Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 1/15 kur. 33-38
  • Tunawafurahia Vijana Wanaotembea Katika Njia ya Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tunawafurahia Vijana Wanaotembea Katika Njia ya Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSHINDA UPINZANI
  • KUSIMAMA IMARA
  • KUSHIRIKI HABARI NJEMA NA WENGINE
  • Vijana—Fanyeni Moyo wa Yehova Ushangilie
    Huduma Yetu ya Ufalme—1993
  • “Kutoka Kinywani mwa Watoto Wachanga”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Mahali pa Vijana Katika Jamii ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 1/15 kur. 33-38

Tunawafurahia Vijana Wanaotembea Katika Njia ya Yehova

“Wewe ndiwe taraja langu, Ee Bwana [Yehova], tumaini langu tokea ujana wangu.”​—Zab. 71:5.

1. Ni jambo gani la maana hata zaidi kwa wazazi kuliko kuona mtoto wao akitembea hatua za kwanza?

WAZAZI wanafurahije mtoto wao mdogo aanzapo kujua kutembea! Wanaona fahari iliyoje kumwona akitembea hatua chache za kwanza! Lakini, wakati upitapo, hatua zake zitamwelekeza katika njia gani? Atajifunza kufuata njia anayoonyesha Yehova? Je! wazazi wake watasaidia kumwelekeza katika njia hiyo? Je! ataijua “njia ya uzima” na “njia iliyonyoka”? Au atageukia njia ya waovu, aifuate njia ya wale wanaomsahau Mungu? Hayo yanategemea sana kuzoezwa kwa mtoto mapema na mafundisho atakayopewa na wazazi wake.​—Zab. 16:11; 27:11; Mit. 4:14, 18.

2. Ni maelekeo gani yanayoonyeshwa na mwandikaji anayejulikana sana?

2 Ilikubaliwa kwamba watoto wengi wanauacha mwendo unaofaa katika makala ya karibuni iliyoandikwa na James Michener. Ingawa kichwa chake kilikuwa “Mambo Yaliyo Mema juu ya Vijana wa Leo,” ilionyesha magumu ya karibuni ya vijana, ikasema juu ya “uasi wa vijana wenye msukosuko wa miaka ya karibuni,” “mtengano wa wazazi na watoto na wa mambo ya utamaduni,” “usitawi wa dawa za kulevya” na maelekeo ya kufanya jeuri. Makala yake ilisema hivi: “Kwa mfano, katika Philadelphia miaka ya karibuni, kumekuwa na mauaji karibu arobaini na manane kati ya watoto wa shule, na mengi yayo yalifanywa walipokuwa wakielekea shuleni au walipokuwa wakielekea nyumbani kutoka shuleni. Hayo si maendeleo; hayo ni maasi makubwa sana sana. Mimi naona vijana wa umri mbalimbali wakiwa wakatili, wakikosa kuitikia adabu na, zaidi ya yote, wamebadili nia yao kabisa juu ya matumizi ya maneno, na sasa wanatumia usemi ulio mchafu zaidi.”

3. Ugumu wa uasi wa watoto ni mkubwa namna gani?

3 Ugumu uo huo unaonekana kwa vijana ulimwenguni pote. Makala moja katika gazeti Daily Mail la London ilisema hivi: “Watoto wa hata miaka 10 wanazidi kuwa wahuni na kuvunja sheria vibaya sana. Upelelezi wa uvunja sheria unaonyesha hesabu ya vijana wanaohusika inaongezeka ajabu.” Habari zilitoka Brazil juu ya “kuanza hatua ya kuadhibu vijana kwa uvunjaji wa sheria unaoenea sana katika Sao Paulo na Rio de Janeiro. Polisi wanakadiri kwamba uasi wa watoto utaongezeka kwa karibu kiasi cha 12 kwa mia mwaka huu. ‘Wazazi wengine hata wanafundisha wana wao njia za kutumia,’ alisema polisi mmoja.” Mwaka jana katika Los Angeles watoto wengi zaidi (jumla ya 104) kuliko watu wazima walifanyiwa kesi kwa sababu ya uuaji. Katika Ireland askari mmoja alikufa wakati kikundi cha watoto kilipopiga gari lake la upelelezi kwa mawe, kukawa na uharibifu mkuu. Katika mji wa New York kisichana cha miaka kumi na mitatu kilikamatwa katika afisi ya kuwekea akiba ya pesa kwa kusimamisha mtu kimnyang’anye. Imeripotiwa kwamba katika United States kwa wastani umri wa vijana wanaotoroka nyumbani sasa ni miaka kumi na mitano, na watoto wa umri huo wanatumia sana dawa za kulevya. Kwa hiyo ni wazi kwamba watoto wanaweza kuingia katika matata makubwa hata wakiwa wadogo. Je! wewe unaweza kusaidia watoto wako waepuke magumu hayo?

4. Kulingana na Biblia, ugumu huo umepaswa kutushangaza, na ni nini kinachosaidia watoto mara nyingi?

4 Ingawa jamaa nyingine zinazojitahidi kuitumia Biblia katika maisha yao bado zinaona watoto wao hawaitikii na wakiwa waasi, hiyo haishangazi hata kidogo tukichunguza kisa cha Yakobo na Esau, wana wawili wa jamaa ile ile moja waliofuata miendo tofauti maishani, au tukifikiria vile unabii wa Biblia unavyoonyesha kwamba “siku za mwisho” watoto wangekuwa “wasiotii wazazi wao.” (2 Tim. 3:1, 2) Lakini, magumu hayo yanatokea mara nyingi zaidi katika jamaa ambamo watoto hawapewi maongozi ya Maandiko.

5. Kwa sababu gani wazazi na watoto wengi wanaweza kusifiwa?

5 Kwa hakika wazazi wenye watoto waamini wamepaswa wasifiwe kwa jitihada ambayo wamefanya kufundisha jamaa zao Neno la Mungu na makusudi yake. Watoto pia wanastahili sifa, hasa tunapofikiria mikazo ambayo wengi wanawekewa na wenzi wasioamini na hata waalimu wanaodharau maoni ya Biblia. Tena, vijana wengi wamethamini hekima ya Neno la Mungu ingawa wamevunjwa moyo au kupingwa na wazazi wao au wengine katika jamaa. Kwa sababu ya kujifunza Biblia wamesema kama alivyosema mtunga zaburi: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.”​—Zab. 119:105.

KUSHINDA UPINZANI

6. (a) Ndugu kijana katika Trinidad alipatwa na upinzani gani? (b) Alifuata shauri gani la Maandiko?

6 Kivulana mmoja aliyejifunza Maandiko Trinidad alipingwa sana na jamaa yake, hasa na shangazi wake. Wakati mmoja shangazi alirarua suruali yake kumzuia asiende mkutanoni. Wakati mwingine alikwenda kwenye Jumba la Ufalme kufanya matata ili amvunje moyo asihudhurie. Mama yake akawa akimpiga. Alipopangwa kutoa hotuba yake ya kwanza ya watu wote viatu vyake vikafichwa, kwa hiyo ikamlazimu aazime vingine kwa jirani. Hata hivyo sasa yeye yumo katika utumishi wa wakati wote wa Kikristo naye ameweza kusaidia wengine katika jamaa yake kiroho. Kwa hiyo, amesema kama isemavyo Zaburi 119:57-61: “[Yehova] ndiye aliye fungu langu, nimesema kwamba nitayatii maneno yako. Nimekuomba radhi kwa moyo wangu wote, unifadhili sawa-sawa na ahadi yako. Nalizitafakari njia zangu, na miguu yangu nalizielekezea shuhuda zako. Nalifanya haraka wala sikukawia, kuyatii maagizo yako. Kamba za wasio haki zimenifunga, sikuisahau sheria yako.”

7. Msichana mmoja alipata baraka gani kwa kulitumaini Neno la Yehova, ujapokuwapo upinzani?

7 Katika jamaa nyingine binti aeleza kwamba ndugu yake ndiye aliyejifunza kweli kwanza kisha akaanza kumfanya yeye apendezwe nayo, lakini kwa sababu fulani mama yao akawakataza wasijifunze. Ili waendelee kujifunza ikawalazimu wafanye hivyo kwa siri, wakawa wakijifunzia chini ya meza wasionekane, lakini karibuni mama yao akawakomesha na kuwakataza hata kulitaja jina la Yehova nyumbani. Baadaye binti huyo alipelekwa kwenye shule ya wasichana akalazimishwa kwenda kanisani, ingawa alimwomba padre aruhusu mmoja wa mashahidi wa Yehova aje na kujifunza naye. Waalimu shuleni walimchokoza sana juu ya imani zake na wanadarasa wengi wakamdhihaki na kujaribu kumchokoza-chokoza ndio wapigane. Baadaye, alipopelekwa akatunzwe katika nyumba ya mwanamume mmoja na mkewe waliokuwa Walutheri, hakuacha imani yake ingawa walimpinga sana na mwishowe wakamfukuza. Alipokuwa katika shule ya masomo ya juu aliikubali nafasi ya kuhutubia darasa lake wakati wa masomo ya sayansi juu ya habari “Je! Mwanadamu Alitokea kwa Mageuzi au kwa Kuumbwa?” Kisha akawaachia vitabu 24 na kuanza funzo la Biblia. Mmoja wa vijana aliojifunza nao sasa ni shahidi wa Yehova aliye wakf, naye dada huyo kijana amekuwa painia wa kawaida zaidi ya miaka mitatu. Mambo kama hayo yaliyoonwa yanaonyesha kwamba vijana wanaweza kutembea katika njia ya Yehova hata uje upinzani gani, wakisema kwa sababu hiyo: “Nimelitumaini neno lako . . . nami nitaishika sheria yako daima, mpaka wakati usiojulikana, hata milele.”​—Zab. 119:42-44, NW; Mhu. 12:1.

8. Wazee wanawezaje kutia nguvu vijana wanaopingwa kwa sababu ya kujitahidi kufuata njia ya Yehova?

8 Inafaa makundi yenye watoto wanaopingwa hivyo na jamaa yawatie moyo yawezavyo. Wazee katika makundi wasaidie na kutia moyo vikundi vikundi vya jamaa, na hasa vijana wanaotoka katika nyumba zilizogawanyika kidini, wazungumze nao katika Jumba la Ufalme, wawatembelee nyumbani kwao ikiwa inafaa, na kuwakaribisha washirikiane kiroho na katika tafrija pia pamoja na jamaa zao wenyewe inapofaa. Mashahidi hao vijana wajulishwe kwamba wengine kundini wanapendezwa sana nao, na ni vema kuzungumza nao juu ya mambo wanayofanya, miradi yao maishani, kuwapa mashauri inapofaa kana kwamba baba zao na kutoa mengine katika Maandiko. Hayo yote yanahusika katika kuwa mzee na yanaonyesha tena kwamba mzee anafurahia vijana hao wanaojaribu sana kutembea katika njia ya Yehova ingawa wanawekewa vizuizi. Kwa kutiwa moyo hivyo na washirika wao kundini, vijana watasema hivi: “Mimi ni mwenzao watu wote wakuchao, na wale wayatiio mausia yako. [Yehova], dunia imejaa fadhili zako, unifundishe amri zako.”​—Zab. 119:63, 64.

KUSIMAMA IMARA

9. Ni maandiko gani yamesaidia vijana watoe ushuhuda mzuri juu ya kutokuwamo kwa Kikristo?

9 Ukamilifu na kutokuwamo kwa vijana wa Kikristo unajaribiwa kwa njia nyingi, hasa wakati wa miaka ya kwenda shule. Mara nyingi ulizo linatokea juu ya nyimbo za taifa au za shule na kusalimu bendera, kwa maana nchi zinataka kutia utukuzo wa taifa ndani ya wanafunzi. Mashahidi wengi wa Yehova wa Kikristo wamepinga mikazo hiyo kwa imara, kwa njia hiyo wakaendeleza kutokuwamo kwao kwa Kikristo ingawa wengine wamefukuzwa shuleni. Lakini, wale ambao wamekumbuka kanuni ya Maandiko iliyo katika Kutoka 20:4, 5 (“Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote . . . usivisujudie wala kuvitumikia”) na mfano ulioandikwa katika Danieli sura ya 3, wa wale Waebrania watatu waaminifu ambao hawakuabudu sanamu, wametiwa nguvu kuvumilia majaribu hayo, na kwa njia hiyo wakatoa ushuhuda mzuri sana kwa wakuu wa shule na wa serikali.​—Mit. 20:11.

10. Kusimama imara kwa mwanashule mmoja kuliletaje baraka?

10 Kisichana cha miaka kumi na mmoja California kilifikiwa na mwanashule mwenzake akakiuliza kama yeye ni mmoja wa mashahidi wa Yehova; mwanashule huyo aliona lazima hiyo iwe ndiyo sababu kisichana hicho hakikusimama wakati wa wimbo wa taifa wala hakikuuimba. Babu na bibi wa msichana mwenye kuuliza walikuwa wamemfanya apendezwe na kweli naye alitaka kujifunza Biblia, ingawa wazazi wake hawakupendezwa. Wengine wakaanza kupendezwa kujifunza, hata wakati mmoja wasichana kumi na mmoja walikuwa wakijifunza pamoja wasipokuwa na masomo shuleni. Wengine walipata ushuhuda mzuri kwa sababu kisichana hicho kilitegemeza imani yacho.

11. (a) Ni maulizo gani mengine yanayowapata Mashahidi vijana? (b) Ni mikazo gani inayowapata vijana kuwaachisha kanuni za Biblia, nayo imeshindwaje?

11 Hata ikiwa ulizo la utukuzo wa taifa si kubwa, huenda mikazo mingine ikatokea. Mwanafunzi hodari huenda akasihiwa aendelee na “masomo ya juu zaidi” au huenda akashawishwa apate faida za kimwili katika kazi ya kimwili. (1 Tim. 6:17, 20, 21) Shuleni wengi wanapatwa na mikazo wafuate mitindo ya mavazi na ya nywele. Lakini Mashahidi vijana wamekataa kuvalia kama vijana wa kilimwengu, wakaepuka kufuata kanuni za mavazi yasiyo ya adabu na yanayoweza kuongoza kwenye ufisadi au kuwafanya wapangwe katika fungu moja na waasi. Dada mmoja kijana alichokozwa-chokozwa akiambiwa yeye ‘hagusiki’ kwa sababu ya kuvalia kwa adabu, lakini yeye akaeleza kwamba alifuata kanuni hiyo kwa kwa kuwa alikuwa mmoja wa mashahidi wa Yehova. Baba mwenye jamaa ya watoto saba alisema kwamba hawajawa na ugumu wa mavazi yasiyo ya adabu wala mitindo ya kupita kiasi ya nywele, kwa maana wazazi walisisitiza juu ya kuwa na urefu fulani wa nywele na adabu katika mitindo ya mavazi. Hiyo imelinda jamaa, kwa maana sasa watoto wanaona mavazi ya wenzao katika ujirani yakiwa ya kustaajabisha na hawataki kushirikiana nao.

12, 13. Kanuni za Biblia zinawezaje kuwa ulinzi?

12 Vilevile, wazazi hao wameweza kuongoza watoto wao juu ya mambo ya kujifurahisha kwa kuwawekea kanuni zinazopatana na zile za Biblia kwa habari ya muziki, kusoma na kutazama televisheni. Mazoezi hayo yanakuwa yenye mafaa sana baadaye, wakati ambapo watoto wamekuwa wa umri wa kujichagulia mambo ya kuwafurahisha, namna za sinema watakazoona, nyimbo watakazoimba, mambo watakayopendezwa nayo.

13 Kuogopa kumchukiza Yehova kutasaidia pia kuepuka mikazo shuleni​—majaribio ya kufanya hivi au vile, kutia na kutumia dawa za kulevya. (Zab. 111:10) Mashahidi wengi vijana wameona kwamba wanajilinda vizuri zaidi wasipatwe na matata au wasiwe na washirika wabaya kwa kueleza wengine imani yao. Mtu akijulikana kuwa shahidi wa Yehova kwa sababu ya kuzungumza juu ya kweli ya Biblia apatapo nafasi, hiyo itafukuza wale wasio na moyo mwema au kanuni bora, lakini itavutia wale walio nazo.

KUSHIRIKI HABARI NJEMA NA WENGINE

14. Mashahidi wengi vijana wamefanya nini washiriki kweli na wengine shuleni? Tia na mambo yaliyoonwa kwenu.

14 Mashahidi wengi vijana wametumia vizuri nafasi za kushiriki habari njema na wengine shuleni, wakatolea waalimu na wanadarasa wenzao ushuhuda. Wengi wametumia habari za Biblia au za vitabu vya Watch Tower Society walipokuwa wakitoa ripoti za shule au maelezo katika mazungumzo ya darasani. Wanafurahia kutumia vizuri nafasi zinazofaa za kutoa ushuhuda shuleni, nyakati nyingine wakitoa magazeti ya pekee yanayopendeza au nakala za kitabu Evolution, nayo maelfu ya nakala za kitabu hicho yameangushwa kwa njia hiyo. Wameona ukweli wa maneno ya mtunga zaburi: “Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote, maana shuhuda zako ndizo nizifikirizo.”​—Zab. 119:99.

15. Simulia mfano wa kutoa ushuhuda uliotolewa shuleni na kijana aliye macho.

15 Katika mkoa wa Arkansas, msichana Shahidi alikumbuka makala ya Awake! iliyozungumza juu ya kushona nayo ingefaa kwa masomo ya kipindi cha siasa ya nyumbani (home economics), kwa hiyo akamletea mwalimu, naye akasomea darasa zima. Baadaye, alipeleka vitabu vingine, naye mwalimu akaanza kujifunza. Katika Ujeremani, kijana Shahidi alifanya uchunguzi wa habari za dawa za kulevya, akiwa na kusudi la kutoa ushuhuda wakati darasa litakapokuwa na mazungumzo baada ya kuonyeshwa sinema iliyohusu dawa hizo. Mwalimu alipomwuliza maoni yake ni nini kama mmoja wa mashahidi wa Yehova, alieleza vizuri sana hata akaruhusiwa kutolea madarasa mawili hotuba kwa zaidi ya saa mbili, akitumia Maandiko na vitabu alivyokuwa ameleta. Baadaye, alikaribishwa ahutubie madarasa kumi na sita kwa saa nne. Kwa ujumla, wanafunzi 691 walisikiliza, na mamia ya magazeti yakaangushwa.

16. Wengine wameshirikije kweli pamoja na wanadarasa wenzao?

16 Katika Cyprus, kivulana cha Kikristo cha miaka tisa kilipata nafasi ya kutoa ushuhuda mzuri ulizo lilipotokea darasani juu ya imani ya mashahidi wa Yehova. Wengine walisema hivi na vile, lakini yeye akasema ndiye anayeweza kujibu ulizo hilo vizuri zaidi maana yeye mwenyewe ni Shahidi kisha akatoa hotuba ya bila kutazamia akionyesha kwamba mashahidi wa Yehova ni Wakristo wanaomwabudu Yehova, kwa maana Yeye ndiye Muumba na Baba pia wa Yesu. Akajibu kipingamizi kimoja kwa kuonyesha kwamba kutohusika katika vita ya kutumia silaha kwapatana na maneno yaliyosemwa na malaika wakati wa kuzaliwa kwa Yesu: “duniani amani miongoni mwa watu wenye nia njema.” (Luka 2:13, 14, NW; linganisha Mathayo 11:25.) Mwingine aliyetumia vizuri nafasi atoe ushuhuda ni msichana wa Kikristo katika California aliyechaguliwa ahutubie darasa lake lenye kuhitimu. Shahidi huyo wa Yehova alihutubia watu 800 juu ya habari “Tumaini Langu la Wakati Ujao,” akatoa ushuhuda mzuri ajabu juu ya ahadi za Biblia. Lakini, kama yeye alivyosema, “Nisingaliweza kufanya hivyo bila msaada wa Yehova.”

17. (a) Tamaa na Jitihada zinawezaje kusaidia kufanya mtu aone yaliyoonwa na Shahidi kijana katika Chile? (b) Wahubiri vijana wenye kutoa ushuhuda wanatumiaje wazo la Zaburi 119:46-48?

17 Je! wewe umepata kutumia vizuri nafasi kama hizo utoe ushuhuda? Huenda ukapata pendeleo zuri sana kama lile alilopata mhubiri wa miaka kumi na mitatu wa ufalme wa Mungu katika Chile. Mwalimu wake alikuwa akieleza darasa kwamba Biblia ni hadithi tu na kwamba mageuzi ni ya kweli, kwa hiyo mhubiri huyo akaeleza sababu hakukubaliana naye. Muda si muda wengine kati ya wanafunzi wakamwomba awafundishe Biblia, na karibuni akawa akifundisha kikundi cha wanafunzi 27 mara mbili kwa juma. Alijitayarisha kwa uangalifu hata akawapa mitihani ya kuandika. Mwishoni mwa mwaka msimamizi wa shule akakubali maksi yaliyopatikana katika mitihani hiyo yahesabiwe kati ya maksi ya masomo mengine ya shule. Sasa watoto watatu kati ya kikundi hicho wanafika mikutanoni.​—Zab. 119:46-48.

18. Wengi wamefurahiaje kumtumikia Yehova wakati wa ujana, nao wamepata faida gani?

18 Wengine wametumia vizuri nyakati za sikukuu na likizo za shule kwa utumishi wa shambani wanapokuwa hawana kazi, na wengi waliobatizwa wameshiriki katika kazi ya upainia wa muda. Hii inasaidia kusitawisha hali yao wenyewe ya kiroho, na vilevile kuelekeza wengine kundini. Mara nyingi utumishi huo wa upainia wa muda unaongoza kwenye utumishi wa kuhubiri wakati wote. Ni kama vile msichana mmoja wa Kikristo ambaye amefurahia kazi hiyo ya wakati wote kwa miaka minne alivyoandika karibuni: “Kama tu nikiweza kuwaonyesha ndugu na dada wote vijana furaha inayopatikana katika kumtumikia Yehova ujanani itakuwa vizuri sana. Huenda vijana wengi wakadhani watakazwa na kazi mno wakiingia kazi ya kuhubiri wakati wote, lakini sivyo kabisa. Ukifanya hivyo unajisikia kana kwamba una uhuru zaidi, maana unajua unafanya linalokupasa kuwa ukilifanya, nawe unapokuwa na wakati wa kutumia kwa mambo yako mwenyewe unaweza kuufurahia ukiwa na amani nyingi ya akili na dhamiri safi.”

19. Imetupasa tufikirie nini tunapojiwekea miradi maishani, nao vijana wanawezaje kusaidiwa katika jambo hilo?

19 Miradi ambayo vijana wanaonyeshwa na jamaa zao na kundi pia inawasaidia watembee katika njia ya Yehova. Wewe una miradi gani? Je! unafikiria utumishi wa shambani wa wakati wote na kufanya mapenzi ya Yehova? Au miradi yako inahusu mapendezi yako mwenyewe tu, kupata kazi, kununua gari, kutazamia ndoa? Ingawa hakuna ubaya wa miradi hiyo, ikiwa peke yake inakosa kitu kinacholeta furaha maishani​—kumtumikia Muumba wetu. Inapatana na tamaa za watu wa siku za Nuhu ‘wasiotambua’ onyo la Nuhu “hata Gharika ikaja, ikawachukua wote.” (Mt. 24:38-42) Watoto wanapotiwa moyo na jamaa watangulize utumishi wa Ufalme katika maisha zao, wanaitikia kwa furaha. Ndivyo imekuwa kwa jamaa moja yenye wasichana watano ambao sikuzote walitiwa moyo waufanye upainia kuwa mradi wao baada ya kumaliza masomo ya juu. Sasa watatu wanashiriki katika utendaji huo na dada zao wadogo wamefurahia kufanya upainia wa muda pamoja na wazazi wao.

20. Mashahidi vijana wanaweza kufanya nini wasaidie kundi katika njia zinazothaminiwa sana?

20 Mtu aingie au asiingie katika kazi ya kuhubiri wakati wote, wote wanaweza kutoa maelezo yenye kujenga mikutanoni na kushiriki katika mpango wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika Jumba la Ufalme. Vijana wanapojitahidi kushiriki katika njia hizo wanafurahiwa na wote. Wengine wanafurahi kushiriki kusafisha jumba liwe lenye kupendeza. Vijana wengi wamefanya kazi pamoja na watu wazima kundini kujenga Jumba la Ufalme, nao wamefurahia ushirika wa kiroho wenye kujenga pamoja na ndugu zao, licha ya kujifunza machache juu ya ujenzi. Na baadaye kunakuwa na nafasi za kushiriki kutunza bustani na viwanja au kusaidia kwa mambo yanayopaswa kufanywa ndani, kupanga jukwaa, kurekebisha vikuza-sauti, kusaidia kusafisha au kazi nyinginezo. Watu wengi wanasifu mwenendo mwema wa wahubiri vijana katika Jumba la Ufalme. Inapendeza sana ndugu na dada wadogo wanaposalimu wageni na kujijulisha kwao au wanapomshukuru msemaji kwa hotuba yake. Na kwa kuwa watoto wengi sana wanakuja mikutanoni, mfano mwema wa wale ambao wamejifunza kuwa na mwenendo wa busara na kusikiliza wakati programu inapoendelea unasaidia sana kuwapa wapya au watoto wadogo zaidi mfano wa kufuata.

21. Ni mapendeleo gani yaliyoko mbele ya wale wanaotembea katika njia ya Yehova?

21 Wazazi wengi wametaja furaha ambayo wamepata kwa kuona watoto wao wakifanya maendeleo ya kiroho, wakishinda mikazo ya kilimwengu na kufikia mapendeleo ya utumishi, wengine wakawa mapainia au wamisionari, wengine wakaanza kazi ya mwangalizi wa mzunguko au wa wilaya, wengine wakawa washiriki wa jamaa ya Betheli, na wengi wakawa watumishi wa huduma na wazee katika makundi. Sifa ya maendeleo mengi kati ya hayo inaweza kutolewa kwa msingi mwema waliowekewa walipokuwa wadogo. Kwa kushirikiana katika mipango hiyo ya jamaa na ya kundi, vijana wanaweza kutazamia kubarikiwa na Yehova na kuthawabishwa.​—Mit. 22:6.

22. Kutoka 20:12 inatumikaje nyakati za kisasa?

22 Si vyepesi kuendeleza ukamilifu mtu anapokuwa katika mkazo wa taratibu hii ya mambo, lakini wale ambao wamekata shauri kutembea katika njia ya Yehova watabarikiwa na kutegemezwa naye. Kama vile Kutoka 20:12 inavyoshauri: “Waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na [Yehova], Mungu wako.” Maneno hayo yalipewa kwa Israeli kabla hawajaingia katika Nchi ya Ahadi na kwa hiyo yana maana sana sana tunapokaribia mwisho wa taratibu hii ya mambo na tunapoona taratibu mpya yenye haki ikikaribia mbio mbio. Ni jambo la maana vijana waheshimu na kustahi si baba na mama zao tu, bali pia Baba wa kimbinguni, Yehova, na tengenezo lake lenye mfano wa mke. (Mit. 1:8, 9) Kwa kufanya hivyo wanaweza kutazamia kwa hakika kuwa na nafasi katika taratibu mpya hiyo ambayo Yehova ameahidi. Naam, tunawafurahia vijana wanaotembea katika njia ya Yehova.​—Mit. 3:1-7.

​—Kutoka The Watchtower, July 15, 1975.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki