Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Mashahidi wa Yehova Wahubiri Vivi Hivi Wakiwa na Matokeo Mazuri
WATU wengi walijulishwa kweli ya Biblia kwa mara ya kwanza wakati mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipowahubiria vivi hivi. Katika hilo Mashahidi hufuata mfano wa Yesu Kristo, aliyehubiri vivi hivi kwa mwanamke Msamaria kwenye kisima alipokuja kuchota maji. (Yohana, sura 4) Katika Afrika Mashariki, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alihubiri vivi hivi kwa mtawa wa kike Mkatoliki. Ofisi ya tawi ya Watch Tower Society yasimulia lililotokea:
◻ Mapema asubuhi moja alipokuwa njiani kwenda mjini, Shahidi huyo alikutana na mtawa wa kike Mkatoliki. Alichukua nafasi hiyo kumwuliza mtawa huyo wa kike hivi: “Wewe waenda wapi wakati huu wa siku?” Jibu lilikuwa: “Naenda kumwomba Mungu wangu.” Kisha akamwuliza mtawa huyo wa kike: “Je! walijua jina la Mungu wako?” Mtawa huyo wa kike akajibu “Je! jina lake si Mungu?” Shahidi huyo akajitolea kumtembelea mtawa huyo wa kike nyumbani kwake alasiri hiyo kuzungumzia jina la Mungu. Baada ya mazungumzo mtawa huyo wa kike alienda kwenye kanisa lake na kumwuliza mmoja wa mapadri ikiwa alijua maana ya neno “Yehova.” Jibu lilikuwa, “Hilo ni jina la Mungu.” Mtawa huyo wa kike alishangaa sana kusikia kwamba padri alijua hilo lakini hakuwa kamwe amelifundisha kwake.
Shahidi huyo alimtembelea mwanamke huyo siku tisa mfululizo na kumfundisha kweli kuhusu Utatu, nafsi, moto wa helo, na tumaini kwa wafu. Mwanamke huyo alishika kila jambo na kisha akamwomba Shahidi ampe wakati fulani wa kufikiria mafundisho hayo yote mapya. Baada ya majuma mawili alikutana na Shahidi huyo tena na kumwomba mazungumzo ya zaidi. Kufikia wakati huo mtawa huyo wa kike alikuwa ameamua kuacha kanisa na alikuwa tayari ameharibu sanamu, tasbihi (rozari), na msalaba wake. Padri alijaribu kumsihi arudi, lakini aliazimia kuifuatia kweli. Alibatizwa baadaye na amekuwa akitumikia akiwa painia msaidizi wa kawaida kwa miezi mingi ijapokuwa afya yake mbaya na umri wake mkubwa.
Kwa kuwa nyumba yake ni kubwa, aliitoa kwa kundi itumiwe kuwa Jumba la Ufalme. Ndugu waliweka paa mpya, wakaondoa kuta za ndani, na kufanya sehemu kubwa ya jengo hilo kuwa mahali pa kukutania panapovutia. Mtawa huyo wa kike huishi katika chumba kilicho nyuma ya jumba hilo. Anafurahi kuwa aliweza kufanya mchango huo kwa ajili ya ibada ya Yehova.
Ono jingine linaloonyesha hekima ya kutoa ushahidi wa vivi hivi latoka Kampala, Uganda. Njiani kwenda ofisi ya serikali, Shahidi mmoja misionari alisema vivi hivi na wale waliokuwa naye katika lifti. Mwanamume mmoja, Bw. L__, alionyesha tamaa ya kukubali fasihi iliyoonyeshwa lakini hakuweza kuipokea wakati huo. Kwa hiyo alimpa misionari huyo jina lake na anwani ya ofisi yake. Baadaye misionari huyo alikwenda huko na kuomba aitiwe Bw. L__. Yeye aliitwa lakini kwa mshangao wa misionari huyo, mwanamume tofauti alitokea. Kulikuwako wanaume wawili wenye jina lilo hilo waliofanya kazi katika ofisi hiyo. Ushahidi mfupi ulitolewa kwa Bw. L__ wa pili, naye alionyesha kupendezwa kwa ajabu. Ingawa Bw. L__ wa kwanza alipoteza kupendezwa kwake, funzo la Biblia lilianzwa na Bw. L__ wa pili. Yeye sasa ni Shahidi aliyebatizwa, na mke na mwana wake wanafanya maendeleo mazuri kuelekea ubatizo.
Yesu Kristo ndiye Mchungaji Mwema na ajua wale wenye mfano wa kondoo walio na mioyo ipendayo uadilifu. Maono hayo huonyesha kwamba yeye anawaelekeza wafuasi wake kwa watu kama hao. Kuhubiri vivi hivi kwaweza kuwa na matokeo mengi!—Yohana 10:14.