Kuchukua Daraka la Utunzaji wa Familia
“AKINA baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Kwa maneno hayo yaliyopuliziwa, mtume Paulo kwa wazi aliweka daraka la utunzaji wa familia mahali pastahilipo—katika uwezo wa baba.
Katika familia zilizo nyingi baba hayuko peke yake katika kutunza watoto wake. Mke wake, aliye mama ya watoto wake, hushiriki hilo daraka kwa shangwe pamoja na mume wake. Hivyo, Mfalme Solomoni alitangaza hivi: “Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.”—Mithali 1:8.
Utunzaji wa Kimwili na wa Kiroho
Wazazi wanaowapenda watoto wao hawawapuuzi kimakusudi. Kwa kweli, kwa Wakristo kufanya hivyo kungekuwa sawa na kukana imani yao, kama tukatavyo kauli kutokana na maneno ya Paulo kwa Timotheo: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii kitu wale walio wake mwenyewe, na hasa kwa ajili ya wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Wakristo hung’amua kwamba kuwalea watoto katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova” huhitaji mambo mengi zaidi kuliko kuwaandalia tu katika njia ya kimwili.
Fikiria himizo lenye bidii la Musa kwa taifa la Israeli walipopiga kambi katika nyanda za Moabu, kabla tu ya kuingia katika Bara Lililoahidiwa. Huko aliwasomea sheria za Mungu kwa mara nyingine tena na kuwaagiza hivi: “Yawekeni maneno yangu mioyoni mwenu na rohoni mwenu.” (Kumbukumbu la Torati 11:18) Mapema alikuwa amewakumbusha kwamba, walipaswa kumpenda Yehova kwa moyo wao wote, kwa nafsi yao yote, na kwa nguvu zao zote, akiongeza kusema hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako.” (Kumbukumbu la Torati 6:5, 6) Ilikuwa muhimu kwa wazazi Waisraeli kuruhusu maneno ya Sheria ya Mungu yapenye mioyo yao. Wakiwa na mioyo iliyojaa ufahamu wa kiroho, wazazi Waisraeli wangeweza kutii kwa matokeo maneno ya Musa yafuatayo: “Nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii [“uyakaze kikiki,” NW] [maneno ya Sheria ya Mungu], na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.”—Kumbukumbu la Torati 6:7; 11:19; linganisha Mathayo 12:34, 35.
Ona kwamba akina baba walipaswa ‘kuyakaza kikiki’’ maneno hayo katika watoto wao na “kuyanena.” Kamusi iitwayo Merriam-Webster’s Collegiate Dictionary hufasili maneno ‘kukaza kikiki’ kuwa “kufundisha na kukazia kwa kurudia-rudia au kwa kuonya mara nyingi.” Wazazi waliponena juu ya Sheria ya Mungu kila siku—asubuhi, adhuhuri, na usiku—hilo liliwafahamisha watoto wao mengi. Vijana walipohisi upendo ambao wazazi wao walikuwa nao kwa Sheria ya Mungu, wao nao walivutwa kusitawisha ukaribu na Yehova. (Kumbukumbu la Torati 6:24, 25) Kwa kupendeza, Musa aliwaagiza kihususa akina baba wawafundishe watoto wao ‘walipoketi katika nyumba zao.’ Kufundisha kwa namna hiyo kulikuwa sehemu ya utunzaji wa familia. Lakini vipi leo?
“Uketipo Katika Nyumba Yako”
“Si jambo rahisi,” aeleza Janet, mama Mkristo mwenye watoto wanne.a “Unahitaji udumifu,” akubali Paul, mume wake. Kama wazazi wengine wengi walio Mashahidi, Paul na Janet hujitahidi sana kujifunza Biblia pamoja na watoto wao angalau mara moja kwa juma. “Sisi hujaribu kuwa na mazungumzo ya Biblia ya familia kila Jumatatu jioni katika wakati uliowekwa,” Paul aeleza, akikiri hivi: “Lakini hatufaulu sikuzote.” Akiwa mzee aliyewekwa rasmi katika kutaniko lake, nyakati nyingine ameitwa kwenda kushughulikia mambo muhimu. Watoto wake wawili walio wakubwa zaidi kwa umri, hutumikia wakiwa wahudumu wa wakati wote. Wao hupata kwamba nyakati za jioni ni zenye matokeo kwa habari ya kuwasiliana na watu katika huduma. Hivyo, wakiwa familia, wamerekebisha wakati wa kufanya funzo lao la familia. “Nyakati nyingine sisi hufanya funzo letu mara tu baada ya mlo wetu wa jioni,” Paul aeleza.
Hata ingawa wazazi huonyesha kubadilikana katika kuweka wakati wa kufanya funzo lao la familia, wao hujaribu kudumisha ukawaida wa hilo funzo. “Ikiwa wakati wa kufanya funzo letu lazima ubadilishwe,” asema binti Clare, “sikuzote Baba huweka huo wakati mpya kwenye mlango wa friji, ili sisi sote tujue funzo litafanywa wakati gani.”
Kukusanyika kwa ajili ya funzo la Biblia la familia la kawaida, pia huandaa fursa nzuri kwa washiriki wa familia walio wachanga zaidi kushiriki mahangaiko na matatizo yao pamoja na wazazi wao. Funzo la namna hiyo huleta matokeo mazuri lisipokuwa gumu sana hivi kwamba, vijana wanasoma tu majibu ya maswali yaliyoulizwa katika kitabu cha mafundisho ya Biblia wanachotumia. “Funzo letu la familia ni kikao cha mazungumzo,” aeleza Martin, ambaye ana wana wawili. “Mkusanyikapo pamoja mara moja kwa juma ili kuzungumzia habari ya Kimaandiko, unapata kujua jinsi familia yako inavyoendelea kiroho,” yeye aeleza. “Sisi hupata kujua mambo mengi tofauti wakati wa hayo mazungumzo. Unapata kujua mambo yanayotukia shuleni, na kwa kupendeza zaidi, unapata kujua watoto wako wanasitawisha mitazamo gani.” Mke wake Sandra akubali na ahisi kwamba, yeye pia hupata kujua mengi kutokana na funzo la familia. “Mume wangu anapoongoza hilo funzo,” yeye aeleza, “Mimi hujifunza mengi kwa kusikiliza jinsi ambavyo wana wangu hujibu maswali yake.” Kisha Sandra hupatanisha maelezo yake ili awasaidie wavulana wake. Yeye hufurahia hilo funzo zaidi kwa sababu yeye hushiriki kwa bidii. Ndiyo, vipindi vya funzo la familia huwapa wazazi ufahamu wenye kina juu ya kufikiri kwa watoto wao.—Mithali 16:23; 20:5.
Uwe Mwenye Kubadilikana na Mwenye Kustahimili
Wakati wa kufanya funzo lako la familia ufikapo, huenda ukaona kwamba mtoto mmoja aweza kuwa chonjo na mwenye kupendezwa, ilhali mwingine ahitaji kubembelezwa ili amakinike na kunufaika. Mama mmoja Mkristo aeleza hivi: “Maisha ya familia yako hivyo! Unajua upaswalo kufanya ukiwa mzazi. Hivyo ukidumu katika kuongoza funzo la familia, Yehova husaidia na huleta matokeo.”
Huenda muda ambao kijana aweza kukaza fikira ukatofautiana kulingana na umri wake. Mzazi mwenye ufahamu hufikiria jambo hilo. Wenzi wawili wa ndoa wana watoto watano, wenye umri wa kuanzia miaka 6 hadi 20. Michael, baba yao, asema hivi: “Wape walio wachanga zaidi fursa ya kwanza ya kujibu maswali. Kisha waache watoto wenye umri mkubwa zaidi waeleze kirefu na kutokeza mambo ambayo wametayarisha.” Njia hiyo ya kushughulika na watoto wao kwa ufahamu, huwasaidia wazazi kufundisha thamani ya kuwafikiria wengine. “Huenda mmoja wa wana wetu akaelewa,” Martin asema, “lakini yule mvulana mwingine ahitaji msaada mwingi ili aweze kuelewa. Mimi hupata kwamba, kipindi cha funzo hupata kuwa uwanja wa mazoezi ya kuonyesha subira ya Kikristo na matunda mengine ya roho.”—Wagalatia 5:22, 23; Wafilipi 2:4.
Uwe tayari kubadilikana ufaane na uwezo tofauti-tofauti na viwango vya ukuzi vya watoto wako. Simon na Mark ambao sasa ni matineja walipata kwamba, walipokuwa wachanga walifurahia kwa kweli kujifunza kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi pamoja na wazazi wao. “Baba yetu alituomba tuigize sehemu tofauti-tofauti za hicho kitabu sawa na mchezo wa kuigiza,” wao hukumbuka. Baba yao hukumbuka akitembea kwa mikono na magoti pamoja na wanawe ili waigize ule mfano wenye somo wa Msamaria mwenye ujirani mwema. (Luka 10:30-35) “Hilo lilikuwa jambo lenye uhalisi na lenye kufurahisha sana.”
Watoto wengi hukinza ile kawaida ya funzo la familia. Je, jambo hilo lapaswa kuwazuia wazazi wasiongoze hilo funzo wakati ambapo limepangwa kufanywa? La, hasha. “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto,” lakiri andiko la Mithali 22:15. Mama mmoja asiye na mwenzi alifikiri kwamba alikuwa akishindwa kuongoza funzo la familia wakati ambapo, katika pindi nyingi, hicho kipindi cha funzo kilionekana kukatizwa na vikengeusha-fikira. Lakini alistahimili. Sasa watoto wake wanamstahi sana na wamekuja kuthamini upendo na hangaiko aliloonyesha kwa kudumu katika kuongoza funzo la familia la kawaida.
Kuwasaidia Wavulana na Wasichana ‘Wasio na Baba’
Wazee Wakristo wapaswa ‘kulichunga kundi la Mungu.’ (1 Petro 5:2, 3) Kuzuru pindi kwa pindi familia zilizo katika makutaniko yao, huwatolea wazee fursa za kuwapongeza wazazi wenye kuchukua madaraka yao ya Kikristo. Ni nani mwenye daraka la kuwafundisha watoto wa wazazi wasio na wenzi? Usisahau kamwe kwamba daraka la kuwafundisha watoto liko mikononi mwa mzazi.
Busara ya Kikristo itawasaidia wazee waepuke hali ziwezazo kuhatarisha maadili yao ya Kikristo ikiwa watachukua daraka la mzazi asiyekuwako. Ingawa ndugu wawili waweza kumzuru dada Mkristo ambaye ni mzazi asiye na mwenzi, nyakati zote watakuwa wenye hadhari katika yale watakayopanga katika njia ya kutegemeza mpango wa funzo la familia. Pindi kwa pindi, kuwaalika watoto (na, kwa kweli, kumwalika huyo mzazi asiye na mwenzi) wajiunge na funzo la familia la huyo mzee mwenyewe, kwaweza kuthibitika kuwa jambo lenye kujenga na la busara. Hata hivyo, usisahau kamwe kwamba, Yehova ndiye Baba yetu mkubwa wa kimbingu. Bila shaka yeye yupo ili kumwongoza na kumsaidia huyo mama aongozapo funzo pamoja na watoto wake, hata ingawa yeye hufanya hivyo akiwa peke yake.
Vipi hali ambako kijana ana mwelekeo wa kiroho, lakini wazazi wake hawahangaiki sana au hawahangaiki kabisa kuhusu madaraka yao ya kiroho? Watumishi waaminifu wa Yehova hawahitaji kukata tamaa kamwe. “Kwako wewe [Yehova Mungu] aliyepungukiwa, mvulana asiye na baba, hu[ji]kabidhi,” akaimba mtunga-zaburi. “Wewe mwenyewe umekuwa msaidiaji wake.” (Zaburi 10:14, NW) Nao wazee wenye upendo katika kutaniko watafanya yote wawezayo ili kuwatia wazazi moyo wawatunzapo watoto wao. Huenda wakapendekeza mazungumzo ya familia, kisha wakahudhuria mazungumzo hayo ili kutoa madokezo fulani yenye kutumika juu ya jinsi ambavyo hiyo familia yaweza kujifunza pamoja. Bila shaka, wazee hawatachukua daraka la wazazi ambalo, wametwikwa Kimaandiko.
Watoto ambao wazazi wao hawakubali ile imani, huhitaji utegemezo mkubwa. Kuwatia katika funzo lako la familia kwaweza kuthibitika kuwa jambo lenye manufaa ikiwa jambo hilo lakubalika kwa wazazi wao. Robert, ambaye sasa ni mtu mzima mwenye familia yake mwenyewe, alihudhuria mikutano ya Kikristo pamoja na wazazi wake alipokuwa na umri wa miaka mitatu tu. Alikuwa na kumbukumbu zenye kupendeza za mikutano hiyo hata baada ya wazazi wake kuacha kushirikiana na kutaniko la Kikristo. Alipokuwa na umri wa miaka kumi, alifahamiana na mvulana Shahidi aliyemchukua kwenda naye kwenye mikutano. Wazazi wa huyo mvulana Shahidi walimtunza Robert kwa furaha akiwa yatima wa kiroho na baadaye wakajifunza naye. Kwa sababu ya utunzaji huo wenye upendo, alifanya maendeleo upesi na sasa yeye hufurahia kutumikia akiwa mzee kutanikoni.
Hata wazazi wapingapo maendeleo ya watoto wao, hao watoto hawako peke yao. Yehova hubaki kuwa Baba yao wa kimbingu. ‘Baba wa yatima [“mvulana asiye na baba,” NW] ni Mungu katika kao lake takatifu,’ yatangaza Zaburi 68:5. Wavulana na wasichana wasio na baba wa kiroho wajua kwamba waweza kumtegemea Mungu katika sala, na atawategemeza. (Zaburi 55:22; 146:9) Tengenezo la Yehova lililo kama mama, hutimiza kwa bidii nyendelevu daraka lake la kutayarisha milo ya kiroho yenye kupendeza ambayo hupakuliwa kupitia vichapo vya hilo tengenezo na kwenye mikutano ya makutaniko ya Kikristo zaidi ya 85,000 ulimwenguni pote. Hivyo, tukiwa na msaada wa kiroho kutoka kwa Baba yetu Yehova, na tengenezo lake lililo kama mama, hata “asiye na baba” atafurahia kujifunza Biblia kwa kiwango fulani.
Wazazi Wakristo wanaoongoza mafunzo ya Biblia ya familia yaliyo ya kawaida pamoja na watoto wao, wastahili kupongezwa. Wazazi wasio na wenzi ambao hudumu katika kuwazoeza vijana wao katika njia za Yehova hustahili uangalifu na sifa ya pekee kwa ajili ya jitahada zao. (Mithali 22:6) Wale wote ambao huonyesha hangaiko kwa ajili ya watoto wasio na baba kiroho wajua kwamba jambo hilo humpendeza Yehova, Baba yao wa kimbingu. Kutunza mahitaji ya kiroho ya familia ni daraka zito. Lakini ‘usife moyo, kwa maana katika majira yapasayo utavuna usipochoka kabisa.’—Wagalatia 6:9.
[Maelezo ya Chini]
a Majina mengine yamebadilishwa.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Funzo la familia huandaa fursa nzuri kwa walio wachanga zaidi kushiriki mahangaiko yao pamoja na wazazi wao
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]
Harper’s