Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Mtawa wa Kike kwa Miaka 25 Ajifunza Ukweli Mwishowe
BIBLIA ilitabiri kwamba “umati mkubwa” kutoka mataifa yote ungekuja na kuabudu kwenye hekalu la kiroho la Yehova. (Ufunuo 7:9, NW) Jambo hilo linatukia leo, nasi tunashangilia kuona kwamba wengi, kwa msaada wa ukweli wa Mungu, kwa njia hiyo wanavunja pingu za dini isiyo ya kweli. Maono yanayofuata yanatoa kielezi cha jambo hili.
◻ Mwanamke mmoja katika Roma, Italia, asimulia hivi: “Kutoka wakati nilipokuwa mdogo tazamio langu lililo kubwa zaidi lilikuwa kuwa mtawa wa kike, kwa kuwa nilitamani kwa moyo wangu wote kumtumikia Mungu. Niliweza kutimiza tamaa yangu nikiwa na umri wa 32, siku ya Desemba 8, 1960, nilipofanya nadhiri zangu za kwanza za utii, umaskini, na ubikira. Mgawo wangu ulikuwa kutunza mchana na usiku karibu watoto 30 maskini na walioachiliwa mbali ambao walikuwa yatima au watoto wa wafungwa. Nilipata uradhi katika mgawo wangu.
“Imani yangu ilitikiswa baada ya miaka kumi ya utumishi wakati ushindani ulipotokea ndani ya shirika lile. Nilishangaa kwa nini, ikiwa Mungu alikuwa akituongoza, angeruhusu magomvi na machafuko ya jinsi hiyo yawe katika nyumba yake mwenyewe.”
Mtawa huyo wa kike alikuwa na dada aliyekuwa akiishi Ufaransa na ambaye alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alimtolea ushahidi mtawa huyo wa kike kwa barua na kumpelekea New World Translation of the Holy Scriptures. Mtawa huyo wa kike anasimulia hivi: “Baada ya miaka 23, hiyo ilikuwa ndiyo mara yangu ya kwanza kuhusiana na Neno la Mungu.” Hapo ndipo yeye alikubali funzo la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Nilipokuwa nikifanya maendeleo na funzo la Biblia, nilipata kumjua Yehova Mungu na matakwa yake na pia sifa zake za ajabu. Nilihisi vibaya sana nilipojifunza kwamba yeye hakubali utumizi wa mifano, kwa kuwa shirika lile lilijaa mifano ya kila ukubwa na aina. Nilielewa kwamba ikiwa nilitaka kumfurahisha Yehova, singeweza kukaa mahali hapo. Baada ya miaka 25 ya utumishi wa kujitoa nikiwa mtawa wa kike, mwishowe nikawa nimeupata ukweli. Hivyo basi siku ya Oktoba 1, 1985, nilitoa taarifa yangu ya kuondoka, ikasikitisha sana wakuu wangu.
“Ndugu na dada zangu wenye upendo walinisaidia kiroho na kimwili pia. Nikiwa mwenye shukrani kwa Yehova na tengenezo lake, mimi nilibatizwa siku ya Agosti 30, 1986, nami nikaanza kutembea katika barabara halisi inayoenda kwenye uhai wa milele.”
Yehova Abariki Tamaa ya Kijana Kumtumikia Mungu
◻ Mwalimu mmoja wa shule katika Brazil aliyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova akiwa anasahihisha karatasi za shule aliona kwamba mwanafunzi mmoja wa miaka 14 aliandika juu ya tamaa yake kujifunza mengi zaidi juu ya Mungu. Mwalimu huyo wa kike alianza funzo la Biblia pamoja na mwanafunzi huyo, lakini msichana huyo alipokuwa akifanya maendeleo, familia yake ya Kikatoliki ilikataza funzo hilo na kuharibu vitabu vyake. Mwanafunzi mchanga huyo alianza kujifunza Biblia wakati wa pumziko la shule, lakini akagunduliwa. Hivyo basi funzo liliendelezwa kwa kuandikiana barua. Ingawa hivyo, upesi familia ikazipata barua zake na kuzichoma. Baba alianza kumlazimisha aende Misa. Msichana huyo alienda naye lakini akachukua nakala ya Mnara wa Mlinzi akaisome wakati wa ibada, akiificha kati ya kurasa za kijitabu cha kanisa. Hilo liliendelea kwa miezi sita, mpaka siku moja akajificha kutoka nyumbani kwao ili kwenda kwenye Jumba la Ufalme. Wakati wa mkutano baba yake alikuja mlangoni akawaambia akina ndugu waambie binti yake kwamba angempiga wakati angerudi nyumbani. Jitihada za akina ndugu kusababu pamoja naye zilikuwa za bure.
Siku iliyofuata, akiwa mwenye furaha na akitabasamu kabisa, alienda kuwaona akina ndugu. Aliwaonyesha majeraha mengi juu ya mwili wake ambapo baba yake alikuwa amempiga sasa hivi. Basi, kwa nini alikuwa mwenye furaha? Baada ya kuondoka kwenye Jumba la Ufalme, baba huyo alikuwa ameuliza watu kadhaa mjini, kutia na mkuu wa mji, juu ya faida na hasara za kuwa kwa binti yake mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mkuu wa mji akasema kwamba Mashahidi ni watu wema, wanaostahili kuaminiwa. Aliongezea kwamba wana maadili bora kabisa na kwamba ingekuwa vizuri sana kuwa na mtoto mwenye viwango hivi, vilivyo vya juu sana kuliko vile vya vijana kwa ujumla.
Ijapokuwa hivyo, msichana huyo akapigwa. Lakini baba huyo akamwambia kwamba alikuwa akimpiga kwa sababu alikuwa ameondoka nyumbani bila ruhusa. Na akasema angempiga tena ikiwa kuna wakati ambapo angeacha kujifunza Biblia au kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova! Sasa binti huyo ni mhubiri mwenye bidii, na wengine wa familia yao wanaonyesha upendezi katika ukweli.
Kwa kweli, Yehova anabariki vijana walio na tamaa ya moyo mweupe kumtumikia, kama ono hili linavyoonyesha.—Zaburi 148:12, 13.y