Waliuona Ufumbuzi wa Amani
DUNIANI mwote watu wengi wamejawa na chuki. Hawafurahii amani na wanadamu wenzao. Watu wa taifa moja, kabila au rangi ya ngozi wanawaonea uadui watu wengine wa taifa jingine, kabila au rangi ya ngozi, mara nyingi kwa sababu walitendewa udhalimu wakati uliopita. Je! watu hao wanaweza kuushinda uadui wao?
Yaliyoonwa na mhudumu mmoja wa mashahidi wa Yehova katika California yaonyesha kinachoweza kufanywa. Yeye alikuwa yumo katika huduma ya nyumba kwa nyumba, akizungumza na watu katika ujirani juu ya makusudi yake Mungu. Yeye anasema:
“Katika mlango mmoja, mwanamume wa kimo cha futi sita alinijibu nikaribie. Mara nilipojifahamisha kwake, akakatiza, akisema, ‘Mimi sitaki kuzungumza na weupe!’ Kwa unyofu nikitaka kusema naye, nikamwuliza ugumu ulikuwa nini. Akaniambia kwamba yeye alikuwa Mhindi wa Kiamerika na kwamba weupe waliwanyang’anya nchi yao na kuwaua watu wake.
“Nilikubali kwamba kosa kubwa lilikuwa limefanywa. Vile vile nikamweleza kwamba mimi nilikuwa Mwarmenia na kwamba kama ningetaka kuwa na nia ile ile, ningejisikia namna ile ile juu ya watu waliokuwa wamechinja maelfu ya Waarmenia bila sababu. Lakini nikamhakikishia kwamba nilikuwa nikiliweka tumaini langu na imani katika Yehova Mungu, nikijua kwamba karibuni angerekebisha mambo kupitia kwa serikali yake ya kimbinguni ya Ufalme. Kisha nikamhakikishia kwamba hii ndiyo sababu nilikuwa mlangoni pake, kueleza namna ambavyo hali zilizopo za ulimwengu zinavyohakikisha kwamba karibuni ufalme wa Mungu utakomesha udhalimu, maoni mabaya ya chuki yasiyo na msingi na uovu duniani mwote.
“Hilo lilimvuta sana hata akakubali kupata kitabu cha kumsaidia katika funzo la Biblia kilichokusudiwa kiwafahamishe watu makusudi ya Mungu. Niliporudi nyumaye, tulianza funzo la kawaida la Biblia. Tangu wakati huo yeye na mkewe wamekuja kila juma kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova nao wanafanya maendeleo ya kasi katika kujifunza tumaini la Biblia lililo hakika kwa wakati ujao.”
Hata watu waliozoezwa vita wanaweza kugeuza njia zao na kuanza kuifuata amani. Mwanamume mmoja kutoka Ubelgiji anasimulia:
“Mimi nilikuwa askari mgeni wa mshahara katika jeshi la Kiafrika la Katanga nami nikapambana na hali nyingi za hatari. Katika shughuli moja jeshi la Katanga liliua kila kiumbe, mwanadamu na mnyama. Nikihofu kupoteza uhai wangu, nikaweka nadhiri, ‘Nikitoka hapa nikiwa hai, nitarudia kanisani.’ Nilitoka nikiwa hai. Katanga ulishindwa na, kana kwamba kwa mwujiza, nikaokoka kufa.
“Miaka mingi hapo kwanza nilikuwa nimeliacha Kanisa la Katoliki. Lakini sasa nikalirudia. Mara ya kwanza niliporudi walihubiri juu ya hell (au mahali panapotajwa kama penye moto zinakotesewa milele nafsi za watenda mabaya wasiotubu). Maelezo yasiyo ya busara ya padre mzee yalinishtua sana hata nikaondoka kanisani mara hiyo. Nyumaye, nilirudi usiku wa Krismas. Nikafika usiku wa manane barabara. Mlango wa kanisa ulikuwa umetiwa kufuli. Nilipobisha hodi, nikafunguliwa. Huko nyuma, nikiwa katikati ya waadhimishaji walevi wa Krismas, nilijisikia sina hatia kamwe ya nadhiri niliyoiweka nikiwa katika uwanja wa vita. Nikaondoka kanisani, nisirudi kamwe.
“Lakini, tangu wakati huo na kuendelea niliwaza zaidi juu ya kuwako kwa Mungu. Nikasali kwa Mungu ajifunue kwangu kwa ishara kusudi kwamba niiondoe nadhiri niliyokuwa nimemwekea.
“Halafu jambo fulani likatokea. Mmojawapo wa mashahidi wa Yehova akatufikia mlangoni petu nami nikachukua kila kitu alichonitolea na kukisoma kwa kupendezwa sana. Nilichunguza, nikalinganisha na kujifunza.
“Karibuni nyumaye, niliamua kuyajaribu mambo niliyokuwa nimejifunza kwa kutembelea Jumba la Ufalme. Kwa kuvutwa na hali ya kirafiki na ya furaha, karibuni nikawa mhudhuriaji wa kawaida. Sijapata kuona upendo na umoja katika maisha yangu yenye mambo mengi na hata hivyo ya kupendeza, pamoja na kusafiri sana, kama ule niliouona katika hili Jumba la Ufalme.”
Mwanamume huyu alikuwa na mageuzi makubwa ya kufanya. Kama alivyoeleza: “Maisha yangu yote nilikuwa nimezoezwa vita ya kutumia silaha na sasa ilinipasa kujifunza kuwa askari wa kiroho wa Kristo.”
Kwa kweli, basi, ujamaa mwema na Muumba, wenye msingi wa ujuzi wa kweli ya Neno lake, ndio ufumbuzi wa amani na wanadamu wenzetu. Ikiwa wewe unasumbuliwa na chuki na maoni ya uadui yasiyo na msingi yaliyopo leo, sababu gani usitafute nafasi ya kuzungumza na mashahidi wa Yehova. Jifunze kwao uhakika uliopo kwamba karibuni Mungu atayaondoa maoni ya uadui yasiyo na msingi ya kitaifa na ya kikabila, na vile vile vita duniani pote. Na vile vile hatua za kusudi hili ambazo tayari zinachukuliwa na mamia ya maelfu ya Wakristo duniani pote.