Sababu kwa Nini Watu wa Namna Zote Wanakuwa Mashahidi wa Yehova
UVUNJAJI wa sheria, jeuri na misukosuko inapozidi kuongezeka duniani pote leo, watu wengi wanaiona haja ya kitu fulani cha kuwapa tumaini imara la wakati ujao. Wengine wanaona kwamba jambo bora ni ‘kupata yote wawezayo kutokana na maisha sasa.’ Wanajaribu kuepuka matatizo kwa kutumia vileo vikali au dawa za kulevya. Ni kweli, wengine wamejaribu kutafuta jibu katika dini. Lakini mara nyingi mno wote wamekatishwa tamaa na matendo na mafundisho ya makanisa ya Kristendomu. Wamekuwako pia wale waliotamani kitu fulani kilicho bora na wakakipata. Kwa njia gani? Waache wengine wa watu hawa wasimulie wenyewe ilivyotukia.
SABABU YA KUISHI
Kiangalie kisa cha mwanamke anayeishi Chicago. Yeye alikuwa na watoto na alikuwa amekuwa akiishi miaka 20 pamoja na mwanamume asiyeolewa naye. Mwanamke huyu aliona kwamba hakuwa na tumaini maishani. Akiisimulia hali yake, anasema hivi:
“Nilifikiria kufa tu. Sikuona furaha yo yote katika maisha niliyoishi. Nilitafuta msaada wa ‘mfafanuzi na mshauri’ wa mambo ya uchawi niliyedhani angeweza kunisaidia. Badala yake, nilizidi kuvunjika moyo tu, kwa maana ziara tatu nilizomfikia zilinigharimu shilingi 700.00, naye alijaribu kunilazimisha nifanye ufisadi. Nilikuwa mwenye wasiwasi sana. Nikaanza kunywa kupindukia, nikijaribu kuitafuta amani niliyoihitaji sana. Lakini hilo halikusaidia. Mwishowe, niliamua kwamba kifo ndiyo ingekuwa njia ya pekee ya kuyaepukia maisha yangu yaliyoelekea kuwa ya bure.
“Lakini nadhani nilikuwa ningali natamani kuishi. Nami nilimgeukia Mungu katika jaribio moja la kukata tamaa nitafute sababu ya kuishi; nikasali kwake anisaidie.
“Siku chache baadaye mashahidi wa Yehova walibisha hodi mlangoni pangu. Niliwaamuru mara moja waende zao. Lakini nikaamua kuwaita tena. Funzo lilipangwa nami nikaanza karibuni kuihudhuria mikutano ya mashahidi wa Yehova pamoja na wanangu.”
Mwanamke huyu alijifunza nini kupitia kwa funzo lake la Biblia kwa kipindi cha miaka miwili kilichoyabadili maoni yake juu ya maisha? Alipata kuona kwamba Yehova Mungu analo kusudi zuri ajabu kwa wanadamu, yaani, kuuondoa uovu wote duniani katika kizazi hiki na kusimamia mambo ya dunia kwa haki kupitia kwa ufalme wake kwa njia ya Yesu Kristo. Pia alipata kuifahamu haja ya kutimiza matakwa ambayo Mungu ameyaweka kwa wale wanaotaka kupata kibali yake na baraka. Kwa hiyo aliolewa na mwanamume aliyekuwa amekaa pamoja naye kwa zaidi ya miaka 20 na kwa njia nyingine akapatanisha maisha yake na Neno la Mungu. Akieleza mambo ambayo yametokea, mwanamke huyu asema: “Ni mwenye furaha kusema kwamba niko wakf na nimebatizwa. Sasa mimi na wanangu twamtumikia Yehova pamoja.”
KULIKUBALI NENO LA MUNGU KABISA
Je! umesikia watu wakisema wenyewe kwamba wameuona uhakika wa kutoshikamana kwa kanisa lao na Biblia? Nyakati nyingine hii imewafanya wafuate njia ya maisha inayotofautiana kabisa na mapenzi ya Mungu. Akisimulia maono yake mwenyewe, mwanamume mmoja wa Texas asema hivi:
“Baada ya karibu miaka miwili ya kuoana, mimi na mke wangu tuliamua kwamba imetupasa tutafute kanisa fulani na kuanza kulihudhuria. Nilijua kwamba lile nililokuwa nimekwenda kwanza kabla hatujaoana halikunifaa mimi. Kwa hiyo, basi, tukajaribu kanisa ambalo mke wangu alikuwa amehudhuria—mara moja—na basi. Kwa hiyo hatukwenda po pote.
“Tulifuata kawaida yetu tu. Hatukuwa na wasiri nasi tulishirikiana na jamaa zetu tu. Jambo hili lisingalikuwa baya sana, isipokuwa wakati tulipokutana pamoja mwisho wake tulilewa.
“Niliona haja ya Mungu na Biblia. Lakini wakati ule ule sikujisikia mwenye haki ya kusali, kwa sababu ya mambo yote mabaya niliyokuwa nimefanya. Kwa kukumbuka mtu mmoja alivyokuwa ameniambia (‘Kama tu ukisali upate maarifa, Mungu atakusaidia’), niliamua kujaribu. Ulikuwa usiku wa Jumamosi. Mke wangu na mtoto walikuwa wamelala. Nikasali: ‘Mungu mpendwa, iwapo kuna Mungu, nisaidie niipate dini iliyo ya kweli.’
“Asubuhi iliyofuata nikaamka nikaelekea kwenye mlango wa mbele. Nikitazama kiooni katika mlango, niliona kipande cha karatasi kikipeperushwa na upepo kuelekea ukumbini. Sikuweza kujua kilikotoka, kwa maana tulikuwa tumekata majani na kuufagia ua jana yake. Hata hivyo, nilitoka nje nikakiokota. Ulikuwa ukaribishaji kutoka kanisa fulani, kama nilivyodhani.
“Nilisisimka, nikiamini Mungu alikuwa ameijibu sala yangu. Nikamwambia mke wangu kwamba ningekwenda kwenye kanisa hilo saa kumi. Yeye hakutaka kwenda. Lakini nilijua kwamba, nikisema ningekwenda yeye aende au asiende, angebadili nia yake. Alifanya hivyo.
“Saa 9.30 alasiri tukafika penye uwanja wa kuwekea magari. Ishara ilisema, ‘Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.’ Sikuwa nimepata kuwasikia mashahidi wa Yehova. Nikielekea kwenye jumba, nilikuwa na mashaka juu ya kuingia. Mawazo yangu yalikuwa, ‘Labda ndio wale watu wanaopata “roho takatifu,” kama waiitavyo, na kugaa-gaa sakafuni.’ Mimi sikutaka nishiriki hilo. Kwa hiyo tulianza kurudia garini. Halafu tukasema, ‘Namna gani hii ikiwa ndiyo dini ya kweli? Tukiondoka sasa, huenda tusirudi tena.’ Kwa hiyo tuliingia.”
Waliona nini penye Jumba la Ufalme? Ni nini kilichowavutia juu ya mashahidi wa Yehova?
Mwanamume huyu anaendelea kusema: “Tuliona chumba kisicho na vitu vingi mno kilichopambwa kwa kiasi. Tulipokwisha pata mahali pa kuketi tulianza kutazama kutuzunguka. Kila mtu alikuwa akisema nao walielekea kupendana kweli kweli. Haukupita muda kabla hawajaanza kutufikia na kutueleza walikuwa akina nani. Baada ya karibu dakika kumi na tano za kujibiwa maulizo, nilisadiki kwamba watu hawa ndio walikuwa na kweli juu ya Biblia. Mambo kama vile kutokuwa na wahubiri wanaolipwa mshahara, kutokuwa na visahani vya sadaka, kwenda mlango kwa mlango hasa kuwaeleza watu juu ya Mungu, na kupendezwa kwa kweli walikotuonyesha yalinivutia mimi.
“Mtu mmoja alitufikia na kuuliza kama tungependa kuwa na funzo la nyumbani la Biblia. Tulikubali kwa vyepesi.”
KUJITENGA NA ULIMWENGU
Kutokana na maono yako mwenyewe wajua kwamba washiriki wa makanisa ya Kristendomu wanajitia kwa kawaida siasani. Lakini namna gani juu ya onyo la Biblia “kujilinda na dunia pasipo mawaa”? (Yak. 1:27) Mashahidi wa Yehova wanafahamu kwamba uaminifu wao wa kwanza lazima uuendee ufalme wa Mungu kwa njia ya Kristo, nao hawajichangamanishi na siasa za ulimwengu. Kujua hili kumewavutia sana watafutao kweli.
Alipokuwa akitembelea watu nyumbani mwao, mmoja wa mashahidi wa Yehova katika nchi ya New York alimkuta mwanamume mwenye urafiki aliyesema hivi: “Mimi ninayo maulizo mawili, nayo majibu yako yataamua kama mazungumzo yetu yataendelea au kama utaondoka. Ulizo la kwanza, Je? nyie mwaamini lo lote jingine kuliko Biblia kuwa kweli?” Shahidi alimhakikishia kwamba mashahidi wa Yehova wanaiamini Biblia tu kuwa kweli iliyoongozwa na roho ya Mungu wala si mapokeo au imani za kubuniwa na wanadamu. “Umenijibu vema ulizo la kwanza,” akasema mwanamume huyo, “lakini pengine hutajibu lifuatalo ifaavyo. Mimi natafuta dini isiyoshughulika hata kidogo na siasa. Je! nyie mwashughulika na siasa?” Alipoarifiwa kwamba mashahidi wa Yehova wanajitenga na siasa zote, hata hawafanyi uchaguzi, mwanamume yule alishangaa kweli. Mwishowe funzo la Biblia lilianzwa pamoja naye na mkewe. Sasa wote wawili ni mashahidi wa Yehova waliobatizwa.
WALIVURUGWA NA MAZOEA NA MAFUNDISHO YA MAKANISA
Wengine zaidi walio mashahidi wa Yehova sasa walifadhaishwa na mafundisho na mazoea ya makanisa yao ya zamani. Wajapokuwa wanyofu, hawakuweza hata kidogo kupata majibu yenye kuridhisha kwa maulizo yao. Mwanamke mmoja wa Chile asimulia:
“Tangu nilipokuwa mwenye umri wa miaka tisa nilitaka nimtumikie Mungu na, kwa kuwa nilikuwa Mkatoliki, nilipendezwa na mapadre na watawa wa kike. Nilipokuwa mwenye umri wa miaka 22 nikaingia katika makao ya watawa nianze mazoezi yangu kama mtawa. Fundisho la Utatu lilinifadhaisha na maelezo ya kwamba lilikuwa fumbo hayakuridhisha. Walakini, niliweka nadhiri zangu za kwanza za kimya, umaskini, kupata taabu na kukaa nikiwa safi. Ndipo macho yangu yalipoanza kufumbuka. Nilidhani kwamba kumtumikia Mungu kama mtawa kungekuwa furaha ya daima. Lo! nilivyokosea! Biblia ilionwa kama kitabu cha maajabu kisichopaswa kuguswa; nadhiri za kimya zilimaanisha kwamba tusingeweza kuzungumza, kusali tu; tulipewa chakula kisichowafaa wanadamu; kila mmoja wetu alitakiwa aende chumbani mwake na kuvua mavazi yake na, akitumia kiboko, ajipige. Wengine walizimia walipokuwa wakijiadhibu. Nilishangaa sana juu ya kama Mungu aliyahitaji haya yote. Baada ya hapo nikaamua kwenda zangu. Mama Mkuu alipokuwa hayupo niliondoka nikielekea nyumbani.
“Siku moja nilijifunza Amri ya Pili, iliyokataza ibada ya sanamu. Hii ilinishangaza, kwa maana ibada ya sanamu ilikuwa sehemu ya maisha yetu ya kila siku katika makao ya watawa. Hii ilichochea ndani yangu tamaa ya kujifunza Biblia. Nilisali kwa Mungu kwa bidii ili kwa njia fulani niweze kupata Biblia na kufundishwa na mtu fulani. (Wakati huu ndipo nilipokuwa nimeamua, kwamba ningerudia makao ya watawa kwa woga.)
“Muda mfupi baadaye mwanamume mmoja alifika mlangoni petu akasema: ‘Habari ya asubuhi, sisi tunawatolea watu mafunzo ya Biblia bila malipo.’ Niliduwaa. Sala yangu ilikuwa imejibiwa!
“Funzo la Biblia likaanza. Lo! namna yalivyokuwa ya ajabu mambo niliyojifunza! Kwa muda fulani sikumwambia Shahidi kwamba nilikuwa nimekuwa nikijifunza nipate kuwa mtawa, nikiogopa kwamba asingeendelea kujifunza nami. Walakini, nilipomfunulia uhakika huu sote tulifurahi sana kwa kunisaidia nitoke katika utumwa huo mkuu.
“Sasa nimejifunza kwamba kumtumikia Yehova ni kama nilivyofikiri kungekuwa, furaha kweli kweli.”
Nyakati nyingine, kwa sababu ya kupata mazoezi ya kidini, wengine wamekuwa na maoni yasiyo na msingi ya kudharau mashahidi wa Yehova. Lakini kukatishwa tamaa na kanisa lao wenyewe kulifanya wayaondoshe maoni haya na kusikiliza. Maono haya yatoka kwa mwanamke mmoja Finland:
“Mimi nililelewa kwa njia ya kidini sana. Nilipokuwa mchanga, baba yangu aliomba kwamba wo wote kati ya watoto wake wasipate kuwa Wakomunisti au mashahidi wa Yehova. Wakati wa kuchagua kazi ulipofika, niliamua kuwa mtumishi wa kanisa. Kwa hiyo nikajiandikisha penye Christian Folk High School. Huko sisi wanafunzi tulionywa mara nyingi juu ya mashahidi wa Yehova. Walisemekana kuwa wazushi wanaoukataa hata ukombozi.
“Mashemasi walipotafutwa kati yetu, nilikuwa mwenye hiari ya kukubali. Hii ilihitaji elimu zaidi. Bila shaka, nilikuwa na hamu ya kujifunza mengi niwezavyo na kwa hiyo niliendelea kuuliza maulizo juu ya mambo mengi. Waalimu wangu hawakupendezwa na hilo. Walijaribu kushughulika nami kwa upole, hata hivyo, wakasema: ‘Ni vema kwamba wayauliza mambo haya, lakini wanadamu wasiokamilika hawawezi wakati wo wote kuielewa Biblia kabisa. Bila shaka umeona kwamba waandikaji wake, kwa mfano, kama vile mtume Paulo, walikuwa wasiokamilika kama sisi. Biblia yote si Neno la Mungu; mawazo ya wanadamu pia yamo ndani yake.’
“Mungu akawa mbali zaidi na asiyejulikana nami, lakini kijapokuwa kila kilichotukia, baada ya miaka sita ya kujifunza nilipokea baraka ya askofu nianze kazi yangu kama shemasi. Walakini, nilikuwa mwenye huzuni. Katika kazi hii utu wangu uliharibika nami nikawa katika hali mbaya sana ya kiroho. Naweza kusema kwamba sikusoma Biblia tena wala sikusikia ikisomwa tena. Wakati fulani baadaye niliolewa nalo hili lilisaidia kuleta wokovu wangu. Mume wangu hakuchukia watu bila sababu na kwa hiyo alikaribisha mashahidi wawili wa Yehova wakati mmoja. Kwa uchaguzi wa mume wangu funzo la Biblia lilianzwa nyumbani mwetu. Kwa sababu ya mazoezi niliyokuwa nimepata mapema, niliwachukua mashahidi wa Yehova kama Wasamaria wachafu, lakini nilishangaa kugundua kwamba wao waliichukua Biblia nzima kama Neno la Mungu. Haukupita muda mwingi kabla ya mimi kujiunga katika funzo la Biblia kwa shauku. Karibuni jamaa yote iliikubali kweli nasi sasa twaifurahia ibada safi ya Yehova.”
WALIUONA USHUHUDA WA UPENDO WA KWELI
Zaidi ya kuona kwamba mashahidi wa Yehova wanafundisha Biblia isemavyo, wengi wamevutiwa na namna wanavyotendeana mmoja na mwenzake. Mwanamke mmoja wa nchi ya Florida asimulia maoni yake:
“Nilipata habari juu ya mashahidi wa Yehova—juu ya namna walivyo wenye upendo na fadhili. Kwa hiyo nikaamua niende kwenye Jumba la Ufalme. Sikuwa na habari mashahidi wa Yehova walikuwa wakifanya nini, sikujua walihubiri nini wala walivyosali.
“Nilipoingia jumbani kwanza, nilikuwa na wasiwasi mwingi. Nikaanza kutembea kumwelekea mmoja wa watu wale nikaseme naye. Kisha nikageuka na kumwona mwanamke niliyekuwa nimemngoja katika duka la dawa ninamofanya kazi. Wakati ule ule nilijisikia heri, kwa maana alikuwako angaa mtu ambaye ningeweza kusema naye juu ya dini hii.
“Baada ya mkutano nilidhani kwamba kila mtu angeinuka na kutoka nje. Lakini kila mtu alinijia na kuniuliza jina langu na nilivyoufurahia mkutano. Niliweza kuona kwamba mwishowe kulikuwa na mtu wa kupendezwa hasa na nilivyoona mambo. Nilifurahi kuwaona namna walivyokuwa wenye fadhili. Hawakujua lo lote juu yangu—nilikuwa mtu wa namna gani. Hata hivyo walinitendea vema.”
Je! wewe u mmoja wa watu wengi leo wanaowatafuta watu wanaojitahidi kuishi kupatana na Biblia? Kwa sababu gani usitembelee Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova upesi uwezavyo? Utakayoyaona na kujifunza huko yaweza kukupa tumaini jipya katika Mungu na mipango yake kwa ajili ya furaha ya wanadamu.