Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 3/15 kur. 15-19
  • Kutafuta “Kondoo” Sehemu za Mashambani Huko Liberia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutafuta “Kondoo” Sehemu za Mashambani Huko Liberia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Yehova Anatafuta “Kondoo” Zake
  • Yehova Analisha “Kondoo” Zake
  • Yehova Anaponesha “Kondoo” Zake
  • Baraka Za Yehova Zinaendelea Kuja
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 3/15 kur. 15-19

Kutafuta “Kondoo” Sehemu za Mashambani Huko Liberia

MCHUNGAJI mrefu Mmandigo amesimama kwa unyamavu juu ya kichuguu (mwinuko) cha mchwa, akiwa amejivika vazi refu la kukinga mwili wake na joto la jua la Afrika. Yeye anawatazama kondoo wake kwa uangalifu mwingi huku wao wakifurahia kuzitafuna nyasi tamu zilizoota kando-kondo ya viziwa vya matope na vibwawa vyenye chumvi vya Ghuba Dogo la Sutter. Kundi analochunga mchungaji huyu ni mchanganyiko wa wanyama. Kuna mbuzi wenye ngozi ya manyoya ya kahawia na meupe na kondoo warefu, wembamba na weupe.

Tukianzia jiji kuu la nchi, Monrovia, la wanyama hao, tunaukumbuka mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi. Yeye alitabiri kwamba mataifa yote yangekusanyika mbele yake kisha yeye angetenga watu walio kama kondoo watakaopata uzima wa milele watoke kati ya wale walio kama mbuzi watakaostahili kuharibiwa. (Mathayo 25:31-46) Kwa hiyo, tunaweza kuuliza hivi: Kazi hiyo ya kutenganisha watu inaendelea namna gani? Je! “kondoo” wamepatikana katika sehemu za mashambani huko Liberia?

Yehova Anatafuta “Kondoo” Zake

Katika nchi ya Liberia wako watumishi wa Yehova zaidi ya 1,000 walio kama kondoo. Je! ungependa kujua njia ambayo Mungu ametumia kuwapata na kuwachunga “kondoo” zake katika nchi hii? Mbona basi usijiunge nasi tunapotembelea sehemu kadha wanakoishi na kukusanyika?

Tukianzia jiji kuu la nchi, Monrovia, tunakuta kijana wa kiume akijifunza Biblia kwenye makao ya wamisionari kule Crown Hill. Zamani yeye alikuwa akikaa huko mbali mashambani, mbali kusikokuwa na ye yote wa Mashahidi wa Yehova. Basi aliwapataje?

“Mimi sikutosheka na dini ya baba,” yeye anasema. “Basi nilimwomba Mungu aniongoze. Siku chache baadaye, niliona nakala ya kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele katika nyumba ya jirani. Nilimwomba aniazime kitabu hicho nami nikakisoma. Nilisadiki kwamba sala yangu ilikuwa imejibiwa, basi nikaiandikia afisi ya Sosaiti katika Monrovia. Lakini nilipatwa na kiherehere nikashindwa kungoja majibu; basi nikasafiri kwenda Monrovia, nikawapata Mashahidi nao wakaanza kujifunza Biblia nami.” Alipoulizwa na mtu wanayefahamiana ulizo la kwamba, “Wewe ulikokotwa na nani akakusukuma kwa nguvu uingie dini ya Mashahidi wa Yehova? ” yeye alijibu, “Nilikokotwa na Yehova mwenyewe.”

Karibu maili 100 (kilomita 160) tunaposafiri kutoka Monrovia na kutelemka pwani, tunalifikia jiji la Buchanan. Jiji hilo lilianzishwa katika miaka ya 1830 na watu walio mchanganyiko wa Waamerika na Waliberia waliokuwa wamekuwa watumwa huko Amerika kisha wakatafuta makao hapa kati ya wenyeji Wabassa. Leo Buchanan ni jiji linalositawi likiwa bandari yenye kuletewa na magari-moshi mawe yenye madini kutoka milima ya Nimba, kisha sehemu-sehemu zisizotakwa zinasafishwa halafu madini yenyewe yanasafirishwa kwa meli. Tunapoliingia jiji hili tunaona Kijumba cha Ufalme chenye rangi ya kijani kibichi kilichojengwa juu ya ukuta mkubwa wa ardhi, barabara ya lami iliyotandazwa kwa kokoto ngumu ikiwa huko chini. Karibu ndani uone namna kilivyo.

Tunapoingia tunasalimiwa na watu 40 wenye kutabasamu. Anayeitwa Kollie ana sababu ya pekee ya kutabasamu (kuchekelea). Yeye ni (mwanamume na ni) mmoja wa watu wengi waliobatizwa miaka ya majuzi. “Nilipokuwa katika shule ya masomo ya juu huko Kakata,” yeye anasema, “wengine wa wanashule wenzangu walikuwa wakinieleza habari za Yehova nao walinikaribisha kwenye Jumba la Ufalme lao; lakini mimi nilikataa kwa kuwa na maoni ya kwamba sheria zao zilikuwa kali mno. Walakini, nilipohitimu masomo na kuhamia Buchanan, nilianza kuona kwamba maisha za Mashahidi zilikuwa zikibadilika na kuwa bora kuliko maisha yangu kwa sababu wao walikuwa wamefunzwa nidhamu (adabu) nzuri zaidi, Basi nikaliandikia kundi barua kuwaomba wanisaidie. Mmoja wa wazee alianza kujifunza nami, na leo mimi nafurahi kuwa mtumishi aliye wakf wa Yehova.” Ndiyo, Yehova ametumia roho yake akawapata watu hao walio kama kondoo kisha akawaelekeza kwenye makundi yake.

Yehova Analisha “Kondoo” Zake

Wengine wa wale ambao sasa wanafurahia “malisho mema” kati ya “kondoo” za Yehova walikuwa na njaa nyingi wakitafuta chakula cha kiroho hapo kwanza katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Kwa upendo Yehova amewaongoza akawapeleka kwa wale ambao wamelitii onyo la upole la Yesu kwamba ‘wawalishe wanakondoo wake.’​—Ezekieli 34:2, 14, 15; Yohana 21:15, NW.

Kati ya wenye kutafuta chakula cha kiroho alikuwako Francis. Yeye anaishi katika moja ya nyumba nyingi zilizosongamana kwenye ukingo wa Kisiwa Bushrod, katika sehemu moja ya Monrovia inayoitwa Clara Town. Yeye alikipataje chakula cha kiroho?

“Mimi nilikuwa mshiriki wa Kanisa la Pentekoste,” anaeleza, “lakini nikaudhika kwa sababu viti vya pekee vilikuwa vikiwekwa vikaliwe na washiriki fulani tu waliochukuliwa kuwa watu wa maana. Nikataka kuifahamu Biblia, lakini mchungaji akatumia mwingi wa wakati wake akisema-sema habari za fedha. Alisema tusipochangia kanisa fedha, tusingeweza kwenda mbinguni. Halafu siku moja mmoja wa Mashahidi wa Yehova akaniachia nakala ya Mnara wa Mlinzi. Kwa kuisoma niliona tofauti nyingi kati ya mafundisho ya Biblia na mazoea ya kanisa langu. Yule Shahidi alirudi akawa akinisaidia kuifahamu Biblia, nami nikapata maarifa zaidi nilipoanza kuhudhuria mikutano. Binamu yangu alijiunga nami katika funzo, nasi sote wawili tukabatizwa.”

Sasa tunaondoka kwenye Kisiwa cha Bushrod na kukiacha nyuma. Gari letu la kukodi linatuvusha Mto Montserrado, tunaipita wilaya ya kibiashara kisha tunaingia Sinkor, hiyo ikiwa ndiyo sehemu ya Monrovia yenye vifaa vilivyo vya kisasa zaidi. Mashahidi wa Yehova wanakutana hapa katika Jumba la Ufalme lililo malidadi. Hapa, pia, tunakuta mtu mwingine aliyekuwa akitafuta majibu fulani. Yeye anatuambia:

“Nilipokuwa katika shule ya masomo ya juu, niliudhiwa na maoni ya walimu wangu wa Biblia. Kwa mfano, kitabu kimoja tulichojifunza kilionyesha kwamba Yesu alikuwa mjinga na mshirikina kwa sababu aliamini kwamba kuna mashetani na kwamba yanaweza kuwaingia watu yakae ndani yao. Mimi nikataka sana kujua kama Biblia ni Neno la Mungu au neno la wanadamu. Nilisumbuka moyoni pia kwa kuona dini zikizidi kuongezeka na huku zinajiita za Kikristo.”

Kijana huyu wa kiume ‘alijisikia akipungukiwa zaidi na hali ya kiroho’ aliposhirikiana baadaye na dini ya Bahai. Yeye anaendelea kueleza hivi:

“Nilikubali kazi ya ualimu katika Ganta, ambako mama alikuwa akiishi. Yeye alikuwa akijifunza pamoja na Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda fulani, mimi pia nilikubali kujifunza Biblia nyumbani lakini kusudi langu lilikuwa kumthibitishia Shahidi aliyekuja kwamba alikuwa akipotezwa na dini yake. Baada ya mazungumzo yetu ya kwanza, ambapo alinistaajabisha kwa kujibu maulizo yangu yote akitumia Biblia, nililazimika kukata kauli kwamba mimi ndimi niliyekuwa nimepotezwa. . . . Nikaamua kusoma vitabu vya zamani vya Watch Tower nione kama ningeweza kuona maneno yasiyopatana na yale ya vitabu vya sasa. Lakini kufanya hivyo kuliongezea imani yangu ya kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Nikaamini zaidi pia kwamba Mashahidi walikuwa watu wake.

“Ndipo nilipoanza kufanya mabadiliko katika maisha yangu. Nikaacha kuvuta sigara, nikajiondoa katika Kanisa la Kimethodisti na kuanza kueleza wengine habari za imani yangu, msichana niliyetaka kuoa akiwa mmoja wa hao. Hata yeye alikubali kuifuata kweli ajapopingwa na jamaa yao na kufukuzwa shuleni kwa sababu ya kudumisha hali ya kutokuwamo kwa Kikristo. Tulioana kisha tukabatizwa mwaka wa 1971.”

Tangu wakati huo watu hao waliooana wamepata pendeleo la kusaidia watu kadha wawe watumishi wa Yehova. Mume mwenyewe anatumikia sasa akiwa mzee aliyewekwa kundini.

Yehova Anaponesha “Kondoo” Zake

“Kondoo” wengi walikuwa wamepotea njia wakaziacha kanuni za haki ya adili za Neno la Yehova, kabla ya yeye kuwapata. Tafadhali angalia mifano inayofuata:

Upande mwingine wa Ghuba Dogo la Sutter anaishi mwanamume wa kabila la Kru anayeweza kuitwa jitu kwa sababu ya umbo la mwili wake. Hapo kwanza yeye alikuwa jitu chokozi lenye matata mengi mpaka akaitwa na rafiki zake “Mzima Moto.” Mke wake, Zoe, tunamkuta akiwa amepika mboga ya majani ya viazi na wali. Tunapokula tukiwa kwenye kivuli cha mwembe, mume wake anatuambia:

“Nilipokuwa mfanya kazi polisi, nilikata tumaini wakati mpango uliokuwa umefanywa nikasomee ng’ambo urubani [udereva wa ndege] ulipofutwa. Nikaamua kumwona ‘mganga wa kienyeji’ [mchawi] anipe ‘dawa’ [hirizi] inisaidie kutimiza lengo hilo nililotaka sana kulitimiza. Lakini wapi, ikawa ni kazi-bure tu. Ndipo Mashahidi wawili walipotutembelea wakaanza kutufunza Biblia. Tulizidi kupendezwa tulipojua kwamba Yehova anakusudia kuifanya dunia hii iwe paradiso ambapo haki ya hukumu na haki ya adili itatawala. Lakini dhamiri yetu ikatusumbua kwa kujua kwamba hatukuwa tukiishi kulingana na kanuni za Mungu za haki ya adili. Tulipojifunza ile kweli kuhusu pepo wabaya, tuliiharibu ile ‘dawa’ na vyombo vingine vya kiuchawi tulivyokuwa navyo. Tukaamua kusafisha maisha zetu, lakini ikatuchukua muda kwa sababu kulingana na sheria Zoe alikuwa angali mke wa mume wake wa kwanza. Baada ya muda fulani aliweza kupata talaka; sisi tukaoana kisha tukabatizwa mwezi uliofuata.”

Sasa tutamtembelea Jerome huko Bong Mine. Tutapanda motokaa Monrovia twende Kakata, umbali unaozidi kidogo tu maili 40 (kilomita 64). Huko njiani, tunapita miti ya kutengenezea mpira ambayo imejipanga mistari-mistari. Tunapofika Kakata tunaiacha motokaa na kupanda basi na sasa tunaingia barabara isiyolainishwa vizuri. Vijiji vya utamaduni halisi wa Waliberia vimetapakaa kati ya mashamba na vichaka vya sehemu zenye joto​—vijiji hivi ni vikundi-vikundi vya nyumba za matope zilizoezekwa kwa makuti (majani ya mitende). Mwishowe, tunaifikia kambi ya wachimba-chuma na kumkuta Jerome akiwa karibu na lile ghuba dogo. Ndiyo kwanza amalize kufulia nguo zake hapo. Tunapongojea Mashahidi wengine wafike nyumbani kutoka kazi yeye anatueleza namna Yehova amemsaidia:

“Mimi nilikuwa napenda kuvuta sigara na kunywa sana pombe. Hata nilikuwa na wanawake wawili. Siku moja, nilipokuwa nikinywa pombe pamoja na rafiki wengine, Shahidi mmoja alizungumza nasi habari za Biblia kisha akatutolea kitabu Kweli. Rafiki zangu walijaribu kunivunja moyo nisikikubali, lakini mimi nikawaza kwamba kama niliweza kuharibu fedha nyingi kwa kununua pombe, ningeweza kutumia [kiasi kidogo cha fedha] kukinunua kitabu hicho. Wao wakaniambia Shahidi huyo asingerudi tena aje kuniona. Lakini alirudi wakati uliopangwa akaanza kunifunza Biblia.

“Nilipoendelea kumjua Yehova, nilitambua kwamba njia yangu ya maisha haikumpendeza yeye na kwamba ningepata faida za kujiokolea fedha nikitumia kanuni za Biblia maishani mwangu. Kwa msaada wa Yehova, niliweza kuacha uvutaji wa sigara na unywaji mwingi wa pombe, nami nikajitenga na ushirika wa wasichana waliokuwa rafiki zangu. Nafurahi kwamba sasa naweza kusaidia watu wajue habari za Yehova Mungu na Mwanawe Yesu Kristo badala ya kuharibu maisha yangu. Nami ninafanya hivyo nikiwa mtangazaji wa wakati wote wa zile ‘habari njema.’”

Tunarudi Kakata kwenye kusanyiko la mzunguko ambako tunasikia jambo lililoonwa lifuatalo likisimuliwa na dada wa kutoka Gbarnga: “Nilipokuwa nikiuza nguo zamani katika soko la Yekepa, wanawake wale wengine sokoni walikuwa wakilalamika kwa kusema kwamba wavulana waliokuwa rafiki zao hawakuwape riziki, bali walikuwa wanachukua kiasi fulani cha fedha ambazo wanawake hao walijitafutia sokoni. Nikawa nikiwaeleza yanayosemwa na Biblia juu ya ndoa yenye kuheshimika na namna matumizi ya kanuni za Biblia yanavyoweza kuletea jamaa amani na furaha. Lakini wao walinicheka tu. Halafu siku moja, nilipokuwa nikifanya upainia-msaidizi, nikakuta mmoja wa wanawake hao tuliokuwa tukiuza pamoja sokoni. Mvulana aliye rafiki yake alikuwa amemtia moyo atoe mimba, naye mwanamke huyu akawa nusura ya kufa. Aliyakumbuka mambo mema niliyokuwa nikimwambia akasema anataka kujifunza Biblia kisha abadili maisha yake. Mwanamke huyu alibatizwa mwaka jana na hivi majuzi aliolewa na Mkristo.”

Baraka Za Yehova Zinaendelea Kuja

Tunatumaini kwamba umefurahia matembezi yako Liberia, na kwamba yamekusaidia ufahamu namna Yehova amewapata na kuwatunza kondoo zake wa kiroho hapa. Lakini namna gani wakati ujao? Sisi tuna tumaini hakika kwamba Mungu ataendelea kubariki jitihada zetu tunapotia bidii kutafuta “kondoo” wengine wengi.

Mwezi wa Desemba 1979 watu 1,956 walihudhuria “Tumaini Lenye Uzima” Kusanyiko la Wilaya tulilokuwa nalo. Tulifurahi kwa sababu watu 17 walibatizwa. Pia, kuna viishara vyenye kutuonyesha sana kwamba kuna “kondoo” wengine wanaohitaji msaada, kwa maana jumla ya watu 4,001 walikusanyika kote kote nchini Liberia siku ya Aprili 19,1981, kukikumbuka kwa utukuzo kifo cha Yesu Kristo.​—1 Wakorintho 11:​23-26.

Kundi la kondoo liendeleapo kukua katika nchi hii, kunatokea pia uhitaji wa kupanua majengo ya kutunzia ukuzi uliopo. Mwezi wa Mei 1979 tulisisimuka kupata habari kwamba Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imeipa ruhusa halmashauri ya tawi la Liberia kuandikisha kisheria shirika lisilo la kujipatia faida na kununua uwanja wa kujengea afisi ya tawi na makao ya Betheli yaliyo yetu wenyewe. Tangu wakati huo, kipande kizuri sana cha nchi kimenunuliwa. Hivi majuzi, maendeleo zaidi yalifanywa wakati mipango yetu ya ujenzi ilipokubaliwa na wakuu wa nchi.

Kwa kweli, tuna sababu ya kufurahi tunapofikiria namna Yehova amewakusanya watu wake na kuwabariki nchini Liberia. Kuanzia maji yenye kutiririka kwa utaratibu mzuri ya Mto Mano mpaka Cape Palmas upande wa kusini, na kuanzia ile misitu yenye hali za joto inayonyesha mvua katika Nimba mpaka zile fuo za bahari zenye mitende kwenye Bahari Kuu ya Atlantiki, “kondoo” wa Yehova wanaendelea kupatikana. Nasi tunasali yeye aendelee kubariki jitihada nyingi zetu za kuzitangaza habari njema za ufalme wake na kufanya watu walio kama kondoo wawe wanafunzi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki