Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 3/15 kur. 9-14
  • Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nguvu za ile Kweli
  • Utumishi wa Kimungu
  • Kuthamini
  • Utendaji Wenye Kufaa
  • Msaada wa kutoka Nje
  • Mfano Wako Mwenyewe
  • Kulea Watoto Wenye Furaha Katika Ulimwengu Wenye Mchafuko Mwingi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Kujenga Familia Yenye Nguvu Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Je! Wewe Unafundisha Watoto Wako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 3/15 kur. 9-14

Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova

“Mwanangu, kama moyo wako una hekima, Moyo wangu utafurahi, naam, moyo wangu.”​—Mithali 23:15.

1. Wazazi wanaweza kuwa na furaha gani ya pekee, na wewe ukiwa mzazi unapaswa kufanya nini kuhusu hilo?

NI FURAHA kama nini kuwaona watoto wadogo wakikua na kuwa watumishi wa Mungu waliokomaa! Hatua kwa hatua wanasitawisha utafiti (kutaka kujua), wanatwaa maarifa, wanakuwa na uwezo wa kutimiza mambo, wanajiweka upande mmoja na kweli ya Kikristo, wanasitawisha ukomavu, wanajiweka wenyewe wakf kwa Mungu na kuwa watumishi wake waaminifu. Ikiwa wewe ni mzazi, unawezaje kuwasaidia watoto wako katika barabara hiyo nzuri? Kwa wazi hilo linachukua wakati. Mtume Paulo aliuliza ingewezekanaje ‘wamwamini yeye wasiyemsikia,’na wasikieje wasipofundishwa na mtu fulani?​—Warumi 10:14.

2. Twawezaje kuwasaidia Watoto wetu wamthamini Yehova Mungu?

2 Watoto wadogo wanakuwa wenye kujawa na mshangao. Kipepeo, ndege, ua,’Unyasi, anga, nyota​—⁠vitu hivyo vyote vinawavutia. Hilo linatupa nafasi nzuri kama nini za kuzungumza juu ya Muumba na sababu tulizo nazo za kumshukuru! Mtunga zaburi aliandika hivi: “Ni neno jema kumshukuru [Yehova].” (Zaburi 92:1) Unaweza kumshukuru kwa ajili ya maajabu ya maumbile, kwa ajili ya mambo ya lazima ya maisha ya kimwili na kwa ajili ya kweli ya Neno lake. Watoto wako wataona hali yako ya kushukuru nao hawataisahau kamwe.​—Zaburi 8:3, 4; 19:1; Warumi 1:20; Kumbukumbu la Torati 8:10; Mithali 22:6.

3. Ni njia gani moja nzuri ya kuwafundisha watoto wetu? Toa mifano.

3 Watoto wanapenda hadithi. Mungu alijua jambo hilo. Yeye aliandikisha hadithi nyingi za kweli katika Biblia​—hadithi ambazo zaweza kuwafunza hata watoto wachanga sana juu ya njia za Mungu. Kwa mfano, hadithi hizo zinaonyesha twapaswa kuwa na imani kama Ibrahimu, kumtumaini Yeye kama walivyofanya Yoshua na Kalebu, kumtii Yeye wakati wa ujana kama walivyofanya Samweli na Timotheo, na kusimama imara kwa ajili ya imani yetu kama vijana Shadraka, Meshaki na Abednego.a

4. Tuna mifano gani ya watoto waliojifunza njia za Mungu, wakati wa leo na katika nyakati za Biblia pia?

4 Watoto wanajifunza haraka sana. Wanajifunza semi za kutangaza bidhaa za kibiashara na mambo mengi ambayo nyakati nyingine unaona afadhali wasingeyasikia. Ni jambo la maana zaidi kama nini kuwasaidia wajifunze juu ya Mungu na njia zake! Watu wengi wametoa maelezo ya mshangao juu ya namna watoto wanavyoweza kutoa maelezo mazuri katika mikutano ya Kikristo, na namna wanavyoweza kushiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi wakiwa wenye umri mdogo. Vijana hao ni mifano halisi ya ubora wa maagizo ya Biblia juu ya kuwazoeza watoto. Wazazi Waisraeli walipaswa kuwafunza watoto wao wakati wote, na hata “watoto” waliletwa wasikilize sheria ya Mungu ikisomwa. Wana wao walipaswa kusikiliza na “kujifunza kumcha [Yehova], Mungu wenu.”​—Kumbukumbu la Torati 31:12, 13; 6:5-9.

5, 6. Unawezaje kuwasaidia watoto wako wajifunze njia za Mungu?

5 Huenda ukawa unajua mengi sana juu ya Neno la Mungu, lakini hilo halimaanishi kwamba watoto wako wanayajua. Wao hawarithi maarifa. Ni juu yako ukiwa mzazi kuwafunza mambo ya ajabu ya Mungu na kuyafanya yavutie, ili watake kujifunza.

6 Je! watoto wako wanayafahamu mafundisho ya Biblia? Je! wamekwisha kujifunza kanuni zayo kwa ajili ya maisha ya kila siku? Je! unakuwa na funzo la Biblia la kawaida la jamaa pamoja nao? Ikiwa wangali wadogo, je, mmejifunza kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu, chenye vichwa vya habari 46 ambazo zimeandikwa kulingana na uwezo wao wa kufahamu? Ikiwa umekwisha kufanya hivyo, na watoto wako wanakua, je, umejifunza nao kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako, ambacho kinatoa habari yenye kutokeza sana ya kuwasaidia vijana wakabili maisha kama yalivyo? Biblia inasema kwamba “tangu utoto” kijana Timotheo alifunzwa mambo kama hayo. Hangaiko la Yakobo juu ya “kadiri ya mwendo wa watoto” walipokuwa njiani kwenda Seiri linaonyesha umaana wa wewe kwenda kulingana na uwezo wa mwendo wao. Funzo lenu pamoja lapasa kuwa la kadiri wanayoweza kufahamu, na la urefu wa kiasi kwa umri wao.​—2 Timotheo 3:15; Mwanzo 33:14.

Nguvu za ile Kweli

7, 8. (a) Kwa sababu gani maarifa ya ile kweli ni ya maana sana? (b) Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wathamini mikutano ya Kikristo?

7 Kweli ya Mungu ni kani yenye nguvu sana. Inaweza kubadili kuwaza na utu wa watu wazima. Biblia inasema “mpate kuuvua utu wa kale unaofanana na namna ya mwenendo wenu wa zamani na . . . mpate kufanywa wapya katika nguvu yenye kuendesha akili zenu.” (Waefeso 4:22-24, NW; Wakolosai 3:9, 10) Ikiwa ni yenye nguvu sana hivyo, kweli ya Kikristo inaweza kuwapa watoto wako ulinzi mkubwa. Tena na tena vijana wanaonyesha kuthamini kwao kwa ajili ya jitihada za kawaida ambazo wazazi wao walifanya za kuwapeleka kwenye mikutano ambako Neno la Mungu linazungumzwa, wawe walitaka kwenda au hawakutaka hapo kwanza. Tineja mmoja alisema: “Kwa kweli hapo kwanza sikutaka kwenda. Sikufahamu mengi sana. Halafu ningesisimuka sana kwa sababu niligundua: He-e-e-he, ninajifunza juu ya Biblia!”

8 Wazazi wengi wanatangulia kujitayarisha pamoja na watoto wao, ili watoto wafahamu. Wengine wanawatia moyo watoto wao wakumbuke mambo machache ya mkutano na kuyazungumza wanapokuwa wakirudi nyumbani. Twaweza kuwazia mazungumzo yenye msisimuko kama hayo wakati jamaa za Kiisraeli zilipokuwa zikirudi kutoka kwa ibada yao Yerusalemu.​—Kumbukumbu la Torati 31:10-13; Luka 2:41, 42.

Utumishi wa Kimungu

9, 10. Unaweza .kufanya nini ili kuwasaidia watoto wako wathamini na kufurahia utumishi wa Kikristo?

9 Kuhusu kushiriki katika kazi ya kuhubiri watu wote, huenda vijana wako wakauona utumishi wa kimungu kidogo kama alivyouona Yeremia: “Aa, Bwana [Yehova]! tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” Kwa hiyo, ni jambo la maana kuwazoeza, hatua kwa hatua. Kwa kulingana na umri wao na maendeleo wanayofanya wanaweza kupiga kengele ya mlango, kutoa ukaribishaji, kusoma Andiko, kutoa vitabu ambavyo msingi wavyo ni Biblia kwenye nyumba katika ujirani wao, pengine hata kuongoza mafunzo ya Biblia.​—Yeremia 1:6, 7.

10 Nia yako mwenyewe itakuwa na matokeo makubwa juu ya watoto wako. Shahidi mmoja kijana anasema hivi: “Hakika mama yangu anafurahia utumishi. Kila mara anaporudi ana jambo zuri la kusimulia.” Vijana wanapofanya kazi za nyumbani za ziada ili mama yao aweze kutumia mwezi mmoja akiwa painia (mhubiri wa wakati wote), wanakuwa na maoni kwamba wao ni sehemu ya utendaji wake na wanatazamia kuwa na mapendeleo hayo wao wenyewe. Kijana mmoja mwenye umri wa miaka ishirini na moja anasema: “Sikuzote wazazi wangu walijulisha wazi kwamba waliwaza kwamba upainia ndio uliokuwa njia bora zaidi ya maisha.” Kijana mwingine alieleza hivi: “Sikumbuki hata wakati mmoja ambao upainia haukuwekwa kuwa mradi.” Vijana wanaweza kufurahi na kujionea mambo yenye furaha wakimtumikia Yehova, kwa maana yeye ndiye “Mungu mwenye furaha,” na Kristo Yesu ndiye “Mtawala pekee mwenye furaha.”​—1 Timotheo 1:11, NW; 6:15, NW.

Kuthamini

11-13. Ni nini baadhi ya faida ambazo watoto wako wanapewa na imani yako kuhusiana na: (a) kuogopa wakati ujao? (b) kuogopa kifo?

11 Ni jambo la maana kuhakikisha kwamba watoto wako wanathamini mambo waliyo nayo ambayo watu wengine huenda wasiwe nayo.

12 Jambo moja walilo nalo ni usalama. Kwa ujumla vijana wa leo wanazungumza matatizo ya ulimwengu shuleni, na wanayaona katika televisheni. Wanazungumza juu ya uchafuzi wa mazingira, vita ya atomu na uwezekano wa ulimwengu kuangamizwa. Tofauti nao, Mashahidi vijana wana uhakika na hisi (maoni) ya kuwa salama. Wanajua kwamba Mungu hataruhusu mambo yafikie hatua hiyo, bali kwamba ‘atawaharibu hao waiharibuo [dunia].’​—Ufunuo 11:18.

13 Wengi wa marafiki wao wanaogopa kufa. Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 13 alisema: “Halionekani kuwa jambo la kufaa ukue na kuwa na tumaini la kufa tu.” Vijana wenu wanajua kwamba Biblia inasema wafu “hawajui neno lo lote,” na kwamba ‘mawazo yao yanapotea,’ kwa hiyo haiwezi ikawa wafu wako katika mateso. Vilevile wanajua kwamba Maandiko yanaahidi uzima​—kwamba watu wengi katika makaburi yao “watatoka,” kwa maana kutakuwako “ufufuo siku ya mwisho.” Vijana wenu wanaweza kusoma vifungu hivyo vya maneno yenye kufariji katika Biblia katika Mhubiri 9:5, 10; Zaburi 146:4; Yohana 5:28, 29 na Yohana 11:11-25.

14. Kwa sababu gani kuwa na kweli kwapasa kuwa jambo la maana kwa watoto wako?

14 Zaidi ya hayo, je, watoto wako wanatambua umaana wa kweli waliyo nayo? Shahidi mmoja kijana alisema: “Kile kilichonivuta mimi ni kweli. Sikuzote nilitaka kuelezwa mambo, sikuzote nikauliza hivi: Kwa sababu gani? Biblia iko wazi kama weupe, kwa kweli unaweza kuitegemea.” Yesu alisema: “Kweli itawaweka huru.” Imeweka huru maelfu mengi, si na utumwa wa kidini bali pia na dawa za kulevya, ufasiki (mwenendo mchafu wa ngono), hatari ya maradhi ya kisonono na kaswende, ushirikina, mafundisho ya uongo na wasiwasi na matata yaliyoko katika ulimwengu huu mbovu.​—Yohana 8: 32.

15. Wazazi na watoto, wote wawili wanapaswa kuchochewaje na kweli zile zilizoandikwa katika: (a) 1 Yohana 4:​9, 10? (b) 2 Petro 3:13?

15 Je! umekwisha kuwafunza watoto wako juu ya umaana wa upendo na rehema ya Mungu? Je! wanathamini yaliyohusika kwake katika kumpeleka Mwanaye duniani kuwa ukombozi? (1 Yohana 4:9, 10; Warumi 8:38, 39) Je! wanalitunza sana taraja la uzima wa milele katika paradiso ya kidunia? (2 Petro 3:13) Kuthamini kwako mwenyewe baraka hizo kutawatia moyo watoto wako wakue wakizithamini. Maandiko yanasema kwamba wazazi wanapaswa kumwogopa Mungu na kutii amri zake “wapate kufanikiwa wao na watoto wao milele!”​—Kumbukumbu la Torati 5:29.

16. Watoto wanapaswa kusaidiwa watambue nini juu ya ubora wa Neno la Mungu katika jamaa yao?

16 Je! watoto wako wanatambua yale ambayo maarifa ya Neno la Mungu huenda yakawa yaliifanyia jamaa yako? Yaweza ikawa watoto wako wana wenzi wa shule ambao, kwa sababu ya talaka, wana mama au baba wawili ama watatu. Ikiwa jamaa yako ni yenye umoja, ambayo wazazi wamejitoa maisha kwa mmoja na mwenzake, je, watoto wako wanathamin kwamba hilo ni kupatana na kanuni za Biblia? (Waebrania 13:4) Je! wanatambua kwamba kanuni zinazopatikana katika Biblia zinawasaidia wajione wana hali ya salama, kuwa na rafiki, ya kutakwa, ya kuwa na kusudi, ya kuwa na uongozi, ya kuweza kutimiza mambo na ya kujiona wao binafsi ni wenye kufaa mambo ambayo vijana wengi hawajapata kuwa nayo?

17, 18. Watoto wanawezaje kuona kwamba Neno la Mungu ni lenye ubora kwao: (a) katika jamaa zilizogawanyika kidini? (b) katika nyumba zenye mzazi mmoja?

17 Lakini huenda ukawa unafikiri hivi ‘Jamaa yetu imegawanyika​—mume (au mke) wangu hafuati kanuni hizo.’ Hilo halikuzui wewe usizifuate. Biblia inasema waume wasioamini huenda wakapata “kuvutwa pasipo neno kupitia mwenendo wa wake zao.” Ikiwa mwenzi wako asiyeamini angeweza kuvutwa na mfano wako mzuri ebu fikiria matokeo ambayo yaweza kuwa juu ya watoto wako kwa wewe kufuata kwa uaminifu kanuni za kimungu!​—1 Petro 3:1, 2, NW.

18 Au huenda ukawa mzazi asiye na mwenzi, na kulazimika kulea watoto wako ukiwa peke yako. Ikiwa ndivyo, tajia watoto wako tatizo hilo waziwazi. Tegemezaneni. Waonyeshe tofauti kati ya maisha yao na yale ya jamaa nyingine zenye ,mzazi mmoja wanazojua. Ni baraka kama nini wao kuishi katika nyumba isiyoinginzwa ulevi, uzoefu wa vileo, uasherati na matendo mengine ya mwili!​—1 Wakorintho 6:9, 10; Wagalatia 5:19-21.

Utendaji Wenye Kufaa

19, 20. (a) Wazazi wanawezaje kusaidia kujaza haja za watoto wao za upashanaji wa habari na urafiki? (b) Matokeo yanakuwa nini?

19 Watoto wanahitaji kucheza. Mojayapo ya hali za furaha ambazo Biblia inahusisha na kurudishwa kwa hekalu la Yerusalemu ni “wavulana, na wasichana, wakicheza katika njia zake.” (Zekaria 8:5) Vilevile watoto wanahitaji wakati wako. Ni kwa kutumia wakati pamoja nao tu, na kuwaruhusu waseme na kusikiliza kweli kweli yale wanayotaka kusema, ndipo unaweza kupashana nao habari, kujifunza juu ya matatizo yao na kuwasaidia. Ingawa watoto Wakristo hawasherehekei sikukuu fulani zenye vyanzo vya kipagani, mara nyingi wazazi wao wanapanga wawe na nyakati za furaha​—matembezi ya nje, vikusanyiko vya chai au namna nyingine za kufaa za jamaa kujifurahisha. Wanapata zawadi mara kwa mara mwakani. Jamaa nyingine zinafanya sherehe babu na nyanya wanapozuru. Wazazi wanatia moyo ushirika unaofaa pamoja na vijana wengine Wakristo. Ikiwa jamaa iko katika mahali palipo peke yake, vijana wanaweza kuwa na marafiki wa kuandikia barua ambao wanakutana nao kwenye makusanyiko ya Kikristo.

20 Baba mmoja anawauliza watoto wake mara nyingi hivi: “Je! unaona umenyimwa katika njia yo yote kwa sababu ya imani yako? ” Jibu ni: “Hakika sivyo! ” Kijana mmoja, akilinganisha maisha yake na yale ya wanashule wenzake, alisema: “Jambo pekee ambalo nimekosa ni matata mengi.”

Msaada wa kutoka Nje

21. Tujapotambua kwamba kuzoeza watoto ni daraka la wazazi, wengine wanawezaje kusaidia?

21 Daraka la kuwafundisha watoto wetu ni daraka letu sisi wenyewe. Biblia inaonyesha kwamba baba anapaswa kuongoza, naye mama anapaswa kusaidia. Inasema: “Mwanangu, [sikiliza nidhamu] ya baba yako, Wala usiiache sheria ya mama yako.” (Mithali 1:8; Waefeso 6:4) Lakini hiyo haimaanishi kwamba wengine hawawezi kusaidia. Kundi ni jamaa moja, na kwa kurudia-rudia wanaume wazee waliokomaa wanaeleza juu ya msaada wa pekee waliopewa na mtu fulani kundini walipokuwa vijana. Mashahidi wenye juhudi wanawakumbuka kwa shauku watu waliowapeleka katika utumishi wa Kikristo zamani sana. Vijana wanathamini kweli kweli wakati wenye umri mkubwa zaidi wanapendezwa nao na kuwasaidia wakae katika njia inayofaa.​—Mithali 13:20.

Mfano Wako Mwenyewe

22. Mfano ambao wewe unaweka ni wa umaana gani?

22 Ni Jambo la Maana watoto wako waone kwamba wewe unamtumainia Mungu akupe uelekezo na umelifanya Neno lake kuwa sehemu yako​—kwamba unaliamini kweli kweli na kulifuata katika maisha yako. (Zaburi 143:10) Wanaiona nia yako. Ikiwa unaiona mikutano ni kazi, kutafutia wazee ugomvi, kulaumu-laumu washiriki wa kundi na kulalamika kwa sababu ya wakati unaotumiwa katika utumishi wa Yehova, inaelekea kwamba watoto wako watafuata mfano wako mbaya. Lakini ukiiona mipango hiyo ya kitheokrasi kuwa baraka bora sana kutoka kwa Yehova, inaelekea kwamba watoto wako wataona vivyo hivyo. Kulea watoto hasa si kufanya mambo makubwa machache bali ni kufanya hesabu kubwa ya mambo madogo. Ukiyafanya mambo hayo madogo-madogo kwa njia inayofaa kila siku, inaelekea utaweza kushughulika na yo yote makubwa-makubwa yanayotokea.​—Luka 16:10; Mathayo 25:21.

23. Matazamio yako yaweza kuwa na matokeo gani kwa watoto wako?

23 Ni jambo la maana sana kwa watoto wako kujua mahali pa pekee walipo napo katika moyo wako. Lazima wajue kwamba wewe unawapenda kweli kweli, na kwamba ungekatishwa tamaa ikiwa wangeshindwa kufuata kanuni za kimungu. Sulemani aliandika hivi: “Mwanangu, kama moyo wako una hekima, Moyo wangu utafurahi naam, moyo wangu.” Vilevile: “Baba yake mwenye haki atashangilia.” (Mithali 23:15, 24) Lakini vipi​—watoto wako wanapokua na pengine kuwa na tamaa ya kujitegemea​—wakifanya jambo ambalo umekwisha kuzungumza nao na kwa hiyo wanajua ni kosa machoni pa Mungu? Usifanye haraka kukubali kushindwa nao wala kuacha kujaribu kuwasaidia. Kumbuka kwamba wao pia hawajakamilika na huenda wakawa wanapitia kipindi kigumu sana cha mabadiliko. Kujapokuwa kukatishwa kwako tamaa, endelea kuonyesha katika njia ya kuhurumia (ufahamu), lakini ya uthabiti na iliyo wazi kwamba kufuata kanuni za Mungu ndiko kutakakowafaa zaidi.​—Yakobo 3:2.

24. Wazazi wanaweza kutazamia thawabu gani iwapo wamewalea watoto wao kulingana na kanuni za kimungu?

24 Ni jambo la kuridhisha kuona watoto wetu wakikua na kuwa vijana wazuri wanaume na wanawake, kuwaona wakitwaa madaraka yao na kufuata maishani mambo tuliyojaribu kuwafundisha. Kama Paulo alivyomsihi kijana Timotheo, ndivyo tunavyowaambia watoto wetu: “Fanya yote yote uwezayo kujiweka mwenyewe mbele za Mungu katika hali ya kukubaliwa, mfanyi kazi asiye na lo lote la kuaibikia, ukitumia lile neno la ile kweli sawasawa.” (2 Timotheo 2:15, NW) Halafu twaweza kusema juu ya watoto wetu wa kimwili, ambao pia watakuwa wamekuwa watoto wetu wa kiroho: “Sina furaha iliyo kuu kuliko hii, kusikia ya kwamba watoto wangu wanakwenda katika kweli​—3 Yohana 4.​—Kutoka The Watchtower, October 1, 1982.

[Maelezo ya chini]

a Masimulizi hayo pamoja na mengine mengi yanasimuliwa katika lugha iliyo rahisi kufahamiwa na watoto wachanga katika Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, kinachopatikana kwa wachapishaji wa gazeti hili, au ye yote wa Mashahidi wa Yehova.

Je! Wewe unakumbuka Mambo Haya?

□ Kwa sababu gani twapaswa kuwa waaminifu katika kuwafunza watoto wetu juu ya Mungu na kweli yake?

□ Unawezaje kufanya mikutano ya Kikristo ipendeze watoto wako?

□ Tukiwa wazazi wenye upendo, tutawaongozaje watoto wetu, hatua kwa hatua, katika utumishi wa kimungu?

□ Tunataka kuhakikisha wanathamini baraka gani?

[Sanduku katika ukurusa wa 11]

Watoto wanahitaji kusahihishwa, kupewa mwongozo na kuwekewa mpaka. Biblia inasema: “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto.” (Mithali 22:15) Walakini wazazi wanapokuwa wenye kupendezwa vya kutosha kuweka mipaka na kuhakikisha kwamba watoto wao wanaifahamu na hawairuki, watoto wanahisi salama​—wazazi wao hawatawaruhusu wafanye mambo yanayoweza kuwaumiza.

[Picha katika kurasa za 12 na 13]

Kijana anapokomaa kimwili . . . wazazi wanaweza kumsaidia afanye maendeleo ya kiroho

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki