Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kweli ya Biblia Yamweka Huru Mtawa wa Kike Katika Bolivia
WATU wengi wenye mioyo myeupe wanakimbia kutoka dini bandia, wakijifunza kweli ya Biblia, na kuja kumtumikia Yehova, Mungu wa kweli. Zaidi ya 7,600 wamefanya hivyo katika Bolivia, kutia na mtawa wa kike.
Alipokuwa na umri wa miaka tisa tu, M—— alikutana kwa mara ya kwanza na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alifungua mlango wakati Shahidi huyo alipotembelea nyumbani kwao, na kwa mara ya kwanza, akasikia jina la Mungu, Yehova, likitamkwa. Hakuweza kulisahau kwa muda wa miaka mingi.
Kwa kuwa yeye alikuwa msichana wa pekee katika familia, iliamuliwa kwamba alipaswa awe mtawa wa kike. “Nilifurahi kama nini kwamba ningepata kuwa katika utumishi wa Mungu—ndivyo nilivyofikiria, angalau,” asema M——. Lakini shangwe yake iligeuka ikawa utamausho alipoona ukosefu wa haki na upendeleo uliozoewa nyumbani mwa watawa. Asema hivi: “Labda sitasahau kamwe vile vipindi vya kushuka moyo na kule kupigwa kimwili na kiroho kuliko umiza sana, kukinifanya nimwone Mungu, si akiwa Yule mwenye upendo, bali akiwa Yule anayeadhibu bila huruma.”
Aendelea hivi: “Kufikia wakati nilipokuwa mtawa wa kike, nilikuwa nimeshindwa kupata jina la Yehova katika Biblia. Nilipata ‘Yahweh’ tu, na hilo lilinitatanisha. Siku moja hata nilienda kuwatafuta wale watu waliosema juu ya Yehova, lakini sikuwapata.
“Wakati ulipita, na siku moja nilipokuwa njiani kwenda nyumbani kwa familia yangu, niliona ubao uliosema, ‘Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.’ Nilitaka kuwaambia kwamba walikuwa manabii wawongo, lakini hakukuwa na mtu katika jumba hilo. Nikarudi Jumapili. Mkutano ulikuwa ukiendelea, na wengi walionekana kuwa wenye mshangao kuona mtawa wa kike mwenye mavazi kamili akihudhuria. Baada ya mkutano, nilijaribu kuondoka upesi. Hata hivyo, mmoja wa Mashahidi hao alinisalimu, kwa hiyo nikamwuliza, ‘Ni kwa nini mnamkufuru Yule Aliye Mtakatifu kwa kuitwa kwa jina hilo?’ Swali langu liliongoza kwenye mazungumzo ya Biblia, na nikafanya mipango anizuru nyumbani kwa familia yangu. Wazazi wangu walimfukuza. Hata hivyo, tulikutana tena miezi miwili baadaye, naye akanialika nyumbani kwake ili kujifunza Biblia. Nilivutiwa sana na habari aliyonionyesha, akithibitisha kwamba Wakristo wapaswa kulitumia jina la Mungu. Ushuhuda huo ukanipa nguvu iliyohitajiwa ili kuyaacha mambo yote yasiyo na maana niliyokuwa nimefundishwa nikiwa mtawa wa kike.
“Ninakumbuka mambo mengi juu ya maisha yangu katika nyumba ya watawa. Kwa mfano, wakati mmoja nilihitaji chakula zaidi cha kula. Kwa hiyo niliandika nikiwaomba wazazi wangu wanipelekee chakula, bila kutambua kwamba barua zilikaguliwa kwenye nyumba hiyo ya watawa. Kwenye mlo uliofuata, kiasi kikubwa cha mkate na jeli kiliwekwa mbele yangu, nami nikalazimishwa nikile chote. Sasa nilikuwa na chakula kingi mno. Niliwaambia marafiki wangu hivyo, na mmoja akadokeza niufinyefinye mkate nisioweza kuula na kuutapanya sakafuni. Nilipofanya hivyo, mtawa mmoja wa kike alinikamata mara moja na kunitupa sakafuni, akiniamuru vikali niilambe sakafu yote iwe safi kwa ulimi wangu. Chumba hicho kilikuwa kikubwa. Nilipokuwa nikitii amri hiyo, nilisikia wengi wakicheka—hakuna rehema yoyote iliyoonyeshwa.
“Sasa naweza kuona jinsi lilivyo jambo zuri ajabu kuwa huru na yote hayo. Kama iwezavyo kutazamiwa, uhuru huo ulitia ndani dhabihu nyingi. Kwanza, baba yangu alinifukuza kutoka nyumbani. Hata hivyo, kabla ya kuacha nyumba ya watawa, nilikuwa na pendeleo la kuwasaidia watawa wa kike wengine wachanga wajifunze kweli. Nashangilia kusema kwamba wengine wetu tumeweka maisha yetu wakfu kwa Yehova Mungu!
“Baada ya kuacha nyumba ya watawa, ilikuwa vigumu kwa baba yangu kuelewa ni kwa nini nilikataa kufanya kazi zenye mishahara ya juu lakini zenye kuhitaji wakati mwingi. Hata hivyo, nilitaka wakati zaidi kwa ajili ya utumishi wa Mungu. Sasa ninatumikia nikiwa painia wa kawaida, nikiwa na maisha yasiyotatanika na hata hivyo yenye kuthawabisha. Na kwa shangwe yangu nyingi, mama na kaka zangu wamejiunga nami katika utumishi wa Yehova.”
Kwa kweli, kweli ya Biblia huweka mtu huru na mfumo wa ulimwengu huu wa dini bandia, na huleta shangwe na furaha za kudumu.—Yohana 8:32.