Watoto Wenye Furaha Katika Ulimwengu Wenye Upotoe
Makala hii iliandikwa kwa ajili ya watoto (vijana) hasa. Kwa hiyo tunawaomba watoto (na vijana) wachukue uongozi wa kutoa maelezo wakati makala hii inapozungumzwa kwenye Jumba la Ufalme.
“Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.”—Mhubiri 12:1.
1. Kwa sababu gani watu wengi wanafikiri huu si wakati mzuri wa kuwa kijana?
WAKATI wa kuwa kijana ni wakati mzuri ajabu! Je! maneno hayo yanakushangaza? Vijana wengi wakisikia hivyo wataanza kutaja hali mbaya wanazoziona—uhalifu unaotendwa kwenye barabara nyingi, uasherati, matumizi mabaya ya dawa za kulevya, mimba ambazo wasichana matineja wanatungwa, utoaji wa mimba na magonjwa ya kisonono na kaswende. Huenda wakaitaja hatari inayoweza kuwapo kukitokea vita ya kutumia makombora ya atomu au ule uchafuaji wa hewa, maji na nchi unaoiharibu dunia. Huenda vijana hawa wakauliza ni jambo gani linalofanya huu usemwe ni wakati mzuri wa kuwa na ujana, kuelekeana na wakati ujao.
2. (a) Kwa sababu gani huu ni wakati mzuri sana wa kuwa hai? (b) Jambo hili linapasa liwe na tokeo gani juu yako?
2 Vijana (watoto) wengine wanajua kwamba unabii mbalimbali wa Biblia unasema kwamba Mungu hatawaruhusu wanadamu waiharibu dunia. Biblia inaahidi kwamba Mungu atabadili mambo—kwamba atajiingiza katika mambo alete hali zenye haki ya adili na amani. (Zaburi 37:10, 11; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-4; 11:18) Je! wewe unaziamini ahadi hizo? Ikiwa ndivyo, zinapasa ziongoze sana maisha yako, kwa maana zinaweza kufanya uwe na hali za kupendeza sana wakati ujao.
3. Kwa nini hakuna mtu aliye mtoto mno asiweze kuhangaikia kutumikia Mungu?
3 Labda wewe unawaza hivi: ‘Ah, mimi ni mtoto mno nisiweze kuhusika katika mambo hayo! ’ Lakini je! wewe ni mtoto mno? Biblia inahimiza vijana—wavulana na wasichana—watumikie Mungu. (Zaburi 148:12, 13) Inaeleza habari za kisichana Kiebrania kilichofanya afisa wa kijeshi Mshami, Naamani, awe mmoja wa watumishi wa Yehova. (2 Wafalme 5:2, 3, 15-17) Inasema kwamba watoto walimfanyia Yesu vigelegele, na kwamba wakati viongozi wa kidini walipoudhiwa na jambo hilo, Yesu aliwauliza hivi: “Je! hata siku moja ninyi hamkuyasoma Maandiko? Kwa maana yanasema, ‘Hata vitoto vidogo vitasifu yeye!’” (Mathayo 21:15, 16, The Living Bible) Yesu alipendezwa kibinafsi na watoto. Alisema waachwe wamjie. Na makundi ya Mashahidi wa Yehova kote kote duniani wanapendezwa sana na vijana leo—pia na mambo mema wanayofanya kutumikia Mungu.—Mathayo 19:14.
KANUNI ZINAZOLETA MAISHA YENYE FURAHA
4. Biblia inaweza kukusaidiaje wewe uishi maisha yenye furaha zaidi?
4 Wewe unajua kwamba wazazi wako wanataka uwe mwenye furaha. Ndivyo na Baba yako wa kimbinguni, Yehova Mungu. Neno lake, Biblia, linatoa maoni yenye mafaa yanayoweza kukuepusha na matata mengi. Halikuambii vijambo vyote vyote unavyopaswa kuvifanya, bali mara nyingi linataja tu kanuni za uongozi. Kanuni hizo ni kweli zinazokupa msingi wa kuamulia mambo, ili uamuzi wako mzuri ukuonyeshe ni jambo gani linalofaa kufanywa. Kwa mfano, inayofuata ni kanuni moja iliyotajwa katika makala iliyotangulia, na labda umeisikia ikizungumzwa mara nyingi: “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.”—1 Wakorintho 15:33, NW.
5. (a) Ni nini nyingine za njia ambazo “mashirika mabaya” yanaweza kuharibu “mazoea mazuri”? (b) Maandiko yaliyoonyeshwa katika fungu hili yanaonyesha nini juu ya (1) usemi mbaya, (2) kueleza visa vyenye sifa mbaya, (3) uasherati?
5 Hiyo maana yake nini? Maana yake ni kwamba tunaletewa uvutano fulani na watu wanaotuzunguka. Ukitumia wakati mwingi kwa kukaa na watu wenye kutumia usemi mchafu-mchafu au wanaoeleza visa (matukio) vyenye sifa mbaya, labda nawe utafuata mfano wao. Ukishirikiana na watu wenye maoni yanayotofautiana na matakwa ya Mungu juu ya ngono na ndoa, utakuja kufikia hatua ambayo hutakuwa ukiona ubaya wo wote katika mambo hayo. Unaweza kuingia katika ushirika wa namna hiyo bila kujua umekwisha kuingia. Unaposoma vitabu au kutazama sinema au televisheni, unaingiza mawazo ya mwandikaji au mtungaji wa vitu hivyo katika akili yako mwenyewe. Ikiwa mawazo hayo ni mabaya, yanaweza kuchafua akili yako. Biblia haisemi ufurahie mambo hayo, bali uyaepuke. (Waefeso 5:3, 4; linganisha 1 Wakorintho 6:18.) Vilevile inasema hivi: “Au, je, hamjui kwamba watu wabaya hawataurithi Utawala wa Mungu? Msijidanganye! Watu wanaoishi maisha ya uasherati, wanaoabudu sanamu, wafiraji au walawiti, wanyang’anyi, wachoyo, walevi, wenye kusengenya, walaghai, hao wote hawatashiriki Utawala wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10, Habari Njema kwa Watu Wote.
6. (a) Watu wamepatwa na matatizo gani kwa sababu wamekosa kujali shauri la Biblia linalohusu ushirika mbaya? (b) Inatupasa tukumbuke nini juu ya akili zetu, na tunaweza kupata wapi ushirika mwema?
6 Ni kweli kwamba tunaletewa uvutano fulani na watu wanaotuzunguka. Ni kama vile The Living Bible inavyolitaja andiko la 1 Wakorintho 15:33: “Ikiwa wewe wasikiliza wao wewe utaanza kuwa unatenda kama wao.” Vijana wameshawishwa wakaingilia uvutaji wa sigara, matumizi mabaya ya dawa za kulevya, kuiba na namna zote za ufisadi kwa sababu washirika wao waliyafanya mambo hayo au wakawafanyia mzaha kwa sababu ya kutokuyafanya. Je! wewe unadhani watu wanaokufanyia mzaha kwa sababu unatenda mambo yanayofaa ni rafiki wazuri? Inafaa ukumbuke kwamba akili yako ni kama kompyuta. Ukiingiza habari zisizofaa ndani yayo, itakutolea maamuzi yasiyofaa. Kwa hiyo lingekuwa jambo la hekima ushirikiane na watu wenye kutenda mambo ya kimungu—ushirikiane na wale wanaokuja kwenye Jumba la Ufalme na wanaofuata mambo wanayojifunza huko.—Mithali 18: 24.
7. (a) Je! kwa sababu watu wanakuja kwenye mikutano ya Kikristo, hiyo tu inaonyesha kwamba kila mmoja anafuata kanuni za kimungu? (b) Ni mfano gani katika siku za Samweli unaoonyesha hilo si jambo geni? (c) Samweli alifanya nini, na matokeo yakawa nini?
7 Lakini ufanye nini ikiwa mtu anayepaswa kuweka mfano mwema hafanyi hivyo? Jambo hilo lilitukia zaidi ya mara moja nyakati za Biblia. Samweli kijana alikuwa na pendeleo kubwa ajabu la kutumikia mahali pa ibada ya Yehova, lakini wale wana wa kuhani mkuu Eli waliweka mfano mbaya sana. Wao walikuwa walaghai (wakora) wabaya sana waliovunja sheria ya Yehova hata wakafanya ngono za haramu na wanawake waliotumikia mahali alipoabudiwa Yehova. Lakini Samweli kijana aliyajua mambo yaliyofaa kufanywa. Yeye hakufuata mfano wao mbaya. Biblia inasema: “Na yule mtoto, Samweli, akazidi kukua akapata kibali kwa [Yehova], na kwa watu pia.” (1 Samweli 2:12-17, 22-26) Samweli alibarikiwa sana na Mungu. Alikuwa mkubwa akawa nabii, kisha akatumiwa kuviandika vile vitabu vya Biblia vya Waamuzi na Ruthu na sehemu fulani ya kitabu cha kwanza cha Samweli, chenye kuitwa kwa jina lake. Yeye ni mfano mmoja unaoonyesha ukweli wa maneno yaliyosemwa katika Mithali 20:11: “Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili.” Ni wazi kwamba ukiona mtu fulani akitenda ubaya, utataka kuwa kama Samweli kijana wala si kama wana wa Eli, walioijua njia ya Yehova wasiifuate.
DHAMIRI YAKO YA KIKRISTO
8. Huenda dhamiri ya Mkristo kijana iliyozoezwa na Biblia ikamzuia asifanye nini?
8 Wewe Mkristo kijana unajua kwamba kuna mambo fulani ambayo dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia haitakuruhusu uyafanye. Kwa mfano, unajua kwamba sikukuu nyingi zina asili (chanzo) ya kipagani. Zimetokana na desturi za dini ya uongo. Kwa hiyo dhamiri yako haitakuruhusu uzisherehekee. Unajua pia kwamba mara nyingi shule zinakuwa na vipindi vya kutukuza taifa au sherehe zinazosifu taifa lazo kwa kulishindanisha na mataifa yale mengine, na basi hazipatani na maoni yako yanayotegemea Biblia, ya kwamba “[Mungu] alifanya kila taifa la wanadamu.” (Matendo 17:26) Pia, unajua kwamba mara nyingi shule zinakazia mno michezo ya kushindana, zikihimiza wanafunzi watumie wakati mwingi sana katika michezo hiyo—si kwa kujipatia tafrija tu bali kwa uchochezi mwingi wa kujipatia ushindi hivi kwamba huenda nyakati nyingine kukatokea matendo ya jeuri.a
9, 10. Wakristo wengine vijana wameshughulikaje na matatizo ya namna hiyo?
9 Je! kufuata kanuni (viwango) bora kunatokezea matatizo? Shahidi mmoja kijana alieleza hivi: “Sisi hatupatwi na matatizo mengi juu ya dhamiri zetu za Kikristo maadamu mwalimu amejulishwa msimamo wetu mapema—kabla tatizo lenyewe halijatokea.” Vijana wanaotumia utulivu na heshima kueleza sababu yao ya kuwa na maoni fulani yanayoitegemea dhamiri yao ya Kikristo—na kufanya hivyo kabla ya mwalimu kuja darasani na kabla jambo linalozungumzwa halijafikia hatua ya kuchacha—hawawi na matatizo mengi sana upande huu.
10 Kijana mmoja aliyekuwa mpenda-muziki na kutaka kuimba akiwa katika kikundi cha shule cha wanamuziki alisema hivi: “Mimi nilimweleza mwalimu wakati wa kuanza shule kwamba ningependa kuwa katika kikundi cha wanamuziki, lakini kwamba kuna muziki wa namna fulani ambao nisingekubali kuimba, na nikamweleza sababu.” Wakati muziki wa namna hiyo unapotokea, mwalimu anajua mapema kwamba mwanafunzi huyo ataketi kimya bila kuimba. Kwa kweli, nyakati fulani-fulani waalimu wamepanga upya kipindi kizima ili kifaane na dhamiri ya Kikristo ya kijana wa namna hiyo. Bila shaka, kama vile watoto wanavyoeleza, ni jambo lenye msaada kwako ikiwa sifa yako shuleni ni nzuri katika mambo mengine yote—ikiwa waalimu wanajua kwamba wewe ni mtu anayeishi kweli kweli kulingana na kanuni za dini yake na kwamba unatia bidii katika masomo wanayoongoza.
MIRADI (MALENGO) INAYOFAA
11. (a) Miradi inaweza kuwafaaje vijana? (b) Kuna miradi gani kati ya ile yenye kufaa?
11 Wewe una mipango gani ya wakati ujao? Je! unajua kwamba watu wengi hawana mpango wo wote? Hawana miradi, na basi wanafanikiwa katika mambo machache. Wanafuatana na jambo lo lote litokealo lakini mafanikio si mengi. Mradi mmoja unaoweza kufanya ni kujaribu kuinua ubora wa masomo yako kwa kadiri fulani. Mwingine unaweza kuwa ni kujifunza kazi fulani ya kukusaidia upate riziki.
12. Ni miradi gani mingine iliyo ya maana zaidi?
12 Lakini Biblia inaonyesha tunahitaji miradi ya kiroho pia—hayo yakiwa ni mambo tunayopaswa kuyachuchumilia (kujinyosha tuyapate) katika utumishi wa Mungu. Inasema mtu ‘anayefuatia haki ya adili’ atapendwa na Yehova na kwamba ‘atapata uzima, haki ya adili na utukufu.’ (Mithali 15:9, NW; 21:21, NW) Yesu alisema: “Tangu zile siku za Yohana Mbatizaji . . . ufalme wa mbingu ndio mradi ambao kuelekea huo wanadamu wanajisogeza mbele kwa nguvu wakaupate.” Paulo alisema: “Nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. . . . Nakaza mwendo, niifikilie mede [mradi, NW].” (Mathayo 11:12, NW; Wafilipi 3:12-14) Hivyo, ni vizuri kuwa na miradi inayofaa.
13. Maarifa yaliyo sahihi yana ubora gani?
13 Wewe uliye kijana leo, je! unakaza mwendo ukajipatie maarifa (ujuzi)? Vijana wengi hawafanyi hivyo. Hata hivyo, kujua habari za Yehova ni jambo la maana sana. Katika sala aliyompelekea Baba yake, Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Kuna sababu gani nyingine ya kutafuta maarifa (ujuzi) inayoshinda hiyo kwa ubora?
14. Ni maendeleo gani ya hatua kwa hatua yanayoweza kukusaidia umjue Yehova na kulifahamu Neno lake?
14 Je! wewe unaliona Neno la Mungu na vitabu vya Sosaiti vinavyolieleza Neno hilo kuwa vyenye kupendeza, au unafikiri ni vigumu kufahamika? Ikiwa unaviona kuwa vigumu kufahamika, Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kitakusaidia uijue historia yote ya Biblia katika mfuatano unaofaa wa matukio. Kitakusaidia uweze kuhusianisha mambo (kuyaunganisha) na kuyashika kwa wepesi zaidi. Halafu tena, kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako kitakusaidia ufahamu kanuni za Biblia zitakazoongezea maisha yako furaha. Kadiri unavyozidi kujifunza mambo mengi, ndivyo kujifunza kutakavyozidi kuwa jambo jepesi, nawe utataka kutayarisha habari zenye kina kirefu, kutia na somo la Mnara wa Mlinzi, habari za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na usomaji wa Biblia wa kila juma. Huwezi kufanya yote hayo kwa siku moja, lakini unaweza kukuza ukomavu wa kiroho ukijiwekea miradi na kusogea mbele hatua kwa hatua ukajipatie maarifa na uwezo wa kufanya mambo.—Mithali 1:5; 2:10-12.
15. Ni miradi mingine gani unayoweza kujiwekea?
15 Je! wewe unakaza mwendo ukajipatie mapendeleo ya utumishi wa Kikristo? Je! una mradi wa kibinafsi wa kutumia kiasi fulani cha wakati katika kazi ya kufundisha watu nyumba kwa nyumba kila juma au kila mwezi? Je! wewe unawatia moyo vijana wengine waende pamoja nawe? Je! una mradi wa kuwa na ujuzi mwingi zaidi wa kufundisha watu wakati wa ziara za kurudia na mafunzo ya nyumbani ya Biblia? Vijana wengine wanakuwa na mradi wa kila mwaka wa kuwa painia (mhubiri wa wakati wote anayejitolea kazi hiyo kwa kupenda kwake) wakati wa malikizo ya shule.
16. Ni miradi gani inayopasa kufikiriwa itimizwe baadaye sana?
16 Namna gani miradi yenye kuchukua muda mrefu? Je! wewe unataka kutimiza nini wakati kama huu wa sasa ufikapo mwaka ujao? Au katika miaka mitano inayokuja, ikiwa mwisho wa hii taratibu ya kale hautakuwa umekuja? Je! una mradi utakaoufikia baada ya muda mrefu wa kuwa mhudumu painia wa kawaida au wa kufurahia mapendeleo mengine, kama vile kuwa mshiriki wa jamaa ya Betheli inayotolea watu vitabu vya kuwasaidia kujifunza Biblia katika sehemu yenu ya ulimwengu? Kujiwekea miradi na kujitahidi ukaitimize ni njia moja ya kuelekeza maisha yako kwa njia yenye mafaa zaidi.
17. (a) Unaweza kupata wapi mifano ya watu waliokuza maarifa na ujuzi wa namna hiyo katika wakati wao wa ujana? (b) Je! wewe unawajua watu fulani waliofanya hivyo?
17 Wafikirie wazee wenye upendo katika kundi lako na waangalizi wenu wa mizunguko na wilaya. Wakati mmoja wao walikuwa vijana kama wewe. Lakini miaka mingi iliyopita walichuchumilia (walijinyosha wapate) maarifa na ujuzi, wakatumikia Mungu na ndugu zao. Je! mfano wao unakutia wewe moyo utumie vizuri wakati ulio nao katika ujana wako? Ikiwa ndivyo, wewe unaweza kuwa sawa na mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu; nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata leo.”—Zaburi 71:17.
MFIKIRIE TIMOTHEO
18. Timotheo alikuwaje mfano mzuri ajabu wa habari ambayo tumekuwa tukiizungumza?
18 Timotheo aliweka mfano mzuri ajabu katika jambo hilo. Paulo alimwambia hivi: “Tangu utoto mchanga wewe umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yanaweza kufanya wewe uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia ile imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (2 Timotheo 3:15 NW) Timotheo alikuwa ameijua ile kweli akiwa mtoto, naye alijua ilikuwa kitu chenye ubora mwingi. Imani na maarifa yake yaliongezeka. Jambo hilo lilionekana wazi na watu, kwa maana Maandiko yanasema “alishuhudiwa vema” na kina ndugu. Akapewa pendeleo zuri ajabu la kuwa mfanya kazi mwaminifu mwenye kusafiri pamoja na mtume Paulo wakati mtume huyo alipokuwa akianzisha makundi katika ulimwengu wa watu wasio Wayahudi.—Matendo 16:2-5.
19. Timotheo angezuiaje watu wasiudharau ujana wake!
19 Wewe unaweza kuwa kama Timotheo. Ishike ile kweli kwa imara. Utumie wakati wa ziada ulio nao sasa, wakati huu ambao bado hujawa na yale madaraka yenye kumaliza wakati ya kuwa na jamaa na migawo mikubwa-mikubwa kundini. Jifunze, ukuze maarifa na ujuzi wako. Vijana walio wengi wanakumbuka kwamba Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Usikubali mtu ye yote akudharau kwa sababu wewe ni kijana.” Lakini ni jambo la maana kumbuka ni kwa njia gani Timotheo hakupaswa kuacha adharauliwe. Paulo alisema: “Uwe mfano kwa wanaoamini: katika usemi wako, mwenendo wako, upendo, imani na maisha safi.” (1 Timotheo 4:12, Habari Njema kwa Watu Wote) Pia, alimwambia Timotheo hivi: “Zikimbie tamaa za ujanani; ukafuate haki, na imani, na upendo, na amani, pamoja na wale wamwitao Bwana kwa moyo safi.” (2 Timotheo 2:22) Ukiyafuatia mambo hayo kweli kweli, utaona kwamba kwa uhakika ni jambo zuri ajabu kuwa hai wakati huu!
20. Maoni yako mwenyewe ni nini, unapouona ulimwengu huu wa kale ukielekeana na mwisho wake?
20 Ulimwengu wa kale unaelekeana na mwisho wenye msiba mkubwa, lakini wewe ukiifuata mifano ya Samweli, Timotheo na watumishi wengine waaminifu wa Mungu, unaweza kutazamia mambo yaliyo mazuri zaidi. Utafute upendeleo wa Mungu. Jitahidi kuuokoka mwisho wa hii taratibu ya kale ukaishi moja kwa moja mpaka ndani ya hali zenye haki ya adili zinazokaribia. Ndiyo, litii shauri la Paulo linalosema “fikiri kwa makini juu ya hayo yote na kuyatekeleza kusudi maendeleo yako yaonekane na wote.”—1 Timotheo 4:15, Habari Njema kwa Watu Wote.—Kutoka The Watchtower, January 15, 1982.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate mazungumzo mazuri juu ya mambo haya, angalia kitabu Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele, kurasa 145-149; Kupata Faida Zote za Ujana Wako, sura ya 16.
VIJANA, MNAKUMBUKA MAMBO GANI JUU YA KUTAFUTA FURAHA YA KWELI?
◻ Kwa sababu gani sasa ni wakati mzuri kuwa kijana?
◻ Ni watoto gani walio kati ya wale waliotumikia Mungu nyakati za Biblia?
◻ Kwa sababu gani inatupasa tuepuke mashirika mabaya?
◻ Wewe unaweza kuepukaje matatizo shuleni?
◻ Kwa sababu gani inakupasa uione miradi kuwa ya maana?
◻ Ni miradi gani inayofaa unayoweza kujiwekea sasa?
◻ Ni miradi gani unayoweza kufuatia ukaitimize baadaye sana?
◻ Ni mradi gani mkubwa unaoweza kujitahidi uufikie, na kwa njia gani?