Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 9/22 kur. 13-15
  • Kwa Nini Kuongea Juu ya Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Kuongea Juu ya Mungu?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu ya Kusitasita kwa Wengine
  • Wajibu wa Kikristo
  • Uwezayo Kutimiza
  • Mahali pa Vijana Katika Jamii ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Kuishi Maisha Maradufu —Kwa Nini Nisifanye Hivyo?
    Amkeni!—1993
  • Nifanye Nini Nikikutana na Mwanafunzi Mwenzangu?
    Amkeni!—2002
  • Yehova Hatasahau Kazi Yenu Enyi Vijana!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 9/22 kur. 13-15

Vijana Huuliza...

Kwa Nini Kuongea Juu ya Mungu?

“Kila mtu ana dini yake mwenyewe. Hupaswi kujaribu kulazimisha watu wengine wafuate Mungu wako.”—Racish mwenye miaka 14, Guyana.

“Mimi husitasita kuongea juu ya Mungu kwa sababu naona aibu juu ya dhihaka itakayofuata.”—Rohan mwenye miaka 17, Guyana.

“Twapaswa kuongea juu ya Mungu kwa sababu yeye ndiye Muumba wetu nasi tuna deni la uhai wetu kwake.”—Marco mwenye miaka 13, Ujerumani.

SIKILIZA kikundi cha vijana wakiongea na labda utakata shauri hili la kusikitisha: Hakika Mungu siye apendwaye kuzungumzwa sana miongoni mwa vijana, sana-sana. Taja tu michezo, mavazi, sinema za karibuni zaidi, au jinsia tofauti nawe kwa kawaida utafyatusha mazungumzo machangamfu. Ingawa hivyo, thubutu kumtaja Mungu, na mara hiyo waweza kusikia kimya-a-a-a.

Vijana fulani hawaamini kamwe kuna Mungu. Huenda wakasababu kwamba kwa kuwa hawawezi kumwona, lazima iwe hayuko—kuongea juu yake huonekana kuwa kupoteza wakati. Hata hivyo, bila shaka vijana wasioamini kuna Mungu ni wachache. Kulingana na uchunguzi wa maoni uliofanywa na Shirika la Gallup, karibu asilimia 95 ya vijana wa Marekani huamini kuna Mungu. Kwa kweli, Gallup lilikata shauri hivi: “Vijana walio wengi hawamwazii Mungu kuwa kanuni fulani isiyoeleweka na isiyo na utu, bali humwazia kuwa Mungu mwenye utu aonaye matendo yao na kuwathawabisha au kuwaadhibu kulingana na yalivyo.” Basi, mbona vijana wengi husitasita sana kuongea juu ya waaminicho?

Sababu ya Kusitasita kwa Wengine

Wengi yaonekana hufikiri tu si adabu kuongea mambo ya imani na kwamba yafaa zaidi mtu kujikalia mwenyewe na mawazo yake ya kidini. Vijana fulani yaonekana huaibishwa na lile wazo tu la kuzungumza juu ya Mungu. ‘Si raha kufanya hivyo,’ wao husababu.

Hata marika wako wawe na maoni gani, wewe una msimamo gani juu ya suala hili? Swali hili lafaa hasa ikiwa wewe umelelewa ukiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa nini? Kwa sababu kutoa ushuhuda, kuambia wengine juu ya Mungu, ndicho kiini cha imani hiyo!—Isaya 43:9, 10; Mathayo 24:14.

Hata hivyo, kwa kuvunjwa moyo na uhasama waukutao pindi kwa pindi, vijana fulani Mashahidi husitasita kujitia katika kazi ya kuhubiri peupe—au hushiriki kwa sababu ya kusihiwa tu na wazazi wao. Wengine hushiriki katika kazi hiyo lakini kwa siri hutumaini kwamba hakuna yeyote wa rafiki zao wa shule atawaona wakifanya hivyo. Shuleni, wengine hujaribu kuweka masadikisho yao ya kidini kuwa siri. Mara nyingi huwa hivyo kwa sababu wao huhofu dhihaka kutoka kwa wanadarasa wenzao. “Mimi niliogopa kuongea juu ya Mungu,” akiri Ryan mchanga, “kwa sababu washirika wangu walikuwa wakinibandika majina na sikuwa na moyo mkuu wa kuendeleza maongezi.”

Halafu kuna wale wasitasitao kwa sababu wao huhofu kwamba hawawezi kuishi kikamili kupatana na viwango vya Biblia. Wakihisi uvutio wa “tamaa za ujanani,” wao husababu ingekuwa vizuri zaidi wasijitambulishe kuwa Wakristo kwa sababu huenda wakatenda kosa fulani.—2 Timotheo 2:22.

Wengine hawaongei juu ya Mungu kwa sababu ya kuhisi tu kwamba si watoshelevu. Wilton mwenye miaka 19 alieleza hilo hivi: “Niliona ikiwa vigumu kuongea na wafanyakazi wenzangu juu ya Mungu kwa sababu nilihisi kwamba sikustahili kuyatetea mambo niliyosema juu yake. Nilihisi kwamba nikidaiwa nitetee imani zangu, singekuwa na jibu la kuridhisha.”

Wajibu wa Kikristo

Je, ingeweza kuwa umesitasita kuongea juu ya Mungu kwa sababu kama hizo? Ikiwa ndivyo, si wewe peke yako. Vijana wengine wamepambana na hisia hizohizo. Hata hivyo, wengi wamekuja kuthamini kwamba, yajapokuwako mambo yote ambayo yangeweza kuvunja mtu moyo asifanye hivyo, kuna sababu za kushurutisha kuongea na wengine juu ya Mungu. Ni nini baadhi yazo?

Marco mchanga, aliyetajwa mwanzoni, alieleza hilo vema aliposema kwamba Mungu ndiye “Muumba wetu nasi tuna deni la uhai wetu kwake.” (Ufunuo 4:11) Ndiyo, uhai ni zawadi yenye thamani kubwa. Mtunga-zaburi alisema hivi juu ya Mungu: “Kwako Wewe iko chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Kwa kuwa ulipokea zawadi hii, je, hupaswi kuonyesha shukrani kwa ajili yayo?

Njia moja ya kuonyesha shukrani ni kusifu tu Yehova Mungu wengine wakiwapo. Yeye ndiye Mwanzilishi wa jua, mwezi, mvua, hewa tupumuayo, na chakula tulacho. (Matendo 14:15-17) “Kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu ni kutoka juu,” akasema mwanafunzi Yakobo. (Yakobo 1:17, NW) Je, wewe humshukuru Mungu kwa zawadi hizi? (Wakolosai 3:15) Kuna njia gani ya kuonyesha shukrani yako iliyo nzuri kuliko kuongea juu ya Mungu?—Luka 6:45.

Ingawa hivyo, kwa kweli Mungu hutuamuru tuseme juu yake. Mwana wake, Yesu Kristo, aliwaamuru Wakristo hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Vijana hawaondolewi wasihusike katika daraka la kushiriki katika kazi hii. Aamuru hivi mtunga-zaburi: “Msifuni BWANA . . . vijana waume, na wanawali, wazee, na watoto; na walisifu jina la BWANA, maana jina lake peke yake limetukuka; adhama yake i juu ya nchi na mbingu.” (Zaburi 148:7, 12, 13) Lakini huhitaji kuona mgawo huu kuwa mzigo. Kwa kweli, ni pendeleo—wewe waweza kwa kweli kuwa mmoja wa “wafanya kazi pamoja na Mungu.”—1 Wakorintho 3:9.

Namna gani ikiwa wahisi tu kuwa hustahili? Nabii Yeremia alikuwa na hisia kama hizo nyakati za Biblia. “Aa, Bwana MUNGU!” akasema. “Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” Itikio la Yehova? “Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru.” (Yeremia 1:6, 7) Ndivyo Yeremia alivyofanya hasa kwa msaada wa Yehova kwa miaka 40!

Vilevile kwa Wakristo leo, “utoshelevu wetu watoka kwa Mungu.” (2 Wakorintho 3:5) Hata ikiwa kwa asili wewe ni ile namna ya wenye haya, wenye kujitenga kando, Mungu aweza kukusaidia uwe na moyo mkuu wa kusema. Ndani ya kutaniko la Kikristo mna maandalizi yawezayo kukusaidia uwe ‘mtoshelevu’ zaidi ukiwa mwalimu wa Neno la Mungu. Ikiwa wahisi wahitaji usaidizi fulani wa kibinafsi, mbona usiongee na mmoja wa waangalizi wa kutaniko? Huenda uhitaji wako ukawa ni kusitawisha tu programu ya funzo la kibinafsi la Biblia au kufanya kazi pamoja na mtu fulani mwenye uzoefu zaidi.

Uwezayo Kutimiza

Kuongea juu ya Mungu kwaweza kukupa hisi halisi ya kutimiza mambo. Kwanza, wengi wa marika wako wanatafuta majibu ya matatizo ya maisha, wakikaribia kupaaza sauti kulilia msaada. Hawana mwelekezo na hawana mwono safi juu ya wakati ujao. Wao hujiuliza, ‘Kwa nini tupo hapa? Tunaelekea wapi? Kwa nini ulimwengu umejawa sana na taabu?’ Wewe uliye Mkristo, unayo majibu, na yaelekea umo katika hali bora zaidi ya kuwapelekea marika wako ujuzi huo. Wao waweza kuelewana vizuri nawe na labda wangeona ni afadhali kuongea na mtu wa umri wao wenyewe kuliko na mtu mzima.

Ni kweli kwamba nyakati fulani utakataliwa. Lakini huenda pia ukapata watu mmoja-mmoja wenye kuupokea ujumbe wa Biblia. Shahidi mmoja wa kike mchanga aliketi ndani ya basi akisoma nakala yake ya kibinafsi ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.a Mvulana aliyeketi karibu naye alianza kuambatana naye kusoma. “Hiki ni kitabu maridadi!” mvulana huyo kapaaza sauti. “Kitabu hiki chaongea juu ya Mungu. Watu walio wengi hawapendezwi na dini.” Yule Shahidi mchanga alitumia hii kuwa fursa ya kufanya mazungumzo ya kina kirefu juu ya habari ya jina la Mungu.

Ni kweli kwamba ujitambulishapo kuwa Mkristo, una wajibu wa kujiendesha kama mmoja. (1 Petro 2:12) Lakini mwenendo mzuri wa Kikristo utaongezea tu ustahili wa ujumbe wako. Fikiria ono la kijana mmoja jina lake Eric. Yeye alivutiwa na mwenendo mzuri wa vijana Mashahidi katika shule yake. Hii iliamsha kupendezwa kwake ajifunze mengi zaidi juu ya Mungu. Funzo la Biblia lilianzishwa pamoja naye, na leo yeye ni Mkristo aliyebatizwa anayetumikia kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova katika New York.

Kuongea juu ya Mungu kwaweza kukusaidia wewe pia! Kwaweza kuwa ulinzi. Waandamani wako wajuapo kwamba wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, wengi watakustahi. Huenda wakapunguza elekeo la kukusonga ujitie katika kutenda makosa watambuapo kwamba una viwango vya juu na wajue kwamba utaelekea kujibu kwa kuwapa ushahidi.

Bila shaka, hii haimaanishi kwamba kila wakati ufunguapo kinywa chako ni lazima unukuu maandiko. Bado utapendezwa na michezo, mavazi, au muziki na utataka kuongea juu ya mambo hayo mara kwa mara. Lakini kumbuka: “Kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.” (Mathayo 12:34) Ikiwa kupenda Mungu kumo katika moyo wako, utataka kiasili kuongea juu yake. Katika toleo la wakati ujao, tutazungumzia njia fulani ambazo waweza kufanya hivyo kwa matokeo.

[Maelezo ya Chini]

a Kimechapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, wewe huaibika kuonwa na wanashule wenzako uwapo katika kazi ya kuhubiri peupe?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki