Vijana Huuliza . . .
Maisha Maradufu Ni Nani Apaswa Kujua?
“Mama na baba walikuwa wamekuwa wakinipeleka kwenye mikutano ya Kikristo, na nilijua mema na mabaya,” akiri Robert. “Lakini nilitaka nipendwe na kukubaliwa na vijana wale wengine shuleni. Kwa hiyo ili nisiwe mshamba na ili nipendwe na wengi, nilianza kuvuta sigareti nikiwa katika darasa la sita. Katika darasa la saba, nilianza kutumia LSD (dawa ya kulevya) na kuvuta bangi. Katika darasa la nane, nilianza kujichanja dawa iitwayo spidi. Nilimdanganya kila mtu—lakini nilikuwa mwenye huzuni.”
VIJANA wengi leo—kutia na baadhi ya wale waliolelewa na wazazi Wakristo—huwa na maisha maradufu. Si kwamba wote huwa watumizi wa madawa ya kulevya, kama vile Robert alivyofanya. Lakini bila wazazi wao kujua, vijana fulani hufanya matembezi na watu wa jinsia tofauti kwa siri, hunywa kileo, kuvaa mavazi ya kiajabu-ajabu, husikiliza muziki usiofaa, huenda kwenye karamu zisizo na utaratibu, na kujiingiza katika mambo mengine mengi yasiyokubaliwa au yanayokatazwa na wazazi wao. Je! unafuata mtindo-maisha kama huo?
Ikiwa ndivyo, labda wajua kwamba yale unayofanya hayafai. Kama vile Robert, huenda hata ukapatwa na maumivu ya dhamiri yenye hatia. (Warumi 2:15) Lakini, wazo la kufunua makosa yako kwa wazazi wako halifurahishi. Na ufikiriapo yale yaelekeayo kuwa matokeo, ile hoja ‘Yale ambayo wazazi wangu hawajui hayatawadhuru’ yaweza kuonekana kuwa ya kiakili. Lakini ingeweza kukuumiza.
Kusababu Kusikofaa
Kwa kielelezo, huenda ukahisi kwamba una malalamiko ya kweli juu ya vile wazazi wako hufanya mambo. Labda unayo. Lakini hata ikiwa nyakati nyingine wao ni wakali kupita kiasi, hawapendi mazungumzo, au ni wenye kutoa sheria, je, hilo lafanya ifae kuendelea kutotii? Si kulingana na Neno la Mungu, ambalo hushauri: “Watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Wakolosai 3:20) Vipi ukihisi kwamba una sababu nzuri ya kukasirikia wazazi wako? Je! ni jambo la akili kuonyesha hasira hiyo kwa kuvunja kisiri viwango vilivyotolewa na Mungu? Kwa kweli, ungetenda kana kwamba ‘wanuna juu ya Yehova.’ (Mithali 19:3) Jambo lifaalo la kufanya lingekuwa kuwafikia wazazi wako na uzungumze nao kwa utulivu juu ya malalamiko yoyote uliyo nayo.—Mithali 15:22.
Jambo lisilofaa vilevile ni itikadi ya kwamba kwa kuendelea kunyamaza wewe walinda wazazi wako wasihuzunike. Mvulana mmoja wa miaka 16 alisema: “Nisingesema jambo lolote ambalo lingewavunja moyo [wazazi wangu].” Tena, kusababu huko kusikofaa ni kujidanganya mwenyewe tu. Kama vile Biblia isemavyo, ni hali ya mtu kutenda kwa ‘kujipendekeza machoni pake kuwa upotovu wake hautaonekana na kuchukiwa.’ (Zaburi 36:2) Unapojali kikweli juu ya hisia za wazazi wako, unaepuka kwanza kutokutii. Zaidi ya hiyo, majaribio yoyote ya kuwaficha wazazi wako mambo, labda yatathibitika kuwa yasiyo na maana kwa sababu haikosi wengine tayari wajua juu ya maisha yako ya siri.
Hakuna Jambo Lililofichika
Waisraeli wa kale waliona jambo hilo walipojaribu kuepa adhabu kwa kuficha makosa yao. Nabii Isaya alionya hivi: “Ole wao wanaojitahidi kumficha BWANA [Yehova, NW] mashauri yao, na matendo yao yamo gizani, nao husema, Ni nani atuonaye? nani atujuaye?” (Isaya 29:15) Waisraeli walisahau kwamba Mungu aliona matendo yao ya mwenendo mbaya. Baada ya muda, aliwataka watoe hesabu kwa ajili ya makosa yao.
Jambo hilohilo lilikuwa kweli kwa baadhi ya Wakristo katika kutaniko la karne ya kwanza. Jisomee mwenyewe kwenye Matendo 5:1-11 masimulizi ya Anania na mkeye, Safira. Hazina ya kipekee ilipoanzishwa ili kuwatunza Wakristo wenye uhitaji, Anania aliuza shamba na akadai kwa ujasiri kwamba alikuwa akichanga fedha zote alizopata kwa kuliuza. Hata hivyo, kwa kweli Anania alikuwa ‘akizuia kwa siri sehemu ya thamani yake’ kwa ajili ya faida yake ya kibinafsi. Je! Mungu alidanganywa na hila hiyo ya ukarimu? La hasha. “Hukumwambia uongo mwanadamu, bali Mungu,” akasema mtume Petro. “Aliposikia maneno haya akaanguka, akafa.” Safira, aliyeshirikiana naye, aliuawa muda mfupi baadaye. Wote wawili yaonekana walisahau kwamba Mungu “ndiye azijuaye siri za moyo.”—Zaburi 44:21.
Vilevile leo, hata ikiwa wafanikiwa kuficha mwenendo mbaya usionwe na wazazi wako, huwezi kuficha mwenendo huo mbaya usionwe na macho yenye uangalifu ya Yehova Mungu. “Hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake,” lasema Waebrania 4:13, “lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yetu.” Je! kuna kufunuliwa kwingine zaidi ya huko? Na baada ya wakati dhambi zako zilizofichika zitafunuliwa kwa wengine pia. Mithali 20:11 yasema: “Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili.” Mithali nyingine husema: “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa.”—Mithali 28:13.
Mwanamke mchanga aitwaye Tammy alijifunza hilo akiwa kijana. Ingawa alilelewa na wazazi Wakristo, yeye alianza kuvuta sigareti, kunywa, na kwenda matembezi na wanaume wasioamini. Tammy alijaribu sana kuficha maovu yake, lakini yeye akumbuka hivi: “Wazazi wangu waliona nimebadilika. Nikawa mwasi na kusitawisha mtazamo wa kujitegemea. Mtu anapokuwa na maisha maradufu, jambo hilo halina budi kujulikana. Kwangu, lilijulikana upesi sana. Baba yangu alinifumania nikikutana na mwanamume rafiki yangu kwenye shule iliyo karibu.”
Jinsi Yehova Ahisivyo
Kwa hiyo, yale ambayo wazazi wako hawajui yaweza kuwaumiza—na labda yatawaumiza—wakati mmoja. Jambo la maana hata zaidi, je, umejiuliza, ‘Yehova huhisije juu ya waongo?’ Zaburi 5:5, 6 lajibu: ‘Yehova huwachukia wote watendao mambo yenye kuumiza. Atawaharibu wasemao uongo; humchukia mtu mwenye hila.’ Usijidanganye mwenyewe kufikiri kwamba waweza kupatana na Mungu kwa kujionyesha tu kuwa mwenye ujitoaji uhudhuriapo mikutano ya kidini. Yeye ajua watu ‘wanapomheshimu kwa midomo ila mioyo yao iko mbali naye.’—Marko 7:6.
Hivyo, kijana aitwaye Ricardo, aliyejiingiza katika mwenendo usio safi kingono alikiri hivi: “Mtu hujihisi vibaya sana ajuapo kwamba amemkosea Yehova.” Lakini je, yawezekana kweli kumkosea Yehova—yaani, kumfanya ahisi vibaya? Ndiyo yawezekana! Taifa la Israeli la kale lilipoacha sheria ya Mungu, “walimhuzunisha hata Yule Mtakatifu wa Israeli.” (Zaburi 78:41) Ni lazima iwe yeye huhuzunika kama nini leo wakati vijana waliolelewa katika “adabu na maonyo ya Bwana” wanapofanya kwa siri mambo yasiyofaa!—Waefeso 6:4.
Wazazi Walioumizwa
Basi, ng’amua kwamba huwezi kujificha kwa siri milele. Wamwia Mungu, wazazi wako, na wewe mwenyewe kusema kweli na kutubu juu ya yale ambayo yamekuwa yakiendelea sirini. Ni kweli, huenda hilo likaleta aibu na labda matokeo fulani yenye kuhuzunisha. (Waebrania 12:10, 11) Ikiwa umeendeleza mwendo wa kusema uwongo na kudanganya, umedhoofisha tumaini ambalo wazazi wako walikuwa nalo kwako. Kwa hiyo usishangae wakikuzuia zaidi ya hapo mwanzoni. Tammy akumbuka: “Baada ya kufumaniwa nikikutana na rafiki yangu mwanamume, baba yangu alihofu. Sasa aling’amua kwamba nisingeweza kutumainiwa. Ilimaanisha angeendelea kunichunga daima.” Lakini Tammy alitambua kwamba alikuwa akivuna tu yale aliyopanda.—Wagalatia 6:7.
Waweza pia kutazamia wazazi wako wahuzunike na kukasirika. Jina lao na sifa yao imetiwa doa. (Linganisha Mwanzo 34:30.) Ikiwa baba yako ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, huenda labda ikambidi kuacha baadhi ya mapendeleo yake ya kutaniko. (Tito 1:5-7) Naam, kama vile Mithali 17:25 husema, kijana mwasi aweza kuwa “huzuni kwa babaye, na uchungu kwa mamaye aliyemzaa.”
Mtungaji-vitabu Joy P. Gage aeleza kwa masikitiko jinsi wazazi fulani huhisi mwana aasipo. Yeye asema: “Wazazi fulani hulia kimya-kimya. Baadhi yao hulia bila kujizuia. Baadhi yao hulia faraghani. Wao hulia kwa sababu ya siku zilizopita. Wao hulia kwa sababu kwa ghafula hakuna wakati ujao. Wao hulia kwa sababu ya yale ambayo afadhali yangetokea. Wao hulia kwa sababu ya yale ambayo hakika yatatokea. Wao hulia kwa sababu ya hasira. Wao hulia kwa sababu ya mfadhaiko.” Kwa kueleweka, haitakuwa rahisi kuwakabili baada ya kuleta huzuni hiyo kwa watu wawili wanaokupenda zaidi ya mwingine yeyote ulimwenguni. Tammy asema: “Mimi hutafakari yale yaliyopita na kutamani nisingeletea baba na mama huzuni nyingi hivyo.”
Hata hivyo, huwezi kurudi nyuma na kubadili yale yaliyopita. Na bila shaka hata ikiwa itakuwa yenye kuumiza na magumu, una jukumu la kujaribu kurekebisha mambo. (Linganisha Isaya 1:18.) Hilo lamaanisha kuwaambia wazazi wako kweli, ukikubali kuumizwa kwao na hasira yao, ukikubali nidhamu yoyote wanayotoa. Kuwaambia kweli kwaweza kuwa hatua ya kwanza katika kuleta shangwe kwenye mioyo ya wazazi wako, na kwa moyo wa Yehova Mungu, kutia na wewe kupata uradhi wenye shangwe wa kuwa na dhamiri safi.—Mithali 27:11; 2 Wakorintho 4:2.
Lakini wapaswa uwaambieje wazazi wako? Uepukeje kuishi maisha maradufu? Maswali hayo yatazungumzwa katika toleo letu linalokuja.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Kusema kweli kwaweza kuleta kitulizo kwako na kwa wazazi wako