Vijana Huuliza...
Kuishi Maisha Maradufu —Kwa Nini Nisifanye Hivyo?
“Nilikuwa nikiishi maisha maradufu—aina moja nikiwa na rafiki zangu Wakristo na nyingine nikiwa na rafiki zangu wa shuleni.
Hali ya mwanamke mchanga aliyenukuliwa hapo juu si ya pekee. Lakini ni nini kinachomaanishwa na “kuishi maisha maradufu”? Ruth Bell, mtungaji wa kitabu Changing Bodies, Changing Lives, alifafanua zoea hili kuwa “lolote unalofanya ambalo huwaambii wazazi wako juu yalo.”[2]
Mtungaji huyu alihoji vijana wengi sana na akaripoti: “Matineja wengi walisema walikuwa na mambo yaliyoendelea katika maisha yao ambayo hata hawangeweza kuwaambia wazazi wao. Mambo yaliyokuwa ya kawaida zaidi ya siri yalikuwa juu ya ngono na dawa za kulevya na kunywa, lakini watu pia walitaja mambo kama vile kuchelewa nje, na matembezi na watu wasiowajua, kuepa shule, kupigana, na kwenda na marafiki ambao wazazi hawawataki.”[2a]
Inasikitisha kwamba, hata vijana fulani waliolelewa na wazazi Wakristo huficha jinsi walivyo kwa wazazi na wengine.a (Linganisha Zaburi 26:4.) Wakiwa na wazazi na waamini wenzao, vijana hawa huonekana kuwa wanyoofu na wenye kuhofu Mungu. Lakini wakiwa mbali nao, wanajiendesha kana kwamba ni watu tofauti kabisa.
Basi ni nini huchochea kijana kuwa na maisha maradufu?
Uvutio wa Kujitegemea
Biblia husema kwamba hatimaye “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Kwa hiyo basi, ni jambo la asili kwako kutaka kukua, kufikiri mwenyewe, na kufanya maamuzi yako mwenyewe. Tatizo ni kwamba huenda usiwe tayari kwa utu-mzima. Ukikosa maarifa ya maisha, ungali wahitaji utegemezo wa wazazi wa kimungu.—Mithali 1:8.
Vijana wengi hukataa ukweli huu. Kulingana na kitabu How to Survive Your Child’s Rebellious Teens, vijana wengi ni kama wanataka “kuonyesha nguvu zao zinazokua, wakijaribu nguvu zao mpya zinazokua, na kutangaza uhuru wao.”[3] Wazazi wanapokosa kuwapa ruhusa ya kufanya mambo wanayoona kuwa yasiyo ya hekima—au mabaya—vijana wengine huasi. Nao huenda wasiwe na majuto kwa usaliti huo. Msichana mmoja tineja asema: “Nahisi vizuri kufanya mambo ambayo [wazazi wangu] hawajui kuwa nayafanya kwa sababu mimi huhisi kuwa wa maana. Nina maisha tofauti na yao na sifikiri kama kweli wanajua hilo kamwe. . . . Hawawezi kuamini nusu ya mambo ninayofanya.”[4]
‘Wazazi Wangu ni Wenye Kushurutisha Sana’
Hata hivyo, kwa nini hata baadhi ya vijana wanaopokea malezi mazuri ya Kikristo hujiingiza katika makosa ya siri? Amkeni! lilipouliza kikundi cha vijana swali hili, msichana mmoja tineja alijibu: “Wao hukasirikia wazazi wao. Wao hutaka kulipiza kwa sababu ya kuwatolea masharti.”[5] Hakuna shaka, Ukristo ni njia ya maisha yenye masharti. Yesu alisema: “Mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani.” (Mathayo 7:14) Ukitaka kupokea zawadi ya Mungu ya uhai wa milele, huwezi kufanya baadhi ya mambo yaitwayo eti raha ambayo vijana wengine hufanya. Kwa kielelezo, karamu zisizofaa, karamu za ulevi, ngono ya kabla ya ndoa, mwenendo mlegevu, yote hayo ni mambo ambayo yamekatazwa katika Biblia.—Wagalatia 5:19-21.
Kisha kuna ukweli kwamba huenda wazazi wengine wakaonekana kuwa wenye kushurutisha kupita kiasi. “Hatuwezi kuona sinema yoyote,” akalalamika msichana mchanga aitwaye Kim. “Pia nilikuwa nimepunguza sana wakati niliotumia kusikiliza muziki, nami nilijaribu kuwa mteuzi. Lakini baba yangu ametukataza kusikiliza karibu muziki wowote! Tumeruhusiwa tu kusikiliza muziki bora na rekodi za jazz.”[6] Wakikabiliwa na yale wanayoona kuwa masharti ya kupita kiasi, vijana wengine huanza kuonea wivu uhuru wanaofurahia marika zao.
Tamaa ya Kukubaliwa na Wengine
Mwanamke mchanga aitwaye Tammy akumbuka: “Nilianza kwa kutumia lugha chafu shuleni. Ilinifanya nihisi kwamba nilikuwa kama vijana wengine shuleni. Baada ya hapo nikaanza kuvuta sigareti. Nilikuwa pia nikinywa kileo mpaka nilewe. Kisha nikaanza kuwa na marafiki wavulana—kisirisiri kwa sababu wazazi wangu walikuwa wenye kushurutisha na hawakuniruhusu niwe na miadi.”[7]
Mvulana tineja aitwaye Pete alikuwa na jambo kama hilohilo: “Nililelewa nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Lakini niliogopa sana kutaniwa, kwa hiyo sikuzote nilikuwa nikijiweka na hali ya umati. Nilijaribu nipendwe na wengine. Nilikuwa nikisema uongo na kutoa udhuru kwa nini sikupokea zawadi za sikukuu.”b Pete alipoanza kuridhiana kidogo-kidogo, haikuwa muda mrefu kabla hajajiingiza katika mwenendo mbaya zaidi.[8]
“Mashirika Mabaya”—Wapi?
Mambo hayo yaliyoonwa yaonyesha ukweli wa maneno ya mtume Mkristo Paulo: “Mazungumzo [mashirika, NW] mabaya huharibu tabia njema.” (1 Wakorintho 15:33) Kwa hiyo ukishirikiana na vijana wasioheshimu viwango vyako na maadili yenye msingi wa Biblia, unawe-za kwa urahisi kuvutwa katika mtindo-maisha wao. Hata hivyo, kwa kupendeza mtume Paulo hakuwa akisema hasa juu ya kushirikiana na wasioamini alipotoa onyo hilo. Alikuwa anaonya juu ya kushirikiana na wale waliomo katika kutaniko la Kikristo wanaoshindwa kushikilia fundisho la Kikristo. (1 Wakorintho 15:12) Vivyo hivyo leo, huenda kukawa vijana wanaoshirikiana na kutaniko ambao hawashikilii au wasio na sifa inayofaa ya maisha ya Kikristo. Hao wanaweza kuweka mbano wa hila kwako ili wakuongoze uishi maisha maradufu.
Fikiria tena, Tammy, anayekubali kwamba wazazi wake ni wenye “upendo sana.” Yeye amweleza baba yake kuwa “karibu kuchemkwa na bidii, sikuzote akiongea juu ya jinsi Yehova anavyotujali sisi.” Yeye hata hutumikia kwenye kutaniko akiwa mzee. Basi, aliongozwaje vibaya? “Mashirika mabaya ndani ya kutaniko,” akasema. “Wengine walikuwa wakiniambia juu ya raha waliyokuwa nayo kwenye karamu mbalimbali na juu ya vile walivyokunywa vileo. Au wangeongea juu ya marafiki wavulana na jinsi walivyoenda kucheza dansi baada ya mikutano ya kutaniko.”[9]
Kuuepuka Msiba
Usiukubali mwenendo huo usiofaa wa vijana kwa kusababu kwamba, ‘Ni sehemu tu ya kukua’ au, ‘Vijana wote huwaficha wazazi wao mambo.’ Angalia onyo ambalo Mungu hutolea vijana kwenye Mhubiri 11:9, 10: “Wewe, kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako, ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako; lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote Mungu atakuleta hukumuni. Kwa hiyo ondoa majonzi moyoni mwako, nawe uuondoe ubaya mwilini mwako; kwa maana ujana ni ubatili, na utu uzima pia.”
Kuishi maisha maradufu huenda kukaonekana kuwa raha. Lakini hatimaye ni mtego wenye kufisha. (Linganisha Zaburi 9:16.) Matendo ya kutotii huongoza bila kuepukika kwenye matendo mabaya zaidi ya kufanya makosa. Kwa kielelezo kijana Pete, alikuwa tayari anajiingiza katika mwenendo mpotovu wa ngono alipotoka nyumbani akiwa na umri wa miaka 17. Akiwa na umri wa miaka 18, Pete alikuwa ametiwa jela kwa unyan’ganyi wa mabavu.[10]
Mara nyingi vijana wengi huelekea kuepuka adhabu kwa mwenendo wao mbaya. Unaweza kuanza kuhisi kwa urahisi kama mwandikaji wa Biblia Asafu, aliyekiri hivi: “Nalikuwa mwenye wivu . . . Nilipoona kuwa mambo yalikuwa mazuri kwa waovu. Hawaumii; wao ni wenye nguvu na afya. Hawaumii kama vile watu wengine.” Lakini ulioonekana kuwa usalama wa waovu ulithibitika kuwa madanganyo mabaya zaidi. Asafu akamalizia “[Mungu] atawaweka penye utelezi naye atawafanya waanguke penye uharibifu!” (Zaburi 73:3-5, 18, Today’s English Version)[11] Basi ni kwa sababu nzuri kwamba Biblia huonya: “Moyo wako usiwahusudu wenye dhambi; bali mche BWANA [Yehova, NW] mchana kutwa.”—Mithali 23:17.
Vipi juu ya wazo la kwamba kutotii wazazi humsaidia kijana akue na aje kujitegemea? Hilo huwa kinyume cha shauri la Biblia la kusikiliza wazazi wako. (Mithali 23:22) Kwa kweli, mwenendo mpumbavu au wa kutojali utachelewesha ukuzi wako wa kihisiamoyo na wa kiroho. Badala ya hivyo, ni kwa kutumia kanuni za Biblia ndipo unapokuwa “mtu mkamilifu” ukiwa na “cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo.”—Waefeso 4:13.
Ni kweli, wazazi wengine huenda wakaonekana kuwa wenye kushurutisha kupita kiasi. Lakini je, si kwa sababu ya upendo wenye kina kirefu kwako na tamaa ya kukulinda wewe? Kwa hiyo ikiwa unahisi kwamba wazazi wako wahitaji kupunguza sharti kidogo, kwa nini usiongee nao—badala ya kuasi kisiri?c Kuasi kutaleta huzuni kuu kwao, kwako, na zaidi ya wote, kwa Yehova Mungu mwenyewe.—Mithali 10:1; 27:11.
Hata hivyo, vipi ikiwa tayari umeanza kuishi maisha maradufu? Kuna njia yoyote ya kuachana nayo? Makala zijazo zitazungumzia maswali haya.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Vijana—Lindeni Dhidi ya Kuendesha Maisha Maradufu,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1988.
b Kwa ajili ya mazungumzo juu ya msimamo wa Mashahidi wa Yehova juu ya sikukuu za kidini, ona broshua Shule na Mashahidi wa Yehova, iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
c Ona sura ya 3 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Je! wewe huishi maisha maradufu?