Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 1/15 kur. 27-32
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUZOEZA JAMAA
  • MRADI WA KWANZA WA KUZOEZA JAMAA NI KUTOKEZA WAKRISTO HALISI
  • MAGUMU KATIKA JAMAA ZILIZOGAWANYIKA KIROHO
  • Kujenga Familia Yenye Nguvu Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Familia Kubwa Zilizoungana Katika Utumishi wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kulea Watoto Wenye Furaha Katika Ulimwengu Wenye Mchafuko Mwingi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 1/15 kur. 27-32

Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe

“Ee [Yehova], unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.”​—Zab. 25:4.

1, 2. (a) Watu wengi wana nia gani juu ya magumu yanayowapata? (b) Sisi wenyewe twawezaje kutumia ufumbuzi wa Biblia?

WATU wengi wanazungumza juu ya magumu yaliyomo ulimwenguni, uvunjaji wa sheria, kupanda kwa bei za vitu, uchafuzi wa hewa, maji na chakula. Lakini wanasema, “Hatuna la kufanya.” Wengine wana maoni ayo hayo juu ya jamaa zao wenyewe, kwa kusema, “Tunashindwa kabisa kufanya watoto watusikilize. Hatuelekei kupatana. Wao wanasisitiza kufuata yao wenyewe, sasa basi tufanyeje?”

2 Kwa kuwa Biblia inaonyesha kwamba ufalme wa Mungu unatoa ufumbuzi hakika wa magumu yanayowapata wanadamu leo, je! sisi pia tusitazamie kuona katika Biblia ufumbuzi wa magumu katika jamaa na mambo fulani ya kuongoza kupatanisha jamaa zaidi? Kukubali mapenzi ya Mungu si shauri la kuutazamia Ufalme utatue tu magumu makubwa yaliyomo duniani, bali kunahusu kutumia pia kanuni za Biblia katika nyumba zetu wenyewe na pamoja na jamaa zetu. Ikiwa tunasali kwa unyofu ufalme wa Mungu uje na mapenzi yake yatendeke duniani, imetupasa tujiulize, Mimi ninafanya nini kuhakikisha kwamba mapenzi yake yanatendeka duniani sasa, katika nyumba yangu mwenyewe? Kila mmoja anaweza kusaidia yatendeke: baba, mama na watoto, kwa maana kila mmoja ana daraka lake katika mpango wa Mungu.

KUZOEZA JAMAA

3. Ni nani aliye na daraka kubwa la kufundisha jamaa, na imempasa alitumieje?

3 Ingawa jamaa nyingi zinategemea shule au makanisa yafundishe na kuzoeza watoto wao, daraka la kwanza alilogawa Mungu liko juu ya wazazi. Bila shaka ndio walio katika hali bora kuwa na matokeo mazuri katika kusitawisha nia na mwenendo wa jamaa. Maandiko yanamshauri baba aongoze jamaa, akitumia ukichwa na usimamizi katika mambo yote. Je! ndivyo ilivyo katika jamaa yako? Kweli nyie akina baba mnasimamia na kuongoza utendaji wa jamaa? Bila shaka, ukichwa wake haupaswi kuwa wa kutumia nguvu wala wa uonezi, bali umepaswa utumiwe kwa upendo, kupatana na 1 Wakorintho 11:3, inayoonyesha kwamba “kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.” Hivyo baba mwenye kutumia Neno la Mungu inavyofaa ajua kwamba ukichwa wake lazima utumiwe kwa njia yenye kumpendeza Kristo na inayopatana na mafundisho yake. Hiyo inatia ndani kufuata shauri la Yesu la kutanguliza faida za Ufalme au mambo ya kiroho.

4. (a) Maandiko yanatiaje mkazo kwamba imempasa baba aongoze katika mambo ya kiroho? (b) Madaraka yake yanatia nini ndani?

4 Katika ulimwengu wetu wa kisasa huenda mwanamume katika jamaa akawa mwenye shughuli nyingi akiiruzuku jamaa yake kimwili. Lakini anakosea akisema kama wengi wafanyavyo, “Mambo ya dini, hayo namwachia mke wangu.” Mungu amempa mwanamume mgawo wa kuruzuku jamaa yake kiroho, kuongoza katika jambo hilo kama katika mambo mengine. Hivyo Zaburi 78:5, 6 inasema hivi: “Maana alikaza ushuhuda katika Yakobo, na sheria aliiweka katika Israeli. Aliyowaamuru baba zetu wawajulishe wana wao, ili kizazi kingine wawe na habari, ndio hao wana watakaozaliwa. Wasimame na kuwaambia wana wao.” Mkazo hapa unatiwa juu ya wanaume walio vichwa vya jamaa na juu ya daraka lao kuwapa wana wao mafundisho ya kiroho. Inampasa mwanamume aongoze katika kutoa mafundisho ya kiroho kwa mke wake na watoto wake na pia awe na funzo la kipekee apate kuwa na afya ya kiroho mwenyewe. Madaraka yake juu ya jamaa yake yanahusu kuwafundisha Biblia, kuwazoeza watoto namna ya kufanya mambo, kuwatia adabu inapokuwa lazima, kuwapa mahitaji ya kimwili, na kupanga wawe na tafrija inayofaa.​—Flp. 4:8, 9.

5. Ni njia gani nyingine mke anavyoweza kuongezea jamaa furaha?

5 Mke wa Kikristo anaweza kuwa na daraka la kusaidia katika jamaa, akimsaidia sana mume wake anapotoa uongozi unaofaa. Imempasa ampende na kumheshimu mume wake, hata maoni ya mumewe yaweje. Mke pia ana daraka la kuhakikisha anatunza nyumba, akifuata mfano mwema wa mke mwema anayetajwa katika Mithali 31:10-31. Imempasa afikirie sana kutumia Neno la Mungu katika maisha yake, vile vile kusaidia watoto wake wafanye hivyo. Mama Mkristo ataona furaha ya pekee anaposaidia kufundisha watoto wake wamthamini Muumba na mambo mengi ambayo ametoa.

6. Watoto wanawezaje kuheshimu baba zao na mama zao?

6 Watoto pia wanaweza kusaidia sana maisha ya jamaa yawe yenye furaha wakitumia Neno la Mungu. Je! nyie watoto mmepata kuwaza juu ya jambo hilo? Ni jambo la kweli, kwa maana Mithali 15:20 inasema hivi: “Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye.” Ni kama vile Waefeso 6:1-3 inavyoshauri: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki. Waheshimu baba yako na mama yako . . . upate heri.” Kushirikiana sana na wazazi kweli ni sehemu ya mgawo wa mtoto Mkristo. Kufanya hivyo hakuonyeshi heshima kwa wazazi wa mtu tu, bali pia kwa Baba wa kimbinguni, Yehova.

7. 2 Timotheo 3:15 inapingaje shauri fulani la kidini juu ya kulea mtoto?

7 Kwa kuwa watoto wanaanza kujifunza mambo mara tu wazaliwapo, wamepaswa waanze kufundishwa katika utoto mchanga, kama vile 2 Timotheo 3:15 inavyoonyesha. Kwa sababu hiyo inashangaza vile waalimu wengine wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) wasivyotia moyo mazoezi ya kidini yaanze mapema. Kwa mfano, Journal and Constitution la Atlanta lilitoa habari za vile mtawa mmoja wa kike alivyohojiwa na wachapaji wa gazeti hilo akasema hivi, “Usijaribu kufundisha mtoto wako mambo mengi mno juu ya Mungu mapema mno.” Mwanamke huyo alishauri hivi, “Haifai kutoa mazoezi yo yote ya mambo ya dini.” Mwanamke huyo alidhani inafaa wazazi wangoje tu, mpaka mtoto akaribie umri wa miaka tisa, ndiyo wamfundishe mambo ya dini.

8. Je! Maandiko yanatia moyo kufundisha watoto mambo ya kiroho? Eleza.

8 Shauri la mtawa huyo wa kike linatofautiana sana na maoni ya Yesu juu ya watoto wadogo. Wakati wa huduma yake wanafunzi wake walijaribu kufukuza watoto wadogo walipoletwa kwake, inaelekea wakidhani kwamba watoto hao walikuwa wadogo mno asiweze kujihangaisha nao. Lakini Yesu aliwakaripia, akisema: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 19:13, 14) Pengine alikumbuka yeye alivyokuwa hekaluni alipokuwa na umri wa miaka kumi na miwili’ akizungumza na waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maulizo. Kwa wazi alipenda mambo ya kiroho alipokuwa mtoto. Agizo la Mungu kwa Israeli lilikuwa lenye hekima sana kwa kusema imewapasa kwa kawaida “wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto . . . wapate kusikia na kujifunza.” (Kum. 31:12) Baadaye maandiko yanatumia mafungu ya maneno kama vile “watoto waaminio” na “watoto wa kutii,” yakionyesha kwamba Wakristo wa kwanza pia waliona uhitaji wa kufundisha watoto wao wafuate njia ya Yehova.​—Tito 1:6; 1 Pet. 1:14.

9. Waalimu wa kilimwengu wanasema nini juu ya kufundisha watoto mapema?

9 Leo waalimu wa kilimwengu wanakazia ubora wa mazoezi ya mapema. Mwaka wa 1964 mwalimu wa Chuo Kikuu cha Chicago alitoa maoni ya kwamba karibu nusu ya akili yote ya kibinadamu inasitawishwa katika umri wa miaka minne. Wazo hilo linaungwa mkono na makala iliyokuwa katika gazeti Newsweek yenye kichwa “Si Wadogo Mno Wasiweze Kujifunza.” Ilisema hivi: “Wazo la kwamba sana sana akili ya kibinadamu inakuzwa katika umri wa kwenda shule ya nasari limekubaliwa na watu wengi​—na kwa hiyo watoto wanapelekwa shule sana katika umri huo.” Kwanza mtoto anajifunza kwa kuonja, kunusa na kugusa, lakini kuanzia umri wa miaka miwili mpaka saba anaweza kujifunza lugha ngumu, hata kujifunza kusoma na kufanya hesabu.

10. Kwa sababu gani ni jambo la hekima wazazi watumie wakati wakiwa pamoja na watoto wadogo?

10 Makala hiyo inamtaja mwalimu ambaye amechunguza uhusiano wa kati ya mama na mtoto kama akishikilia kauli ya kwamba, “Mwaka wa pili akili ya mtoto inaweza kutengenezwa au kuharibiwa.” Nia ya mtoto na maendeleo ya akili yake yanaweza kuongezwa akipendwa na kutiwa moyo, lakini sivyo itakavyokuwa akiachiliwa mbali au kuvunjwa moyo. Imeonekana pia kwamba mtu anayependa watoto zaidi, awe ni mzazi, babu, bibi (nyanya) au mtu mwingineyo, ndiye anayeweza zaidi kuongeza maendeleo ya mtoto ya kujifunza, kwa maana kwa asili watoto wanafurahia na kuiga wale wanaowapenda zaidi. Kwa hiyo, nyie akina mama, je! mnatumia wakati wa kutosha mkiwa na watoto wenu tangu wanapokuwa vitoto vichanga? Je! mmemwomba Yehova awasaidieni kufundisha watoto wenu kama Manoa alivyofanya?​—Amu. 13:8.

11. Mfano wa dada ya Lazaro Mariamu unawezaje kusaidia wanawake leo?

11 Leo wanawake wana mengi ya kufanya katika nyumba zao, na mara nyingi pia wanaona ni lazima wasaidie kuruzuku jamaa zao. Hii inafanya liwe jambo la maana hasa watafute wakati wa kuangalia faida za kiroho za jamaa, kutoacha mambo mengine yazivuruge. Ugumu huo wa kuwa na kiasi kinachofaa kati ya mambo ya kimwili yaliyo ya lazima na mambo ya kiroho ulitokea wakati mmoja Yesu alipotembelea nyumba ya dada za Lazaro. Martha alikaza fikira zake upande akifanya kazi za nyumbani naye alitaka dada yake Mariamu amsaidie, lakini Yesu akasema hivi: “Mariamu amelichagua fungu lililo jema [kukaza fikira juu ya mambo ya kiroho], ambalo hataondolewa.” (Luka 10:38-42) Ni jambo jipi unaloona kuwa la maana zaidi nyumbani mwako?

12. Uhusiano mwema unawezaje kuwekwa kati ya wazazi na watoto?

12 Ingawa kuna wakati na nafasi ya kufanya kila jambo, maelekeo ya kawaida ni kutojali mambo ya kiroho. Lakini, hata wakati mchache unaopangwa kwa kawaida uwe wa funzo la kipekee au wa kufundisha watoto unaweza kufaidi sana. Wazazi wanaweza kutumia vizuri pia nafasi zao wafundishe watoto wao namna ya kufanya kazi na kupata ufundi mbalimbali utakaowafaa baadaye. Hata kufanya jambo dogo sana pamoja na mzazi kunasaidia mtoto asitawishe uhusiano mwema na heshima kwa mpango wa jamaa. Lakini, zaidi ya yote, wazazi wanapojitahidi kukaza sana kumpenda Yehova na Neno lake ndani ya watoto wao, huo utadumu kuwa uongozi wa kweli kwa maisha ya baadaye.​—Kum. 6:5-9.

MRADI WA KWANZA WA KUZOEZA JAMAA NI KUTOKEZA WAKRISTO HALISI

13. Jamaa ya Kikristo imepaswa kuwa na mpango gani? Kwa sababu gani?

13 Ili wazazi au watoto watumie Neno la Mungu katika maisha zao, lazima walijue kwanza. Kila jamaa imepaswa kuwa na mpango wa funzo la Biblia sawa na ule wa makundi, ikiwa na mradi wa kusaidia kila mmoja awe Mkristo halisi. Ingawa jamaa nyingi zinashirikiana sana, hazina mradi huo ulio wa maana sana. Imewapasa Wakristo wa kweli wapendezwe na kuzoeza jamaa zao wakitazamia uzima wa milele. Kama vile 1 Timotheo 4:8 inavyosema, mazoezi hayo ya kiroho ndiyo yenye kufaidi hasa, ‘yaani, yanayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.’ Ikiwa watoto watazoezwa wafikie kukomaa kwa Kikristo, lazima wazazi wahakikishe kwamba watoto wanasadiki kabisa Biblia ni yenye hekima, badala ya kuacha akili zao zijae maoni ya taratibu ya mambo iliyopo.​—1 Yohana 2:15-17.

14, 15. (a) Mathayo 4:4 inaonyesha nini juu ya uhitaji wa chakula cha kiroho? (b) Kwa habari ya mipango ya funzo la jamaa, ni nini kitakachosaidia kufundisha watoto? (c) Mengine ya mambo yanayoweza kufikiriwa katika funzo la jamaa ni nini?

14 Katika funzo lo lote ukawaida ni wa maana. Kulingana na maneno ya Yesu kwamba “mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu,” inaonekana kwamba ni lazima tule chakula cha kiroho kwa kawaida ile ile tunayokula chakula cha kimwili. (Mt. 4:4) Wazazi walio na mpango huo wa kuruzuku jamaa zao kiroho wameona ni vizuri kufanya funzo hilo la jamaa liwe lenye kubadilishwa-badilishwa na kulinganishwa na mahitaji ya sasa na faida za jamaa, na kwa ufupi hii inategemea umri wa watoto wanaohusika. Kwa kawaida jambo linalokuwa la kwanza ni orodha ya kusoma Biblia. Si vizuri kusoma mradi mmalize tu, bali ni vizuri pia kupata maelezo ya watoto kuhakikisha wanafahamu wanayosoma na wanaweza kuyatumia.

15 Jamaa zilizo nyingi zinaona inafaa kulinganisha urefu wa wakati wa kujifunza na umri wa watoto, kwa maana ni vigumu kufanya watoto wasikilize kwa muda mrefu. Wakati wa funzo hilo la jamaa unategemea inapofaa zaidi jamaa iwe nalo​—wengine wanafurahia kuwa nalo asubuhi wanapokuwa wamechangamka, wengine wanafurahia jioni wakati wote wako nyumbani. Wazazi wengi wameuona ubora wa kueleza watoto wao maoni ya Biblia wakiwa na umri mdogo na kuyarudiarudia ili kuyakaza kikiki katika akili za watoto wao. Mpango wa funzo wenye mambo mbalimbali unaweza kusaidia pia, kuwasaidia kutayarisha hotuba au kujitayarisha kwa utumishi wa shambani, kuzungumza maulizo yanayotokea na kutayarisha watoto kwa magumu yatakayowapata.

16. (a) Kufikiria kwa watoto kunawezaje kusaidia wazazi waamue watajifunza nini nao? (b) Ni nyingine gani za habari ambazo mafaa wazazi wazungumze na watoto wao?

16 Sikuzote ni jambo la maana kwa wazazi kujua watoto wao wanafikiria nini. Hakuna faida ya kujifunza juu ya ufufuo au “Utatu” ikiwa watoto wamekaza fikira zao juu ya mitindo ya mavazi, kucheza dansi au kutembea na wavulana (ikiwa ni wasichana) na kutembea na wasichana (ikiwa ni wavulana). Kwa watoto wakubwa zaidi, habari kama vile matumizi yasiyofaa ya dawa za kulevya, mwenendo wa Kikristo unaofaa ni nini, namna ya kuendeleza dhamiri njema au matokeo ya mitindo ya mavazi zimeonekana kusaidia sana zinapozungumzwa na jamaa nzima, nazo zinawezesha wote wapate maoni ya Maandiko na ya wazazi pia.

17. Wazazi wanawezaje kusaidia watoto wao wapate maoni yanayofaa juu ya mambo yaliyo ya maana hasa maishani?

17 Daraka kubwa la wazazi ni kuwekea watoto wao miradi inayofaa. Kwa kuwa jamii ya kisasa ina maoni ya kutafuta mali za kimwili, upesi watoto wanaweza kuwashwa na tamaa ya pesa na mali za kimwili wazazi wasipowapa maoni ya kiasi juu ya mambo yaliyo ya maana hasa. Lakini ikiwa wazazi sikuzote wanakaza fikira juu ya mali za kimwili, pengine wao wenyewe wakisema wanataka sana kuwa na gari au kinanda, kana kwamba hayo ndiyo mambo makubwa maishani, nao watoto watakuwa vivyo hivyo. Hata hivyo, kujua na kufuata Biblia na kutanguliza faida za ufalme kunaweza kuleta furaha nyingi zaidi kuliko mali za kimwili.

MAGUMU KATIKA JAMAA ZILIZOGAWANYIKA KIROHO

18. (a) Ni kanuni gani zimepaswa zikumbukwe katika jamaa ikiwa mume si mwamini? (b) Lazima mke wake apatanishe wajibu gani mbalimbali?

18 Ingawa ni vigumu sana kutumia Neno la Mungu kwa matokeo mema katika jamaa iliyogawanyika kidini, mara nyingi hilo linaweza kufanywa. Na ikumbukwe kwamba Yehova wala Neno lake halibadiliki hata hali zetu wenyewe ziweje. (Yak. 1:17) Hivyo ukichwa wa jamaa unaendelea kuwa wa mwanamume awe anaukubali ukichwa wa Kristo au sivyo. Lakini, huenda watoto wakazikosa faida nyingi za kiroho ambazo zingaliweza kuja kutoka kwa baba ambaye angaliweza kuwalea “katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova,” isipokuwa kama mama yao anaweza kuwasaidia. (Efe. 6:4, NW) Lakini mke anayeamini anaweza kufanya nini ikiwa mumewe anamwagiza asipeleke watoto wao kwenye mikutano ya Kikristo? Mwanamke aliye katika hali hiyo amepaswa kutimiza wajibu mbalimbali​—wajibu kwa Yehova Mungu, kwa mume wake ambaye ndiye kichwa, na kwa watoto wake wapendwa. Anawezaje kupatanisha Matendo 5:29 (kutii Mungu kuliko wanadamu) na 1 Wakorintho 11:3 (kwamba kichwa cha mwanamke ndiye mwanamume)? Lazima mwanamke mwenyewe afanye uamuzi wa mwisho. Huenda maoni ya mumewe yakabadilika. Huenda kutumia busara kwa muda fulani kukasaidia anapomwonyesha mumewe ubora wa kusaidia watoto wao wafuate uongozi mwema wa Maandiko badala ya kufuata mfano wa vijana wengi wa leo.

19. Mke anayeamini anaweza kufanya nini asaidie watoto wake kiroho?

19 Bila shaka imempasa asali juu ya jambo hilo na kujaribu kusaidia watoto wake wamjue Yehova. Anaweza kutimiza mengi kwa maneno anayowaambia na mfano anaowawekea pia ili kuwazoeza vizuri nyumbani. Hata funzo la kawaida la Biblia lisipowezekana, kwa kuzungumza nao kila siku anaweza kukaza ndani yao kumpenda sana Yehova na kuliamini Neno lake. Mazoezi yaliyotolewa kwa Timotheo na mama yake Eunike na bibi (nyanya) yake Loisi ndiyo yaliyomfanya aendelee kutembea katika njia ya uzima. (2 Tim. 1:5) Kulingana na maneno yake mwenyewe, inaelekea Mfalme Lemueli pia alipata nyingi ya imani yake na mafundisho kutoka kwa mama yake, kwa maana Mithali 31:1 inataja “mausia aliyofundishwa na mama yake [kumrudi].” Tena, mama mwenye busara katika nyumba iliyogawanyika anaweza kutia sana watoto wake moyo kwa njia ya kiroho kwa kukaribisha marafiki wengine wa jamaa walio Mashahidi wawatembelee, kusudi lao likiwa kusaidia wasioamini.

20. Kutumia Neno la Mungu kunawezaje kusaidia jamaa iliyogawanyika?

20 Lakini, hata hali katika jamaa ziweje, Neno la Mungu limepaswa litumiwe kwa wema na kwa njia yenye kujenga, hata katika jamaa iliyogawanyika. Kama vile 2 Timotheo 2:24-26 inavyoonyesha, nia yetu juu ya asiyeamini imepaswa iwe ya upendo na saburi, si ya kushindana, kwa maana “haimpasi mtumwa wa Bwana kuwa mgomvi; bali kuwa mwanana kwa watu wote . . . akiwaonya kwa upole wao washindanao naye,” ili pengine wao wapate maarifa yaliyo sahihi juu ya kweli. Kuzungumza juu ya kweli kwa busara, kuzungumza yaliyoonwa na habari ulizopata mikutanoni na katika vitabu kunaweza kusaidia sana kufanya nyumba iliyogawanyika iwe jamaa yenye umoja. (1 Kor. 7:12, 16; 1 Pet. 3:1-4) Ingawa Yesu aliona mapema kwamba habari njema zingeleta migawanyiko katika jamaa nyingi, migawanyiko hiyo haipaswi kutokea kwa sababu ya nia au mwenendo wa mwamini mwaminifu.​—Mt. 10:35, 36.

21. Ni kwa njia gani hasa wazazi wanavyoweza kusaidia watoto wao waone ubora wa mashauri ya Biblia?

21 Hata ikiwa mzazi mmoja ndiye anayetumia Neno la Mungu katika maisha yake, huyo anaweza kuamua kusaidia watoto wafuate njia ya Yehova. Na hakuna kitu kinachosadikisha watoto zaidi ubora wa kanuni za Biblia kuliko wakati wazazi wote wawili wanafuata kwa uangalifu yanayofundishwa na Biblia. Kuna ugumu mkubwa kwa kila mmoja wetu kutumia Neno la Mungu katika maisha zetu, tuwe vijana au wazee, hasa kwa sababu ya kupatwa na mikazo na upinzani unaozidi kuongezeka kutoka kwa taratibu ya ulimwengu iliyopo. (Ufu. 12:17; Mt. 24:9) Kwa kujifunza na hasa kutumia Neno la Mungu katika jamaa zetu, tutakuwa tukionyesha tunataka kulifuata shauri lenye hekima la Mithali 4:10-13, linalosema hivi: “Mwanangu, sikiliza, na kuzipokea kauli zangu; na miaka ya maisha yako itakuwa mingi. Nimekufundisha katika njia ya hekima; nimekuongoza katika mapito ya unyofu. Uendapo, hatua zako hazitadhiikika, wala ukipiga mbio hutajikwaa. Mkamate sana elimu, usimwache aende zake; mshike, maana yeye ni uzima wako.”

22. Ni kwa njia gani kutumia Neno la Mungu kunaleta faida?

22 Jamaa zinazojaribu kulitumia Neno la Mungu kwa bidii na unyofu katika maisha zao wataona kwamba wanapata baraka nyingi kwa kufanya mambo kulingana na njia Yake. Watakuza hali ya kiroho kwa sababu ya kujifunza Neno Lake na kupata furaha na uradhi mwingi zaidi kutokana na utendaji wao katika utumishi wa shambani na katika kundi la watu wa Yehova kwa sababu ya kuwa tayari zaidi kwa mapendeleo hayo. (Gal. 6:7) Watapata furaha na umoja zaidi pia katika jamaa kwa sababu ya kutumia matunda ya roho ya Mungu katika maisha yao ya jamaa na uongozi mwema unaotolewa na wazazi na washiriki wakubwa zaidi wa jamaa. Kwa sababu hiyo watoto watashirikiana nao zaidi. Watakuza akili itakayowalinda na hatari za taratibu hii ya kale, nao watakapokuwa wakiendelea kukua, watakuwa na miradi ya kitheokrasi. Ikiwa wewe unataka jamaa yako iwe hivyo, basi endelea kulitumia Neno la Mungu kila wakati. Tutaona kama kweli hiyo inasaidia katika mambo hakika yaliyoonwa katika makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kuthamini mambo ya kiroho kunaweza kufunzwa kuanzia umri mdogo

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kufanya mambo pamoja kunatia nguvu vifungo vya jamaa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki