Mahali pa Vijana Katika Jamii ya Kikristo
“Msifuni (Yah) . . . (enyi) vijana waume, na wanawali.”—Zab. 148:1, 12.
1, 2. (a) Unaposahauliwa matokeo yanakuwa yapi? (b) Yehova Mungu na Yesu Kristo wanawaonaje watoto?
PENGINE umekwisha kuona jambo kama hili: Ulialikwa kwenye karamu kubwa ambapo kulikuwako ishara za kuonyesha mahali pa kila mgeni. Walakini kwa sababu ya kusahaulika hakukuwa na mahali ulipowekewa. Hii inaweza kuwa hali isiyo nzuri na ya kuaibisha. Kuachwa au kusahauliwa si jambo linalopendeza, sivyo?
2 Katika njia iyo hiyo, watu wengi wanaweza kuwa na maelekeo ya kuwasahau au kuwaacha vijana, wakiwaona kuwa watu wasiostahili kuangaliwa au kushughulikiwa. Walakini hivyo si ndivyo Yehova Mungu na Mwanawe, Yesu Kristo wanavyowaona vijana. Wakati wanafunzi wake walipoelekea kufukuza watoto, Yesu aliwakaripia: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, msiwazuie.” (Marko 10:14) Akikazia kwamba hata viumbe vidogo ni vyenye thamani kwa Mungu, Yesu alisema hivi: “Je! mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu.” (Mt. 10:29) Basi, ikiwa Yehova huona ndege wadogo kuwa wenye thamani, watoto wadogo hawatakuwa wenye thamani kwake zaidi sana!
3. Sababu gani si watoto wote, wala malaika wote, wanaothaminiwa na Mungu?
3 Hata hivyo, kuthaminiwa hivyo na Mungu si jambo linalokuja vivi hivi tu. Si vijana wote wenye thamani kwa Mungu—wala si malaika wote. Biblia yasema hivi: “Na malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu.” (Yuda 6) Malaika wana migawo ya kazi mbinguni, wakimtumikia Yehova Mungu kama sehemu ya tengenezo lake la kimbinguni. Walakini malaika ambao wanazungumzwa juu yao hapo juu waliona kitu kingine kilichowavutia, na kwa hiyo wakaacha “makao yao yaliyowahusu.” Waliona nini?
4, 5. (a) Sababu gani wengine wa malaika wakaacha kutumikia Mungu, naye Mungu alishughulikaje na huu hali mbaya zilizotokea? (b) Twaweza kujifunza somo gani kutokana na hili?
4 Biblia inaeleza hivi: “Wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua.” (Mwa. 6:2) Je! hawa “wana wa Mungu” walikuwa wanadamu wa vivi hivi tu hapa duniani? Hapana. Hakika walikuwa wana wa kimalaika wa Mungu ambao waliacha mahali pao palipowapasa mbinguni na kuchukua umbo la kibinadamu ili wafanye ngono na wanawake wenye sura nzuri duniani. Kama matokeo ya uvutano wao wa uasherati, na baadaye ule wa watoto wao wasio wa kawaida, upesi hali duniani ziliharibika, na kutokeza uamuzi wa Mungu wa kuleta gharika ya duniani pote. Biblia yasema hivi: “[Yehova] akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. [Yehova] akasema, nitamfutilia mbali mwanadamu niliyemwumba usoni pa nchi.”—Mwa. 6:5, 7.
5 Hapa kuna somo kwetu sote, kwa watu wachanga na wazee. Ndilo hili: Yehova ana mahali kwa watumishi wake wa kweli, na wanapaswa kupashikilia ipasavyo. Ndiyo, ili kuwa wenye thamani kwa Yehova, ni lazima tujue mahali petu katika mpango wake na kupashikilia. Vijana, mahali penu panapowapasa ni mahali gani?
MAHALI PA VIJANA KATIKA MPANGO WA MUNGU
6. (a) Mahali pako panapokupasa ni mahali gani? (b) Ni kitu gani kinachotufanya kuwa wenye thamani kwa Mungu?
6 Kwa kuwahangaikia sana watu kwa upendo, Yehova alimtoa Mwanawe, Yesu Kristo, ili kutujulisha sisi mahali panapotupasa sisi sote. Kristo aliweka misingi ya jamii ya Kikristo. Leo jamii hiyo ya waabudu wa kweli ipo kati ya Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, mahali panapowapasa vijana na wazee vilevile ni katika jamii ya Kikristo. Walakini angalia kwamba: Si kuhudhuria tu mikutano ya Mashahidi wa Yehova au kushirikiana nao kunakomfanya mtu kuwa mwenye thamani kwa Yehova; badala yake ni uaminifu wa mtu kwa Yehova! ‘Kinachohitajiwa,’ lasema 1 Wakorintho 4:2, ‘ni mtu kuwa mwaminifu.’ Mtu mwaminifu mwenye umri wa miaka sita, au mwenye umri wa miaka 16, ni mwenye thamani zaidi kwa Yehova kuliko wale malaika wenye nguvu walioacha makao yao yaliyowahusu na kuwa wasiokamilika. Malaika hao hawana mahali po pote katika mpango wa Mungu tena.
7. Ni kazi gani ya maana ambayo sisi sote inatupasa tuifanye?
7 Kama sehemu ya jamii ya Kikristo, sisi sote—vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake—tuna kazi moja sote, kazi ya maana ya kufanya kwa uaminifu. Kazi hiyo ni kujulisha makusudi ya Baba yetu, kutumikia kama Mashahidi, kwa mwenendo wetu na kwa kuzungumza juu yake. Kwa kufanya hivyo ndivyo tu tunapokuwa katika mahali panapotupasa. Zaburi ya 148 yasema: “Msifuni [Yah] .[enyi] vijana waume, na wanawali, wazee na watoto; na walisifu jina la [Yehova].” Sana sana vijana wanasihiwa: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.”—Mhu. 12:1.
8, 9. (a) Vitu visivyo na uhai vinatimizaje kusudi lavyo katika uumbaji? (b) Sisi tutalitimizaje kusudi letu la kuwa hai?
8 Ulizo ni hili: Je! wewe uko katika mahali panapokupasa? Je! kwa kweli, wewe unampa Yehova sifa? Fungua Biblia yako katika Zaburi hiyo ya 148. Angalia vile mwito wa kumsifu Yehova unavyorudiwa-rudiwa mara nyingi. Kwani! jua, mwezi, nyota, miti, wanyama, ndege; ndiyo, viumbe vyote vya Mungu vinasihiwa vimsifu. Ebu fikiria namna vinavyofanya hivyo kwa njia ya ajabu. Kuchomoza kwa jua au kuchwa kwake likiangaza kwa rangi zenye kupendeza ni sifa ya ajabu kwa Muumba Mkuu wa jua. Nyota usiku kama almasi zenye kung’aa juu ya mawimbi ya bahari, huonyesha kwamba Muumba Mkuu ndiye mwenye vitu hivi vyote vya kupendeza. Hekima ya wanyama ya kisilika, miruko ya ndege wenye kuhama—twaweza kuendelea zaidi na zaidi kutaja namna vitu ambavyo Yehova ameumba vinavyomsifu. Walakini namna gani ninyi “vijana waume, na wanawali”—nyie wanawake vijana?
9 Miili yenu yenyewe yamletea Yehova sifa. Uzuri wake, wepesi pamoja na fahari ya miendo ya wanaume na wanawake vijana katika michezo huzungumza juu ya kazi ya Mbuni Stadi. Walakini wanadamu vilevile walikusudiwa wamsifu Yehova kwa mwendo wao wa unyofu wa maisha na kwa mambo mazuri wanayozungumza juu yake na kazi zake. Twapaswa kuwa na azimio kama la mtunga zaburi Daudi: “Kinywa changu kitazinena sifa za [Yehova].” Vilevile mwenendo wetu unapaswa kuwa mzuri. Wakristo wanasihiwa ‘waache mabaya, watende mema.’ (Zab. 145:12;1 Pet. 3:11) Je! wewe unamwonyesha Yehova kuthamini wema wake kwa kumsifu katika njia hizi? Je! wewe upo katika mahali pako panapokupasa?
NAFASI ZA KUMSIFU YEHOVA
10. Huenda nyakati nyingine vijana Wakristo wakaonaje juu ya mahali pao kundini?
10 Kwa kusikitisha, wanadamu wana maelekeo ya kuhangaikia cheo. Ndivyo ilivyokuwa kwa mitume wa Yesu; Yakobo na Yohana wakati mmoja hata walimwomba Yesu awape vyeo vyenye sifa kumfuata yeye katika ufalme wake. (Marko 10:35-37) Vijana wengine leo wana maoni kama hayo. Wanaona kwamba wanakosa mapendeleo au nafasi za kufanya mambo kundini. ‘Mimi ni kijana tu. Naweza kufanya nini?’ huenda wakauliza. Hata hivyo, ukweli ni kwamba, nyie vijana mna nafasi za kumsifu Yehova.
11. Ni nafasi zipi za pekee walizo nazo vijana za kumsifu Yehova?
11 Wakati mwingi wa mwaka, mnakuwa karibu na wanadarasa wenzenu, pamoja na waalimu wenu. Kwa hiyo, mwenendo wenu unakuwa kama kwamba uko jukwaani, ukionekana na watu wote. Jiulize mwenyewe: Je! mwenendo wangu unamletea Yehova sifa, Mungu ambaye watu wanitambulisha naye? Kumbuka kwamba, ama tabia yako itamletea sifa ama itamletea suto. Na hapa kuna jambo jingine la kufikiria: Je! mimi ninatumia kwa faida nafasi shuleni kuzungumza juu ya makusudi ya Yehova? Je! maoni yetu hayapaswi kuwa kama yale ya mtunga zaburi “Kinywa changu kitazinena sifa za [Yehova]”? (Zab. 145:21) Vijana wengi Wakristo wamesitawisha maoni ya kwamba shuleni ni “eneo” lao, na kwa hiyo wanakuwa macho kuona nafasi zile wanazoweza kutoa ushuhuda. Namna gani wewe?
12. (a) Sababu gani vijana wanaona vigumu kuwatolea ushuhuda wanafunzi wenzao pamoja na waalimu? (b) Ni jambo gani aliloona kijana moja?
12 Walakini vijana wengine wanaona vigumu kutoa ushuhuda kwa wanadarasa wenzao pamoja na waalimu wao. Sababu moja ni kwamba wanaona aibu kuonwa kama wanafunzi wa Biblia au watu wanaopendezwa katika kuzungumza juu ya Mungu. Kwa sababu hiyo, kijana mmoja kutoka California alijaribu kuwaficha wengine kwamba yeye alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kama unavyoweza kuwazia, kuogopa wengine wasijue hakukumpa furaha. Mwishowe kijana huyu alifikiri kwa uzito juu ya jambo hili. Alikuwa na hakika kwamba imani yake ndiyo ya kweli, kwa hiyo, kwa sababu gani aone aibu juu yake? Aliamua kuonyesha waziwazi dini yake, na kueleza wengine busara ya mafundisho ya Biblia katika nyakati zenye kufaa. Kama matokeo, si kwamba tu alikuwa mwenye furaha zaidi, bali pia aliheshimiwa na waalimu na wanadarasa wengi.
13, 14. Ni zipi nafasi nyingine za kutoa ushuhuda shuleni?
13 Kijana huyu alipata kuona kwamba alipokuwa shuleni alikuwa na nafasi nyingi za kujulisha wengine namna Mungu anavyoona mambo. Kwa mfano, huenda darasa likawa likizungumza juu ya vitabu vya mwandishi mwenye kujulikana sana ambaye aliandika juu ya kutokufa kwa nafsi, au habari nyingine ya Biblia inayofanana na hiyo. Katika ripoti yako iliyoandikwa, au katika mazungumzo ya darasa, unaweza kuonyesha kwa busara namna maoni ya mwandishi huyo yalivyo yakilinganishwa na yale yanayosemwa na Biblia juu ya habari hiyo. (Eze. 18:4, NW; Mhu. 9:5, 10) Vijana Mashahidi wamefanya jambo ilo hilo, nalo hilo limefungua njia ya mazungumzo zaidi ya Biblia shuleni.
14 Pindi fulani katika wakati wa masomo ya shule ya mtu, asili ya mwanadamu mara nyingi hutokea katika mazungumzo ya darasani na hii pia hutokeza nafasi nzuri ya kutoa ushuhuda. Unaweza kutumia habari katika kitabu Did Man Get Here by Evolution or by Creation? ukionyesha ushuhuda unaounga mkono uumbaji. Vijana Mashahidi wamefanya hivyo, na kama matokeo, wamewaangushia waalimu na wanadarasa wenzao vitabu vingi. Au, katika mojawapo la madarasa yenu mazungumzo ya matembezi ya vijana na wasichana, maoni juu ya ngono, dawa za kulevya, kulewa, au mazungumzo mengine kama hayo huenda yakatokea. Mara nyingi vijana wametumia kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako, ambacho huzungumza mambo hayo yote, nao waalimu pamoja na wanafunzi wenzao wamefurahia na kufaidika kutokana na kitabu hiki.
15-17. (a) Ni mambo gani ya kupendeza yaliyoonwa na vijana ambao wametoa ushuhuda shuleni? (b) Vijana Wakristo wanapaswa kujiuliza maulizo gani mawili?
15 Ushuhuda mzuri katika shule kuzunguka ulimwengu wote umetolewa na vijana Wakristo waaminifu na walio macho, wanaochukuwa hatua ya kwanza kufanya hivyo. Kwa mfano, kijana Mkristo anaandika hivi: “Wakati wa vipindi vya darasa visivyo na somo lo lote nilikuwa na nafasi nyingi za kutoa ushuhuda, sana sana wakati wa likizo. Kwa kuacha vitabu vya Biblia juu ya dawati (deski) yangu ambapo wengine wangeweza kuviona, wanafunzi wengi wenye kupendezwa walinijia. Tukio lenye kuthawabisha zaidi lahusu mwalimu wangu wa mambo ya kijamii. Nilikuwa nimemwangushia kitabu mmoja wa wanafunzi ‘wake, naye msichana huyo akawa anakisoma darasani siku moja wakati mwalimu huyo wa somo la mambo ya kijamii alipokiona na kumwuliza alipokuwa amekipata,” Matokeo yakawa nini? Muda si muda, mazungumzo ya kila siku ya Biblia yalikuwa yakifanywa pamoja na mwalimu huyo wakati wa chakula cha mchana. Mwishowe hesabu fulani ya wanafunzi walianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Naye mwalimu huyo akafanya maendeleo hata kufikia hatua ya kuwa Shahidi aliye wakf!
16 Katika kisa kingine, Shahidi kijana aliazimia kwamba atakuwa akimtolea mwalimu wake nakala za magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Baada ya siku chache akawa akimwuliza mwalimu kwa upole hivi: “Je! ulipendezwa na makala niliyokupa?” Mwanzoni, mwalimu alikuwa akipuza tu maulizo ya mwanafunzi wake. Hata hivyo, upesi upole wa kijana huyo wenye kuendelea ulimvutia. Mwalimu huyo aliwaza kwamba ikiwa alisisitiza kwamba mwanafunzi wake asikize na kujifunza juu ya masomo ya shule, sababu gani naye pia, asimlipe mwanafunzi huyu kwa kujifunza zaidi juu ya Biblia. Kama matokeo, mazungumzo mengi juu ya makala katika magazeti yakawa yakifanywa. Mwishowe, mwalimu huyo aliandikisha magazeti haya, akahudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme pamoja na jamaa yake, kisha akawa Shahidi aliyebatizwa!
17 Mambo yaliyoonwa kama hayo ni mengi sana. Ndiyo, maelfu ya watu wamepata maarifa ya kweli ya Mungu kupitia kwa ushuhuda uliotolewa na vijana shuleni. Kama kijana Mkristo, je! Wewe una ujasiri na unampenda Mungu hivi kwamba waweza kutetea Neno lake na kanuni zake? Na lililo la maana jinsi iyo hiyo: Je! wewe una nguvu za adili za kujiendesha kwa kupatana na matakwa ya Mungu yenye haki? Ikiwa ndivyo, basi umo kati ya kundi la vijana waliochaguliwa ulimwenguni pote ambao wanashikilia mahali pao panapowapasa. Wanatumia nafasi zao kumsifu Yehova.
18. Sababu gani sana sana vijana mara nyingi wanaweza kuwa na matokeo katika kutoa ushuhuda?
18 Sana sana mara nyingi vijana wanaweza kuwa na matokeo katika kutoa ushuhuda. Kwa mfano, unaweza kusimulia vizuri zaidi vijana wengine; inakuwa kama kwamba unazungumza ‘lugha’ yao. Vilevile, watu wengine wazima wanaelekea kusikiliza vijana, kama vile wanaume wazee katika hekalu huko Yerusalemu walivyomsikiliza Yesu mwenye umri wa miaka 12. (Luka 2:46, 47) Kwa hiyo, usidharau nafasi nzuri uliyo nayo ya kusaidia kumletea Yehova sifa. Ukimruhusu, Mungu anaweza kukutumia katika njia kubwa ili kutimiza kusudi lake la kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme duniani pote.—Mt. 24:14.
19. Vijana wanaweza kumleteaje Yehova sifa katika kundi la Kikristo?
19 Ndani ya kundi vilevile, vijana wanaweza kusaidia sana kumletea Yehova sifa. Ulimwenguni leo vijana wengi hutumia usemi mchafu, wanavalia vivi hivi na kukosa adabu njema. Kwa hiyo wakati ninyi vijana Wakristo mnapokuwa wapole, na kujipamba vizuri pamoja na kupendezwa kikweli na mambo ya kiroho, kwa kufaa wageni wanaohudhuria kwenye Jumba la Ufalme watavutiwa. Sana sana wanavutiwa wanapowasikia mkitoa hotuba za wanafunzi zilizotayarishwa vizuri, au wanapowasikiliza mkitoa maelezo yenye shauku na yenye kusadikisha kweli kweli; au wanapowaona mkifanya mambo kama vile kuangalia vikuza sauti, kusalimia wengine kabla na baada ya mikutano, kusaidia katika meza za vitabu na kusafisha jumba. Ndiyo, wageni wanaweza kuvutiwa sana na mifano ya vijana Wakristo hata wasukumwe kukata shauri hivi kuhusu kundi, “Mungu yu kati yenu bila shaka.”—1 Kor. 14:25.
20. Kwa hiyo ni maoni gani wasiyopaswa vijana kuwa nayo, nao wanaweza kuwa na uhakika gani?
20 Kwa hiyo usiwe na maoni yasiyofaa ‘Mimi ni kijana tu. Naweza kufanya nini?’ Unaweza kufanya mambo mengi sana ya kusaidia ndugu na dada zako, na ya kumletea Yehova sifa. Nawe unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ataona na kukuthawabisha. “Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.”—Ebr 6:10.
21. Ni mambo gani mengine tutakayochunguza katika makala inayofuata?
21 Ukweli ni kwamba, katika ulimwengu ulioharibika tabia ambamo twaishi si rahisi kumtumikia Yehova, hasa kwenu nyie vijana Wakristo. Kuna mikazo mingi inayoletwa ili kujaribu kuwalazimisha mwache mahali penu panapowapasa. Majaribu ni makubwa, na wakati ule ule, ni yenye hila nyingi. Kumbuka kwamba hata wengine wa malaika wa Mungu mbinguni walishawishwa wakaacha mahali pao palipowapasa, nao wamepoteza kibali ya Yehova milele. Nacho ni nini kilichowafanya wapaache? Tamaa za ngono zisizofaa. Kwa hiyo hatupaswi kushangaa kwamba majaribu makubwa leo ni yale ya ngono. Ebu na tuchunguze baadhi ya mikazo ya kilimwengu yenye kusudi la kuvunja imani ya vijana Wakristo.