“Kutoka Kinywani mwa Watoto Wachanga”
SAMWELI alipokuwa mvulana mchanga, alishika kwa uthabiti kanuni za haki ijapokuwa uovu wa wana wa Eli Kuhani Mkuu. (1 Samweli 2:22; 3:1) Katika siku za Elisha, msichana mdogo Mwisraeli aliyetekwa nyara katika Siria alimtolea mke wa bwana wake ushahidi kwa moyo mkuu. (2 Wafalme 5:2-4) Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, aliwasemesha walimu wa Israeli kwa ujasiri, akiwauliza maswali na kutoa majibu yaliyowashangaza watazamaji. (Luka 2:46-48) Katika historia yote, Yehova ametumikiwa kwa uaminifu na waabudu wake wachanga.
Je, walio wachanga leo wanaonyesha roho ya uaminifu kama hiyo? Kwa kweli, ndiyo! Ripoti kutoka ofisi za tawi za Watch Tower Society zaonyesha kwamba waamini wachanga walio wengi sana “wanajitoa kwa hiari” katika utumishi wa Yehova. (Zaburi 110:3) Matokeo mazuri ya juhudi zao yanatia moyo Wakristo wote, wachanga kwa wakubwa, ‘wasichoke katika kutenda mema.’—Wagalatia 6:9.
Kielelezo kizuri ni Ayumi, msichana mdogo Mjapani aliyepata kuwa mhubiri akiwa na umri wa miaka sita na kufanya uwe mradi wake kutolea ushahidi kila mtu katika darasa lake. Alipata ruhusa kuweka vichapo kadhaa katika maktaba ya darasani, akijitayarishia kujibu maswali yoyote ambayo wanashule wenzake huenda wakauliza. Karibu wanadarasa wenzake wote na mwalimu vilevile walipata kuvijua vichapo hivyo. Katika miaka yake sita ya masomo ya msingi, Ayumi alipanga kuwa na mafunzo ya Biblia 13. Alibatizwa akiwa katika gredi ya nne, na mmoja wa rafiki zake aliyejifunza naye alibatizwa akiwa katika gredi ya sita. Zaidi ya hayo, mama na dada wakubwa wa mwanafunzi huyu wa Biblia pia walijifunza na kubatizwa.
Mwenendo Mzuri Ni Ushahidi
“Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa,” akasema mtume Petro, na Wakristo walio wachanga huchukua amri hii kwa uzito. (1 Petro 2:12) Kama tokeo, mwenendo wao mzuri mara nyingi hutoa ushahidi mzuri. Katika nchi ya Kiafrika ya Kamerun, mwanamume fulani alihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa mara ya pili na ikatokea kwamba aliketi kando ya msichana mdogo. Wakati msemaji alikaribisha wasikilizaji watazame fungu fulani katika Biblia, mwanamume huyo alitambua kwamba msichana huyo mdogo alipata mstari ule haraka katika Biblia yake mwenyewe na kwa makini akawa anafuatia usomaji. Mwelekeo wa msichana huyo ulimvutia sana hivi kwamba wakati mkutano ulipoisha, alimwendea msemaji na kusema: “Msichana huyu mdogo amenifanya nitake kujifunza Biblia pamoja nawe.”
Katika Afrika Kusini kuna shule ambapo wanafunzi 25 ni watoto wa Mashahidi wa Yehova. Mwenendo wao mzuri umefanya Mashahidi wa Yehova wapate sifa njema. Mwalimu mmoja alimfunulia siri mzazi mmoja Shahidi kwamba hakuelewa jinsi Mashahidi walivyofaulu kufundisha watoto wao kwa njia nzuri namna hii, hasa kwa sababu dini yake mwenyewe ilikuwa imeshindwa kusaidia walio wachanga. Mwalimu mmoja mpya alikuja kusaidia katika shule na bila kukawia alitambua mwenendo mzuri wa watoto Mashahidi. Akamuuliza mmoja wa wavulana Mashahidi alipaswa kufanya nini ili awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alimweleza kwamba alipaswa kujifunza Biblia, naye akafanya mpango na wazazi wake ili wafuatie kupendezwa huko.
Katika Kosta Rika, Rigoberto aliitambua kweli wakati wanadarasa wenzake walipotumia Biblia kujibu maswali yake kuhusu Utatu, nafsi, na moto wa helo. Waliyoyasema yalimvutia si kwa sababu tu ya uwezo wao wa kutumia Maandiko bali pia kwa sababu ya mwenendo wao mzuri sana uliokuwa tofauti kabisa na alichokuwa ameona katika dini za Jumuiya ya Wakristo. Ijapokuwa upinzani mwingi kutoka kwa familia, Rigoberto anafanya maendeleo mazuri katika funzo lake la Biblia.
Katika Hispania Mashahidi wa Yehova wawili—mmoja wao akiwa na umri wa miaka tisa—walimtembelea mwanamume mmoja aliyeitwa Onofre. Wakati Shahidi aliyekuwa mtu mzima alishiriki katika mazungumzo mengi, Shahidi mchanga alisoma Maandiko kimya-kimya akifuatana nao na kunukuu maandiko fulani ya Biblia kutoka akilini. Onofre alivutiwa. Aliamua kwamba alitaka kujifunza Biblia mahali pale-pale ambapo kijana huyo mchanga alijifunzia kufungua Maandiko kwa njia nzuri hivyo. Kwa hiyo, mapema siku ya Jumapili asubuhi iliyofuata, alienda kwenye Jumba la Ufalme. Ilimbidi kungoja hadi alasiri, wakati Mashahidi walipokuja kwa ajili ya mikutano yao. Tangu hapo na kuendelea, alifanya maendeleo mazuri na karibuni alionyesha wakfu wake kwa ubatizo wa maji.
Mashahidi Wachanga Wenye Matokeo
Ndiyo, Yehova huwatumia walio wachanga na watu wazima pia kuwafikia wenye moyo mpole. Jambo kama hilo lilionekana katika ono kutoka Hungaria. Huko, muuguzi aligundua kwamba wakati wowote wageni walipokuja kumwona mgonjwa fulani mwenye umri wa miaka kumi, wangemletea kitu cha kusoma pamoja na chakula. Akiwa amevutiwa, alishangaa ni kitu gani cha kusoma ambacho kingempendeza msichana huyo mdogo naye akagundua kwamba ilikuwa Biblia. Muuguzi huyo, akazungumza naye na kusema hivi baadaye: “Tangu dakika ya kwanza, alikuwa ananifundisha sana.” Wakati msichana huyo mdogo alipoondoka hospitalini, alimwalika muuguzi huyo ahudhurie mkusanyiko, lakini muuguzi hakufika. Hata hivyo, baadaye alikubali kuhudhuria “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya. Muda mfupi baadaye, alianza kujifunza Biblia, na mwaka mmoja baadaye akabatizwa—yote hayo yakiwa kama tokeo la msichana mdogo kutumia wakati wake hospitalini kusoma fasihi ya Biblia.
Ana Ruth, katika El Salvador, alikuwa katika mwaka wake wa pili katika sekondari. Alikuwa na zoea la kuacha fasihi ya Biblia juu ya dawati lake ili wengine waisome ikiwa wangetaka kufanya hivyo. Alipogundua kwamba fasihi ilikuwa haipatikani na mara inapatikana baada ya muda fulani, Ana Ruth aligundua kwamba mwanashule mwenzake, Evelyn, alikuwa akiisoma. Baada ya muda mfupi, Evelyn alikubali funzo na akaanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Mwishowe, alibatizwa, na sasa anatumika akiwa painia-msaidizi wa kawaida. Ana Ruth ni painia wa kawaida.
Katika Panama dada mmoja alianzisha funzo pamoja na mwanamke mmoja ambaye mumeye alianza kupinga kweli kiasi cha kwamba karibu funzo likome. Hata hivyo, polepole maoni ya mume huyo yakaanza kubadilika. Muda fulani baadaye, ndugu yake wa kimwili, ambaye ni Shahidi, akamwomba amwekee kengele ya kuzuia wezi katika nyumba yake. Alipokuwa akiweka kengele hiyo, mpwa wake wa kike mwenye umri wa miaka tisa akarudi nyumbani akiwa anaonekana mwenye huzuni sana. Akamuuliza ni nini kilikuwa kibaya, naye akamwambia kwamba yeye na dada yake mkubwa walikuwa wameenda kuongoza funzo la Biblia lakini hawakumpata mtu huyo nyumbani, kwa hiyo hakuweza kumfanyia Yehova kitu chochote siku hiyo. Mjomba wake akamwambia: “Kwa nini usinihubirie mimi? Halafu utakuwa umemfanyia Yehova kitu.” Mpwa wa kike wake akakimbia kwa furaha kuleta Biblia yake, na funzo likaanzishwa.
Mama yake (ambaye ni wifi wa mtu huyo) alikuwa akisikiliza. Alifikiri kwamba jambo lote hilo lilikuwa mchezo tu, lakini kila wakati mtu huyo alipowatembelea nyumbani, alimwomba mpwa wake wa kike amfundishe Biblia. Wakati mama huyu alipoona kwamba shemeji yake alichukulia mambo kwa uzito na kuuliza maswali magumu, aliamua kuongoza funzo hilo mwenyewe bintiye akiwapo. Akaanza kujifunza mara mbili kwa juma na kufanya maendeleo haraka. Mwishowe, akafikia hatua ya kujiweka wakfu na akabatizwa katika kusanyiko lilelile ambalo mkeye alibatizwa—yote hayo kwa sababu ya maoni mazuri ya mpwa wake wa kike mchanga.
Moyo Mkuu wa Walio Wachanga Hutoa Ushahidi Mzuri
Biblia husema: “Uwe na moyo mkuu na acha moyo wako uwe imara. Ndio, tumaini katika Yehova.” (Zaburi 27:14, NW) Maneno hayo yanahusu watumishi wote wa Mungu, na walio wachanga na wakubwa pia waliyatumia katika mwaka uliopita. Katika Australia, wakati msichana mwenye umri wa miaka mitano alipoanza shule mpya, mamaye alimwendea mwalimu kumweleza imani za Mashahidi wa Yehova. Mwalimu huyo akasema: “Tayari najua yale mnayoamini. Binti yako amekwisha nieleza kila kitu.” Msichana huyu mdogo hakuwa mwoga sana kumwendea mwalimu wake akiwa peke yake kumweleza imani yake.
Andrea mwenye umri wa miaka mitano katika Rumania pia alionyesha moyo mkuu. Wakati mamaye aliacha imani ya Orthodoksi ili awe Shahidi, jirani zake walikataa kumsikiliza. Siku moja kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko, Andrea akasikia mwangalizi wa utumishi akikazia uhitaji wa kuhubiria jirani. Alifikiri kwa uzito juu ya jambo hili, na waliporudi nyumbani akamwambia mamaye: “Baada ya wewe kwenda kazini, nitaamka, nipange fasihi ndani ya mfuko wangu kama ufanyavyo tu, mama, na nisali kwa Yehova anisaidie nizungumze kuhusu kweli pamoja na majirani.”
Siku iliyofuata Andrea alifanya yale aliyokuwa ameahidi. Halafu, akijipa moyo mkuu, akapiga kengele kwa jirani. Jirani alipoitikia, msichana huyu mdogo akasema: “Najua kwamba tangu mama yangu awe Shahidi, hamumpendi. Amejaribu kuzungumza na nyinyi mara kadhaa, lakini humkutaka kumsikiliza. Hili halimfurahishi, lakini nataka mjue kwamba tunawapenda.” Halafu, Andrea akaendelea kumtolea ushahidi mzuri sana. Kwa siku moja, aligawanya vitabu sita, magazeti sita, vijitabu vinne, na trakti nne. Tangu wakati huo, amekuwa wa kawaida katika utumishi wa shambani.
Katika Rwanda ndugu zetu wamelazimika kuonyesha moyo mkuu kwa ajili ya mzozo ulioko huko. Katika pindi moja familia moja ya Mashahidi waliwekwa ndani ya chumba ambapo wanajeshi walijitayarisha kuwaua. Familia hiyo ikaomba ruhusa ya kusali kwanza. Waliruhusiwa, na wote isipokuwa binti yao, Deborah, walisali kimya-kimya. Kulingana na ripoti moja, Deborah alisali kwa sauti kubwa: “Yehova, juma hili baba na mimi tuliangusha magazeti matano. Tutaweza kurudije kwa watu hawa ili tuwafundishe kweli na kuwasaidia kupata uhai? Isitoshe, nitawezaje sasa kuwa mhubiri? Nilitaka kubatizwa ili nikutumikie.” Aliposikia hayo, mwanajeshi mmoja akasema: “Hatuwezi kuwaua kwa sababu ya msichana huyu mdogo.” Deborah akaitikia: “Asanteni.” Familia hiyo ikahifadhiwa.
Yesu alipoingia Yerusalemu kwa ushindi karibu na mwisho wa maisha yake ya kidunia, alipokewa na mkutano mkubwa sana, wenye furaha. Mkutano huo ulifanyizwa na watoto pamoja na watu wazima. Kulingana na rekodi hiyo, wavulana wachanga “waliokuwa wakipaaza kilio hekalu na kusema: ‘Okoa Mwana wa Daudi, twasihi!’” Wakati wakuu wa makuhani na waandishi walipowakataza jambo hili, Yesu akawaambia: “Je, nyinyi hamkusoma kamwe hili, ‘Kutoka kinywani mwa watoto wachanga na watoto wanyonyao umetoa sifa’?”—Mathayo 21:15, 16, NW.
Je, si jambo la kusisimua kuona kwamba maneno ya Yesu ni ya kweli hata leo? “Kutoka kinywani mwa watoto wachanga na watoto wanyonyao”—na, ebu tuongeze, matineja na vijana wavulana na wasichana—Yehova ameweka sifa. Kwa kweli, kwa habari ya kumsifu Yehova, hakuna umri wa chini zaidi.—Yoeli 2:28, 29.