaza fikira kwa Mathayo juu ya tarakimu kunaonyesha pia yeye alikuwa mtoza kodi. Ni yeye peke yake anayetuambia kwamba Yuda alimsaliti Yesu kwa ajili ya vipande 30 vya fedha. (Mathayo 26:15) Zaidi ya hayo, mahali ambako wale wengine walitaja kitu kimoja au kusema mambo kama kitu kimoja, Mathayo anataja mambo waziwazi na kutaja viwili au kusema mambo kwa wingi. (Linganisha Mathayo 4:3; 8:28; 20:29, 30 na Marko 5:2; 10:46, 47; Luka 4:3; 8:27; 18:35-38.) Kwa kweli, inaonekana Mathayo alikuwa anapenda nambari. Kwa hiyo katika sura ya sita twaona ameandika maombi saba katika Sala ya Kielelezo (kulinganisha na yale tano ya Luka), mifano saba katika sura ya 13, na ole saba alizozisema Yesu juu ya viongozi wa kidini Wayahudi wa siku zake katika sura ya 23. Na Mathayo anagawanya nasaba ya Yesu kuwa vikundi vitatu vya watu 14.​—Mathayo 1:1-17.

Sehemu zenye kutokeza za Injili ya Mathayo vilevile zinaonekana wazi tunapoangalia jinsi masimulizi yake yanavyokamilisha yale ya Luka. Hilo ni jambo la kutazamiwa tunapofikiria jinsi kuwaza kwa mtoza kodi kulivyo tofauti na kule kwa daktari. Wala hatuwezi kusahau sehemu iliyotimizwa na roho takatifu katika jambo hilo. Halafu, pia, Mathayo alikuwa akiandika ili awasadikishe Wayahudi waaminifu kwamba Yesu alikuwa ndiye yule Masihi aliyeahidiwa tangu zamani, hali Luka anaonyesha Yesu kuwa Mwokozi wa wanadamu wote. Kwa hiyo Mathayo anaonyesha nasaba ya Yesu kurudi mpaka Ibrahimu kupitia Daudi, ambapo Luka anaionyesha kurudi mpaka ‘Adamu mwana wa Mungu.’ (Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-38, NW) Kwa wazi Mathayo anafuatisha nasaba ya Yesu ya halali kupitia baba-mlezi wake, Yusufu, ambapo, Luka anaifuatisha kupitia nasaba ya asili ya mama Yake, Mariamu. Mathayo ameandika kwamba malaika alimtokea Yusufu, baba mlezi wa Yesu. Luka anasimulia juu ya malaika Gabrieli akimtokea Mariamu, mama ya Yesu. Vivyo hivyo, Mathayo anatuambia juu ya wanajimu wakija kumtembelea mtoto Yesu, “mfalme wa Wayahudi,” na kumletea zawadi za bei kubwa, ambapo Luka anatuambia juu ya wachungaji wa cheo cha chini wakialikwa waje kumwona Mwokozi aliyetoka kuzaliwa.

MAHUBIRI YA MATHAYO JUU YA MASIHI

Katika kuandika juu ya maisha ya Yesu, Mathayo hakukosa kutumia hata nafasi moja kuthibitisha kwamba kweli kweli Yesu alikuwa Masihi aliyetabiriwa. Alifanyaje hivyo? Kwa kuyataja Maandiko ya Kiebrania mara 100 hivi ili kuunga mkono kichwa chake cha habari. Kwa mfano, anapofasili (anapotoa maelezo kwa urefu) juu ya kuzaliwa kwa Yesu yeye anakazia kwamba kuzaliwa kwa Yesu na bikira Myahudi Mariamu kulikuwa ni utimizo wa unabii. (Isaya 7:14; Mathayo 1:21-23) Akiandika juu ya kimbio la Yusufu na jamaa yake ili kuepuka amri ya Mfalme Herode ya kutaka kuua, Mathayo anaonyesha kwamba jambo hilo lilikuwa hivyo ili andiko litimizwe: “Nikamwita mwanangu atoke Misri.” (Hosea 11:1; Mathayo 2:14, 15) Huzuni iliyoletwa na agizo la Herode kwamba watoto wote wavulana wa miaka miwili kurudi chini katika Bethlehemu na majimbo yake, kama anavyoonyesha Mathayo, vilevile ilikuwa imetabiriwa.​—Yeremia 31:15; Mathayo 2:16-18.

Katika sura za tatu na nne Mathayo anaarifu juu ya mtangulizi wa Yesu, Yohana Mbatizaji, anaeleza juu ya Yesu akibatizwa naye na juu ya Mungu mwenyewe akikubali kwamba Yesu ni Mwanaye. Halafu linafuata lile jaribu lenye sehemu tatu juu ya Yesu jangwani na Yesu kuanza huduma yake ya kuhubiri “ufalme wa mbinguni umekaribia,” wakati uo huo akifanya miujiza mingi ya kuponya. Kuhubiri kwa Yesu kunaonyeshwa kuwa ni utimizo mwingine wa unabii.​—Isaya 9:1, 2; Mathayo 4:13-17.

Mathayo hajaribu sana kueleza jinsi matukio yalivyotokea kulingana na wakati, isipokuwa katika sura zake 10 za mwisho. Kwa kuwa Mahubiri ya Mlimani ya Yesu ni fundisho lenye kutokeza sana, Mathayo anayasimulia mara tu akiisha kueleza juu ya mwanzo wa huduma ya Yesu, ingawa kwa kweli Yesu aliyatoa mwaka mmoja hivi baadaye. Hakuna shaka kwamba hayo ndiyo mahubiri makuu zaidi yaliyopata kuhubiriwa, na Mathayo anatupa ripoti kamili kabisa juu yayo. Yanaanza na zile “furaha” tisa zenye kufariji kweli kweli watu wote wenye kupenda ile kweli na uadilifu. Bila maelezo mengi, na iangaliwe kwamba hizo ni “furaha,” wala si “baraka” (“heri, Union Version). Kwa sababu hiyo The Jerusalem Bible na Today’s English Version zinatumia “furaha” badala ya “baraka” (“heri”), sawa na New World Translation.

Kuhusu Mahubiri ya Mlimani, inaripotiwa kwamba Mahatma Gandhi alimwambia hivi aliyekuwa mtawala mdogo wa India, Lord Irwin: “Wakati nchi yako na yangu zitakapoungana pamoja katika mafundisho yaliyotolewa na Kristo katika Mahubiri ya Mlimani, tutakuwa tumetatua matatizo ya ulimwengu wote, wala si yale ya nchi zetu tu.” Vilevile Mahubiri hayo yana ile kanuni ya kutendea wengine kama unavyotaka utendewe. Kwa kupatana na kichwa cha habari cha Mathayo, yeye anaeleza kwamba Yesu hakuwa amekuja kuiharibu sheria ya Musa bali kuitimiza na kwa kweli Sheria na manabii walikuwa wakizungumza juu ya kanuni ya kutendea wengine kama unavyotaka utendewe.​—Mathayo 5:17; 7:12.

Inaonekana kwamba Mathayo alivutiwa sana hasa na mafundisho ya Yesu. Yakilinganishwa na zile Injili nyingine, si kwamba tu masimulizi yake ya Mahubiri ya Mlimani ni yenye maelezo mengi zaidi, bali pia ndivyo ilivyo ripoti yake juu ya Yesu kuwatuma mitume Wake 12 (sura ya 10), masimulizi yake ya ile mifano saba ya Ufalme (sura ya 13) na maandishi yake juu ya shauri la Yesu la uhitaji wa kuonyesha rehema, kuwa na nia ya kusamehe “mara sabini na saba” (NW).​—Sura ya 18.

Katika sura za 8, 9, 11, 12 na 14-17, Mathayo anaripoti hasa juu ya miujiza mingi ya Yesu kama vile akilisha watu 5,000 katika pindi moja na katika pindi nyingine akalisha “wanaume elfu nne, bila wanawake na watoto.” Vilevile sura hizo wanashutumiwa viongozi wa kidini Wayahudi waovu kwa kukusudia na wenye unafiki, ambao walikuwa wamefanya ile dhambi isiyo na msamaha. Zaidi ya hayo, katika sura hizo tunaona itikio la waziwazi la Petro “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai” na masimulizi ya kubadilika sura, ambako kwa mara nyingine Yehova Mungu alishuhudia Yesu Kristo kuwa ni Mwanaye kweli.​—Mathayo 16:16; 17:1-9.

SIKU ZA KUMALIZIA ZA HUDUMA YA YESU

Sasa tukifikia matukio ya kumalizia ya huduma ya Yesu, tunaona kwamba Mathayo ameandika kufuatana na utaratibu wa kutokea kwa mambo. Sehemu kubwa ya yale ambayo Mathayo alitangulia kuandika yalitukia katika Galilaya, lakini sasa anagusia kidogo juu ya huduma ya baadaye ya Yesu katika Perea. Viongozi wa kidini wanamtokezea Yesu utatizi juu ya talaka, wakitumaini watamwaibisha. Lakini, badala yake, wanashindwa kwa sababu ya hekima ya Yesu na maarifa yake mengi ya Maandiko: Msingi pekee wa talaka ni “uasherati.” Mtawala mmoja kijana ambaye ameridhika na alivyo anamjia Yesu akiuliza anayopaswa kufanya ili apate uzima wa milele, lakini anaenda zake akiwa na kadirio lililopunguzwa sana la wema wake mwenyewe, kwa maana kwake utajiri wake ulikuwa wa maana zaidi ya uzima wa milele. Roho ya mashindano inagawanya mitume wa Yesu, na kusababisha Yesu awakumbushe kwamba yeye alikuja, ‘si kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.’​—Mathayo 19:1–20:34.

Katika juma ya mwisho ya Yesu duniani akiwa mwanadamu, sehemu ya nchi inabadilika na kuwa Bethania na Yerusalemu, na tunasoma juu ya kuingia kwake katika mji huo kwa ushindi. Baada ya tukio hilo Yesu anaenda hekaluni na kulisafisha kwa kuwafukuza wapunjaji wote wa kidini. Halafu, anasimulia juu ya mfano unaohusu wale wakulima waliomwua mrithi wa shamba la mizabibu, na kuacha adui zake wajue kwamba yeye anafahamu yaliyo akilini mwao.​—Mathayo 21:1-46.

Ingawa walishindwa tena na tena katika mazungumzo yao yaliyotangulia pamoja na Yesu, wapinzani wake wa kidini kwa mara nyingine wanajaribu kumwaibisha kwa kumwuliza maulizo ya ujanja juu ya kodi ya Waroma isiyopendwa na watu wengi, juu ya ufufuo na juu ya amri iliyo kuu zaidi. Majibu yake ya hekima na ya Kimaandiko yanawanyamazisha. Kisha, Yesu alishauri wanafunzi wake juu ya uhitaji wa kuwa wanyenyekevu. Vilevile aliwakemea vikali wapinzani wake wa kidini wenye unafiki, akatangaza ole saba juu yao. Kwa sababu ya upinzani wao nyumba yao ingeachwa.​—Mathayo 22:1-23:39.

Mitajo ya mitume fulani wake juu ya uzuri mwingi sana wa hekalu la Herode inampa Yesu nafasi ya kutoa unabii wake mkuu juu ya mwisho wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi, na juu ya kurudi kwake, parousia yake, ambayo ni maneno yametimizwa kwa njia ya ajabu tangu 1914. Halafu anatoa mifano mitatu ambayo imetimizwa katika siku zetu, mfano wa wanawali wenye hekima na wapumbavu, wa talanta na wa kondoo na mbuzi.​—Mathayo 24:1-25:46.

Halafu Mathayo anatupa masimulizi ambayo yeye mwenyewe alijionea kwa macho, yaani, kuanzishwa kwa Chakula cha Jioni cha Bwana na Yesu katika kukikumbuka kifo chake. Akiendelea, Mathayo anasimulia yaliyompata Yesu katika Gethsemane, kukamatwa kwake, Petro kumkana, Kristo kufikishwa mahakamani, Pilato akisita na kusafisha mikono yake, halafu kutundikwa kwa Yesu katikati ya wahalifu wawili akiwa Mfalme wa Wayahudi juu ya kilima kinachojulikana kuwa Kalvari.​—Mathayo 26:1-75.

Yesu alipokamatwa mitume wake wote walitoroka, bila shaka walishuka moyo kwa sababu ya badiliko la ghafula la matukio. Lakini si kwa muda mrefu. Katika siku ya tatu wanajua juu ya kufufuliwa kwa Yesu kutoka kwa wafu. Baadaye, wanakutana na Yesu katika Galilaya, ambapo, bila shaka muda mfupi kabla hajapaa kwenda mbinguni, anawapa agizo la kuwaaga: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza . . . Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Mathayo 28:19, 20, NW.

Bila shaka, Mathayo anathibitisha kichwa chake cha habari kwamba Yesu wa Nazareti hakika ndiye Masihi, Mwana wa Mungu. Mathayo anafanya hivyo kwa kuelekeza kwenye unabii mwingi ambao Yesu alitimiza, kwenye miujiza ambayo Yesu alifanya na kwenye kweli zile alizofunza Yesu. Hakika Mathayo alikuwa na akili yenye makini na yenye kuthamini, yenye kufanywa chapuchapu na roho takatifu ya Mungu. Kwa sababu roho ya Mungu ilimwongoza na kumkumbusha mambo ambayo Yehova Mungu alitaka yaandikwe, yeye aliweza kuandika maandishi yenye kutia mambo mengi na yenye mkazo sana juu ya maisha ya Yesu.

Tunaweza kuwa wenye shukrani kama nini kwa Yehova Mungu kwamba Yeye aliongoza mtumishi wake huyo mnyenyekevu, mwenye moyo mnyofu na asiye na choyo na pia mfuasi wa Mwanaye aandike masimulizi hayo yenye kutia nguvu juu ya huduma ya kidunia ya Yesu! Na tufahamiane na masimulizi hayo kweli kweli ili tuweze kuishi kulingana na kanuni alizotoa Yesu na kuwaambia wengine katika kila nafasi “habari njema” kwamba Masihi aliyeahidiwa kwa muda mrefu amekwisha kuja katika wakati uliowekwa wa Mungu na kutimiza unabii mwingi ulioandikwa katika Maandiko ya Kiebrania.​—Mathayo 24:14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki