Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
United States ya America
MASIMULIZI yetu yaanza katikati ya karne ya kumi na tisa. Magari ya farasi yaliyofunikwa bado yanajikokota katika nyanda, yamechukua walowezi kwenye sehemu za mbali za Amerika ya Magharibi. Makundi makubwa ya mbogo au nyati, ambao walikuwa karibu milioni ishirini mwaka wa 1850, yangali yatanga-tanga kati ya Milima ya Appalachia na Rocky.
Hata hivyo, “mwisho wa taratibu ya mambo” ulikuwa unakaribia. Kwa kweli lazima “ngano,” Wakristo wa kweli, iwe mahali fulani katika shamba la Mungu la duniani pote ikilimwa. Lakini wapi?
‘SIKU YA MAMBO MADOGO’
Ni karibu mwaka wa 1870; ni katika Mji wa Allegheny, Pennsylvania. Allegheny, ambapo baadaye pakawa sehemu ya Pittsburgh, ni mji wenye makanisa mengi. Jioni moja kijana wa miaka kumi na minane anatembea katika mojawapo ya barabara za Allegheny. Kulingana na vile yeye mwenyewe alivyokubali baadaye, alikuwa “ametikisika katika imani juu ya mafundisho mengi yaliyokuwa yamekubaliwa kwa muda mrefu” akakaribia kuwa asiye mwaminifu kwa mafundisho hayo. Lakini usiku wa leo avutwa na uimbaji unaoendelea mahali fulani. Aingia katika jumba chafu-chafu na lenye vumbi-vumbi. Kusudi lake ni nini? Kama alivyosema, ni “kuona kama wachache waliokutana humo walikuwa na jambo la akili zaidi kuliko imani za makanisa makubwa.”
Kijana yule akaketi akasikiliza. Jonas Wendell wa dini ya Second Adventist akatoa mahubiri. “Maelezo yake ya Maandiko hayakuwa wazi kabisa,” ndivyo alivyosema msikilizaji huyo baadaye. Lakini yalisaidia. Alilazimika kukubali hivi: “Yalitosha, kwa uongozi wa Mungu, kuimarisha tena imani yangu kwamba Biblia iliongozwa na Mungu, nayo yalitosha kuonyesha kwamba maandishi ya Mitume na Manabii yanakamatana kabisa. Mambo niliyoyasikia yakanifanya niichunguze Biblia yangu kwa bidii na uangalifu zaidi kuliko wakati mwingine wo wote.”
Kijana huyo mchunguzi alikuwa Charles Taze Russell. Alizaliwa katika Allegheny Februari 16, 1852, naye alikuwa mwana wa pili wa Joseph L. na Ann Eliza (Birney) Russell, wote wawili wakiwa wa ukoo wa mchanganyiko wa Waskoti na Waireland. Mama yake Charles, ambaye alikuwa amemweka wakf kwa kazi ya Bwana alipozaliwa, alikufa Charles alipokuwa kivulana cha miaka tisa. Lakini Charles alipata maoni yake ya kwanza juu ya dini kwa wazazi wake Wapresbyteri alipokuwa mdogo. Mwishowe alijiunga na Congregational Church lililokuwa karibu kwa sababu lilikuwa na maoni bora zaidi.
Alipokuwa kivulana cha miaka kumi na mmoja, Charles alishirikiana na baba yake katika biashara, kijana huyo akawa ndiye mwandikaji wa makala za mapatano ya biashara yao. Alipokuwa wa miaka kumi na mitano alikuwa akishirikiana na baba yake katika shirika lenye maendeleo la maduka ya mavazi ya wanaume. Baadaye, wakawa na maduka katika Pittsburgh, Philadelphia na kwingineko.
Wakati huo wote, kijana Charles alikuwa mwanafunzi mnyofu wa Maandiko. Alitaka kumtumikia Mungu kama alivyoweza. Kwa kweli, wakati mmoja alipokuwa wa miaka kumi na miwili baba yake alimkuta katika duka la jamaa saa nane ya usiku, akisoma sana kamusi ya Biblia, bila kujali ni saa ngapi.
Alipokuwa anaendelea kusonga katika umri, Russell alifadhaika kiroho. Alihangaika hasa juu ya mafundisho ya adhabu ya milele na lile fundisho la kwamba mambo yote yanayotokea yanaandikwa na Mungu hata hayawezi kuepukwa. Yeye aliwaza hivi: “Mungu anayeweza kutumia nguvu zake aumbe wanadamu ambao alijua na akawaandikia mateso ya milele, hawezi kuwa mwenye hekima, mwenye haki wala mwenye upendo. Kanuni yake ingekuwa ya chini kuliko ya wanadamu wengi.” (1 Yohana 4:8) Hata hivyo, kijana Russell aliendelea kuamini Mungu yuko. Akili yake ikiwa inahangaikia mafundisho, alichunguza imani mbalimbali za Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu), akachunguza dini kubwa za Mashariki akafa moyo kabisa. Kweli ingepatikana wapi?
Kijana Russell alikuwa na mawazo hayo alipoingia katika jumba lile chafu-chafu katika Allegheny akasikia mahubiri ‘yaliyoimarisha tena imani yake yenye kutikisika ya kwamba Biblia iliongozwa na Mungu.’ Alifikia vijana kadha aliofahamiana nao, akawaeleza anataka kujifunza Maandiko. Karibuni kikundi hicho kidogo cha karibu watu sita kikaanza kukutana kila juma kujifunza Biblia kwa utaratibu. Katika mikutano yao ya kawaida kuanzia mwaka wa 1870 mpaka 1875, mawazo ya kidini ya watu hao yalibadilika sana. Baada ya muda fulani, Yehova aliwabariki kwa kuwaongezea nuru na kweli ya kiroho.—Zab. 43:3; Mit. 4:18.
Karibu na Januari wa 1876, Russell alipokea nakala ya gazeti la kidini liitwalo The Herald of the Morning (Mjumbe wa Asubuhi). Kutokana na jalada, akajua ni la Waadventist, lakini yaliyokuwamo yalikuwa ya kushangaza. Mhariri, N. H. Barbour wa Rochester, New York, alifahamu kwamba kusudi la kurudi kwa Yesu Kristo halikuwa kuharibu bali kubariki jamaa zote za dunia na kwamba angekuja kama mwizi wala si katika mwili, bali kama roho. Kwa kweli, kwa kuangalia unabii mbalimbali wa Biblia wenye kuonyesha wakati, Barbour alidhani Kristo alikuwako wakati huo na kwamba kazi ya mavuno ya kukusanya “ngano” na “magugu” ilikuwa imekwisha anza. Kwa hiyo, Russell akapanga pamoja na Barbour kuwe na darasa la Biblia katika Pittsburgh la karibu watu 30 wakiwa wameungana na kikundi kikubwa kidogo kuliko hicho cha Barbour kilichokuwa katika Rochester, New York. Russell akachanga pesa zake mwenyewe kuchapisha gazeti Herald, ambalo wakati huo lilikuwa karibu kuacha kuchapwa kwa muda, kwa hiyo akawa mhariri-msaidizi wa gazeti hilo.
Alipokuwa wa miaka 25 katika mwaka wa 1877, Russell alianza kuuza biashara zake akaingia katika utendaji wa kuhubiri wa wakati wote. Wakati huo alikuwa akisafiri mji kwa mji akitoa hotuba za Biblia katika makusanyiko ya hadhara, barabarani na katika makanisa ya Waprotestanti. Kwa sababu ya kufanya kazi hiyo, akajulikana kama “Pastor” Russell. Aliamua kuweka utajiri wake kama akiba ya kuenezea kazi, kisha ajitoe kufanya kazi hiyo maisha yake yote, akataze mkusanyo wa sadaka katika mikutano yote na kutegemea michango iliyochangwa na watu bila kuombwa wafanye hivyo ndio aendeleze kazi pesa zake mwenyewe zikiisha.
Katika mwaka wa 1877, Barbour na Russell walichapa kitabu Three Worlds, and the Harvest of This World. Linalofaa kuangaliwa ni kwamba kitabu hicho kilionyesha kwa usahihi kabisa mwisho wa Majira ya Mataifa, “nyakati zilizowekwa za mataifa.” (Luka 21:24, NW) Kilionyesha (katika kurasa 83 na 189) kwamba kipindi hicho cha miaka 2,520 ambacho katika hicho mataifa yasiyo ya Kiyahudi yangetawala dunia bila kukatizwa na ufalme wo wote wa Mungu, kilianza wakati Babeli ilipopindua ufalme wa Yuda mwishoni mwa karne ya saba B.C.E. na kwamba kingekoma mwaka wa 1914 C.E. Kulingana na hesabu hizo, mwaka wa 1914 ulikuwa mwisho wa nyakati hizo na ukawa wakati wa kuzaliwa kwa ufalme wa Mungu mbinguni Kristo Yesu akiwa ndiye mfalme. Ebu wazia hilo! Yehova alijulisha watu wake jambo hilo karibu miongo minne ya miaka (miaka 40) kabla nyakati hizo hazijakoma.
Mambo yote yaliendelea sawasawa kwa muda. Ndipo yakaingia masika ya mwaka wa 1878. Barbour alikuwa akitazamia kwamba wakati huo watakatifu waliokuwa hai duniani wangechukuliwa mara moja wakiwa na miili yao wakawe pamoja na Bwana mbinguni milele. Lakini haikuwa hivyo. Kulingana na alivyosema Russell, Barbour “alielekea kufikiri lazima apate jambo jipya la kufanya watakatifu walio hai waache kufikiria namna walivyokosa kuchukuliwa mara moja wote kwa pamoja.” Karibuni alifanya hivyo. Masimulizi ya Russell yasema, “Tulipatwa na mshangao na kuudhika Bw. Barbour alipoandika makala ya Gazeti Herald karibuni akikana fundisho la upatanisho—akikana kwamba kifo cha Kristo hakikuwa bei ya ukombozi wa Adamu na wazao wake.”
Katika toleo la Septemba la Herald makala ya Russell iitwayo “Upatanisho” ilitokea ikiunga mkono ukombozi na kupinga kosa la Barbour. Ubishi uliendelea kuwamo katika kurasa za gazeti hilo mpaka Desemba 1878. Russell kaandika, “Sasa ilikuwa wazi kwangu kwamba Bwana asingeniruhusu tena nisaidie kwa pesa, wala nitambuliwe kwa njia nyingine yo yote yenye kuonyesha upinzani kwa kanuni ya msingi ya dini yetu takatifu.” Kwa hiyo, C. T. Russell kafanya nini? Aendelea kusema hivi: “Kwa hiyo, baada ya kutia jitihada ya uangalifu sana lakini isiyo na matokeo ya kumrudisha mwenye kukosa, nikajitenga kabisa na gazeti The Herald of the Morning na Bw. Barbour.” Lakini hiyo haikutosha kuonyesha ‘alikuwa anaendelea kuwa mwaminifu kwa Bwana na Mkombozi wetu.’ Kwa hiyo, akachukua hatua nyingine. Russell aandika hivi: “Kwa hiyo nikaelewa ni mapenzi ya Bwana nianze gazeti jingine, ambamo lazima kanuni ya Msalaba iheshimiwe sana, fundisho la Ukombozi litetewe na Habari Njema za Furaha kuu zitangazwe kote kote kama iwezekanavyo.”
C. T. Russell aliona ni uongozi wa Bwana aache kusafiri na kuanza kuchapa gazeti fulani. Hivyo katika Julai mwaka wa 1879 toleo la kwanza la Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence lilitokea. Sikuzote gazeti hilo ambalo linajulikana ulimwenguni pote kama Mnara wa Mlinzi liliunga mkono fundisho la Biblia la ukombozi. Kama vile Russell alivyoandika wakati mmoja: “Tangu mwanzo, limekuwa likitetea Ukombozi kwa njia ya pekee; na, kwa neema ya Mungu, twatumaini ndivyo litakavyokuwa mpaka mwisho.”
Mwanzo wa gazeti hilo ulikuwa “siku ya mambo madogo,” kwa maana toleo lake la kwanza lilikuwa na nakala karibu 6,000 tu. (Zek. 4:10) Mwenyekiti wa darasa la Biblia lililokuwa katika Pittsburgh, C. T. Russell, ndiye aliyekuwa mhariri na mchapaji. Kwanza wanafunzi wa Biblia wengine watano walitumikia kama waandikaji wa kawaida wa gazeti hilo. Gazeti lilikuwa wakf kwa Yehova na kwa faida za ufalme wa Mungu. Walimtegemea Mungu kama inavyoonyeshwa kwa mfano na yaliyosemwa katika toleo la pili: “Tunaamini ‘Zion’s Watch Tower’ linategemezwa na YEHOVA, na maadamu ndivyo halitaomba kamwe wala kusihi wanadamu walisaidie. Wakati Yeye anayesema: ‘Dhahabu yote na fedha ya milima ni vyangu,’ atakapokosa kutoa pesa zilizo za lazima, tutafahamu ni wakati wa kuacha kulichapa.” Gazeti hilo halijaacha kuchapwa kamwe. Bali, uchapaji wake umeongezeka sana ukawa wastani ya nakala 10,000,000 kila toleo mwishoni mwa mwaka wa 1975.
Mwaka wa 1879 na wa 1880 C.T. Russell na washirika wake walikuwa wameanzisha karibu makundi 30 katika Pennsylvania, New Jersey, New York, Massachusetts, Delaware, Ohio na Michigan. Russell mwenyewe alipanga kutembelea kila kundi. Programu yake ilihitaji afanye mkutano mmoja au mingi ya Biblia na kila kikundi.
C. T. Russell na washirika wake waliamini walikuwa wakiishi wakati wa mavuno, nao walikuwa wachache—karibu watu 100 tu wenye nguvu mwaka wa 1881. Lakini watu walihitaji kweli yenye kukomboa, na kwa fadhili zisizostahilika za Mungu wangeipokea. Kichwa chenye kuvutia cha makala iliyokuwa katika Zion’s Watch Tower la Aprili 1881 kilikuwa kikisema “Watakiwa Wahubiri 1,000.”
Wahubiri elfu moja waliotakiwa hawakuuitikia mwito wa kuchukua hatua wakati huo. (Mwaka wa 1885 walikuwako makolpota karibu 300.) Lakini watumishi wa Yehova walijua kwamba imewapasa kuzihubiri habari njema. Kwa kufaa, Zion’s Watch Tower la Julai na Agosti mwaka wa 1881 lilisema hivi: “Je! wewe unahubiri? Tunaamini kwamba hakuna mtu atakayekuwa wa kundi dogo isipokuwa wahubiri. . . . Naam, tuliitwa tutaabike pamoja naye na kuzitangaza habari njema sasa, ili kwamba katika wakati wake tuweze kutukuzwa na kufanya mambo yanayohubiriwa sasa. Hatukuitwa, wala kutiwa mafuta tupate heshima na kukusanya utajiri, bali kutumia na kutumiwa, na kuzihubiri habari njema.”
Mwaka uo huo—1881—C. T. Russell alimaliza vikaratasi viwili vikubwa. Kimoja kiliitwa “Tabernacle Teachings.” Kile kingine kilichoitwa Food for Thinking Christians kilifunua makosa fulani ya mafundisho kikaeleza kusudi la kimungu.
Hapo kwanza uchapaji wote wa trakti na Zion’s Watch Tower ulifanywa na mashirika ya kibiashara. Lakini ikiwa ugawaji wa vitabu ungeongezeka, na ikiwa Wanafunzi wa Biblia (kama mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo) wangepokea michango kuendesha kazi, sosaiti ya namna fulani ilitakiwa. Kwa hiyo, mapema mwaka wa 1881, Zion’s Watch Tower Tract Society lilianzishwa likiwa shirika lisilohalalishwa C. T. Russell akiwa ndiye msimamizi. Yeye na wengine walichanga karibu shilingi 245,000 kuendesha shirika hilo la uchapaji. Mwaka wa 1884 Sosaiti hiyo ambayo haikuwa imehalalishwa ilihalalishwa (iliandikishwa kisheria) kama Zion’s Watch Tower Tract Society, Russell akitumikia kama msimamizi (president) wake. Leo shirika hilo la kidini linajulikana kama Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania.
Uenezaji wa kweli za Biblia uliongezeka ulipotokea mfululizo wa vitabu vilivyoitwa “Millennial Dawn” (baadaye vilivyoitwa, “Studies in the Scriptures”). Volume 1 kilichoandikwa na C. T. Russell kwa usemi wenye kufahamika vyepesi, kilichapwa mwaka wa 1886. “The Divine Plan of the Ages” ambacho kwanza kiliitwa “The Plan of the Ages” kilizungumza mambo kama vile “Kuwako kwa Muumba Mkuu Zaidi ya Wote Mwenye Akili,” “Kurudi kwa Bwana Wetu—Kusudi Lake, Kurudishwa kwa Vitu Vyote,” “Siku ya Hukumu,” “Ufalme wa Mungu” na “Siku ya Yehova.” Kwa kipindi cha miaka 40, nakala milioni sita za kitabu hicho zilienezwa, zikasaidia mamia ya watafutaji wanyofu wa kweli watoke katika utumwa wa dini ya uongo na kuingia katika uhuru wa Kikristo.
Muda ulipopita, C. T. Russell aliandika vitabu vitano vingine vya Mfululizo wa “Millennial Dawn.” Hivyo vilikuwa: Volume II, The Time Is at Hand (1889); Volume III, Thy Kingdom Come (1891); Volume IV, The Battle of Armageddon (1897; kilichoitwa hapo kwanza “The Day of Vengeance”); Volume V, The At-one-ment Between God and Man (1899); Volume VI, The New Creation (1904). Russell hakuendelea kuwa hai aweze kuandika kitabu cha saba cha mfululizo huo. Vitabu hivyo vya Kikristo viliitikiwa sana.
Shauku ya kuzihubiri habari njema inaonyeshwa katika mawazo yaliyoandikwa kwa Sosaiti. Kwa mfano, mwaka wa 1891 mwanamume mmoja na mkewe waliandika hivi: “Tumeweka wakf vitu vyote tulivyo navyo kwa Bwana na kwa utumishi wake vitumiwe kwa utukufu wake; na, Bwana akipenda, nitajaribu kufanya kazi ya ukolpota upesi nitakavyoweza kupanga mambo, na kama Bwana akiukubali utumishi wangu na kunibariki ninapofanya kazi yake, tutagawana kazi ya kutunza nyumba kisha mke wangu na mimi tutaingia katika kazi ya mavuno.”
Barua ambayo Sosaiti ilipokea mwaka wa 1894 kwa mtu aliyekuwa amepokea vitabu vya Millennial Dawn kwa wanawake wawili waliokuwa makolpota ilikuwa ya kupendeza sana. Alivisoma vitabu hivyo, akaagiza nakala za ziada, akaandikisha Zion’s Watch Tower, kisha akavutwa kuandika hivi: “Mke wangu mpenzi na mimi bi nafsi tumevisoma vitabu hivi tukapendezwa sana sana, nasi tunaona Mungu ametuletea baraka kubwa kwa kuwa na nafasi ya kuvipata. Vinasaidia kweli kweli kujifunza Biblia. Kweli kubwa zinazofunuliwa wakati wa kujifunza mfululizo wa vitabu hivi zimegeuza malengo yetu ya kidunia; na kwa kuwa tumeiona kwa kadiri fulani nafasi kubwa ya kumfanyia Kristo jambo fulani, tunakusudia kutumia nafasi hiyo vizuri kuvigawa vitabu hivi, kwanza kati ya watu wa ukoo wetu na marafiki zetu, kisha kati ya maskini wanaotaka kuvisoma wasiweze kuvinunua.” Barua hiyo ilitiwa sahihi na J. F. Rutherford, ambaye alijiweka wakf kwa Yehova miaka kumi na miwili baadaye na mwishowe akamfuata C. T. Russell kama msimamizi (president) wa Watch Tower Society.
—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.