Vijana Huuliza . . .
Naweza Kukabilianaje na Dhihaka Kali?
VIJANA wanaotenda na kuvaa tofauti na marika wao huenda wakadhihakiwa vikali. Ndivyo ilivyo hasa kwa vijana Wakristo, walio na mwenendo tofauti kabisa na vijana wengine. Je, Kristo hakusema hivi juu ya wafuasi wake wa kweli: “Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia”?—Yohana 15:20.
Jambo hili huwaathirije vijana walio Mashahidi wa Yehova? Baadhi yao hudhihakiwa kwa sababu hawasherehekei sikukuu fulani; wengine wanashutumiwa kwa sababu hawaisalimu bendera. Baadhi yao hata wanatendwa vibaya kwa sababu hawatumii dawa za kulevya, ni wenye kufuatia haki, na kwa sababu wanategemeza viwango vya adili vya Biblia.
Tatizo hilo si jipya. Kwa kweli, mtume Petro aliwaambia Wakristo wa karne ya kwanza hivi: “Kwa sababu nyinyi hamwendelei kukimbia pamoja nao [watu wa mataifa] . . . , wao watatanishwa na kuendelea kuwasema nyinyi kwa maneno yenye kuudhi.” (1 Petro 4:4) Tafsiri nyingine husema, wao “huwatukana” (Knox) au, “Huwafedhehesha nyinyi.”—Today’s English Version.
Je, umewahi kudhihakiwa kwa sababu ya usadikisho wako wa kidini? Ikiwa ndivyo, jipe moyo. Si wewe peke yako! Na utafurahi kujua kwamba unaweza kujifunza kukabiliana na tatizo la kudhihakiwa kwa sababu ya imani yako.
Sababu Inayowafanya Wadhihaki
Kwa nini watu wengine huwadhihaki watu walio na itikadi na mwenendo unaotofautiana na wao? Nyakati nyingine wadhihaki—sawa na waonezi—hujihisi hawana usalama. Huenda wakakudhihaki ili wasifiwe na marika wao. Yaelekea kwamba wanapokuwa peke yao, ni wadhihaki wachache wanaopendezwa—au wanaokuwa na ujasiri—wa kukushutumu waziwazi.
Kwa upande mwingine, wadhihaki wengine, “hutatanishwa” kama Petro alivyoandika. Naam, huenda wakaduwazwa kihalisi na mwenendo wako. Kwa mfano, ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, kwa kweli huenda wakaliona kuwa jambo la ajabu kwa sababu hushiriki shughuli zinazohusianishwa na sikukuu fulani. Huenda hata wakawa wamepokea habari iliyopotoka juu ya Mashahidi kutoka kwa wapinzani wa dhati.
Hata sababu iwe nini, unaposhambuliwa kwa maneno ya dhihaka, huenda ukakubaliana na mithali hii ya Biblia: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga.” (Mithali 12:18) Lakini kumbuka kwamba wale wanaoshiriki mazungumzo hayo labda hawafanyi hivyo kwa sababu wanakuchukia wewe binafsi. Yaelekea kwamba wanafanya sawasawa na vile mithali ya Biblia inavyosema—‘kunena bila kufikiri.’
Hata hivyo, bado dhihaka inaweza kuumiza, kama jeraha lililochomwa kwa upanga. Huenda hata ukashawishwa uridhiane imani yako ili ukomeshe shambulio la matusi. Unaweza kukabilianaje basi, na kudhihakiwa kwa sababu ya imani yako?
Kujitetea
Mtume Petro aliwaonya Wakristo kwa upole: Sikuzote mwe “tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwenu sababu ya tumaini lililo katika nyinyi, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:15) Ili kutetea imani yako unahitaji utwae ujuzi sahihi na ufahamu sababu za itikadi zako.
Hata hivyo, ni lazima pia ujifunze jinsi ya kujitetea kwa “staha yenye kina kirefu” au kama vile The Bible in Basic English hufasili mstari huo, “bila kiburi.” Ujuzi wako wa Biblia na mafundisho yake haupasi kukufanya ujione kuwa bora kuliko wengine. Kinyume na hilo, unapaswa kujitahidi kukuza mtazamo wa mtume Paulo, aliyeandika hivi juu ya huduma yake: “Nimejifanya mwenyewe mtumwa kwa wote, ili nipate kuwapata watu walio wengi zaidi sana.”—1 Wakorintho 9:19.
Ikiwa unahofu kutetea imani yako, usikate tumaini. Vijana wengi walio Mashahidi wamehisi vivyohivyo. “Nilipokuwa katika shule ya msingi,” asema Jamal, “sikujua jinsi ya kuwaeleza wengine kwa nini sikusherehekea sikukuu au kusalimu bendera au hata kwa nini ninaenda kwenye huduma ya mlango kwa mlango.” Ni nini kilichomsaidia? “Baba yangu aliendelea kunisaidia hadi nilipoweza kueleza mambo hayo hatimaye, na hili lilileta badiliko kubwa.” Iwapo unashindwa kuwaeleza wengine itikadi zako, labda unaweza kumwomba mzazi msaada au mshiriki mwingine mkomavu wa kutaniko la Kikristo ili upate kufahamu kikamili ujuzi juu ya Mungu.—Waefeso 3:17-19.
Kijana Shahidi mwenye umri wa miaka 16 alisema kwamba programu ya kibinafsi ya funzo la Biblia ilimsaidia kupata ujasiri wa kunena waziwazi shuleni. “Hapo awali, wanadarasa wenzangu waliponidhihaki kwa kuwa Shahidi, sikujua la kusema,” yeye akiri. “Sasa, nikiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote, mimi hujifunza Biblia zaidi, nami huwa tayari kutoa jibu. Kusoma kwa ukawaida makala za karibuni zaidi kwenye magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! hunisaidia kuzungumza na wanashule wenzangu juu ya itikadi zangu.”
Bila shaka, hali hutofautiana. Kila hali itahitaji kushughulikiwa kwa njia tofauti. Hata hivyo, unapochokozwa kwa usemi wenye kuudhi, haifai hata kidogo ‘kurudisha ovu kwa ovu.’ (Waroma 12:17-21) Jibu kali, hata liwe linaonekana kuwa lafaa, litaongeza tu chuki na huenda hata likazidisha dhihaka. Kwa sababu hiyo, wengine wameona ni bora kupuuza matusi hayo.
Katika visa vingine, kwa mfano wakati usemi unapokuwa tu na nia nzuri ya kujaribu kuchekesha, huenda hata likawa jambo la busara kucheka badala ya kukasirika. (Mhubiri 7:9) Mdhihaki anapoona kwamba maneno yake hayakuathiri sana, huenda akaacha kabisa kukusumbua.—Linganisha Mithali 24:29; 1 Petro 2:23.
Kusema Waziwazi
Ingawa hivyo, kuna nyakati ambazo huenda ikawezekana kutoa elezo fupi, la busara juu ya itikadi zako. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 13 alijaribu kufanya hivyo akapata matokeo bora sana. “Nilikuwa nikielekea darasani,” yeye asema, “wakati wanafunzi kadhaa walipoanza kuwadhihaki Mashahidi wa Yehova. Nilitaka kusema waziwazi, lakini wakaenda huku wakiendelea kunicheka—isipokuwa mwanafunzi mmoja.” Mwanafunzi huyo Shahidi alieleza hivi: “Msichana anayeitwa Jaimee alinigeukia na kuniambia kwamba alikuwa na kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani.a Alisema kwamba alikuwa amekisoma sana na alipenda kupata habari zaidi juu ya itikadi zetu. Nilianza kujifunza Biblia na Jaimee.” Baada ya kutiwa moyo na jambo hilo, kijana huyo Shahidi alianza kuzungumza na vijana wengine. “Mimi huwazuru kwa ukawaida wanafunzi wenzangu wanne wanaopendezwa na ambao nina hakika watajifunza karibuni,” akasema.
Miaka iliyopita mwanafunzi mmoja katika nchi ya Liberia katika Afrika alipata jambo kama hilo. Wakati wa somo la soshiolojia, alieleza kwa heshima kwamba akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, aliamini uumbaji badala ya mageuzi. Mwanzoni, wengi wa wanafunzi wenzake walimshutumu sana. Lakini mwalimu alimruhusu aeleze itikadi zake darasani, baada ya hapo mwalimu alikubali kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?b
Baada ya kukisoma kitabu hicho, mwalimu aliliambia darasa: “Kitabu hiki hakina kifani. Ni mojawapo ya vitabu bora vya sayansi nilivyowahi kusoma.” Kisha mwalimu akaeleza kwamba alikusudia kutumia kitabu Creation pamoja na vitabu vingine vya mafundisho kwa mihula miwili ijayo, naye akawaagiza wanafunzi wapokee nakala kutoka kwa yule mwanafunzi Shahidi. Vichapo vingi viliangushwa, na wanafunzi wengi wakabadili maoni yao juu ya Mashahidi wa Yehova!
Imani Iliyojaribiwa Ni Imani Yenye Nguvu
Kwa kawaida, nyakati nyingine huenda ukahisi umehofia idadi ya watu wasioshiriki—au kuthamini—msimamo wako unaotegemea Biblia. (Linganisha Zaburi 3:1, 2.) Kwa hiyo, ni jambo la hekima kutafuta ushirika wa wale walio na usadikisho na itikadi kama zako. (Mithali 27:17) Namna gani ikiwa katika shule au katika ujirani wenu hakuna vijana wenye imani kama yako?
Ikiwa ndivyo ilivyo, kumbuka kwamba Rafiki yako mkubwa ni Yehova Mungu, naye anaweza kukutegemeza. Amekuwa lengo kuu la dhihaka za Shetani Ibilisi kwa maelfu ya miaka. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba unapobaki imara kwa ajili ya imani yako unafurahisha moyo wa Yehova. Mwendo wa aina hiyo humpa Yehova fursa ya ‘kumjibu Shetani, anayemlaumu.’—Mithali 27:11.
Mara kwa mara unaweza kutarajia kwamba imani yako itajaribiwa. (2 Timotheo 3:12) Na bado, mtume Petro atuhakikishia kwamba ubora wa imani yetu uliojaribiwa, ni wenye “thamani kubwa zaidi sana kuliko dhahabu ambayo huharibika ijapokuwa kuthibitishwa kwayo na moto.” (1 Petro 1:7) Kwa sababu hiyo, unapoaibishwa kwa sababu ya imani yako, ione kama fursa ya kuimarisha imani yako na kudhihirisha uvumilivu wako. Mtume Paulo aliandika kwamba uvumilivu hutokeza “hali yenye kukubaliwa.” (Waroma 5:3-5) Naam, ile tamaa ya kupata kibali cha Yehova hukupa kichocheo chenye nguvu ili ukabiliane unapodhihakiwa kwa ajili ya imani yako!
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Je, unaweza kuitetea imani yako?