Yehova Hatasahau Kazi Yenu Enyi Vijana!
“Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu na mwaendelea kuhudumu.”—WAEBRANIA 6:10.
1. Kitabu cha Biblia cha Waebrania na Malaki kinaonyeshaje kwamba Yehova huthamini utumishi wako?
JE, UMEWAHI kumfanyia rafiki fulani tendo la fadhili naye akakosa kukushukuru? Unaweza kuhisi uchungu sana wakati unapomtendea mtu kwa fadhili lakini anakosa kuonyesha uthamini au hata anasahau kabisa kukushukuru. Hata hivyo, ni tofauti kama nini tunapomtumikia Yehova kwa moyo wote! Biblia inasema: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu na mwaendelea kuhudumu.” (Waebrania 6:10) Hilo linamaanisha nini? Yehova angeliona jambo hilo kuwa ukosefu wa uadilifu kwa upande wake, yaani dhambi, kama angesahau kile ambacho umefanya na unachoendelea kufanya katika utumishi wake. Yeye ni Mungu mwenye shukrani kama nini!—Malaki 3:10.
2. Kwa nini kumtumikia Yehova ni jambo la pekee sana?
2 Una pendeleo la pekee la kumwabudu na kumtumikia Mungu huyo mwenye shukrani. Pendeleo hilo ni la pekee sana kwa kuwa kati ya watu bilioni sita ulimwenguni pote, ni watu wapatao milioni sita tu wanaomwabudu Yehova. Isitoshe, kusikiliza na kukubali kwako ujumbe wa habari njema kunaonyesha kwamba Yehova anapendezwa nawe. Ndiyo sababu Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Naam, Yehova huwasaidia watu wanufaike na dhabihu ya Kristo.
Kuthamini Pendeleo Lako la Pekee
3. Wana wa Kora walionyeshaje uthamini kwa pendeleo la kumtumikia Yehova?
3 Kama tulivyozungumzia katika makala iliyotangulia, una pendeleo la pekee la kuufurahisha moyo wa Yehova. (Mithali 27:11) Hupaswi kamwe kupuuza pendeleo hilo. Wana wa Kora walionyesha uthamini wao kwa pendeleo la kumtumikia Yehova katika mojawapo ya zaburi walizoandika chini ya mwongozo wa roho. Tunasoma hivi: “Siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu. Ningependa kuwa bawabu nyumbani mwa Mungu wangu, kuliko kukaa katika hema za uovu.”—Zaburi 84:10.
4. (a) Ni nini kinachoweza kufanya wengine waone kwamba ibada ya Yehova inawanyima uhuru? (b) Yehova huonyeshaje kwamba anawatambua watumishi wake na anatamani kuwapa thawabu?
4 Je, hivyo ndivyo unavyohisi kuhusu pendeleo lako la kumtumikia Baba yako wa mbinguni? Ni kweli kwamba huenda nyakati nyingine ukahisi kwamba ibada ya Yehova inakunyima uhuru. Bila shaka, unahitaji kujidhabihu kwa kadiri fulani ili kuishi kupatana na kanuni za Biblia. Hata hivyo, chochote ambacho Yehova anataka ufanye ni kwa faida yako. (Zaburi 1:1-3) Isitoshe, Yehova anaona jitihada zako naye anaonyesha wazi kwamba anathamini uaminifu wako. Kwa kweli, Paulo aliandika kwamba Yehova “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Yehova anatafuta nafasi za kukupa thawabu. Nabii mwadilifu wa Israeli la kale alisema: “Kwa maana macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.
5. (a) Mojawapo ya njia bora zaidi za kuonyesha kwamba moyo wako ni kamili kwa Yehova ni ipi? (b) Kwa nini huenda ikaonekana kuwa vigumu kuwaeleza wengine kuhusu imani yako?
5 Njia moja bora zaidi ya kuonyesha kwamba moyo wako ni kamili kwa Yehova ni kuwaeleza wengine juu yake. Je, umewahi kupata nafasi ya kuwaeleza baadhi ya wanafunzi wenzako kuhusu imani yako? Huenda mwanzoni jambo hilo likaonekana kuwa gumu na pengine ukaogopa kidogo. Huenda ukajiuliza, ‘Vipi wakinicheka au wakiona kwamba dini yangu ni ya kiajabu-ajabu?’ Yesu alisema kwamba si kila mtu atakayesikiliza ujumbe wa Ufalme. (Yohana 15:20) Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba utadhihakiwa na kukataliwa daima. Kinyume cha hilo, vijana wengi Mashahidi wamesikilizwa, na hata wameheshimiwa na wanafunzi wenzao kwa sababu wanaishi kupatana na imani yao.
“Yehova Atakusaidia”
6, 7. (a) Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 17 aliwezaje kuwatolea wanafunzi wenzake ushahidi? (b) Umejifunza nini kutokana na kisa cha Jennifer?
6 Lakini unawezaje kupata ujasiri wa kuzungumza kuhusu imani yako? Mbona usiazimie kusema waziwazi watu wanapokuuliza kuhusu dini yako? Fikiria kisa cha Jennifer mwenye umri wa miaka 17. Anasema hivi: “Tulikuwa tukila chakula cha mchana shuleni. Wasichana walioketi karibu nami walikuwa wakizungumza juu ya dini na mmoja wao akaniuliza mimi ni mfuasi wa dini gani.” Je, Jennifer aliogopa alipojibu? Anasema: “Bila shaka niliogopa kwa sababu sikujua watasema nini.” Kwa hiyo Jennifer alifanya nini? Anaendelea: “Niliwaambia wasichana hao kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwanza walishangaa. Yaelekea, walifikiri kwamba Mashahidi wa Yehova si watu wa kawaida. Hilo lilifanya waniulize maswali, nami niliweza kusahihisha maoni fulani yasiyofaa waliyokuwa nayo. Hata baada ya siku hiyo, baadhi ya wasichana walinijia mara kwa mara ili kuuliza maswali.”
7 Je, Jennifer alighairi kwamba alizungumza kuhusu imani yake? Hata kidogo! Anasema: “Nilifurahi sana baada ya kipindi hicho cha mapumziko ya mchana. Sasa wasichana hao wanaelewa imani ya Mashahidi wa Yehova vizuri zaidi.” Jennifer anatoa ushauri huu: “Ukiona ni vigumu kuwatolea wanafunzi wenzako au walimu ushahidi toa sala fupi. Yehova atakusaidia. Utafurahi kwamba ulitumia vizuri nafasi hiyo kutoa ushahidi.”—1 Petro 3:15.
8. (a) Sala ilimsaidiaje Nehemia alipokabili hali isiyotazamiwa? (b) Huenda ukahitaji kutoa sala fupi ya moyoni kwa Yehova unapokabili hali zipi shuleni?
8 Ona kwamba Jennifer anapendekeza ‘utoe sala fupi’ kwa Yehova unapopata nafasi ya kutoa ushahidi kuhusu imani yako. Hivyo ndivyo Nehemia, mnyweshaji wa Mfalme Artashasta wa Uajemi, alivyofanya alipokabili hali isiyotazamiwa. Nehemia alionekana kuwa mwenye huzuni kwa sababu alikuwa ameelezwa juu ya hali mbaya ya Wayahudi na kwamba ukuta na malango ya Yerusalemu yalikuwa yameharibika. Mfalme aliona kwamba Nehemia alikuwa na wasiwasi, basi akamwuliza alikuwa na tatizo gani. Kabla ya kumjibu, Nehemia alisali ili kupata mwongozo. Kisha kwa ujasiri akaomba ruhusa ya kurudi Yerusalemu akasaidie kujenga upya jiji lililobomoka. Artashasta alikubali ombi lake. (Nehemia 2:1-8) Unajifunza nini kutokana na hilo? Ukiwa na wasiwasi unapopata nafasi ya kutoa ushahidi kuhusu imani yako, usikose kutoa sala ya moyoni. Petro aliandika hivi: ‘Mtupieni Yehova hangaiko lenu lote, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.’—1 Petro 5:7; Zaburi 55:22.
“Tayari Kujitetea”
9. Leah mwenye umri wa miaka 13 aliwezaje kuwaachia wanafunzi wenzake nakala 23 za kitabu Vijana Huuliza?
9 Fikiria kisa kingine. Leah, mwenye umri wa miaka 13, alikuwa akisoma kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazia wakati wa mapumziko ya mchana shuleni. Anasema: “Wanafunzi wengine walikuwa wakinitazama, punde si punde wanafunzi wengi walisimama nyuma yangu na kutazama. Kisha wakaanza kuuliza maswali kuhusu kitabu hicho.” Wasichana wanne walimwomba Leah kitabu Vijana Huuliza siku hiyo. Muda mfupi baada ya hapo wasichana hao walisoma vitabu hivyo pamoja na wengine, kisha hao pia wakataka nakala zao. Leah aliwaachia wanafunzi wenzake na marafiki wake nakala 23 za kitabu Vijana Huuliza katika majuma machache yaliyofuata. Je, ilikuwa rahisi kwa Leah kutoa ushahidi hapo mwanzoni wengine walipomwuliza juu ya kitabu alichokuwa akisoma? Sivyo! Anasema hivi: “Mwanzoni, nilikuwa na wasiwasi. Hata hivyo, nilisali, na nilijua kwamba Yehova alikuwa pamoja nami.”
10, 11. Msichana mdogo Mwisraeli aliwezaje kumsaidia mkuu wa jeshi la Siria ajifunze kumhusu Yehova, na mtu huyo alifanya mabadiliko gani baadaye?
10 Huenda kisa cha Leah kikakukumbusha hali iliyompata msichana mdogo Mwisraeli aliyepelekwa utekwani huko Siria. Mkuu wa jeshi la Siria, Naamani, alikuwa mwenye ukoma. Inawezekana kwamba mke wake ndiye aliyeanzisha mazungumzo yaliyomsukuma huyo msichana mdogo kumweleza imani yake. Alisema: “Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake.”—2 Wafalme 5:1-3.
11 Kwa sababu ya ujasiri wa msichana huyo mdogo, Naamani alipata kujua kwamba “hakuna Mungu duniani mwote, ila katika Israeli.” Hata aliazimia kwamba ‘hangetoa tena sadaka ya kuteketezwa wala dhabihu kwa miungu mingine, ila kwa BWANA.’ (2 Wafalme 5:15, 17) Bila shaka Yehova alibariki tendo la ujasiri la msichana huyo mdogo. Anaweza, na anataka kuwabariki vijana leo pia. Leah amepata baraka kama hizo. Baada ya muda mfupi, baadhi ya wanafunzi wenzake walimwendea na kumwambia kwamba kitabu Vijana Huuliza kimewasaidia kufanya mabadiliko katika mwenendo wao. Leah anasema, “Nilifurahi kwa sababu nilijua kwamba nilikuwa nikiwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova na kufanya mabadiliko maishani.”
12. Unawezaje kuimarishwa kutetea imani yako?
12 Wewe pia unaweza kupata matokeo mazuri kama Jennifer na Leah. Fuata ushauri wa Petro, aliyeandika kwamba sikuzote Mkristo anapaswa kuwa ‘tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwake sababu ya tumaini lililo katika yeye, akifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.’ (1 Petro 3:15) Unawezaje kufuata ushauri huo? Iga mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza waliomwomba Yehova awasaidie kuhubiri “kwa ujasiri wote.” (Matendo 4:29) Kisha uwe na ujasiri unapozungumza na wengine juu ya imani yako. Huenda ukapata matokeo mazuri kuliko ulivyotazamia. Isitoshe, utaufurahisha moyo wa Yehova.
Video na Miradi Hususa
13. Vijana fulani wametumia nafasi zipi ili kutoa ushahidi? (Ona masanduku kwenye ukurasa wa 20 na 21.)
13 Vijana wengi wamewaeleza wanafunzi wenzao au walimu imani yao kwa kutumia video. Nyakati nyingine, wamepata nafasi ya kumsifu Yehova kupitia miradi mbalimbali ya shule. Kwa mfano, wavulana wawili wenye umri wa miaka 15, ambao ni Mashahidi wa Yehova, waliambiwa waandike ripoti katika somo lao la historia kuhusu mojawapo ya dini za ulimwengu. Wavulana hao walishirikiana kuandika ripoti kuwahusu Mashahidi wa Yehova wakitumia habari iliyo katika kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu.b Pia, walipaswa kutoa hotuba ya dakika tano. Baadaye, mwalimu na wanafunzi walikuwa na maswali mengi sana hivi kwamba wavulana hao waliendelea na mazungumzo darasani kwa dakika nyingine 20. Kwa majuma kadhaa baadaye, wanafunzi waliendelea kuuliza maswali kuwahusu Mashahidi wa Yehova!
14, 15. (a) Kwa nini kuwaogopa wanadamu ni mtego? (b) Kwa nini unapaswa kuwaelezea wengine imani yako bila woga?
14 Kama inavyoonyeshwa na visa hivyo, unaweza kupata baraka nyingi kwa kuwaeleza wengine juu ya imani yako ukiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Usipoteze pendeleo na shangwe ya kuwasaidia wengine wamjue Yehova kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu. Biblia inasema: “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; bali amtumainiye BWANA atakuwa salama.”—Mithali 29:25.
15 Kumbuka kwamba ukiwa kijana Mkristo, una kitu fulani ambacho vijana wenzako wanahitaji sana, yaani, maisha bora sasa na ahadi ya kuishi milele wakati ujao. (1 Timotheo 4:8) Ijapokuwa huenda ukafikiri kwamba watu hawapendezwi na dini nchini Marekani, jambo la kupendeza ni kwamba kura ya maoni ilionyesha kuwa nusu ya vijana nchini humo wanapendezwa sana na dini, na theluthi moja wanasema kwamba dini ni ‘muhimu sana maishani mwao.’ Yaelekea ndivyo ilivyo katika sehemu nyinginezo ulimwenguni. Kwa hiyo huenda wanafunzi wenzako wakafurahia kusikiliza mambo unayowaeleza kuhusu Biblia.
Mkaribie Yehova Ewe Kijana
16. Mbali na kuongea na wengine kumhusu Yehova, ni nini kingine kinachohitajiwa ili kumpendeza?
16 Bila shaka, haitoshi tu kuzungumza juu ya Yehova ili kuufurahisha moyo wake. Unahitaji pia kufuata kanuni zake maishani mwako. Mtume Yohana aliandika: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Ukimkaribia Yehova, utaona kwamba amri zake si zenye kulemea. Unawezaje kufanya hivyo?
17. Unawezaje kumkaribia Yehova?
17 Tafuta wakati wa kusoma Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia. Kadiri unavyojifunza mengi kumhusu Yehova, ndivyo itakavyokuwa rahisi kumtii na kuwaeleza wengine juu yake. Yesu alisema: ‘Mtu mwema hutokeza mema katika hazina njema ya moyo wake, kwa maana katika wingi wa moyo kinywa chake husema.’ (Luka 6:45) Hivyo, jaza moyo wako mambo mema. Mbona usijiwekee miradi ya kufanya hivyo? Labda unaweza kufanya maendeleo katika kutayarisha mikutano ya kutaniko ya juma lijalo. Huenda mradi mwingine ukawa kutoa maelezo mafupi kutoka moyoni. Bila shaka ni muhimu pia kutenda kulingana na yale unayojifunza.—Wafilipi 4:9.
18. Unaweza kuwa na hakika gani hata unapopingwa?
18 Kumtumikia Yehova huleta baraka za milele. Ni kweli kwamba huenda pindi fulani ukapingwa au kudhihakiwa kwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Lakini mfikirie Musa. Biblia inasema kwamba “alikaza macho kuelekea malipo ya thawabu.” (Waebrania 11:24-26) Wewe pia unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atabariki jitihada zako za kujifunza na kuzungumza juu yake. Hakika, ‘hatasahau kamwe kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’—Waebrania 6:10.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
Je, Unakumbuka?
• Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anathamini utumishi wako?
• Ni njia gani za kutoa ushahidi shuleni ambazo vijana fulani wameona kuwa zenye matokeo mazuri?
• Unawezaje kuimarishwa kuwatolea wanafunzi wenzako ushahidi?
• Unawezaje kumkaribia Yehova?
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]
Hata Watoto Wanamsifu Yehova!
Hata watoto wamefaulu kutoa ushahidi shuleni. Fikiria mambo yafuatayo.
Wanafunzi wa darasa la tano la Amber mwenye umri wa miaka kumi, walikuwa wakisoma kitabu fulani kuhusu jinsi Wayahudi walivyoshambuliwa na Wanazi wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Amber aliamua kumletea mwalimu wake video Purple Triangles. Mwalimu alishangaa kujua kwamba Mashahidi wa Yehova pia waliteswa wakati wa utawala wa Nazi. Mwalimu alionyesha wanafunzi wote video hiyo.
Alipokuwa na umri wa miaka minane, Alexa aliwaandikia wanafunzi wenzake barua na kuwaeleza kinachofanya asisherehekee Krismasi. Mwalimu wake alivutiwa sana na barua hiyo na akamwomba Alexa aisome mbele ya wanafunzi wenzake na hata wale wa madarasa mengine mawili! Mwishoni mwa barua hiyo alisema: “Mimi nimefundishwa kuwaheshimu watu walio na imani tofauti na yangu, nami nawashukuru kwa kuheshimu msimamo wangu wa kutosherehekea Krismasi.”
Muda mfupi baada ya kuanza darasa la kwanza, Eric alibeba Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia shuleni na kuomba ruhusa awaonyeshe wanafunzi wenzake. Mwalimu wake alisema: “Mbona usiwasomee wanafunzi hadithi moja?” Eric alifanya hivyo. Baadaye akawaomba wote waliotaka kitabu hicho wainue mikono. Wanafunzi kumi na wanane, pamoja na mwalimu waliinua mikono! Sasa Eric anaona ana eneo lake la pekee la kuhubiri.
Whitney, aliye na umri wa miaka tisa, anathamini broshua Mashahidi wa Yehova na Elimu.c Anasema: “Mama yangu amekuwa akiwapa walimu wangu broshua hiyo kila mwaka, lakini mwaka huu mimi ndiye niliyewapa. Mwalimu wangu alinichagua kuwa ‘mwanafunzi bora wa juma’ kwa sababu ya kichapo hicho.”
[Maelezo ya Chini]
c Vichapo vyote vilivyotajwa vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]
Hali Fulani Ambazo Wengine Wametumia Kueleza Imani Yao
Wanapopewa mgawo wa kutayarisha ripoti au kufanya mradi fulani shuleni, wengine wamechagua habari itakayowapatia nafasi ya kutoa ushahidi
Vijana kadhaa wamempa mwalimu wao video, kitabu, au gazeti linalohusu habari ambayo itazungumziwa darasani
Vijana fulani waliokuwa wakisoma Biblia au kitabu ambacho kinazungumzia Biblia wakati wa mapumziko, wamefikiwa na vijana wengine na kuulizwa maswali
[Picha katika ukurasa wa 18]
Walio na uzoefu wanaweza kuwazoeza vijana wamtumikie Yehova