Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 1/22 kur. 18-20
  • Naweza Kuachaje Maisha Maradufu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kuachaje Maisha Maradufu?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Toba—Hatua ya Kwanza
  • Kuwaambia Wazazi Wako
  • Kubadili Mashirika Yako
  • Vijana Lindeni Dhidi ya Kuendesha Maisha Maradufu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Kuishi Maisha Maradufu —Kwa Nini Nisifanye Hivyo?
    Amkeni!—1993
  • Maisha Maradufu Ni Nani Apaswa Kujua?
    Amkeni!—1994
  • Kuwa na Nyuso Mbili—Kuna Ubaya Gani?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 1/22 kur. 18-20

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuachaje Maisha Maradufu?

“Nilipuuza kila kitu walichosema wazazi wangu,” akiri Ann.a “Nilikuwa mkaidi na kuanza kuwadanganya. Ningewaambia kwamba naenda dukani, kumbe kwa kweli nilikuwa nikienda kukutana na mvulana fulani.”[1]

ANN alikuwa akiishi maisha maradufu, na upesi alikuwa akipuuza wazazi wake na vilevile dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. Waona, Ann alikuwa akifanya ngono kisiri na mvulana rafiki yake. Yeye akumbuka hivi: “Nilijaribu kumsahau Yehova kabisa.” Hata hivyo, upesi alitambua ukweli wa mambo kwamba ‘chochote wapandacho watu, ndicho watakachovuna.’ (Wagalatia 6:7) Ann alipata mimba. “Nampenda mtoto wangu kwa moyo wangu wote,” yeye asema, “lakini mtu asithubutu kupitia mambo haya. Si ukiwa mseja. Si ukiwa peke yako.”[2]

Je! umenaswa kwa njia fulani katika maisha maradufu—ukificha utu wako halisi kutoka kwa wazazi wako na Wakristo wenzako? Labda unazurura-zurura tu na baadhi ya wanafunzi walio marafiki ambao wewe unajua wazazi wako hawapendi. Au labda umeangukia tabia mbaya zaidi, kama vile kuvuta sigareti, utumizi mbaya wa dawa za kulevya, au ngono ya kabla ya ndoa. Kwa vyovyote vile, kama ilivyokuwa na Ann, matokeo mabaya zaidi yatakuja kutokea kwa muda wa wakati.b

Hata hivyo, baadhi ya vijana huyapuuza mambo hayo ya hakika na kuendelea na mwendo wao wa ukaidi. Wao ni kama mtu anayejiangalia katika kioo na ‘kusahau jinsi alivyo.’ (Yakobo 1:23, 24) Twatumaini kwamba wewe ni wa aina tofauti. Labda umeanza kujichunguza sana—na hupendi kile uonacho. Wataka kubadilika. Waona uhitaji wa kubadilika. Swali ni hili, utabadilikaje?

Toba—Hatua ya Kwanza

Kwanza, ni lazima ufanye uamuzi wa dhati wa kubadilika. Matendo 3:19 yahimiza hivi: “Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana [Yehova, NW].” Hata hivyo, toba ni zaidi ya kuwa jambo la akilini tu. Kutubu kwamaanisha “kughairi, majuto, au masikitiko, kwa yale ambayo mtu amefanya.”[3] Mwandikaji wa Biblia Yakobo alihimiza hivi: “Huzunikeni na kuomboleza na kulia. Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza, na furaha yenu kuwa hamu. Jidhilini mbele za Bwana [Yehova, NW] naye atawakuza.” (Yakobo 4:9, 10) Waweza kusikitikaje kwa tendo ambalo kufikia sasa umekuwa ukifurahia? Fikiria jinsi tendo hilo lilivyo baya. Fikiria jinsi limehuzunisha Mungu. Fikiria matatizo ambayo mwendo wako umekuletea na uwongo ambao umelazimika kusema ili kuficha tendo hilo. Jikumbushe kwamba Mungu achukia udanganyi! (Zaburi 5:6) Kutafakari juu ya mambo hayo kwaweza kukusaidia ukatae mwenendo mbaya akilini na moyoni.

Kuhisi tu vibaya juu ya tendo unalofanya hakutoshi. Kijana mmoja aitwaye Robert, aliyejihusisha kisiri na matumizi ya dawa za kulevya, akiri hivi: “Nilikuwa na huzuni. Nilijua mema na mabaya. Na bado niliendelea kuishi maisha maradufu.”[4] Hivyo, tendo lenye moyo mkuu lahitajiwa! Katika 2 Mambo ya Nyakati 7:14, Mungu alisema kwamba kama watenda dhambi “watajinyenyekesha, na kuomba, na ku[m]tafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, [yeye mwenyewe atasikia] toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao.”

‘Kutafuta uso wa Mungu’ kwamaanisha kumwendea kwa sala, kuungama dhambi yako, na kuomba msamaha. Huenda jambo hilo lisiwe rahisi, lakini bila shaka utahisi umeondolewa mzigo mkubwa kwa kufanya hivyo. Mtunga-zaburi alisema: “Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana kutwa. Kwa maana mchana na usiku mkono wako ulinilemea. . . . Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuficha upotovu wangu.”—Zaburi 32:3-5.

Kuwaambia Wazazi Wako

Mtu mwingine apaswa kujua juu ya matatizo yako. Lakini ni nani? Tineja mmoja aitwaye Brian akiri hivi: “Mojapo makosa yangu makubwa zaidi lilikuwa ni kuwaendea na matatizo wale niliowaita eti marafiki badala ya kumwendea mama yangu Mkristo. Lakini niliogopa kuwasiliana naye kwa sababu niliogopa jinsi angeitikia, kwa hiyo niligeukia marafiki wangu, walioniongoza mbali zaidi na zaidi kutoka kwenye kweli.”[5] Wewe usifanye kosa hilohilo. Uwaeleze wazazi wako wenye kumcha Mungu. (Linganisha Mithali 23:26.) Wana haki ya kujua mambo ambayo umekuwa ukifanya. Sura 2 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi ina madokezo kadhaa ya jinsi unavyoweza kuzungumza na wazazi wako kuhusu jambo hilo.c

Bila shaka hawatafurahi kwa kuwa ulikuwa umewadanganya. Lakini wazazi huwa na hisia zenye nguvu kwa watoto wao. Mwandikaji Clayton Barbeau aonelea hivi: “Hawatakukana kwa sababu umetenda kosa ama kwa sababu uliingia katika tatizo fulani. Watoto wamepata mimba, wamepatwa na maradhi yanayopitishwa kingono, wamesitawisha matatizo ya kileo ama dawa za kulevya ama wamejiingiza katika matatizo mengine na kufikiri kwamba wazazi wangeitikia kwa hofu na machukizo makuu, waache nyumba yao na kuhama eneo hilo. Lakini wanapokuwa wamewaeleza wazazi wao, wamejikuta wamekumbatiwa ama kuwekelewa mkono mabegani, na kuambiwa, ‘Naam, kwa kweli umo katika matatizo makubwa, na tutaona jinsi tukavyokusaidia.’”[6] Ndiyo, mshtuko wa kwanza na hasira inapopoa, wazazi wengi hujaribu kuwa wenye utegemezo. Na jambo hilo lawa kweli zaidi kama nini ikiwa wazazi wako ni wenye kumcha Mungu! Hangaiko lao kuu halipasi kuwa kukuaibisha au kukuumiza bali kunyoosha mambo. (Linganisha Isaya 1:18.) Kwa habari hiyo wao pia waweza kupanga ili uzungumze pamoja na wazee wa kutaniko.—Yakobo 5:14, 15.

Ni kweli kwamba kutakuwa na adhabu nyinginezo zinazostahiliwa kutoka kwa wazazi wako za kuvumiliwa na labda hata vikwazo vikali zaidi. Lakini hayo yaweza hasa kukusaidia usizirudie tena njia zako za zamani. Isitoshe, kuongea pamoja na wazazi wako na kuona hangaiko lao lenye upendo kwaweza kwa kweli kubadili maoni yako kuwaelekea. Kufikia sasa, huenda umekuwa ukichukia sheria zao na vizuizi vyao. Msichana mmoja aitwaye Paulette akiri hivi: “Ni vigumu kukubali shauri na miongozo tunayopewa na wazazi wetu. Lakini nimekuja kutambua kwamba hayo yote ni kwa faida yetu na furaha yetu ya kudumu.”[7]

Kubadili Mashirika Yako

Ni nadra sana kwa kijana kufuatia maisha maradufu akiwa peke yake. Labda hata ulisikia marika wako wakikushangilia pamoja katika ukaidi wako! Ili kuepuka kurudia maisha ya kisiri, wahitaji kubadili mashirika yako. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Sikuketi pamoja na watu wa ubatili, wala sitaingia mnamo wanafiki.” (Zaburi 26:4) Si rahisi kuacha urafiki wa zamani. Kama mtunga-zaburi, huenda ukahitaji kusali hivi: “Uniokoe na mtu wa hila asiye haki.” (Zaburi 43:1) Tenda kwa kupatana na sala hiyo kwa kuwaeleza mashirika wako wa zamani kwamba umebadilika na umeazimia kufanya yaliyo sawa. Badala ya kuwa mfuasi wa siri wa Yesu, uwaeleze wengine juu ya imani yako. (Linganisha Yohana 19:38.) Mara nyingi mashirika mabaya watatafuta upesi washiriki wengine.

Kisha, wahitaji kubadili mashirika mabaya kwa kupata marafiki wazuri. Je! kuna vijana wenye kumcha Mungu wachache sana? Basi fikiria nabii Yeremia, aliyesema hivi: “Sikuketi katika mkutano wao wanaojifurahisha, wala sikufurahi; naliketi peke yangu kwa sababu ya mkono wako.” (Yeremia 15:17) Ni afadhali uwe peke yako kuliko kujihusisha na vijana ambao watakudhoofisha kiroho. Hata hivyo, mara nyingi marafiki wa kweli waweza kupatikana ukitia bidii kuwatafuta. Kwa kielelezo, Tammy alianza kushiriki pamoja na binamu yake aliyekuwa mhudumu wa wakati wote. “Tukawa na ushirika wa karibu sana,” Tammy akumbuka. “Katika siku ambazo sikuwa shuleni, nilikuwa nikienda naye katika kazi ya kuhubiri. Kufanya hivyo kulinisaidia nifanye mabadiliko katika maisha yangu.”[8]

Lakini “ulinzi bora zaidi,” asema kijana mmoja Mjerumani, “ni dhamiri njema, itokanayo na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu.”[9] Msichana mmoja aliyetumbukia katika maisha maradufu akiri hivi: “Sikupata kamwe kusitawisha uhusiano wa karibu na Baba yangu, Yehova.” Kupitia sala na funzo la binafsi, alianza kubadili mambo. “Sasa nina uhusiano pamoja na Yehova ambao hakuna mtu awezaye kuchukua,” yeye asema kwa fahari.[10] Wewe pia waweza kufurahia urafiki wa karibu jinsi hiyo pamoja na Mungu. Yeye atakuongoza na kukutegemeza, hata unapopata ugumu wa kubadili njia zako za zamani. Zaburi 37:24 yasema hivi juu ya mtumishi mwaminifu wa Mungu: “Ajapojikwaa hataanguka chini, BWANA [Yehova, NW] humshika mkono na kumtegemeza.” Naam, kwa msaada wa Yehova, waweza kuacha kuishi maisha maradufu.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Ona makala za “Vijana Huuliza . . .” zilizotokea katika matoleo yetu ya Desemba 22, 1993, na Januari 8, 1994.

c Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

“Nilijaribu kumsahau Yehova kabisa”

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Ni lazima ufanye uamuzi wa dhati wa kubadilika

[Picha katika ukurasa wa 20]

Eleza marafiki wako wa zamani kwamba umebadilika na hutajiunga nao tena katika matendo yao mabaya

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki