Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 6/15 kur. 267-270
  • Waaminifu Kwa Mungu Kujapokuwa na Mateso Makali

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waaminifu Kwa Mungu Kujapokuwa na Mateso Makali
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • KUSIMAMA IMARA
  • KUKIMBILIA ZAMBIA
  • HAKUNA KUKUBALIANA NA WATESI
  • UVUMILIVU CHINI YA JARIBU REFU
  • KUSIMAMA IMARA KUJAPOKUWA NA MATESO ZAIDI
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 6/15 kur. 267-270

Waaminifu Kwa Mungu Kujapokuwa na Mateso Makali

KWA mara ya nne katika miaka ya karibuni, Wakristo wanyofu wanateswa vikali katika nchi ya Afrika ya Malawi. Kama ilivyoripotiwa katika Mnara wa Mlinzi wa Mei 15, maelfu ya Mashahidi wa Yehova walioruhusiwa kuingia katika nchi ya Msumbiji iliyo jirani, mwaka wa 1972, baada ya mateso mabaya sana kutokea Malawi walirudishwa Malawi. Huko wamepatwa tena na ukatili mbaya sana, unyama.

Lakini mambo hayo hayawapati Wakristo hawa kwa sababu wanaasi sheria. Ulimwenguni mwote Mashahidi wa Yehova wanajulikana kuwa raia wenye kushika sana sheria. Ni kama vile alivyoandika Guy Wright katika gazeti Examiner la San Francisco: “Mnaweza kuwachukua kama raia bora. Wao hulipa kodi kwa bidii, huangalia wagonjwa, hujitahidi kuondoa hali ya kutojua kusoma na kuandika.” Tena inajulikana kwamba kati yao hakuna uvunjaji wa sheria, hongo wala ufisadi ulioenea sana duniani leo.

Lakini katika Malawi na kwingineko, Mashahidi wa Yehova huendelea kwa kupatana kuwa na msimamo wao wenye msingi wa Biblia wa kutokuwamo katika siasa. Yesu alisema hivi juu ya wafuasi wake, “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:14) Kwa hiyo, katika Malawi wao wamekataa kununua kadi za uanachama zinazotolewa na chama chenye kutawala kiitwacho Malawi Congress Party, nazo kadi hizo zina picha ya Rais wa Maisha wa Malawi, Dkt. H. Kamuzu Banda, mzee wa Presbyterian Church. Kukataa kufanya hivyo kumefanya wateswe vikali sana, baada ya fitina kuchochewa kwa wakuu wa serikali.

KUSIMAMA IMARA

Roho ya Mashahidi hao Wamalawi imewatia moyo sana wao wenyewe na pia ndugu na dada zao wa kiroho katika nchi nyingine. Wameuonyesha ulimwengu kwamba katika miaka hii ya 1970 hakika wako Wakristo wanaoendeleza imani yao katika Mungu bila kujali mateso makali yanayowapata.

Hiyo ilionyeshwa na maneno ya Mashahidi wengi Wamalawi waliosema hivi walipohojiwa: “Sisi hatutaacha kumwamini Mungu kamwe hata tukitishwa na kifo na washambuliaji hawa wakali.”

Shahidi mmoja mzee Mmalawi aliyehojiwa alisema hivi: “Twajua kwamba bila shaka Yehova ana kusudi la kuachilia mambo haya yatupate. Sisi tumekata maneno kufuatana naye mpaka kusudi lake litakapotimizwa.”

Mwenye kuchunguza alisema hivi: “Mashahidi wote, pamoja na watoto wao, walionekana wenye nguvu sana kiroho.” Pia, mwenye kuwahoji aliripoti kwamba waangalizi wao wa Kikristo “hawakuonyesha woga wa cho chote, bali walikuwa wamekata maneno kuendelea kufanya kazi yao ya uchungaji, hata kutokee nini.”

Lo! jinsi imani yao ilivyo ushuhuda kwa ulimwengu wote! Katika vizazi vyote vinavyokuja katika taratibu mpya ya Mungu, wakati matendo ya Wakristo wa kweli ya wakati huu wa mwisho yatakapokuwa yakisimuliwa, mwendo wao mwaminifu wa sasa utasifiwaje!

KUKIMBILIA ZAMBIA

Hivi majuzi, wakati makumi ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova waliokuwa wamekuwa wakiishi Msumbiji walirudishwa Malawi kwa nguvu, maelfu yao walikimbilia Zambia iliyo katika ujirani. Huko watoro hao walipiga kambi katika Sinda Misale katika wilaya ya Chipata, ambako makundi ya karibu ya Mashahidi wa Yehova yalipewa nafasi ya kuwapelekea vitu vya kuwasaidia, pamoja na chakula na dawa. Karibu watoro Mashahidi 4,800 walikuwa wamepiga kambi katika upande wa mashariki ya mbali ya jimbo la Zambia karibu na mpaka wa Malawi mpaka mwishoni mwa Oktoba.

Wenye kutembelea kambi hiyo walishangazwa na utendaji wa umoja na bidii uliokuwa ukiendelea humo. Mmoja wao alisema hivi: “Kulikuwa na kazi kila mahali. Ndugu wengine walikuwa wakitia alama sehemu za nchi ambako wenye kufika karibuni wangejenga vibanda vyao, huku wengine waliokuwa wamekwisha pewa mahali wakijenga kwa bidii. Sehemu ya kambi iliyokuwa imemalizwa ilikuwa malidadi na safi.”

Mtazamaji huyu aliwaona Mashahidi wengi pia​—⁠wanaume, wanawake na watoto wakubwa​—⁠wakiwa wametawanyika vichakani wakikata miti na majani ya kuezekea vibanda hivyo. Wanawake walikuwa wakikusanya udongo mweusi wa sakafu za vibanda vyao.

Mashahidi wa Yehova walipokuwa wakipakua vitu vya kusaidia, mkuu wa watoro aliyekuwa akisimamia kambi hiyo aliombwa maoni yake. Akasema hivi: “Mimi nimeshangazwa sana na watu hawa. Wao hufanya kazi kwa bidii sana hata hawahitaji kusimamiwa sana. Mimi nina hakika watu hawa wakipewa kipande cha nchi na kuagizwa wakilime, wanaweza kufanya kazi ya ajabu sana.”

Kazi ngumu na adabu zilionekana wazi pia katika clinic (kihospitali kidogo) kilichokuwa kimeanzishwa kambini. Humo, kikoa cha Mashahidi kiliangalia wagonjwa kwa kushirikiana na watumishi wa serikali ya Zambia wa mambo ya utabibu. Ilionekana kwamba Mashahidi waliokuwamo kambini walikuwa wenye nguvu na bidii sana, ingawa wengi wao walikuwa wamekonda kwa sababu walikuwa bila chakula vichakani kwa siku nyingi kabla ya kufika Sinda Misale.

HAKUNA KUKUBALIANA NA WATESI

Ripoti nyingi zilitolewa katika kambi ya Sinda Misale juu ya mateso waliyoteswa Mashahidi-watu-wazima na watoto wao pia na wakuu wa Malawi Congress Party, vijana na mapolisi.

Kwa mfano, Septemba 28, 1975, Mashahidi sita, wanaume na wanawake, walipelekwa kwenye tawi la Chimutu la Malawi Congress Party katika eneo la Lilongwe. Waliagizwa wanunue kadi za chama, lakini wote wakakataa. Ndipo Mashahidi hao walipofungwa kwa kamba na kupigwa kikatili.

Katika kijiji cha Mkochi, mwanamke Shahidi mzee alipigwa vibaya sana na vijana kwa sababu ya kukataa kununua kadi ya chama cha kisiasa. Mojawapo la meno yake liling’olewa alipokuwa akipigwa, akaachwa amezimia.

Shahidi mwingine mzee, wa kutoka kijiji cha Mambala, aliripoti kwamba alipofika nyumbani Agosti 26 kutoka Msumbiji akiwa na binti yake mja mzito, wakuu wa chama walidai kwamba wanunue kadi za kisiasa. Walipojua kwamba wanawake hao wawili wasingezinunua, waliwafukuza kijijini. Shahidi yule mzee pamoja na binti yake mja mzito waliendelea kulala nje ya kijiji chini ya mti.

Siku chache baadaye, ukafika wakati wa binti kuzaa mtoto. Mama akawaomba wanakijiji wamruhusu amwingize binti yake katika mojawapo ya nyumba azalie mtoto humo. Wanakijiji wote walikataa. Headman wa kijiji alimfanyia mzaha, akisema: “Mwite Mungu wako Yehova akupelekee ngazi ili umpeleke binti yako mbinguni akazalie huko.”

Mwanamke huyo kijana alizaa mtoto wake akiwa chini ya mti huku wanakijiji wakiwa wamesimama wakitazama. Mara tu baada ya mtoto kuzaliwa, headman wa kijiji pamoja na watu wake wakamfukuza mama mkubwa, akabaki binti yake na kitoto kipya chini ya mti.

Habari nyingi kama hizo zilisimuliwa na watoro katika kambi ya Sinda Misale. Hata hivyo, ripoti zote zilionyesha kwamba wenye kuteswa waliendelea kuwa imara. Ni kama vile mtazamaji mmoja alivyosema; “Mpaka wakati huo hawakuwa wamepokea ripoti hata moja ya kuonyesha wengine walikubaliana na madai ya watesi ingawa habari nyingi zilionyesha waliteswa kikatili ajabu.”

UVUMILIVU CHINI YA JARIBU REFU

Ripoti moja ilitoka kwa wanaume Mashahidi wanne ambao majuzi walikuwa wamefunguliwa jela katika Malawi. Wao, pamoja na Shahidi mwingine, walizuiwa gerezani mwaka mmoja na miezi mitano kabla ya kuletwa kesini Juni mwaka wa 1974. Wakati huo wote, waliteswa kwa njia nyingi kujaribu kuwafanya wakane imani yao katika Mungu. Walipigwa-pigwa vikali na kuulizwa-ulizwa maulizo na wakuu. Waliombwa watoe majina ya Wakristo wenzao, kama vile waangalizi wenye madaraka. Walakini, wao waliendelea kunyamaza, wasisaliti ndugu zao.

Halafu wakuu wa gereza wakaagizwa wasiwape Mashahidi hao watano chakula cho chote kwa siku tisa. Walifungiwa pia katika chumba chenye giza wasiruhusiwe kuona jua wala nuru kwa siku kumi na tisa. Kisha wakahamishwa kupelekwa kwenye kijumba kingine kichafu-chafu. Mmoja wa wanaume hao alikufa kwa sababu ya kutendwa hivyo, lakini hakukubaliana na madai ya watesi. Wale wengine saba walisema kwamba walisali kwa Yehova kwa shauku wakatiwa nguvu za kuvumilia jaribu hilo.

Wakati mmoja wakuu walikuja kwenye vijumba vya gereza wakaletea Mashahidi hao chakula. Lakini wakadai kwamba wasali kwa sauti kabla ya kula. Kwa sababu Mashahidi wa Yehova humshukuru Mungu nyakati za chakula, wakasali. Walakini, mara tu sala ilipokwisha wote walishtakiwa kuwa ‘wenye kuendesha shirika la haramu.’ Hiyo ni kwa sababu mwenye kusali alitumia maneno yanayotumiwa kwingineko na Mashahidi wa Yehova, kutia na jina la Mungu, Yehova.

Juni walipelekwa mahakmani wakahukumiwa kufanya kazi ngumu sana. Lakini wakati wakuu wa gereza walipoona kwamba Mashahidi hao waliifanya kazi yao ngumu kwa uaminifu sana, waliwekwa wasimamie wafungwa wengine. Wakuu wa gereza wakaanza kuwaheshimu sana Mashahidi hao.

Pia, Mashahidi wanne hao walipewa uhuru wa kuzungumza juu ya Biblia pamoja na wafungwa wengine. Nayo idara ya gereza ilileta Biblia kumi na tisa za lugha ya Cinyanja za kutumiwa na kikundi hicho. Mkuu mwenye kusimamia akawaambia Mashahidi hao hivi; “Twataka mtumie Biblia hizi kufundisha wavunja sheria hawa hapa gerezani ili nao wawe watu wema kama ninyi wenyewe.” Karibuni, mafunzo manane ya Biblia yalianzwa, moja likaanzwa pamoja na mlinzi wa gereza!

Mwishowe, mwanzoni mwa Oktoba 1975, Mashahidi hao wanne walifunguliwa gerezani. Wakaenda Zambia, kwenye kambi ya Sinda Misale, ambako walisimulia mambo waliyoona. Katika majaribu yao yote, walijisikia kwamba uwezo wa Yehova wenye kutia nguvu ulikuwa pamoja nao.

KUSIMAMA IMARA KUJAPOKUWA NA MATESO ZAIDI

Mwishoni mwa Oktoba, serikali ya Malawi ilipanga kurudisha Malawi maelfu haya ya Mashahidi waliokuwa katika kambi ya Zambia. Hivyo, Mashahidi walikabiliwa tena na unyama waliotendwa na Malawi Congress Party.

Ijapokuwa walipatwa na hayo, Mashahidi wa Yehova katika Malawi wamesimama imara​—⁠wanaume, wanawake na hata watoto wadogo. Wameazimu kutoacha wanayojua kuwa haki, wanayojua kuwa ndiyo mapenzi ya Mungu. Hawataacha uaminifu wao kwa Mungu kwa kuacha kumwamini.

Kwa hiyo leo matendo mengine ya imani yanatokea katika nchi ya Malawi yenye utawala wa kutumia nguvu. Matukio haya yanapatana na yale ya watu wengi waaminifu wa kale wanaotajwa katika Biblia katika Waebrania sura ya 11. Humo yasema kwamba watu kama Gideoni, Baraka, Samsoni, Yeftha, Daudi, Samweli na wengine “ambao kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki.” Yasema pia kwamba “wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi,” yaani, wasikubali kuachwa kwa kukana imani yao katika Yehova Mungu.

Sura ii hii ya Waebrania yasimulia pia: “Wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya; watu ambao ulimwengu haukustahili kuwa nao.”​—⁠Ebr. 11:32-38.

Waebrania sura ya 12, mstari wa 1, huwaita watu waaminifu hawa “wingu kubwa la mashahidi.” ‘Wingu kubwa hilo la mashahidi’ bila shaka sasa linatia ndani na Wakristo waliomo katika nchi ya Malawi wanaoonyesha imani ya aina ile ile katika Mungu. Ingawa huenda wengine wakafa; na wengine wengi wakatendwa kinyama, Wakristo waaminifu Malawi wamekata maneno kutomwacha Shetani Ibilisi wala mawakili wake hapa duniani wavunje imani yao. Nao wamehakikishiwa kabisa kwamba, hata wakifa kwa sababu ya kuwa wakamilifu kwa Mungu, watapata “ufufuo ulio bora,” wenye tumaini la kuishi milele.​—⁠Ebr. 11:35.

Pia, Wakristo hawa wanafahamu kwamba, kama vile Yehova alivyoruhusu mateso yawapate watu wake hapo kwanza, kama vile Ayubu, ndivyo Yeye anavyoyaruhusu leo, mpaka wakati Wake utakapofika wa kukomesha ulimwengu wa Shetani. Na ingawa kipindi cha majaribu kinaelekea kuwa kirefu, kama kilivyoelekea kuwa kwa Ayubu, Mashahidi wa Yehova Malawi wana hakika kwamba, kama ilivyokuwa kwa Ayubu, matokeo yatakuwa ya kutosheleza kabisa, yatawapa thawabu ya madhara yo yote wanayopata sasa kwa kuteswa kikatili.​—⁠Ayubu 1:9-12; 2:3-7; 42:12-17.

Karibuni, Mungu atafikiliza hukumu zake juu ya taratibu hii ya mambo ya Kishetani. Ataiondolea dunia uovu na waovu kuwe na ‘mbingu mpya na dunia mpya’ ambazo ameahidi. (2 Pet. 3:13) Maadui wa Mungu na wenye kuendelea kupinga watu wake “wataondoka wakakatiliwe mbali milele, lakini wenye haki wataingia katika uzima wa milele.”​—⁠Mt. 25:44-46, NW.

Kwa hiyo, ingawa Mashahidi wa Yehova Malawi wanateswa vikali sana kwa sababu tu ya kumwamini Mungu, wamehakikishiwa kabisa na Mungu kwamba watapewa nafasi ya kupata uzima wa milele katika taratibu yake mpya. Kwa sababu hiyo wanaweza kufurahi, wakijua kwamba ‘kujaribiwa kwa imani yao, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kwaweza kuonekana kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo.’​—1 Pet. 1:6, 7; Zab. 37:10, 11, 28, 29.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki