Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 7/15 kur. 4-10
  • Kulea Watoto Wenye Furaha Katika Ulimwengu Wenye Mchafuko Mwingi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kulea Watoto Wenye Furaha Katika Ulimwengu Wenye Mchafuko Mwingi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MIFANO YA KIBIBLIA
  • USHIRIKA MBAYA
  • MATATIZO YA KIJAMAA
  • MAARIFA NA ELIMU
  • MRADI ULIO JUU
  • Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Kujenga Familia Yenye Nguvu Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Je! Wewe Unafundisha Watoto Wako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 7/15 kur. 4-10

Kulea Watoto Wenye Furaha Katika Ulimwengu Wenye Mchafuko Mwingi

Hii ndiyo ya kwanza kati ya makala mbili za kujifunza. Hii ni kwa ajili ya wazazi na watoto, lakini ile ya pili ni kwa ajili ya watoto wenyewe hasa.

“Laiti wangekuwa na moyo kama huu ndani yao sikuzote, wa kunicha, na kushika amri zangu zote sikuzote, wapate kufanikiwa wao na watoto wao milele!”​—⁠Kumbukumbu la Torati 5:29.

1. Kwa sababu gani habari ya somo hili ni ya maana sana kwetu?

“WEEE, KITOTO CHANGU CHA KWANZA, WEEE!” Hayo ni maneno ya furaha gani yanayosemwa na mama mwenye kukumbatia kifuani toto lenye kupendeza sana! Biblia inataja habari za mama mwenye kunyonyesha mtoto na kuutumia huo kama mfano wa shauku ya upendo inayopasa kuwa ndani ya kundi la Kikristo. Hata watu wasio haki wanapenda watoto wao, tena wanawapa vitu vizuri. Kwa uhakika inatupasa sisi tunaopenda haki ya adili tuhangaikie watoto wetu hata zaidi, kisha tuwazoeze waweze kuishi vizuri katika ulimwengu wa leo!​—1 Wathesalonike 2:7; Zaburi 127:3-5; Mathayo 7:11.

2. Ni nini chanzo kilicho bora zaidi cha maoni yenye mafaa na uongozi juu ya kulea watoto? Kwa sababu gani?

2 Lakini baada ya muda mfupi kupita mtu ambaye amekuwa mzazi hivi juzi anatambua kwamba ni daraka zito sana kulea watoto. Wewe unaweza kupata wapi maoni yenye mafaa na uongozi? Kwa nini usimtegemee Muumba? Yeye ndiye aliyepanga watoto wawe wakizaliwa. (Mwanzo 1:28) Yeye amekuwa akiona uzaliwa wa kila mtoto ambaye amepata kuzaliwa, hata akayaona matokeo ya hatua walizozichukua wazazi. Kwa sababu hiyo yeye ndiye anayeweza kututolea mafundisho yaliyo bora zaidi. Mafundisho hayo yameandikwa katika Biblia​—pamoja na mifano ya watu waliofuata kanuni zake, na ya wengine ambao hawakufanya hivyo.​—Mithali 3:5, 6.

3. (a) Ni nini mengine ya mambo ambayo watoto wetu wanahitaji? (b) Kwa nini haifai jambo hilo lituvunje moyo?

3 Kitabu hicho kilicho kizuri sana kinatufundisha nini juu ya kulea watoto? Kinaonyesha mambo mengi ambayo wataalamu wa kisasa wanadhani wao ndio waliojivumbulia. Kati ya mambo mengine, kinaonyesha kwamba watoto wanahitaji kupendwa na kujisikia wakiwa na usalama. Wanapaswa kufundishwa habari za Mungu na Neno lake. Wanahitaji elimu nzuri, kujionea mambo mengi yenye faida maishani, kuwekewa mifano myema na kuwa na ushirika pamoja na watu wanaofaa. Kinaonyesha wanapaswa kujifunza kutii na kuheshimu mamlaka. Wanapaswa kufundishwa maadili (tabia njema) na habari za ndoa, habari za namna wanavyoweza kuwa waume au wake wema, na namna ya kuwa wazazi wema. Labda wewe mzazi utakuwa na maoni ya kwamba hiyo ni kazi ngumu mno. Lakini kumbuka kwamba Biblia inaweza kumpa mtu hekima. Inaweza “kuwapa wajinga werevu,” na kijana “maarifa na hadhari” [maarifa na uwezo wa kufikiri, NW]. Acha tuchunguze mengine ya mambo inayotuambia juu ya kulea watoto.​—Mithali 1: 4.

MIFANO YA KIBIBLIA

4. (a) Watoto wa wazazi wenye kumwogopa Mungu walijifunza nini? (b) Mafundisho hayo yalitolewa na nani na kwa njia gani?

4 Biblia inaonyesha kwamba watoto wa wazazi wanaomwogopa Mungu walilelewa katika usalama siku za zamani, wakalelewa na jamaa zilizohangaikia udhaifu wao mbalimbali na uhitaji wao wa kulindwa. (Mwanzo 33:14; 43:8) Watoto walifundishwa njia ya kujitafutia riziki​—Daudi alikuwa kivulana mchungaji, na Yesu alikuwa seremala. (1 Samweli 16: 11; Marko 6:⁠3) Walijifunza pia jambo fulani la maana hata zaidi​—maajabu ya Mungu aliye mkuu, YEHOVA. Hawakufunzwa mambo hayo katika madarasa ya kidini kwa njia ya maulizo na majibu wala katika shule za Jumapili za watoto wadogo. Walifunzwa na watu waliotaka zaidi sana kuona watoto hao wakipata faida iliyo kubwa zaidi​—wazazi wao wenyewe. Yehova aliwatazamia Waisraeli wajulishe wana na wajukuu wao njia zake. (Kumbukumbu la Torati 4: 9, 10) Wazazi walipaswa kufundisha watoto wao nyakati zote​—⁠wakiwa nyumbani au mbali na nyumbani, wakati wa kulala au wa kuamka. Walipaswa kufundisha kwa maneno na kwa mfano wao wenyewe, hivyo wakapitishia vizazi vilivyofuata kweli nzuri ajabu.​—Kumbukumbu la Torati 11:18-21.

5. Kamusi ya Biblia inayojulikana sana inasema nini juu ya kuwapa watoto mazoezi?

5 Ile kamusi ya Kifaransa inayojulikana sana, Dictionnaire de la Bible, inasema kwamba mara tu mtoto alipoweza kuongea alifundishwa vifungu kadha vya sheria ya Kibiblia. “Mama yake alikuwa akirudia kutaja-taja mstari fulani; mtoto huyo alipoujua, ndipo mama alipompa mstari mwingine. Baadaye, watoto walipewa maandishi ya mistari waliyoweza kuitaja kwa moyo neno kwa neno. Hivyo, waliwekewa chanzo cha kuweza kusoma na, wakati walipopata umri mkubwa zaidi, wangeweza kuendeleza mafundisho yao ya kidini kwa kusoma na kuitafakari sheria ya Bwana.”a Kitabu hicho kinaendelea kusema hivi: “Mtoto alipaswa kupokea masomo yake ya kwanza yenye kumfaa zaidi katika adili akiwa chini ya ulinzi wa jamaa na kupakatwa na baba na mama yake.”​—Vol. II, Safu ya 1596.

6. (a) Watoto Waisraeli walikuwa na matukio gani yenye kuwasisimua? (b) Je! watoto wako wamepata kufurahia matukio kama hayo, na ikiwa ndivyo, walipata faida gani?

6 Mungu alijua kwamba watoto wanafurahia upesi kushughulika na mambo mapya na kwamba mambo hayo yanaweza kusaidia wazazi kufundisha watoto. Kwa sababu hiyo hao “watu wadogo” walifuatana na wazazi wao katika safari zenye kusisimua za kwenda Yerusalemu wakaisikie sheria ya Mungu ikisomwa. (Kumbukumbu la Torati 31:12, 13, NW) Watoto wako wanaweza kufurahia baraka kama hizo, wakihudhuria kwa ukawaida makusanyiko ya mizunguko na ya wilaya ya Mashahidi wa Yehova. Huko wanaweza kufaidika kutokana na mafundisho yanayotolewa, wanaweza kushiriki kujitolea kazi, na kupata rafiki wapya huko. Wewe unaweza kuwakazia watoto wako matukio hayo ili wayaone kuwa mambo makubwa ya maisha zao, kama vile safari za kwenda Yerusalemu zilivyokuwa matukio ya pekee kwa watoto Waisraeli.

7. Kwa nini ni jambo la maana sana kuweka mfano unaofaa?

7 Mungu aliujua ubora wa kuweka mfano mwema. Watoto wanaiga yale wanayoyaona. Ingawa ni vigumu sana kujifunza lugha, watoto wanaweza kujifunza kwa kuiga maneno wanayoyasikia yakisemwa. Mungu alisema: “Laiti [wale watu] wangekuwa na moyo kama huu ndani yao sikuzote, wa kunicha, na kushika amri zangu zote sikuzote, wapate kufanikwa wao na watoto wao milele!” Biblia inasema hivi: “Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi.” (Kumbukumbu la Torati 5:29; Mithali 13:22) Basi, kama watoto watafaidika au hawatafaidika sana inakutegemea wewe. Sisi wazazi tunapaswa tufanye yote tuwezayo tuweke mfano unaofaa, kwa maana pasipo shaka tusingetaka watoto wetu wawe wakifuata mfano mbaya.

USHIRIKA MBAYA

8. Inatupasa tujiulize maulizo gani juu ya mashirika ya watoto wetu?

8 Mungu anakaza fikira zetu kwenye hatari za ushirika mbaya pia. Neno lake linasema hivi: “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” (1 Wakorintho 15:33, NW) Basi ni jambo la maana ujue watoto wako wanashirikiana na nani. Je! wewe unajua kweli kweli rafiki za watoto wako? Je! unawaambia walete rafiki zao nyumbani, ndani ya nyumba, ili wewe upate kujuana na rafiki hao? Au unaambia watoto wakatembee, ili upate nafasi ya kufanya mambo yako bila kusumbuliwa nao? Je! unajua ni usemi wa namna gani unaosikiwa na watoto wako kwa watu wengine, na je! unajua maoni ya washirika wao juu ya kusema uongo, kuiba na kutumia dawa za kulevya?

9. Ni hatua gani zenye lengo zuri unazoweza kuchukua usaidie watoto wako wapate rafiki wazuri zaidi?

9 Ikiwa watoto wenzao si watu wanafaa kwa ushirika, watoto wako wanaweza kupata wapi rafiki wazuri zaidi? Ni katika kundi la Mashahidi wa Yehova​—ambamo usemi mchafu-mchafu, kusema uongo, kuiba na matumizi mabaya ya dawa za kulevya hayaachiliwi. Je! kuna siku ambayo wewe ulijisikia kwamba ingefaa wengine kundini washirikiane zaidi na watoto wako? Basi mbona usiwaeleze watu hao habari hizo? Je! wewe umechukua hatua ya kwanza kuwafikia watu hao? Mbona usikaribishe watoto wengine waje kwako, au uwaombe wajiunge nawe kutoa ushuhuda wa Kikristo au kufurahia mambo mengine yanayofaa?

10. Unaweza kuwasaidiaje watoto wako wawe washirika wazuri zaidi kwa wenzao?

10 Ikiwa umejaribu kufanya hivyo na bado unaona tatizo la kupata washirika wa watoto wako, ingefaa ujiulize, Sababu gani sikuwapata? Je! umeanza juzijuzi tu kufuata kanuni za Biblia? Nyakati nyingine inakuwa kwamba vijana wanaoletwa kwenye Jumba la Ufalme hawajarekebisha matatizo fulani hata waweze kuwa washirika wema. Kijana mmoja alisema hivi juu ya kijana mwenzake: “Msichana huyo anapokuwa kwenye Jumba la Ufalme anajifanya mtu mzuri, lakini ukiona vile anavyofanya shuleni, weee!” Maoni mapotovu ya msichana huyo kuhusu mambo ya ngono shuleni yalifanya wengine wakawa hawataki kuonekana wakishirikiana naye. Wewe unaweza kusaidiaje watoto wako wabadili nia yao katika mambo hayo? Mambo yanayoweza kusaidia sana ni mafundisho unayotoa, funzo la Biblia la jamaa yako, ushirika wenu wa jamaa katika kutoa ushuhuda wa Kikristo, mfano wako mwenyewe katika usemi, mwenendo na unyofu wa kutenda mambo, na jitihada zako za kujaribu kuufikia moyo wa mtoto kwa kutumia kanuni zinazofaa. Kukiwa na uhitaji, wazee wa kundi pia wanaweza kuitwa wasaidie kwa njia yenye upendo.​—Yakobo 5:13-15.

MATATIZO YA KIJAMAA

11. Kwa nini haikupasi ukate tumaini ikiwa watu fulani katika jamaa yako mwenyewe wanaweka mfano mbaya?

11 Lakini namna gani ikiwa mna matatizo mazito mle mle ndani ya jamaa yako mwenyewe? Namna gani kama mwenzi asiyeamini anaishi maisha yaliyo kinyume kabisa cha kanuni za Biblia zinazofaa? Usikate tumaini. Uvutano wako mzuri na msaada wa roho ya Mungu unaweza kufanya maajabu. Kuna watoto ambao wamepambana na matatizo yaliyoelekea kutokushindika kisha wakayaweza, wakawa vijana wazuri. Wanadamu walifanyizwa na Mungu, na hata watoto wadogo wanaweza kuonyesha wema wa kustaajabisha wanapoelekezwa kunakofaa na rafiki, na mtu mzima mwenye kutumia akili zake vizuri, au na mzazi mmoja tu aliye mwamini katika jamaa yenye kujawa na watu wengi wasioamini.

12. Mifano ya Loti na Timotheo inatoaje kipa-moyo katika jambo hili?

12 Ufikirie mfano wa Loti. Jamaa yake iliishi katika jiji la Sodoma lenye maovu, na inaonekana kwamba mkewe alitaka kubaki humo. Lakini Loti na binti zake walikimbia wakauokoka uharibifu wa jiji hilo. (Mwanzo 19:15-17, 23-26) Baba ya kijana Timotheo hakuwa mwamini, lakini mama na nyanya (bibi) yake walimfundisha Maandiko kisha wakaja kumwona akiwa mfuasi mwaminifu wa Yesu Kristo na mwenzi mshikamanifu wa mtume Paulo. (2 Timotheo 1:5; 3:14, 15) Kwa hiyo, hata kama mwenzi wako si mwamini, Mungu anaweza kukusaidia ukaze kikiki katika mioyo ya watoto wako hali ya kuipenda kweli na haki ya adili.

MAARIFA NA ELIMU

13. (a) Kwa nini inawapasa Wakristo vijana waichukue elimu kuwa jambo lisilo la kuchezewa ovyo tu? (b) Mfano wa Sulemani unaonyeshaje ubora wa kutumia usemi sahihi?

13 Je! wewe unawatia moyo watoto wako wajifunze mambo, shuleni na kundini pia? Je! kujifunza mambo kunaonwa na jamaa yako kuwa jambo la maana? Kulikuwa jambo la maana kwa Waisraeli. Mitaa ya watu wa Israeli ilikuwa ya watu wenye kujua kusoma na kuandika. Zaidi ya kusoma, watoto wako wataongea na wengine habari za Neno la Mungu. Je! wao wanatumia kanuni zinazofaa za sarufi (usahihi wa mitungo ya maneno na ufasaha)? Je! wewe umesahihisha matamko mabaya ya maneno ambayo umekuwa ukiyafanya muda wa miaka mingi kusudi watoto wako wakusikie ukiyatamka kama ifaavyo? Sulemani alichagua kwa uangalifu maneno ya kumsifia Mungu. Kwa hiyo, tunasoma hivi: “Huyo Mhubiri [mkusanyaji, NW] akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.”​—Mhubiri 12:10.

14. Tunaweza kusaidiaje watoto wetu wajifunze kufanya maamuzi yanayofaa?

14 Ni wazi kwamba tunataka watoto wetu wawe watu wazima waliokomaa na waweze kufanya maamuzi yanayofaa yenye kupatana na Neno la Mungu. Basi ingekuwa vema kuanza mapema kuwafundisha kanuni zinazofaa​—si amri-amri tu wanazopaswa kuzitii bali pia sababu za kuzitii amri hizo. Hapo ndipo watoto wataweza kujifunza namna ya kujifanyia wenyewe maamuzi yanayofaa.

15. Watoto wetu wanatuhitaji tuwaunge mkono kwa njia gani ya maana? (b) Tunahitajiwa tujihadhari na nini?

15 Watoto wetu wanaelekeana na ulimwengu wenye mambo ya upotoe. Ni jambo la maana watuone sisi tukiwa na imara ya kutenda mema na kushikilia sana yanayofaa. Tena wanapaswa kujulishwa kwamba, kama wametenda yanayofaa, sisi tutawaunga mkono, kama vile Sara alivyomkinga Isaka asiumizwe na Ishmaeli (Mwanzo 21:9, 10) Inatupasa pia tukumbuke kwamba tunapotazamia kuona mambo yenye kufaa yakitendwa, mambo yanaelekea zaidi kuwa hivyo. “Unajua kwa nini sisi hatukusumbui-sumbui?” Shahidi kijana alimwuliza baba yake. “Ni kwa sababu wewe hujaribu kututega utukute tukiwa na makosa​—wewe unatazamia tutende mambo yanayofaa, basi sisi hatutaki kufanya jambo lo lote lililo kinyume.” Wazazi wanalaumu watoto wao mara nyingi kwa kusema wamefanya jambo fulani na kumbe sivyo! Wewe ukilaumu watoto wako juu ya kusema uongo halafu iwe si kweli, huenda wao wakafikiri unawatazamia waseme uongo, na huenda wakausema safari ile nyingine.

16. (a) Ni maoni gani yenye mafaa yametolewa juu ya mikutano ya Kikristo? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba mikutano hiyo ina faida kubwa kwa watoto? (c) Je! wewe unajua mifano inayoonyesha ubora wa mikutano hiyo kwa watoto?

16 Watu wengi wameliona kuwa jambo la hekima kupeleka watoto wao kwenye mikutano ambako Neno la Mungu linazungumzwa, tangu wanapokuwa na umri ndogo zaidi​—si kuketi chumba hiki watoto wakiwa katika chumba kingine, wala si kuwatembeza huko nyuma-nyuma katika jumba la mikutano (isipokuwa kwa dakika chache kunapokuwa na sababu nzuri) bali kuwafundisha kuketi kwa utulivu, na kuiheshimu mikutano hata kufaidika na mambo mema yanayozungumzwa. Leo, watu wazima ambao ni wenye nguvu nyingi katika ile imani wanakumbuka juhudi waliyokuwa nayo wazazi wao kwa kuwapeleka sehemu nyingi za mbali kwa ukawaida wakahudhurie mikutano ya namna hiyo, labda kwa kupanda matatu au motokaa iliyokuwa kazi-kwisha. Mzee mmoja wa kundi anakumbuka unabii mbalimbali uliokuwa mgumu kufahamika aliousikia ukizungumzwa na wazazi wake wakati wa kutayarisha funzo la Mnara wa Mlinzi siku za kule nyuma, alipokuwa kitoto chenye kucheza huku na huku kwenye sakafu ya nyumba. Wao hawakujua alikuwa akiwasikiliza​—achia mbali jambo la kwamba angekuja kuyakumbuka maelezo yenyewe zaidi ya nusu-karne baadaye!

17. Ni mifano gani ya Kibiblia unayoweza kutaja ya watoto wenye kuhudhuria mikutano, na ni maulizo gani tunayoweza kujiuliza juu ya mifano hiyo?

17 Siku za Ezra watu wote wenye akili za kuwawezesha kusikiliza walisimama kuanzia mapambazuko mpaka adhuhuri wayasikie Maandiko yakisomwa. (Nehemia 8:2, 3) Kama wewe ungalikuwa hai wakati huo, je! watoto wako wangalikuwako, au ungalikuwa na maoni ya kwamba habari zenye kusemwa zilikuwa ngumu mno, na usomaji wenyewe ulichukua muda mrefu mno wasistahili kuwako, kisha uwaambie waende zao wakacheze? Yusufu na Mariamu walikuwa na ‘desturi ya kwenda Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya’ kupitwa. Ndiyo sababu walikuwa huko Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12. (Luka 2:41-49) Je! kama ingalikuwa ni wewe, je! ungalikwenda umbali huo, kwa miguu au kwa kupanda punda-kihongwe, ukalihudhurie kusanyiko hilo? Wakati makundi mbalimbali yenye watu wengi, kutia na “watoto,” walipokuja kuyasikia maneno ya Yesu, kisha kukawa hakuna chakula cho chote, Yesu aliwalisha kimwujiza. (Mathayo 14:21; 15:38) Kama wewe ungalikuwako wakati huo, je! watoto wako wangalikuwako, au wewe ungalibaki nyumbani uwalishe chakula kingine ambacho kwa maoni yako walikihitaji sana?

18. Ni kwa njia gani zaidi tunaweza kuonyesha tunathamini mikutano ya Kikristo?

18 Je! watoto wako wanajua kwamba wewe unaichukua mikutano ya kujifunza Biblia kuwa ya maana sana? Je! wanaona kwamba wewe unaiona kuwa yenye ubora wa kukufanya ushiriki katika hiyo kwa kutoa maelezo yanapotakwa, badala ya kuhudhuria na kujinyamazia? Kwa mfano, je! wewe unakuwa umelitayarisha somo lenyewe pamoja na watoto wako, na je! wewe pamoja na watoto wako mtatoa angalau elezo moja kwenye mkutano unaohusika?

MRADI ULIO JUU

19. Inatupasa tuwe na maoni gani ya kutazamia mema katika kuwalea watoto wetu wapendwa?

19 Je! kuna mtu ye yote anayeyafanya yote hayo kikamilifu? Ni wazi hakuna! Mambo yaliyozungumzwa hapa ni mambo yanayopasa kutiliwa jitihada yaweze kutimizwa, wala si miradi iliyokwisha kufikiwa ikatimizwa. Nyakati zote kutakuwa na matatizo katika ulimwengu huu, lakini Biblia inatutolea njia za kushughulika nayo, nasi tukijaribu kufanya mambo kwa njia ya Mungu, yeye atatusaidia. Wakati alipoulizwa kwa nini watoto wake walionekana kuwa wenye nguvu katika imani, baba mmoja Mkristo alisema hivi: “Kwa hakika mimi sijui sababu. Sisi hatukufanya jambo lo lote la ajabu lisilofanywa na wengine. Tumejaribu tu kufuata mashauri tuliyopata katika Biblia na katika tengenezo.”

20. (a) Ni mambo gani kati ya mengine mengi unayoweza kufanya ulee watoto wenye furaha leo? (b) Andiko la kichwa cha habari yetu hapo mwanzoni mwa somo hili, na andiko la Mithali 20:7 pia, linatutiaje moyo katika jambo hili?

20 Unapolichunguza jambo hilo juu-chini, utaona hiyo ndiyo njia ya kulea watoto wenye furaha leo. Wawekee mfano unaofaa. Wafundishe watoto kufuata mfano huo. Wanapofanya mema furahi, kisha ujaribu kuwasaidia warekebishe yale mengine. Wanapopatwa na mambo yenye kuwafurahisha maishani, nawe furahi pamoja nao. Waonyeshe upendo. Fanya mambo kwa njia ya Mungu, naye atazibariki jitihada zako. Yakumbuke maneno haya Sulemani yaliyoongozwa na Mungu, yanayoleta faraja: “Mwenye haki aendaye katika unyofu wake, watoto wake wabarikiwa baada yake’’​—Mithali 20:7.

[Maelezo ya Chini]

a Katika nyakati za Biblia, sawa na leo, watu wengine waliweza kusoma na wengine hawakuweza, lakini huenda ikawa kwamba watu wa sehemu nyingi sana waliweza kusoma, wala si kama vile watu wengi wamekuwa wakidhani kwamba wengi hawakujua kusoma siku hizo. (Linganisha Isaya 29:11, 12.) Kwa kweli, kitabu The Encyclopedia of the Jewish Religion kinasema hivi: “Inaonekana hali ya kujua kusoma na kuandika ilienea kote katika Israeli wa kale.”

Amri za Mungu zilipasa kuandikwa kwenye mihimili ya mlango na kufungwa mikononi​—na ingalikuwa kazi isiyo na maana kufanya hivyo kwa watu ambao hawakuweza kusoma. (Kumbukumbu la Torati 6:8, 9; 27:8) Mfalme alipaswa kuandika nakala yake mwenyewe ya sheria na kuisoma kila siku. (Kumbukumbu la Torati 17:15, 18, 19) Mwanamume mmoja kijana wa Sukothi aliyaandika majina ya wanaume wenye kuongoza watu katika mji wa kwao.​—Waamuzi 8:14.

Wenye kisomo sio peke yao waliojua kusoma na kuandika. Katika maelezo yake juu ya kitabu cha Waamuzi, James D. Martin aliandika akasema kwamba “mengine ya maandishi yenye ushuhuda ulio wa zamani zaidi yanayoonyesha watu walitumia mwandiko wa alfabeti (a, b, c, na kadhalika) yamekwaruzwa kwenye kuta za mapango na watumwa waliokuwa katika mashimo ya madini ya Sinai.” Amosi alikuwa mfuga kondoo wa hali ya chini. Mika alikuwa nabii wa mashambani wa kijiji cha Moreshethi. (Amosi 1:1; Mika 1:1) Hata hivyo wote wawili waliandika vitabu vya Biblia.

Kitabu kisichohesabiwa kuwa kati ya vitabu vinavyokubalika vya Maandiko Matakatifu, Wamakabayo cha Kwanza, ambacho kinaelekea kuwa kiliandikwa karibu na sehemu ya mwisho wa karne ya pili K.W.K., kinaonyesha kwamba watu walikuwa na nakala za ile Torati katika nyumba zao. (1 Wamakabayo 1:55-57) Yosefo mwanahistoria Myahudi aliyataja maoni yake ya karne ya kwanza kwamba ile Torati inaagiza kwamba watoto “watapaswa kufundishwa kusoma, na watajifunza sheria za babu zao hata matendo yao.”​—Kitabu Against Apion, II uku. 375 (25).

NINYI WAZAZI NA WATOTO, MNGEYAJIBUJE MAULIZO HAYA?

◻ Inawapasa wazazi watafute wapi maoni yatakayowasaidia kulea watoto, na kwa sababu gani?

◻ Ni nini mingine ya mifano ya Biblia juu ya kulea watoto ifaavyo?

◻ Ni kwa njia gani zenye mafaa wazazi wanaweza kulinda mashirika ya watoto wao?

◻ Matumizi ya kanuni za Biblia yanaweza kushindaje matatizo katika jamaa ziIizogawanyika?

◻ Ni hatua gani ambazo inawapasa wazazi wachukue kwa kutazamia watoto wao wawe na elimu (kisomo) inayofaa?

◻ Je! wazazi na watoto wanaweza kutazamia kufanya mambo yote kikamilifu? Hata hivyo wanaweza kufanikiwa kwa njia gani?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kivulana mmoja alimwuliza mama yake ulizo hili: “Hakika ni kazi ngumu sana kulea mtoto​—wewe unaona ingalikuwa afadhali kama hungalinizaa?” Baada ya miaka mingi kupita yeye anasisimuliwa na shauku yenye upendo kwa kulikumbuka jibu hili la mama yake. “Kitu cho chote chenye faida kinachukua wakati wa mtu na kumtoa jasho.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ni mara ngapi ninyi wazazi mnapoweka mfano mwema wa kushiriki kutoa maelezo kwenye mikutano ambako Neno la Mungu linazungumzwa, badala ya kuhudhuria na kujinyamazia?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki