Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 2/15 kur. 9-12
  • Familia Kubwa Zilizoungana Katika Utumishi wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Familia Kubwa Zilizoungana Katika Utumishi wa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Familia Kubwa Mno Leo
  • Lazima Wazazi Wawe Watu wa Kiroho
  • Kufanya Mambo Pamoja
  • Mawasiliano Mazuri, Miradi ya Pamoja
  • Kumtegemea Yehova
  • Usikate Tamaa!
  • Kujenga Familia Yenye Nguvu Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Kuchukua Daraka la Utunzaji wa Familia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 2/15 kur. 9-12

Familia Kubwa Zilizoungana Katika Utumishi wa Mungu

“Wana ndio urithi wa Bwana,” akaandika mtunga-Zaburi. “Uzao wa tumbo ni thawabu. Kama Mishale Mkononi mwa shujaa, ndivyo walivyo wana wa ujanani. Heri mtu yule aliyelijaza podo lake hivyo.”​—ZABURI 127:3-5.

NAAM, watoto wanaweza kuwa baraka kutoka kwa Yehova. Na kama tu vile mpiga-mishale apatavyo uradhi kwa kujua jinsi ya kuelekeza mishale iliyo katika podo lake, ndivyo wazazi wapatavyo furaha wanapoelekeza watoto wao katika njia iongozayo kwenye uhai udumuo milele.—Mathayo 7:14.

Zamani za kale, familia ‘zilizojaza podo zao’ kwa watoto wengi zilikuwa za kawaida miongoni mwa watu wa Mungu. Kwa kielelezo, fikiria miaka yao utekwani huko Misri: “Wana wa Israeli walikuwa na uzazi sana, na kuongezeka mno, na kuzidi kuwa wengi, nao wakaendelea na kuongezeka nguvu; na ile nchi ilikuwa imejawa na wao.” (Kutoka 1:7) Idadi ya Waisraeli walioingia Misri inapolinganishwa na idadi iliyoondoka Misri yadokeza kwamba familia zilizokuwa na watoto kumi zilikuwa za kiwango cha kawaida!

Baadaye, Yesu alikulia katika familia ambayo huenda ikaonekana kubwa kwa wengi leo. Yesu alikuwa mzaliwa wa kwanza, lakini Yosefu na Maria walikuwa na wana wengine wanne na mabinti kadhaa. (Mathayo 13:54-56) Uhakika wa kwamba walikuwa na watoto wengi sana labda hufafanuliwa na jinsi ambavyo Maria na Yosefu wangeweza kufunga safari ya kurudi kutoka Yerusalemu bila kutambua kwamba Yesu hakuwa katika kikundi chao.—Luka 2:42-46.

Familia Kubwa Mno Leo

Leo, Wakristo wengi huamua kuwa na familia ndogo kwa sababu ya mambo ya kiroho, kiuchumi, kijamii, na sababu nyinginezo. Hata hivyo, familia zilizo kubwa zingali ni za kawaida katika jamii nyingi. Kulingana na kichapo The State of the World’s Children 1997, eneo lililo na kiwango cha juu zaidi cha uzazi ni sehemu ya Afrika iliyo kusini mwa Sahara. Huko, mwanamke wa kawaida huzaa watoto sita.

Kuhusu wazazi Wakristo wenye familia kubwa, kulea watoto wao ili wampende Yehova si rahisi, lakini wengi wamefanikiwa kufanya hivyo. Mafanikio yategemea ikiwa familia imeungana katika ibada safi. Maneno ya mtume Paulo kwa kutaniko la Korintho hutumika vilevile kwa familia za Kikristo leo. Yeye aliandika hivi: “Sasa nawahimiza nyinyi kwa bidii, akina ndugu, . . . kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko miongoni mwenu, bali kwamba mpate kuunganishwa kwa kufaa katika akili ileile na katika mstari uleule wa fikira.” (1 Wakorintho 1:10) Muungano huo waweza kufikiwaje?

Lazima Wazazi Wawe Watu wa Kiroho

Jambo kuu ni kwamba lazima wazazi wajitoe kikamili kwa Mungu. Fikiria yale ambayo Musa aliwaambia Waisraeli: “Sikiza, Ee Israeli; BWANA, Mungu wetu, BWANA ndiye mmoja. Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.”—Kumbukumbu la Torati 6:4-7.

Ona kwamba Musa alikazia kwamba amri za Mungu zilihitaji kuwa ‘mioyoni’ mwa wazazi. Ndipo tu wazazi wangeelekea kuwapa watoto wao mafundisho ya kiroho kwa ukawaida. Kwa hakika, wazazi wanapokuwa wenye nguvu kiroho, wanakuwa na hamu ya kuwafundisha watoto wao mambo ya kiroho.

Ili mtu awe wa kiroho na ampende Yehova kwa moyo wake wote, ni muhimu kusoma, kutafakari, na kutenda kupatana na Neno la Mungu kwa ukawaida. Mtunga-zaburi aliandika kwamba yule anayefurahia sheria ya Yehova na kuisoma “mchana na usiku” yeye “atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.”—Zaburi 1:2, 3.

Kama vile mti uzaavyo matunda mazuri ukimwagiliwa maji kwa ukawaida, ndivyo pia familia zilizolishwa vizuri kiroho huzaa matunda ya kimungu, ili jina la Yehova lisifiwe. Familia ya Uwadiegwu, anayeishi Afrika Magharibi ni mfano mmoja. Ijapokuwa Uwadiegwu na mke wake wana watoto wanane, wote wawili wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida, au wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Yeye asema: “Familia yetu imedumisha funzo la Biblia la ukawaida kwa zaidi ya miaka 20. Tumefundisha watoto Neno la Mungu tangu walipokuwa watoto wadogo, si wakati wa funzo la familia tu, bali pia katika huduma na nyakati nyinginezo. Watoto wetu wote ni wapiga-mbiu wa habari njema za Ufalme, na yule ambaye hajabatizwa bado ni yule mdogo zaidi tu aliye na umri wa miaka sita.”

Kufanya Mambo Pamoja

“Nyumba hujengwa kwa hekima,” Biblia husema. (Mithali 24:3) Katika familia, hekima hiyo hutokeza kazi ya pamoja. “Kapteni” wa familia ni baba; yeye ndiye kichwa cha nyumba aliyechaguliwa na Mungu. (1 Wakorintho 11:3) Mtume Paulo aliyepuliziwa alikazia uzito wa daraka la ukichwa alipoandika hivi: “Ikiwa yeyote hawaandalii kitu [kimwili na vilevile kiroho] wale walio wake mwenyewe, na hasa kwa ajili ya wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.”—1 Timotheo 5:8.

Kupatana na shauri hilo la Neno la Mungu, waume Wakristo wanahitaji kutunza hali ya kiroho ya wake zao. Wake wakilemewa na kazi za nyumbani, hali yao ya kiroho itaathiriwa. Katika nchi moja ya Kiafrika, Mkristo aliyetoka tu kubatizwa alilalamikia wazee wa kutaniko lake kwamba mke wake alionekana kuwa mwenye ubaridi kwa mambo ya kiroho. Wazee walidokeza kwamba mke wake alihitaji msaada wenye kutumika. Kwa hiyo, mume akaanza kumsaidia kufanya kazi za nyumbani. Pia alitumia wakati naye akimsaidia kuboresha usomaji wake na ujuzi wake wa Biblia. Aliitikia vizuri, na sasa familia nzima imeungana katika utumishi wa Mungu.

Akina baba pia wanahitaji kujishughulisha wenyewe na mambo ya kiroho ya watoto wao. Paulo aliandika: “Nanyi, akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Wazazi wanapotii onyo la kutowasumbua watoto wao, na pia mwelekezo wa kuwazoeza, watoto huhisi kwamba wao ni sehemu ya familia. Tokeo linakuwa kwamba watoto wanaelekea kusaidiana na kutiana moyo kufikia miradi ya kiroho.

Kazi ya pamoja hutia ndani kuwapa watoto madaraka ya kiroho wanapokuwa tayari kufanya hivyo. Baba mmoja, mzee Mkristo mwenye watoto 11, huamka asubuhi na mapema ili kuongoza mafunzo na watoto kadhaa kabla ya kwenda kazini. Wale wakubwa, wanapobatizwa, huwasaidia ndugu na dada zao wachanga kwa zamu, hiyo yatia ndani kushiriki katika kuwafundisha Biblia. Baba huwasimamia, akiwapongeza kwa jitihada zao. Sita kati ya watoto hao wamebatizwa, na wengine wanaendelea kujitahidi kufikia mradi huo.

Mawasiliano Mazuri, Miradi ya Pamoja

Lililo muhimu katika familia zilizoungana ni mawasiliano yenye upendo na miradi ya kiroho ya pamoja. Gordon, mzee Mkristo anayeishi Nigeria, ni baba ya watoto saba wenye umri wa kati ya miaka 11 hadi miaka 27. Sita kati yao ni mapainia, kama vile wazazi wao. Yule mdogo zaidi, aliyebatizwa hivi majuzi, hushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kufanya wanafunzi na wale wengine katika familia. Wana wawili ambao ni watu wazima ni watumishi wa huduma katika kutaniko.

Gordon aliongoza mwenyewe mafunzo ya Biblia pamoja na kila mmoja wa watoto wake. Mbali na hilo, familia hiyo ina programu yenye mambo mengi ya elimu ya Biblia. Wao hukutana kila asubuhi ili kuchunguza andiko la Biblia kisha kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.

Mojawapo ya miradi iliyowekwa kwa kila mshiriki wa familia ni kusoma makala zote katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Hivi majuzi, waliongezea usomaji wa Biblia wa kila siku katika kawaida yao ya usomaji. Kwa kuzungumzia yale wanayosoma, washiriki wa familia hutiana moyo kuendeleza zoea hilo.

Funzo la Biblia la familia la kila juma limeimarika vizuri sana hivi kwamba hakuna mtu ambaye huhitaji kikumbusha—kila mtu hulitazamia. Kwa miaka kadhaa, mambo yaliyomo, muundo wake, na urefu wa funzo la familia, yametofautiana kulingana na umri na mahitaji ya watoto. Familia hiyo imekuwa na ukaribu pamoja na watumishi wengine waaminifu wa Mungu, na hilo limekuwa na matokeo yenye kunufaisha watoto.

Wakiwa familia, wao hufanya mambo pamoja na kutenga wakati wa tafrija. Mara moja kwa juma wao hufurahia “tafrija ya jioni ya familia,” ambayo huwa na maswali ya kutahini, mizaha ifaayo, kupiga piano, kusimulia hadithi, na kupumzika tu. Mara nyingine, wao huenda pwani na sehemu nyingine zenye kupendeza.

Kumtegemea Yehova

Hakuna moja kati ya mambo yaliyotajwa juu ambayo hurahisisha ugumu wa kulea familia kubwa. “Ni vigumu sana kuwa baba mzuri wa watoto wanane,” Mkristo mmoja asema. “Hali hiyo hutaka chakula kingi cha kimwili na cha kiroho kuweza kuwatosha; lazima nifanye kazi kwa bidii ili kupata fedha za kutosha kuwategemeza. Watoto walio wakubwa kidogo kwa umri wako katika miaka yao ya utineja, na wote wanane huenda shuleni. Najua kwamba mazoezi ya kiroho ni muhimu, lakini baadhi ya watoto wangu ni watundu na wasiotii. Wao hunihuzunisha, lakini najua nyakati nyingine mimi hufanya mambo ambayo huhuzunisha moyo wa Yehova, naye hunisamehe. Kwa hiyo, lazima niendelee kuwasahihisha watoto wangu kwa subira hadi warekebike.

“Najaribu kufuata kielelezo cha Yehova kwa kuwa yeye ni mwenye subira kutuelekea kwa sababu hutaka wote wafikie toba. Najifunza na familia yangu, na baadhi ya watoto wangu wanajitahidi kufikia mradi wa ubatizo. Sitegemei nguvu zangu mwenyewe ili kupata matokeo haya; nguvu zangu haziwezi kutimiza mengi. Najaribu kumkaribia Yehova katika sala na kutumia mithali isemayo: ‘Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.’ Yehova atanisaidia nitimize mazoezi ya watoto wangu.”—Mithali 3:5, 6.

Usikate Tamaa!

Nyakati nyingine kuzoeza watoto huonekana kuwa kazi ngumu isiyothaminiwa, lakini usikate tamaa! Vumilia! Watoto wako wakikosa kuitikia kwa njia inayofaa au kuthamini jitihada zako sasa, huenda wakafanya hivyo baadaye. Huchukua muda mrefu ili mtoto akue kufikia kuwa Mkristo mwenye kuzaa matunda ya roho.—Wagalatia 5:22, 23.

Monica, anayeishi Kenya, ni mmoja wa watoto kumi. Yeye asema: “Wazazi wangu walitufunza kweli ya Biblia tangu utotoni. Baba alikuwa akitufunza vichapo vya Kikristo kila juma. Kwa sababu ya kazi yake, funzo halikuwa siku ileile sikuzote. Nyakati nyingine, alipokuwa akirudi nyumbani kutoka kazini, angetuona tukicheza nje na kutuambia kwamba baada ya dakika tano ilitupasa tuingie ndani kwa ajili ya funzo letu la Biblia. Baada ya funzo letu la Biblia, tulikuwa tukitiwa moyo kuuliza maswali na kuzungumzia matatizo yetu.

“Alihakikisha kwamba tulishirikiana na watoto wenye kumhofu Mungu. Baba alitembelea shule yetu kwa ukawaida na kuuliza walimu kuhusu mwenendo wetu. Katika ziara moja alisikia kwamba kaka zangu watatu walikuwa wamepigana na wavulana wengine na kwamba nyakati nyingine walikuwa wajeuri. Baba aliwaadhibu kwa kukosa adabu, lakini pia alichukua wakati kueleza kutoka katika Maandiko sababu waliyohitaji kujiendesha wenyewe katika njia ya kimungu.

“Wazazi wetu walituonyesha manufaa za kuhudhuria mikutano kwa kutayarisha sehemu za mkutano pamoja nasi. Tulizoezwa kuwa wahudumu kwa kujizoeza nyumbani. Kuanzia utotoni tuliandamana na wazazi wetu katika utumishi wa shambani.

“Leo, kaka zangu wawili ni mapainia wa pekee, dada mmoja ni painia wa kawaida, na dada mwingine, ambaye ameolewa ana familia, naye ni Shahidi mwenye bidii. Dada zangu wawili wachanga, mmoja mwenye umri wa miaka 18 na yule mwingine miaka 16, ni wahubiri waliobatizwa. Wavulana wawili wachanga wanazoezwa. Nimekuwa nikitumikia katika ofisi ya tawi ya Kenya ya Mashahidi wa Yehova kwa miaka mitatu. Nawapenda na kuwathamini wazazi wangu kwa sababu wao ni watu wa kiroho; walituwekea kielelezo chema.”

Haidhuru una watoto wangapi, usikate tamaa kamwe katika kuwasaidia watembee kwenye njia ya uhai udumuo milele. Yehova anapobariki jitihada zako, utarudia maneno ya mtume Yohana kuhusu watoto wake wa kiroho: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.”—3 Yohana 4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki