Vijana Huuliza...
Kwa Nini Napaswa Kutii Wazazi Wangu?
STAN alilelewa na wazazi wahofu-Mungu. Lakini katika umri wa miaka 16 aliasi. Stan aeleza hivi: “Nilitaka kukutana na watu na kukubaliwa nao. Nilitaka kuwa na vitu vyote walivyo navyo watu wengine.” Wazo la Stan la kutimiza miradi hii lilikuwa kuwa mchuuzi wa dawa za kulevya. Kama itazamiwavyo, alilazimika kusema uongo juu ya nyendo zake na juu ya fedha zote alizokuwa akileta nyumbani. “Dhamiri yangu ilikuwa imekufa,” akumbuka Stan.
John alibatizwa kuwa Mkristo akiwa na miaka 11. “Lakini kwa hakika ile kweli haikuwa moyoni mwangu,” yeye akiri. “Nilifanya hilo kwa sababu familia yangu ilinitarajia nifanye. Nilipofika shule ya sekondari, nilianza kuwa mtu wa fujo. Muziki wa roki pia uliniathiri vibaya. Niliingilia mchezo wa kubebwa na mawimbi ya maji na nikaanza kushinda sana ufuoni pamoja na vijana wasioongozwa na kanuni za Biblia. Kulikuwako dawa nyingi za kulevya.” Punde si punde akawa amehama nyumba ya wazazi wake na kuanza mtindo-maisha uliokuwa dhidi ya kila kitu alichokuwa amefundishwa.
Sababu Ifanyayo Waasi
Ni jambo la kawaida kwa vijana kujaribu kutahini mipaka yao na kusitawisha ujitegemeo wa kadiri fulani. Lakini mwenendo wa uasi, wa tabia za kushangaza, na wa kujiangamiza ni kitu tofauti kabisa. Ni nini huuchochea? Sababu ni nyingi na zatofautiana. “Wakati wewe ni kijana,” aeleza John, “unatafuta ufurahisho. Wataka kujistarehesha.” Hata hivyo, kwa sababu vijana hawana maarifa maishani, wao hawatumii uamuzi mzuri sana sikuzote. (Waebrania 5:14) Kwa hiyo wazazi wenye kufikiri vizuri huweka vizuizi vyenye usababu wa kiasi juu ya watoto wao—vizuilio ambavyo vijana fulani huchukizwa navyo kwa ukali sana.
Kwa kusikitisha, vijana fulani hata wameyapa kisogo mazoezi waliyopokea kutoka kwa wazazi wahofu-Mungu. (Waefeso 6:1-4) Yesu alisema kwamba Ukristo ungekuwa njia ya maisha iliyo ‘nyembamba’ na ‘iliyosonga.’ (Mathayo 7:13, 14) Kwa hiyo mara nyingi vijana Wakristo hawawezi kufanya mambo wafanyayo wanashule wenzao. Walio wengi hukubali kwa urahisi kufuata vizuizi, wakithamini kwamba sheria za Mungu kwa kweli si mzigo. (1 Yohana 5:3) Kwa kweli, sheria hizi hulinda vijana na matatizo kama vile mimba za nje ya kifungo cha ndoa, utumizi mbaya wa dawa za kulevya, na maradhi yapitishwayo kingono. (1 Wakorintho 6:9, 10) Lakini vijana fulani hukataa kuchukua mambo hivyo; wao huhisi kwamba sheria za Biblia husonga mtindo wao.
Uchukizo huenda ukawa mwingi hasa ikiwa kijana ahisi wazazi wake ni wagumu kupita kiasi kwa habari ya nidhamu, tafrija, na utumbuizo. “Mimi nafikiri wazazi wangu ni wagumu mno,” aliomboleza msichana mchanga mmoja. Kweli, yaweza kutamausha usiporuhusiwa kufanya mambo ambayo wazazi wengine Wakristo huyaruhusu. (Wakolosai 3:21) Vijana fulani huonyesha mivurugiko yao ya hisia kwa kutotii.
Kwa upande ule mwingine, vijana fulani huenda kombo kwa sababu wazazi wao hawaonyeshi staha yoyote ile kwa kanuni za kimungu. “Baba alikuwa mraibu wa alkoholi,” akumbuka John. “Yeye na mama walikuwa wakibishana kwa sababu alikunywa mno. Tulihama mara kadhaa ili tumwepuke.” Waraibu wa alkoholi na watumiaji wengine wa dutu za uraibu hawawezi kutunza mahitaji ya watoto wao vya kutosha. Katika makao ya jinsi hiyo, huenda ikawa ni kawaida ya kila siku kijana kutandikwa kwa maneno na kuaibishwa.
Vijana wengine huasi kwa sababu wazazi wao hutenda kwa njia ionyeshayo ni kama wamewaachilia au wamewapuuza. Huenda uasi ukaonekana kama njia ya kuvuta uangalifu wa wazazi wao—au kuwaumiza. “Kwa kadiri niwezavyo kukumbuka ya nyuma, wazazi wangu hawakuonekana kamwe kuwapo,” asema msichana mchanga jina lake Taylor atokaye katika familia tajiri. “Waona, ni mimi tu niliyekuwa mtoto, na kwa kuwa wazazi wangu hawakuwapo muda mwingi vya kutosha, sikuzote walikuwa wakiniachia fedha nyingi.” Kwa kukosa usimamizi, Taylor alianza kuhudhuria klabu za usiku na kulewa. Msichana huyo alipokamatwa kwa kuendesha akiwa mlevi ndipo wazazi wake walipong’amua kwamba alikuwa na tatizo.
Kwa kuongezea, kuna ile hali iliyoonyeshwa na mtume Paulo alipouliza kikundi cha Wakristo hivi: “Mlikuwa mkipiga mbio vizuri; ni nani aliyewazuia msiitii kweli?” (Wagalatia 5:7) Mara nyingi ushirika mbaya ndio tatizo. (1 Wakorintho 15:33, linganisha NW.) “Mimi nilihusika na umati usiofaa,” asema tineja jina lake Elizabeth. Yeye akiri kwamba kutokana na msongo wa marika, ‘alianza kuvuta sigareti na kutumia vibaya dawa za kulevya.’ Aongezea hivi: “Uasherati ulikuwa kitu cha kila siku.”
Sababu Ifanyayo Uasi Uwe wa Kipumbavu
Labda wewe pia wajikuta katika hali ionekanayo kuwa ya kuvuruga hisia—au hata yenye uonevu. Huenda ikaonekana yashawishi kuwakaidi wazazi wako na kufanya utakalo kulifanya. Lakini kama vile mwanadamu mwadilifu Ayubu alivyoonywa, “jihadhari isije hasira kali ikakuvuta kwa chambo uingie katika [vitendo] vya inda. Jikinge usije ukageukia lililo la kuumiza.”—Ayubu 36:18-21, NW.
Mwenendo wenye inda, wa tabia za kushtusha huenda ukapata tendo-mwitikio kutoka kwa wazazi wako, lakini halielekei litakuwa la kupendeza. Vyovyote vile, labda watakuweka chini ya vizuizi zaidi. Zaidi ya hilo, mwenendo wenye kuumiza utasababishia wazazi wako maumivu makubwa. (Mithali 10:1) Je, hilo ni jambo la upendo? Je, kweli litaboresha hali yako? Mfikio wenye akili zaidi ni kuongea nao ikiwa wahisi una malalamiko halali.a Huenda ikawa hasa wana nia ya kufanya marekebisho fulani katika njia wakutendeayo.
Jambo jingine la kufikiria ni tokeo ambalo matendo yako huenda yakawa nayo juu ya Mungu. ‘Juu ya Mungu?’ huenda ukauliza. Ndiyo, kwa sababu kuasi dhidi ya wazazi wako ni sawa na kuasi dhidi ya Mungu mwenyewe, kwa kuwa ndiye akuamuruye uwaheshimu wazazi wako. (Waefeso 6:2) Kutotii huko hufanya Mungu ahisije? Biblia husema hivi juu ya taifa la Israeli: “Ni mara nyingi kama nini wao walikuwa wakiasi dhidi yake nyikani.” Tokeo likiwa nini? “Wao walikuwa wakimfanya [Mungu] ahisi umizo!” (Zaburi 78:40, NW) Ni kweli, huenda ukaudhika na wazazi wako, ukihisi kwamba wao ni wazuilivu mno. Lakini je, wewe kweli wataka kuuletea umivu moyo wa Yehova Mungu—yule akupendaye na atakaye uishi milele?—Yohana 17:3; 1 Timotheo 2:4.
Gharama Kubwa ya “Uhuru”
Basi, sisi twahitaji kumsikiliza Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo tukiwa na sababu njema. Usipumbazwe na ahadi bandia za “uhuru.” (Linganisha 2 Petro 2:19.) Huenda ikaonekana kwamba vijana fulani huponyoka wakiwa na mwenendo mbaya. Lakini mtunga-zaburi alionya hivi: “Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya, usiwahusudu wafanyao ubatili. Maana kama majani watakatika mara, kama miche mibichi watanyauka.” (Zaburi 37:1, 2) Mara nyingi vijana ambao huasi hulipa bei kubwa kwa ule ambao huitwa uhuru wao eti. Biblia yasema hivi kwenye Wagalatia 6:7: “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.”
Mfikirie Stan, aliyetajwa pale mwanzoni. Sawa na vile alivyotumaini, yeye alikuja kupendwa na rafiki zake wasio murua. “Nilihisi nimekubaliwa,” yeye akumbuka. Hata hivyo, muda si muda mambo yalianza kwenda mrama. Asema: “Nimepata kupigwa risasi, nikafungwa jela, na sasa ninaenda gerezani. Na lile tu niwezalo kujiuliza ni kwamba, ‘Je, ilistahiki kupata hayo?’”
Namna gani utafutaji wa “uhuru” wa John? Baada ya kukamatwa kwa kuwa na dawa za kulevya, aliondoshwa katika kutaniko la Kikristo. Kuanzia hapo alididimia katika mwenendo wa kupotoka hata zaidi. “Niliiba magari ili nipate fedha,” John aungama. “Nilikuwa mjeuri sana.” John alipata fedha nyingi kutokana na utendaji wake mbalimbali wa uhalifu. Lakini akumbuka hivi: “Nilizifyeka fyu. Tulivuta kasumba weee.” Na wakati John hakuwa akipigana, akiiba, au akilewa, alikuwa akiwakimbia polisi. “Nimekamatwa karibu mara 50. Kwa kawaida walishindwa kuthibitisha mashtaka yoyote, lakini safari moja nilionja mwaka mzima jela.” Ndiyo, mbali na kuwa mwanamume huru, John alijikuta ametopezwa katika “fumbo za Shetani.”—Ufunuo 2:24.
Yaweza kusemwa vivyo hivyo kuhusu Elizabeth. Kusakatika kwake na rafiki za kilimwengu kulimtusha jela hatimaye. Msichana huyo aungama hivi: “Hata nilipata mimba—na kwa sababu ya utumizi wangu wa dawa za kulevya nilifiwa na kitoto hicho. Dawa za kulevya zilikuwa maisha yangu—ilionekana niliishi kwa ajili ya duru ile ifuatayo ya kusisimuliwa na dawa za kulevya. Hatimaye nilipoteza kijumba changu. Singeweza kwenda nyumbani, nami niliona aibu hata kumwomba Yehova msaada.”
Vielelezo vingi kama hivyo vingeweza kutolewa vya vijana ambao wamekataa kanuni za kimungu kumbe wakaja kupatwa na masaibu tu. Biblia huonya hivi: “Ile uifikiriyo kuwa barabara ifaayo huenda ikaongoza kwenye kifo.” (Mithali 14:12, Today’s English Version) Basi, jambo la hekima kufanya ni kujaribu kupatana na wazazi wako, kuzungumzia—badala ya kuasi dhidi ya—vizuizi vyovyote uhisivyo kuwa vya kudhulumu.
Ingawa hivyo, namna gani juu ya vijana ambao habari hii imewafikia kwa kuchelewa mno, vijana ambao tayari wajikuta wameingia sana katika mwenendo wenye makosa? Je, kuna njia yoyote wawezayo kunyoosha mambo na wazazi wao—na Mungu? Makala yetu inayokuja katika toleo linalofuata itapeleleza maswali haya.
[Maelezo ya Chini]
a Makala kadhaa zimeandaa habari zenye msaada kuhusiana na mambo haya. Ona, kwa kielelezo, zile makala za “Vijana Huuliza . . .” katika matoleo yetu ya Amkeni! Januari 8, 1985, Agosti 8, 1992, na Novemba 8, 1992 (ya Kiingereza).
[Picha katika ukurasa wa 26]
Kuasi dhidi ya wazazi wako huenda kukakupa “uhuru” mwingi zaidi, lakini je, umeyafikiria matokeo?