Je! Watoto Wako ni Wanafunzi wa Kristo?
“Maneno haya ninayokuamuru . . . uwafundishe watoto wako kwa bidii.”—Kum. 6:6, 7.
1, 2. (a) Wazazi wengine wanaonaje juu ya kukuza watoto? (b) Ni sababu gani zilizopo kwa kupendezwa na malezi bora ya mtoto?
KWA sababu gani hata tutumie wakati tukilitafakari ulizo hilo katika kichwa chetu? Kwa sababu gani tusitoe yanayotakiwa na sheria ya Kaisari tu—chakula, mavazi, nyumba, elimu—kisha tumruhusu mtoto ajiamulie mwenyewe mambo ya kidini na maadili atakapokuwa mwenye umri wa kutosha? Kama ungefanya hivyo usingekuwa peke yako katika kuufuata mwendo huu.
2 Lakini kuna sababu nzuri za kuuliza ulizo hili. Je! ongezeko katika jeuri limekufanya ujione kukosa usalama? Je! kuongezeka kwa udhalimu kumekuhuzunisha wewe? Je! ongezeko la haraka la matumizi mabaya ya dawa za kulevya na ufisadi limekusumbua kidogo? Je! maongezeko ya kodi yamekupata wewe? Ikiwa ndivyo, basi kwa sababu vijana wanapatwa na magumu haya, wewe unayo sababu nzuri walau ya kujiuliza kama malezi bora ya watoto yasingalisaidia.
3. N’nini kinachoonyesha kwamba watoto wengi wanaweza kulelewa wakawe namna ambavyo wazazi wao wanataka wawe?
3 Usisahau hata kidogo. Kwa kawaida watoto wanaweza kulelewa wakawe namna ambavyo wazazi wao wanataka wawe. Wachunguzi katika ukuzi wa watoto wamegundua kwamba utu mwingi wa mtoto unakuwa umekwisha anzishwa mbele ya kuingia shuleni na kwamba tabia hizo za utu si nyepesi kugeuzwa nyuma ya hapo. Katika Neno lake Biblia, Muumba wa mwanadamu anasema hivi: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mit. 22:6) Kanuni za msingi zinazoongoza mwenendo zilizosisitizwa wakati wa utoto kwa kawaida hazisahauliki ijapokuwa huenda mtu akageukia kutenda jambo baya kwa sababu ya kutokamilika. Wazo hili limetiwa ndani katika mfano wa Yesu wa mwana mpotevu aliyemwomba baba yake mwenye kuamini urithi wake kisha “akasafiri kwenda nchi ya mbali; akatapanya mali zake huko kwa maisha ya uasherati.” (Luka 15:13) N’nini kilichomrudisha? Kwanza, yeye alimkumbuka baba yake. Siyo misaada ya kimwili tu ambayo baba yake aliitoa sikuzote bali upendo wa baba yake wa mambo ya kiroho. Yeye alisema hivi: “Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako.” (Luka 15:18) Ndiyo, malezi yafaayo wakati wa utoto ni jambo la maana katika kuongoza maisha ya mtoto.
4. (a) Kwa sababu gani kupanga ni kwa lazima katika malezi ya mtoto? (b) Mradi umepaswa uwe nini?
4 Bila shaka, ili yapate kufanikiwa malezi hayo lazima yapangwe. Lazima wazazi wajue wanayoyataka na yatakayotiwa ndani katika kuyatimiza. Ni vema kufikiria yanayotamaniwa yatokee mwishowe na kuyazungumza pamoja. (Mit. 21:5; 15:22) Mradi hapa umepaswa uwe kutokeza mtu mzima awezaye kufikiri mwenyewe, aliyejitoa kwa haki, amjuaye Mungu, nia na imara ya kumtumikia Mungu kwa kumwiga Yesu Kristo, na mwenye kufurahia kufanya mambo kwa ajili ya wengine. Lakini malezi yanapoachwa yakitegemea bahati tu ya kwamba huenda yakawa mazuri, matokeo yanakuwa kama yale yanayotajwa katika Mithali 29:15: “Mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.” Hili laweza kuepukwa wakati wazazi wanapotumia mamlaka yao kwa kupendezwa na hali njema yenye kuendelea ya mtoto.
FIMBO YA MAMLAKA
5, 6. (a) Inawapasa wazazi wakumbuke nini juu ya adhabu wanayopaswa kutoa? (b) Yehova anawekaje mfano katika matumizi ya adhabu ya wazazi?
5 Inampasa mtu mwenye mamlaka atoe hesabu mwishowe kwa mwenye kuagiza mamlaka hiyo. Hivyo wazazi wanalo daraka zito katika kulea watoto wao kwa maana lazima watoe hesabu kwa Mungu ya agizo walilopewa wao. Ni kama vile Zaburi 127:3 inavyowakumbusha wazazi: “Tazama, wana ndio urithi wa [Yehova].” Kwa hiyo mtume Paulo anashauri hivi: “Ninyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana.” (Efe. 6:4) Kufanya hivi kwatia ndani na kufundisha watoto wako kwamba Yesu alituachia ‘kielelezo, tufuate nyayo zake’ kupatana na mapenzi yake Yehova.—1 Pet. 2:21.
6 Katika Israeli, fimbo ilikuwa chombo cha kuadhibia. Katika 2 Samweli 7:14 Yehova alisema hivi juu ya mrithi wa Mfalme Daudi: “Akitenda maovu nitamwadhibu kwa fimbo ya binadamu na kwa mapigo ya wanadamu.” Vile vile, mtume Paulo anaandika hivi kwa washiriki wa Israeli wa kiroho katika 1 Wakorintho 4:15-21: “Walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili. . . . Mnataka vipi? Nije kwenu na fimbo, au nije katika upendo na roho ya upole?” Kitabu cha Mithali kinasema hivi: “Usimnyime mtoto wako mapigo; maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa. Utampiga kwa fimbo, na kumwokoa nafsi yake na Kuzimu.” (Mit. 23:13, 14; 22:15) Namna ambavyo fimbo hii ya wazazi ya adhabu iliyoamriwa inavyotumiwa ni shauri zito. Wazazi wana wajibu kwa Mungu, anayetoa mamlaka ya kuadhibu, kuitumia “fimbo” ifaavyo. Kushindwa kufanya hivi kwaweza kutokeza kifo cha mtoto, kama vile mithali inavyosema, na vile vile kukataliwa kwa kimungu kwa wazazi. Yehova mwenyewe anaweka mfano katika matumizi yafaayo ya mamlaka ya baba ya kuadhibu, kama inavyoonyeshwa katika Waebrania 12:7, 9, 10: “Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? Maana ni hakika, hao kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake.” Yehova anawaadhibu watu wake, siyo kwa sababu amekasirishwa, bali “kwa faida yetu,” ili tuweze kuwa na kibali chake na kuishi. Yeye anatazamia baba za Kikristo wawatendee watoto wao vivyo hivyo, wakikusudia wawe wanafunzi wa kweli wa Mwana wake.
YATIMA
7, 8. (a) Eleza kupendezwa kwa Yehova na yatima. (b) Kwa sababu gani nyumba isiyokuwa na baba ilikuwa jambo la msiba?
7 Namna ambavyo Yehova aliwaamuru Waisraeli wawaangalie yatima yakazia moyoni mwetu wema ambao baba mwenye kumcha Mungu aweza kutimiza katika jamaa. Angalia kupendezwa kwa Yehova na hao waliofiwa: “Usipotoshe hukumu ya mgeni, wala ya yatima; wala usitwae mavazi ya mjane, yawe rehani; bali kumbuka ya kuwa ulikuwa mtumwa katika Misri, [Yehova], Mungu wako, akakukomboa huko; kwa hiyo nakuamuru kutenda neno hili.” (Kum. 24:17, 18) Hakuna kutia shaka kwamba Mungu hakuufahamu ukiwa uliokuwa katika nyumba hiyo iliyofiwa.
8 Nyumba isiyo na baba ilikuwa yenye msiba kwa njia nyingi. Baba ndiye aliyepaswa kutoa mambo ya kimwili yaliyo ya lazima. Angeweza kuwalinda na wale ambao wanaweza kuiba, kuwanyang’anya ama sivyo kuwaonea. Yeye alikuwa akimpa mwana uongozi wake, na maonyo, ushirika na upendo. Kwa hiyo, Torati ilitoa makumbusho juu ya haja ya kupendezwa kwa pekee baba asipokuwapo.—Kut. 22:22-24.
9. (a) Nia juu ya ‘yatima’ ilikuwaje wonyesho wa hali ya kiroho ya taifa? (b) Maoni ya mtu juu ya hao wenye huzuni yanakamatanaje na Ukristo?
9 Usemi “yatima” hata ulitiwa ndani wakati Mungu alipokuwa akisimulia kadiri ya uaminifu wa taifa zima la Israeli. Wakati ambapo taifa lilipata kudhoofika kwa kiroho nalo likaanza kupotosha haki, yatima alikuwa kati ya walio wa kwanza kutaabika. Hivyo Yehova akamfanya nabii Yeremia aandike hivi: “Maana kama mkitengeneza kabisa njia zenu na matendo yenu; kama mkihukumu hukumu ya haki kati ya mtu na jirani yake; kama hamwonei mgeni, wala yatima, wala mjane, wala kumwaga damu isiyo na hatia mahali hapa, wala kuifuata miungu mingine kwa hasara yenu wenyewe; ndipo nitakapowakalisha mahali hapa, katika nchi hii niliyowapa baba zenu, tokea zamani hata milele.” (Yer. 7:5-7) Maoni ya Mungu juu ya jambo hili hayajageuka. Njia moja ya kujua Wakristo wa kweli leo ni kutazama wanavyowaangalia waliofiwa. Katika Yakobo 1:27 inasema: “Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.”
10. Leo kijana mwanamume awezaje kuwa ana baba na hali awe yatima kwa njia fulani? (b) Kwa hiyo, wazazi wanayo sehemu gani katika kuwa kwa watoto wao wanafunzi wa Kristo?
10 Je! yawezekana leo kijana mwanamume akawa ana baba na hali, kwa njia fulani, akawa ni yatima? Kwa bahati mbaya, hii yaweza kuwa kweli. Ikiwa kijana mwanamume anaona ni lazima aende peke yake kwenye mikutano ya Kikristo, ijapokuwa baba yake kweli angeweza kuwa pamoja naye, basi kijana mwanamume huyo ni yatima wakati huo. Ikiwa lazima mvulana atazamie mtu mwingine ili apate mazoezi yo yote katika huduma ya shambani ya Kikristo, basi yeye ni yatima katika sehemu hiyo ya maisha yake. Ndivyo ilivyo na kwa njia nyingine. Lakini ni jambo jema kama nini wakati baba wa Kikristo anapochukua madaraka yake: akiongoza funzo la jamaa la Biblia, akipanga tafrija, akijifanya mwenyewe apatikane afikiwe magumu yanapotokea, na kutoa mazoezi mwenyewe katika kuangalia madaraka nyumbani ili aweke msingi mzuri wa kuchukulia madaraka katika maisha ya nyumaye. Maagizo yafaayo katika maisha yote ya Kikristo yanahitajiwa. Watoto hawawi wanafunzi wa Kristo kwa njia yo yote ile ati kwa kuwa wazazi wao wanajidai kuwa hivyo. Wanahitaji msaada wa kipekee. Baba ambaye ndiye msaidizi katika hatua zote za maisha ya mtoto ni baraka kweli kweli.
KAWAIDA YAKO YA KILA SIKU
11, 12. Kumbukumbu la Torati 6:6, 7 linasema nini juu ya ibada, na matumizi ya shauri hilo yaweza kuwapasaje washiriki wa jamaa zetu?
11 Katika Kristendomu, kwa kawaida wale ambao wangali wakienda kanisani wanasikiliza mahubiri mafupi Jumapili, na watoto wanakuwa na kipindi cha kila juma katika “Sunday school.” Hii inatazamiwa kuyaangalia mahitaji ya kidini ya jamaa. Je! hii yalinganaje na yale ambayo Yehova aliyapanga kwa jamaa? Kumbukumbu la Torati 6:6, 7 linasema hivi: “Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” Kutokana na haya ni wazi kwamba ibada ya Yehova ilipaswa kuwa njia ya maisha na kwamba kuzungumza makusudi yake kulipaswa kuwe katika vipindi vyenye kufaa wakati wote wa kawaida ya mtu ya kila siku.
12 Inakuwa vema namna gani wakati ambapo mawazo ya kwanza ya mtu yanakuwa juu ya Yehova na Mwanawe anapoamka! Je! kuna mambo yaliyo bora ya kuzungumza unapoanza utendaji wa siku kuliko matendo ya Mungu? Ibada ya Yehova haiwezi ikatenganishwa na kawaida ya kila siku ya maisha. Wakati usemi na mwenendo wa wazazi unaposadikisha kwamba ndivyo ilivyo, watoto watakua wakiona ubora wa kwamba Mungu anaona kila kitu wanachokifanya naye anapendezwe na namna wanavyokifanya, kwamba ni jambo la maana kuwa mwigaji wa Mwana wa Mungu katika kila walifanyalo. Kwa hiyo Mungu na Mwanawe wamo katika mawazo ya mtoto nyakati zote, siyo nyakati za pekee zinapowekwa kando kwa ajili ya ibada tu. Watakuwa wakiitazamia baraka ya Yehova juu ya kila kazi watakayoifanya nao watautafuta uongozi anaoutoa kupitia kwa Maandiko Matakatifu Wakati mtoto anapopokea namna hii ya malezi, itaelekea sana kuwa kweli kwamba “hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”—Mit. 22:6.
13. Kwa sababu gani ni jambo la maana kumkumbuka Mungu katika mawazo yetu nyakati zote?
13 Lakini lo! watu wengi wanaona ni vyepesi namna gani kuendeleza kawaida yao ya kila siku na kumwondoa Mungu katika mawazo yao! Walakini, kufanya hivi kwa mtu nyumaye kwaweza kumfanya akawa kama wale ambao juu yao Yesu alisema hivi: “Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.” (Mt. 24:37-39) Lakini kwa hekima alitia moyo kumkumbuka Mungu mchana kutwa bila ya kujali tunafanya nini. Yeye alisema hivi: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Aliwapa Wakolosai onyo la namna ile ile: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova], wala si kwa wanadamu.” (Kol. 3:23) Hivyo ndivyo afanyavyo mwanafunzi wa Kristo. Je! wewe unawafundisha watoto wako wafanye hivyo?
14. Toa mfano wa namna ambavyo Mungu anaweza kuingizwa katika mazungumzo baba na mwana wanapofanya kazi pamoja katika kawaida fulani ya kila siku.
14 Je! wewe na mwana wako mnafanyia kazi motokaa ya jamaa mkiwa pamoja mara kwa mara? Je! sehemu hii ya kawaida ya kila siku inao ukamatano gani na Biblia? Basi, motokaa ilipaswa kuundwa na kutengenezwa kupatana na sheria zilizowekwa na Muumba, nawe lazima uendelee kuzitambua sheria hizo za asili ikiwa utaiendesha kwa mafaa. Kulinganisha sauti kwa pindi kwa pindi na marekebisho, kutia mafuta na kuyageuza vyote ni vya lazima kwa sababu ya sheria za Mungu. Je! unamkumbusha mwanao mambo haya anapofanya kazi? Jambo jingine: Je! Kaisari wa serikali anazo sheria fulani za usalama zinazoongoza uendeshaji wa motokaa katika nchi yako? Je! lazima mipira, taa na breki zifikie kanuni fulani kusudi kwamba ajali ziweze kuepukwa na maisha kulindwa? Ni jambo la muhimu kadiri gani kujipatanisha na matakwa haya? Katika Warumi 13:1 twaambiwa hivi: “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo imeamriwa na Mungu.” Je! wewe unatia mawazo haya moyoni mwa mwanao mnapofanya kazi pamoja?
15. Toa mfano wa namna ambavyo Mungu anaweza kuingizwa katika mazungumzo mama na binti wanapofanya kazi pamoja.
15 Je! wakati wo wote mama na binti wanafanya kazi pamoja katika kutengeneza vazi? Je! hii inao ukamatano gani na Maandiko? Litakuwa la mtindo gani? Je! litapatana na 1 Timotheo 2:9, 10, anayesema hivi: “Wanawake na wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi”? Utalipamba kwa kitu gani, naye binti yako atalivaa pamoja na vitu gani? Sehemu iliyobaki ya andiko hilo hilo yasema kwamba wanawake wanaomheshimu Mungu imewapasa wajipambe, “si kwa kusuka nywele, wala kwa dhahabu na lulu, wala kwa nguo za thamani; bali kwa matendo mema.” Yawezekana mtu asipovaa sikuzote mavazi ya bei kubwa sana, atajifunza uwekevu mzuri na “kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.” (Efe. 4:28) Kuna kanuni nyingi za Maandiko ambazo binti yako anaweza kujifunza mnapofanya kazi pamoja kuitimiza kazi ya kila siku nyumbani, ‘mkifanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’
16. (a) Imewapasa wazazi na watoto vile vile watumie namna gani ya usemi, na kwa sababu gani? (b) Ijapokuwa hatuwezi tukawa tukisoma Biblia na vitabu vya Biblia wakati wote, twaweza kufanya nini?
16 Je! wewe unatumia usemi wa namna gani katika ushirika wa kila siku na watoto wako? Wanafunzi wa Yesu wanajua kwamba matumizi yafaayo ya ulimi ni ya maana. (Mt. 12:36) Biblia inaonya: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia.” (Efe. 4:29; Tito 2:6-8) Bila ya kujali habari yenyewe, maoni yanayosemwa yamepaswa yapatane na maongozi ya roho ya Mungu yaliyoandikwa na mtume Paulo, wakati aliposema hivi: “Mambo yo yote yaliyo ya kweli, yo yote yaliyo ya staha, yo yote yaliyo ya haki, yo yote yaliyo safi, yo yote yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema; ukiwapo wema wo wote, ikiwapo sifa nzuri yo yote, yatafakarini hayo.” (Flp. 4:8) Ni kweli kwamba hatuwezi tukawa tukisoma Biblia au vitabu vya Biblia mchana kutwa. Lakini, sikuzote twaweza kuwa tukiwaza, kusema na kufanya kazi kupatana na Maandiko kwa kumwiga Kristo. Ikionyesha maoni haya, Zaburi 119:97 inasema hivi: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.”
VIPINDI VYA PEKEE VINAVYOWEKWA KANDO
17. Kwa sababu gani funzo la kawaida la jamaa ni jambo la maana katika kulea watoto?
17 Zaidi ya kufundisha na kulea watoto wako wakati wa kawaida ya kila siku, ili ufanikiwe kweli ni jambo la maana kuweka kando vipindi vya pekee kwa funzo la jamaa la kawaida. Ukawaida katika hili ni wa maana kama vile ulivyo ukawaida katika kula na kunywa. Si ajabu sana kwamba kwa kawaida tunataja kweli ya Maandiko kama chakula cha kiroho, tukizikumbuka nguvu kinazozitoa, furaha katika kukila na uhitaji wake unaoendelea.—Mt. 4:4; 5:3.
18. N’nani anayepaswa kuamua mambo ambayo jamaa itajifunza, na kwa sababu gani?
18 Habari ya kusomwa yapaswa ichaguliwe na kichwa cha jamaa. Kama vile yeye anavyoamua mambo ya kimwili ambayo jamaa itakuwa nayo, ndivyo lilivyo na daraka lake kuamua yale ambayo jamaa itajifunza. Yeye ndiye aliyemo katika hali bora kujua yanayohitajiwa na jamaa. Zaidi ya hayo, anaweza kuuliza wengine mambo wanayodhani yatakuwa yenye faida, kisha ayafikirie. Kila jamaa itakuwa na mahitaji fulani ya pekee nyakati nyingine. Huenda makala zinazozungumza juu ya matumizi mabaya ya dawa za kulevya, mwenendo kati ya wanaume na wanawake, uaminifu, mashirika, fadhili, na mengineyo zikafaa, ikitegemea hali zinazositawi.
19. Kwa kawaida, jamaa itajikuta ikijifunza nini?
19 Kwa kawaida, jamaa itaona kwamba wanafaidika sana kwa kuifuata njia ya funzo iliyotayarishwa kwa ajili ya kundi, wakijitayarisha washiriki mikutanoni. Ikiwa hapana haja ya pekee katika jamaa, sababu gani usikaze fikira zako juu ya habari ya funzo ambayo wengine wote katika kundi wanaifikiria na kuizungumza? Itakuwa na matokeo yenye kuunganisha sana na kila mmoja aweza kushiriki sana katika mazungumzo penye mkutano iwapo jamaa zinajitayarisha nyumbani kupatana na orodha ya kundi. Bila shaka, waliobarikiwa na wakati mwingi zaidi wa kujifunza wanaweza kufanya uchunguzi zaidi.
20. Ikiwa kujitayarisha kwa ajili ya mikutano kunasikika kama jambo la kuchosha na lisilopendeza kwa wengine, huenda ugumu ukawa nini, nao utatuzi ungeweza kuwa nini?
20 Kujitayarisha kwa ajili ya mikutano kwaweza kusikika kama jambo lisilopendeza kwa watoto wengine. Hiyo ni kwa sababu ya maoni yao. Yaelekea wao wanafikiria kutayarisha maelezo machache tu juu ya maulizo ya funzo. Ijapokuwa huu waweza kuwa mradi ufaao wa kuanzia, mradi wenyewe umepaswa kuwa kuishika habari ya Maandiko kisha kusaidia wengine wafanye hivyo kwa maelezo yaliyotolewa. Karibuni funzo linakuwa lenye kupendeza kwa mtu apendaye kweli, akiwa na kusudi hili.—Zab. 1:1, 2.
21. Ni mambo gani mengine ambayo wazazi wanaweza kuyafanya ili kulifanya funzo la jamaa lenye kuchangamsha na kupendeza?
21 Kuna mambo mengine ambayo wazazi wanaweza kuyafanya ili kulifanya funzo la jamaa lenye kuchangamsha na kupendeza. Kuacha hali iwe ya kirafiki na ya kuburudisha kutasaidia. Hapana ye yote anayejifunza vema anapokuwa katika mkazo au woga. Akili za watoto hazitaitikia sana ikiwa wazazi ni wakali na wenye kutaka mambo yafanywe kwa nguvu. Ijapokuwa imara ya kutosha inahitajiwa ili kuendeleza utaratibu na kuonyesha uzito wa wakati, hata hivyo kuna nafasi nyingi ya ile namna ya uchangamfu na kupendezwa kwa mtu na mwenzake kunakoiunganisha jamaa.
22, 23. (a) Kwa sababu gani haiwapasi wazazi kujiona hafifu kwa watoto wao ati kwa sababu elimu zao zinatofautiana? (b) Watoto wanaweza kusaidiwa wafahamu nini kwa njia yenye faida?
22 Ni kweli kwamba nyakati nyingine wazazi hawana elimu ambayo watoto wao wadogo wanaipata sasa. Wazazi wengine wametoka nchi nyingine, nao watoto wao waingiapo shuleni wanaifahamu lugha mpya, lakini wazazi wasiweze. Katika jamaa za kilimwengu watoto walio chini ya hali hizi mara nyingi wanajichukulia nia ya kujiona wakuu kupita wazazi. Lakini je! kizuizi hiki chaweza kushindwaje katika jamaa ya Kikristo wakati wazazi wanapojaribu kuchukua daraka lao walilopewa na Mungu juu ya watoto, “kuwalea katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova”?—Efe. 6:4, NW.
23 Wazazi hawana haja ya kujiona hafifu kwa watoto wao ati kwa sababu nyingine za hali zilizotajwa juu zinasitawi. Cheo chao cha mamlaka katika nyumba wamepewa na Mungu. Zaidi ya hayo, miaka yao ya maono na hali za maisha vinawafanya wanaofaa zaidi kuiruzuku jamaa, kuisimamia nyumba, na kuongoza katika funzo la jamaa na ibada. Katika hali inayolingana huenda wakawako ndugu vijana wanaokaribia umri wa 20 katika kundi au ambao ndio sasa wanauanza na ambao wanaweza kutoa habari za wanafunzi za kupendeza zaidi kuliko wengine wa ndugu wazee, lakini hii haiwastahilishi kuwa wazee. Mengi zaidi yanatiwa ndani katika uzee. Ndivyo ilivyo na kwa watoto wakilinganishwa na wazazi wao katika jamaa. Bila ya kujali elimu na hali ya wazazi, inawapasa wao kupanga wakati wa funzo la jamaa, kisha waruhusu kila mmoja aeleze anayoweza, kwa faida ya wengine. Ikiwa watoto wanao uwezo mkubwa zaidi katika pande fulani, wanaweza kusaidiwa wafahamu kwamba siyo akili tu iliyo ya maana kwa Yehova, bali unyenyekevu na wingi wa kujitoa. Yesu alisema hivi: “Ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa.” (Mt. 23:12) Roho ya Yehova itakamilisha mambo yo yote ambayo huenda mzazi anajisikia hanayo. Ufuate mpango wa Maandiko wa funzo la jamaa kwa matumaini, pasipo kujali uwezo wa namna mbalimbali wa akili wa washiriki mbalimbali wa jamaa.
24. Wazazi watajuaje kama watoto wao kweli ni wanafunzi wa Kristo?
24 Je! watoto wako ni wanafunzi wa Kristo? Basi, ikiwa wao hawakujitoa tu kwa ubatizo wa Kikristo lakini vile vile wanayafanya mazoea ya kuweka maamuzi yao juu ya msingi wa aliyoyasema Yesu na akayafanya, ikiwa wao hawaonyeshi upendo kwa njia mbaya za ulimwengu lakini wanakaza macho kwenye mradi wa kutumikia faida za Ufalme sikuzote, ikiwa wao wanajitiisha kwa mamlaka yako kwa hiari na kufurahia kuzungumza njia za Yehova, ikiwa wanaujaza moyo wako na upendo wenye kuchangamsha kwa maana unayaona mambo haya ndani yao, haitakupasa kukisia. Wewe utajua kwamba wao kweli ni wanafunzi wa Kristo.
[Picha katika ukurasa wa 343]
Kanuni za Maandiko zinazotumika kwa mavazi zaweza kufundishwa wakati mama na binti wanapotengeneza mavazi pamoja
[Picha katika ukurasa wa 344]
Ukawaida katika kufundisha watoto wako ni wa muhimu kama ulivyo ukawaida katika kula na kunywa