Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 8/1 kur. 10-14
  • Vijana Wenye Furaha Katika Utumishi wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vijana Wenye Furaha Katika Utumishi wa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Imani Yako Mwenyewe
  • Pata Maarifa
  • Kua Katika Uthamini
  • Songa Mbele Katika Kumtumikia Mungu
  • Watoto Wenye Furaha Katika Ulimwengu Wenye Upotoe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Kufanye Kumtumikia Mungu Milele Kuwe Lengo Lako
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Kuwalea Watoto Wako Wampende Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vijana—Imarisheni Tamaa Yenu ya Kumtumikia Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 8/1 kur. 10-14

Vijana Wenye Furaha Katika Utumishi wa Yehova

“Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili.”—MITHALI 20:11.

KIJANA SAMWELI mchanga huenda akawa alikuwa na umri wa miaka mitatu hadi mitano tu alipoanza ‘kuhudumu’ kwenye tabenakulo ya Yehova katika Shilo. Moja ya kazi zake ilikuwa kufungua “milango ya nyumba ya BWANA [Yehova, NW].” Biblia husema kwamba “Samweli akazidi kukua akapata kibali kwa BWANA [Yehova, NW], na kwa watu pia.” Alipokua, alirudisha Israeli kwenye ibada ya kweli. Alitumikia Mungu “siku zote za maisha yake.” Hata alipokuwa “ni mzee, mwenye mvi” alikuwa angali akiwahimiza watu ‘wamche Yehova, wakamtumikie kwa kweli.’ Je! halingekuwa jambo zuri ajabu kama watu wangeweza kusema mambo haya mazuri juu yako kama vile Biblia iyasemavyo juu ya Samweli?—1 Samweli 1:24; 2:18, 26; 3:15; 7:2-4, 15; 12:2, 24.

2 Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova au wewe huhudhuria mikutano yao ya Kikristo, tazama huku na huku katika Jumba la Ufalme ambamo mwajifunza somo hili. Waona watu wa umri wote. Labda mna watu ambao tayari ni ‘wazee na wenye mvi.’ Pia mna wazazi, vijana, watoto wadogo, na hata vitoto vichanga vya kushikwa. Je! tayari walio wadogo kabisa wanajifunza? Ndiyo. Wewe waulize tu wale ambao wao wenyewe waliletwa kwenye mikutano ya jinsi hiyo wakiwa wadogo. Watakuambia kikweli kwamba kuanzia miaka yao ya mapema, walikuwa wakijifunza kustahi Mungu, kupenda watu wake, na kuthamini mahali-mahali ambapo yeye huabudiwa. Wakati upitapo, wadogo-wadogo hujifunza kweli zilizo nzuri ajabu. Baada ya kukua katika maarifa na uthamini, vijana wengi huwa sehemu ya ‘wanaume vijana na mabikira, wanaume wazee na wavulana’ ambao mtunga zaburi alihimiza ‘wasifu jina la Yehova, kwa maana jina lake pekee ndilo lililo juu kwa njia isiyofikika.”—Zaburi 148:12, 13, NW.

3 Ikiwa wewe ni kijana ambaye huletwa na wazazi kwa ukawaida kwenye mikutano ya jinsi hiyo, wewe ni mbarikiwa sana. Vijana wengine wengi hutaabishwa na matatizo ya ulimwengu. Huenda baadhi yao wakaogopa kwamba wanadamu wataiharibu dunia. Wewe wajua kwamba Mungu hataacha hilo litendeke, kwamba hataruhusu wanadamu waendelee kuiangamiza sayari hii yenye upendezi. Badala ya kuacha hilo litendeke, kulingana na Biblia Mungu ‘atawaangamiza wale wanaoangamiza dunia.’ Wewe wajua kuwa Biblia yaahidi kwamba wakati mwangavu katika ulimwengu mpya mwadilifu wa Mungu u karibu.—Ufunuo 11:18; Zaburi 37:29; 2 Petro 3:13, HNWW.

Imani Yako Mwenyewe

4 Hapo kwanza, huenda ikawa wazazi wako ndio waliokuwa wakifuatia njia ya ukweli wa Kikristo. Labda wewe ulikuja kwenye mikutano ya Kikristo kwa sababu wao walikuleta, na huenda ikawa ulishiriki katika utumishi wa kimungu kwa sababu wao walifanya hivyo. Hata hivyo, kadiri wakati upitavyo, kutumikia na kutii Mungu kwaweza kuwa shangwe yako mwenyewe. Mama ya kijana Samweli ndiye aliyemwanzishia mwendo katika njia ifaayo, lakini ikawa ni lazima Samweli binafsi aifuate. Twasoma hivi: “Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili.”—Mithali 20:11.

5 Maandiko hutuambia yale Mungu atakayo kwetu. Hutuonyesha wazi jinsi ya kumfurahisha, yakiandaa habari nyingi sana ziwezazo kutufaidi sana. Mtume Paulo alimwambia hivi msaidizi wake mchanga zaidi Timotheo: “Kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu, na linafaa kwa mafundisho, na kwa kuonya watu juu ya makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa mafundisho katika haki; ili mutu wa Mungu awe mukamilifu, ametengenezwa kabisa kwa kila tendo jema.”—2 Timotheo 3:16, 17, ZSB.

6 Pia Biblia hutuambia ‘tusikilize nidhamu na kuwa wenye hekima.’ Husema ‘tuhazini’ amri za Mungu, ‘tupaaze sauti kuomba uelewevu,’ na ‘kuendelea kutafuta’ ufahamu kama vile wewe ungetafuta hazina za thamani zilizofichika. Ukifuata ushauri huo, hapo ndipo “wewe utaelewa hofu ya Yehova, na wewe utapata maarifa yenyewe ya Mungu.” Pia twapata shauri hili: “Sasa, Enyi wana, nisikilizeni; ndiyo, wenye furaha ni wale ambao hushika njia zangu zenyewe. Sikiliza nidhamu na uwe mwenye hekima, na usionyeshe kutojali kokote. Mwenye furaha ni binadamu anayenisikiliza . . . Kwa maana anipataye mimi kwa uhakika atapata uhai, naye apata nia njema kutoka kwa Yehova.” Je! wewe waithamini Biblia kadiri hiyo na kutia jitihada ya aina hiyo katika kujifunza mambo isemayo?—Mithali 2:1-5; 8:32-35, NW.

Pata Maarifa

7 Vijana fulani wajua takwimu zote za mi-chezo, au wao waweza kukuambia kila jambo juu ya kikundi cha wanamuziki ambacho wao hufurahia zaidi. Wao huona ni rahisi kujifunza mambo haya na kuyakumbuka kwa sababu wapendezwa nayo. Lakini swali lililo la maana zaidi ni hili, Wao wajua nini juu ya Mungu? Ebu fikiria yale amefanya. Mungu alifanyiza ulimwengu wote mzima. Alitabiri yale ambayo wanadamu wangefanya na yale ambayo yangetukia kabla hakujawa na matukio. Si kwamba Biblia hutuambia tu juu ya Mungu bali pia hutufundisha jinsi twaweza kumpendeza. Hutuonyesha jinsi twaweza kuwa na maisha yenye furaha sasa na jinsi twaweza kupata uhai wa milele katika ulimwengu mpya wake wenye uadilifu. Je! umaana wa jambo hilo hauzidi kwa mbali kujua ni nani aliyeshinda mchezo fulani wa mpira au kujifunza majina ya wanamuziki ambao karibuni watu watawasahau?—Isaya 42:5, 9; 46:9, 10; Amosi 3:7.

8 Mfalme kijana Yosia alipokuwa na umri wa miaka 15, ‘alianza kumtafuta-tafuta Mungu wa Daudi baba yake wa zamani.’ Yesu alipokuwa na miaka 12, alipatikana ‘ameketi katikati ya walimu’ katika hekalu la Yehova, ‘akiwasikiliza na kuwauliza maswali.’a Hata uwe una umri gani, je! wewe kama Yosia na Yesu umesitawisha upendezi halisi katika kujifunza mambo ambayo Mungu amefanya na ambayo bado atafanya?—2 Nyakati 34:3; Luka 2:46.

9 Hata hivyo, huenda wewe ukasema: ‘Funzo ni kazi ngumu.’ Watu wengi, vijana kwa wazee, hawajasoma mambo ya kutosha kuweza kufanya usomaji uwe rahisi. Kadiri usomavyo zaidi, ndivyo kusoma kuzidivyo kuwa rahisi. Kadiri ujifunzavyo zaidi, ndivyo kujifunza huwa rahisi zaidi. Washikamanisha mawazo mapya na mambo ujuayo tayari, hiyo ikifanya iwe rahisi zaidi kuyaelewa na kuyakumbuka.

10 Ni nini kiwezacho kukusaidia ujifunze mengi zaidi juu ya Mungu? Labda wewe ungeweza kuwa wa kawaida zaidi katika kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Je! ungeweza kutayarisha mapema na ushiriki kikweli? Kwa kielelezo, je! ungepata kiwango cha maarifa ya kina kirefu zaidi kutokana na somo hili kwa kufungua Maandiko ambayo yameonyeshwa bila kunukuliwa? Je! umeandika neno moja au mawili pambizoni ili kukumbusha kila moja la maandiko haya laongezea nini kwenye fungu au kwenye somo? Je! wewe una zoea la kutia angalau moja la maandiko hayo katika elezo fulani lionyeshalo ufahamu wako wa mazungumzo ya Kimaandiko? Mzee mmoja wa kundi ambaye amehudhuria mikutano kwa ukawaida kwa miaka mingi asema hivi: “Mimi huona ikiwa vigumu kuweka akili yangu juu ya somo lolote ambalo sikutayarisha kikweli, lakini mimi huwa na ufurahio wa kabisa kabisa kufuatana na somo ambalo nimejifunza kikamili.”

11 Usikilizapo hotuba za Biblia, je! wewe huandika mambo mafupi kukusaidia uchanganue jinsi hotuba hiyo inasitawishwa na kuweka akili yako juu ya yale yanayosemwa? Je! wewe hulinganisha yale usikiayo na yale uyajuayo tayari ili uweze kuielewa hotuba kwa urahisi zaidi na kuikumbuka vizuri zaidi? Yesu alisali hivi: “Hii ndiyo maana ya uhai wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3, NW) Je! maarifa yaongozayo kwenye uhai siyo maarifa bora kabisa ambayo yawezekana wewe kuyapata? Angalia yale ambayo Biblia yasema juu ya jambo hilo: “Kwa kuwa BWANA [Yehova, NW] huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu. Maana hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa yatakupendeza nafsi yako; busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi.”—Mithali 2:6, 10, 11.

Kua Katika Uthamini

12 Je! kweli sisi twathamini yale ambayo Mungu ametufanyia? Yeye aliumba dunia yenye upendezi na akaitayarisha kwa ajili ya uhai. Aliumba wazazi wetu wa kwanza, hivyo akifanya iwezekane sisi kuzaliwa. Alipanga ili tupate tegemezo la familia zetu na la kundi lenye upendo. (Mwanzo 1:27, 28; Yohana 13:35; Waebrania 10:25) Alituma Mwana wake mwenyewe mzaliwa wa kwanza duniani atufundishe mengi zaidi juu Yake mwenyewe na kuandaa ukombozi ufanyao iwezekane kupata uhai wa milele. Je! kweli wewe wathamini zawadi hizo zilizo nzuri sana? Je! zakusukuma wewe kukubali mwaliko wake ujifunze mengi zaidi juu yake na kumtumikia?—Mathayo 20:28; Yohana 1:18; Warumi 5:21.

13 Muumba wa ulimwengu wote mzima apendezwa na watu. Alimwita Abrahamu “rafiki yangu,” na alisema hivi kwa Musa: “Ninakujua kwa jina lako.” (Isaya 41:8; Kutoka 33:12, ZSB) Kitabu cha Ufunuo chaonyesha kwamba Mungu ana kitabu cha ufananisho, au “hati-kunjo ya uhai,” yenye majina ya watumishi wake waaminifu “kuanzia kuwekwa msingi wa ulimwengu.” Je! jina lako pia litatiwa humo?—Ufunuo 3:5; 17:8, NW; 2 Timotheo 2:19.

14 Kanuni za Mungu hufanya kazi. Kufanya mambo kwa njia yake huondolea mbali matatizo mengi—ukosefu wa adili, uzoelevu wa dawa za kulevya, uzoelevu wa alkoholi (vileo), mimba zisizotakwa, magonjwa yaambukizwayo kingono, jeuri, uuaji, na orodha ndefu ya masumbufu mengine. Kufuata njia zake kutasaidia pia kupata rafiki za kweli na kuishi maisha yenye furaha zaidi. Je! haihalisi kufanya jambo hilo? (1 Wakorintho 6:9-11) Hata kijana ambaye tayari ana azimio la kufanya mambo kwa njia ya Mungu aweza kupata imara zaidi ya kufanya yafaayo. Biblia yasema hivi: “Kwa mtu mwaminifu-mshikamanifu [Yehova] atatenda kwa uaminifu-mshikamanifu.” Pia hutuhakikishia kwamba yeye ‘hataacha waaminifu-washikamanifu wake’ wala ‘kuachilia mbali watu wake.’—Zaburi 18:25; 37:28; 94:14; Isaya 40:29-31, NW.

Songa Mbele Katika Kumtumikia Mungu

15 Je! kitovu cha miradi yako kimo katika ulimwengu wa kale unaokufa au katika ule mpya ulio mwadilifu? Je! wewe husikiliza Mungu, au wewe husikiliza watu wenye hekima ya kilimwengu ambao hupinganisha Mungu? Je! tafrija, elimu ya juu zaidi, au kazi-maisha yenye kula wakati ndiyo hutangulizwa mbele ya Mungu na utumishi wake? Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika kitabu kizima cha Biblia cha Mhubiri kuonyesha jambo lipasalo kuja kwanza katika maisha zetu. Alimalizia hivi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo. Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:1, 13.

16 Ndugu wote Wakristo wenye umri mkubwa zaidi uwajuao—wazee, mapainia, na waangalizi wa mizunguko na wilaya—walikuwa watoto wakati mmoja. Ni nini kilichoongoza kwenye baraka ambazo wao wazionea shangwe leo? Wao walimpenda Mungu wakataka kumtumikia. Wengi wao waliutumia kwa faida wakati wa ziada waliokuwa nao ujanani ili wapate maarifa na ujuzi. Walijifunza na kushiriki katika mikutano. Walishiriki katika kufundisha, na wakajitahidi kufikia mapendeleo ya ziada—kupainia, utumishi wa Betheli, au utendaji mwingine unaothawabisha. Hawakuwa ‘vijana supa’ (wasio wa kikawaida); wao walikuwa na mapendezi na mahangaikio yale ya kawaida uliyo nayo. Na bado, walijitumikisha kwa bidii kupatana na shauri hili: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu.”—Wakolosai 3:23; linganisha Luka 10:27; 2 Timotheo 2:15.

17 Namna gani wewe? Je! kweli wewe wathamini mambo ya kimungu? Je! wewe huchagua marafiki miongoni mwa wale wawekao mambo ya kiroho kwanza? Je! wewe huwatia wengine moyo washiriki pamoja nawe katika utendaji wa Kikristo? Je! wewe huenda katika utumishi wa Kikristo pamoja na walio na umri mkubwa zaidi, wenye ujuzi mwingi zaidi ili ujifunze kwao, uonje shangwe yao, na utiwe moyo na kazi zao njema? Shahidi mmoja wa kike aikumbuka siku ile ambapo, karibu miaka 20 iliyopita, mtu mwenye umri mkubwa zaidi alimwalika kwa uchangamfu aambatane naye katika huduma ya shambani. Yeye asema hiyo ilikuwa hatua ya badiliko kubwa katika maisha yake: “Kwa mara ya kwanza ikawa kwamba ninaenda kwa sababu mimi nilitaka kwenda, wala si kwa sababu tu wazazi wangu walikuwa wakinipeleka.”

18 Ikiwa unafanya maendeleo katika kufanya mambo kwa njia ya Mungu, huenda karibuni ukaanza kufikiria ubatizo. Ni jambo la maana kukumbuka kwamba ubatizo si kipitio cha kidesturi tu cha kuingia katika utu mzima wa kijana. Hauonyeshi kwamba wewe unakua uwe mtu mzima, wala si jambo upaswalo kufanya kwa sababu rafiki zako wamechukua hatua hiyo. Kabla hujapeleka ombi la ubatizo, wapaswa uwe na maarifa fulani ya msingi ya ukweli na uwe unaishi kupatana na Neno la Mungu. Wapaswa uwe na ujuzi wa kiasi kifaacho katika kushiriki maarifa hayo na wengine na ung’amue kwamba hii ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Pia wapaswa kujua kwamba baada ya kuchukua hatua hii ya maana ya Kikristo utatarajiwa uishi kupatana na kanuni za uadilifu za Biblia.b Katika moyo wako, wapaswa uwe umekwisha kuweka wakfu maisha yako kwa Baba yako wa kimbingu mwenye upendo.—Linganisha Zaburi 40:8, 9.

19 Ubatizo ni hatua uchukuayo uamuapo kwa uthabiti kwamba hata litukie jambo gani katika maisha yako yaliyobaki, utamtumikia Mungu. Ni ishara ya peupe kwamba wewe umefanya wakfu kamili usiobakiza nje sehemu yoyote, na usio na masharti kwa Yehova kupitia Yesu Kristo ili kufanya mapenzi ya Mungu. Mzee mmoja Mkristo aikumbuka siku ile ambapo, karibu nusu-karne iliyopita, aling’amua hivi: “Ni lazima mimi nichukue hatua fulani kuhusu jambo hilo!” Michelle, Shahidi mchanga aliyebatizwa katika Newcastle, England, miaka michache iliyopita, asema hivi: “Kwenye umri wa miaka 13, niling’amua kwamba napaswa kuweka wakfu maisha yangu na kubatizwa; mimi naona hakuna jambo ambalo lingekuwa afadhali nilifanye kuliko kutumikia Mungu.”

20 Makumi ya maelfu ya vijana wamebatizwa majuzi. Wao walikuwa wamejifunza Neno la Mungu na wakajifunza njia zake, halafu kwa kubatizwa katika maji wakaterema kujiunga na watu wengi wa umri mkubwa zaidi katika kufanya ufananisho wa peupe wa wakfu wao kwa Mungu. Wao wajua kwamba ubatizo sio mwisho bali ni mwanzo tu wa njia ya maisha ya kujiweka wakfu kikweli hivi kwamba wana azimio la kufuata katika utumishi wa Yehova milele.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Watumishi Wenye Ujana Katika Nyakati za Biblia” kwenye ukurasa wa 4.

b Hii haimaanishi kwamba kusema, ‘Sijabatizwa bado’ ni udhuru wa kutenda kosa. Mara tu tujuapo yale ambayo Mungu ayataka, ni wazi kwamba tuna daraka la kumtii.—Yakobo 4:17.

Wewe Ungejibuje?

◻ Kwa nini maarifa ya Neno la Mungu ni ya maana sana?

◻ Waweza kupataje faida nyingi zaidi kutokana na mikutano ya Kikristo?

◻ Ni mibaraka gani kutoka kwa Mungu inayopasa kutuchochea tumtii?

◻ Wewe waweza kusongaje mbele katika utumishi wa Mungu?

◻ Mtu apasa kubatizwa lini?

[Maswali ya Funzo]

 1. Ni nini baadhi ya mambo ya kutokeza ambayo Biblia husema juu ya Samweli?

 2. Wadogo-wadogo hujifunza nini kwenye mikutano ya watu wa Yehova leo?

 3. Ni jinsi gani vijana waijuao Biblia huyaona maisha kwa njia iliyo tofauti na ya wale wasioijua?

 4. Kujua njia za Mungu huweka daraka gani juu ya wazazi, na kijana Samweli alikuwaje kielelezo kizuri cha jambo hilo?

 5. (a) Biblia ni ya thamani gani kubwa? (b) Paulo alimwambia Timotheo nini juu ya umaana wa Neno la Mungu lililoandikwa?

 6. Kitabu cha Mithali husema nini juu ya umaana wa maarifa na hekima ya kumcha Mungu?

 7. Ni mambo gani ya maana kabisa tupaswayo kujifunza?

 8. Ni kielelezo gani chema kilichowekwa na Yosia na Yesu?

 9. (a) Vijana wengi wana tatizo gani? (b) Ni nini chaweza kurahisisha kusoma na kujifunza, na je! wewe binafsi umeona kwamba hiyo ni kweli?

 10. (a) Wewe waweza kupataje faida nyingi zaidi kutokana na mikutano ya Kikristo? (b) Wewe mwenyewe umeonaje katika jambo hilo?

 11. Waweza kupataje mengi zaidi kutokana na hotuba zenye msingi wa Biblia, na kwa nini hilo ni jambo la maana?

 12. Ni nini baadhi ya mambo yenye kutokeza ambayo Mungu ametufanyia?

 13. Kwa nini wewe wahisi kwamba Mungu apendezwa na watu mmoja mmoja?

 14. Kufuata kanuni za Mungu kwawezaje kuleta maendeleo katika maisha yako?

 15. Sulemani aliwapa vijana ushauri gani wa kimungu?

 16. Vijana waweza kujitahidije kufikia mapendeleo zaidi?

 17. Ni nini kiwezacho kusaidia vijana wafanye maendeleo katika utumishi wa Mungu?

 18. Ni mambo gani ya kufikiria kabla ya kujitoa kwa ajili ya ubatizo?

 19. Mtu apaswa kubatizwa lini?

 20. (a) Ni kielelezo gani kizuri ambacho tayari kimewekwa na makumi ya maelfu ya vijana? (b) Hatua hii yapasa kuonwaje?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki