Vijana Wakristo Iweni Imara Katika Imani
“NI LAZIMA kila mtu ahudhurie.” Hilo ndilo lililokuwa tangazo. Wanafunzi wote katika shule fulani ya Kijapani walipaswa waweko kwenye kusanyiko la watu wote katika jumba. Mwanafunzi Mkristo mchanga hakuweza kukubaliana na mawazo fulani katika wimbo wa shule. “Basi,” akawaza, “najua kwamba wimbo wa shule utapigwa. Lakini sitakuwa na magumu yoyote. Nitaketi nyuma tu kama kawaida.”
Hata hivyo, Shahidi wa Yehova mchanga huyo alipoingia jumba, alipata kwamba walimu wote walikuwa wameketi kwenye viti vya nyuma. Hivyo, alilazimika kuketi mbele yao. Wanafunzi wengineo waliposimama kwa ajili ya wimbo wa shule, alibaki ameketi kwa heshima. Lakini walimu walikasirikwa na hilo. Walijaribu kumfanye asimame kwa kutumia nguvu. Je! waweza kujiwaza ukiwa katika hali kama hiyo? Ungalifanya nini?
Sababu kwa Nini Imani Yenye Nguvu Inahitajiwa
Ingekuwa vema kama watu wangeacha Wakristo pekee yao na kuwaruhusu waishi kulingana na dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia. Hata hivyo, mara nyingi, Wakristo wanapaswa kukabili hali zenye kusonga sana. Hilo halipasi kutushangaza, kwa kuwa Mwana wa Mungu mwenyewe, Yesu Kristo, alisema hivi: “Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa na ninyi pia.” (Yohana 15:20, HNWW) Zaidi ya kunyanyaswa waziwazi, watumishi wa Yehova hukabili majaribu mengine mbalimbali ya imani.
Mara nyingi vijana Wakristo huhitaji imani yenye nguvu ili kukabili majaribu wanaopata shuleni. Huenda wakalazimika kushiriki pamoja na wanadarasa wenzao ambao hutumia lugha yenye ukosefu wa maadili au walio na mielekeo isiyomheshimu Mungu. Wakristo wachanga huenda wakakabiliwa na ongezeko la mkazo juu ya kupendelea taifa na mbano wa kuhusika katika vilabu mbalimbali, siasa za shule, au utendaji mwingine mbalimbali ambao huenda ukawa wenye kudhuru kiroho. Walimu au wanafunzi wenzao huenda wakajaribu kuwabana Wakristo wachanga ili waridhiane. Hivyo, ni lazima vijana wa kimungu wategemee roho ya Yehova kwa ajili ya imani inayohitajiwa ili kutoa ulinzi wa wazi wa tumaini lao.—Mathayo 10:19, 20; Wagalatia 5:22, 23.
‘Mwe Tayari Sikuzote Kujitetea’
Shauri la mtume Petro linafaa kwa Wakristo wachanga na wazima pia. Alisema hivi: “Mwe tayari sikuzote kumjibu [kujitetea mbele ya, NW] kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu.” (1 Petro 3:15) Ni nini inayohitajiwa ili kuwa tayari kujitetea? Kwanza, ni lazima ufahamu mambo ambayo Biblia hufundisha. Kuchukua msimamo imara shuleni juu ya mambo kama vile utukuzo wa taifa, siasa, kutumia vibaya dawa za kulevya, au maadili, ni lazima kwanza ufahamu sababu ya msimamo wa Kikristo na ni lazima uuamini kikweli.
Kwa mfano, mtume Paulo aliwaambia Wakristo wenzake hivi: “Msidanganyike [Msipotoshwe, NW]; Mazungumzo [mashirika, NW] mabaya huharibu tabia njema.” (1 Wakorintho 15:33) Je! unakubaliana na hilo? Kama vile Paulo alivyoonyesha, ni rahisi kupotoshwa katika jambo la mashirika. Mtu huenda akaonekane kuwa mwenye urafiki na mwenye kupendeza. Lakini kama hashiriki hangaiko lako kwa ajili ya utumishi wa Yehova au hata haamini katika ahadi za Biblia, yeye ni mshirika mbaya. Kwa nini? Kwa sababu maisha yake yanategemea kanuni tofauti, na mambo ambayo huenda yakawa yenye maana sana kwa Mkristo huenda yasiwe na maana kubwa kwake.
Hilo halishangazi, kwa kuwa Yesu alisema juu ya wafuasi wake: “Wao si wa [sehemu ya, NW] ulimwengu, kama mimi nisivyo wa [sehemu ya, NW] ulimwengu.” (Yohana 17:16) Ni jambo lisilowezekana kwa mtu kuwa Mkristo wa kweli na wakati ule ule kuwa sehemu ya ulimwengu huu, ambao Shetani ni Mungu wao. (2 Wakorintho 4:4) Je! unaona jinsi kujitenga huko na ulimwengu kunavyolinda Mkristo asipatwe na upotovu na ugomvi unaowapata wengi leo? Ikiwa ndivyo, basi unaweza kufahamu kwa nini ni lazima uendelee kujitenga, hata kama hiyo inamaanisha kwamba huwezi kujiunga katika utendaji fulani fulani wa shule.a
Umaana wa kuwa imara katika imani na kutanguliza masilahi ya Ufalme maishani ulionyeshwa katika kisa cha msichana mmoja Mkristo aliye mchanga. (Mathayo 6:33) Mazoezi ya uhitimu wake yalipotangazwa, aliona kwamba yaliratibiwa kuwa siku ile ile ya kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova ambalo alikuwa amepanga kuhudhuria. Aliandika barua yenye heshima akieleza kwa nini hangeweza kuwako kwenye mazoezi hayo akampa mwalimu wake kabla ya kuanza masomo. Baada ya masomo, mwalimu alimwita aongee naye faraghani akamwuliza aeleze tena kwa nini hangekuwako kwenye yale mazoezi. Msichana huyo asema hivi: “Alitaka kuona kama maneno yangu yalikuwa yale yale. Je! hayo yalikuwa maoni yangu, au barua hiyo ilikuwa tu na maneno ya mama yangu? Alipoona kusadikishwa kwangu kibinafsi kwa jambo hilo, hakunipinga.”
‘Jitetee Mbele ya Kila Mtu’
Mara nyingi Vijana Wakristo huona kwamba wakifanya msimamo wao ujulikane waziwazi kwa walimu na wanafunzi kabla ya suala kuzuka, mbano hauwi mkubwa sana wakati matatizo yapasapo kukabiliwa. Mkristo mmoja Mjapani aliye mchanga asimulia kwamba alipokuwa mwenye umri wa miaka 11, shule yake ilihitaji kwamba wanafunzi wote wahudhurie karamu ya Krisimasi. Wanafunzi katika madarasa ya juu zaidi walimbana ili ashiriki, lakini hakuwako, na mwalimu wake alielewa msimamo wake. Kwa nini? Kwa sababu karibu na mwanzo wa mwaka wa shule, Shahidi huyo na wazazi wake walikuwa wamekutana na mwalimu huyo na kumweleza sehemu tofauti-tofauti za msimamo wao wa Kikristo.
Wanaposhiriki katika huduma ya shambani, baadhi ya Wakristo wachanga huhofu kukutana na wanadarasa wenzao au na walimu. Je! wewe huwa na maoni hayo? Ikiwa ndivyo, kwa nini usichukue hatua ya kwanza na kuwajulisha wanadarasa wako kwamba wewe wahubiri nyumba kwa nyumba na sababu ya wewe kufanya hivyo. Shahidi mmoja wa Yehova mwenye umri wa miaka 14 aliripoti hivi: “Kila mtu shuleni ajua msimamo wangu nikiwa Mkristo. Kwa kweli, wanaujua vizuri sana hivi kwamba nikikutana na mwanadarasa mwenzangu ninaposhiriki katika huduma, sioni haya. Kwa kawaida wanafunzi wenzangu husikiza, na nyakati nyingi wao hupokea vichapo vya Biblia.” Kijana mwenye umri wa miaka 12 aripoti kwamba yeye kutazamia kukutana na wanadarasa wenzake anaposhiriki katika huduma. Badala ya kuwa na hofu anapofikiria hilo, yeye hujizoeza yale atakayosema jambo hilo likitukia. Hivyo, yeye yu tayari kutoa sababu nzuri kwa ajili ya imani yake.
Katika shule nyingi, utendaji mwingi wa baada ya shule unasemwa kuwa jambo la kujiamulia. Lakini kikweli, walimu na wanafunzi huwabana mtu mmoja mmoja wajiunge katika utendaji kama huo. Mkristo mwenye umri wa miaka 20 aligundua njia nzuri ya kuuweza mbano huo. Asema hivi: “Nilitumika nikiwa painia msaidizi miaka yote ya shule ya upili. Kila mtu alijua nilikuwa mwenye shughuli nyingi sana katika utendaji wangu wa kidini nisiweze kujihusisha katika mambo mengine.” Dada mchanga zaidi wa Shahidi huyo alifuata mwendo uo huo. Vijana wengi-ne Wakristo huingia moja kwa moja kwenye utumishi wa painia msaidizi katika muda wa miaka ya shule hadi utendaji wa painia wa kawaida wakiwa wapiga mbiu wa Ufalme wa wakati wote masomo yao yanapokwisha.
Usisahau kamwe matokeo mazuri ya mwenendo wako mzuri na kutoa kwako ushahidi kwa moyo mkuu. Badala ya kubaki kimya, kwa nini usionyeshe kwamba uko imara katika imani kwa kuongea kwa heshima lakini kwa ujasiri? Hilo ndilo jambo lililofanywa na msichana Mwisraeli aliyekuwa ametekwa akaja kuwa katika nyumba ya Naamani jemadari Msiria. (2 Wafalme 5:2-4) Jina la Yehova lilisifiwa kwa sababu msichana huyo mchanga alichukuwa hatua ya kwanza. Imani iyo hiyo kwa upande wako yaweza pia kumletea Mungu heshima na huenda ikawasaidia wengine kuchukua msimamo wakiwa wenye kulisifu jina lake.
Jambo la uhakika ni kwamba hatuwezi kuridhiana na kuacha imani yetu kisha tubaki tukiwa Wakristo. Yesu alisema: “Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni. Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.” (Mathayo 10:32, 33) Kubaki imara katika imani ukiwa mfuasi wa Yesu ni daraka lenye uzito, sivyo?
Msaada Wapatikana
Ili uwe na msimamo imara ukiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, unahitaji imani yenye nguvu. Ili upate, ni lazima ujifunze Biblia kwa bidii-nyendelevu, uhudhurie mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika huduma ya shambani. Ikiwa bado unahisi kwamba jambo fulani linakosekana, waweza kufanya nini? Mwanafunzi Yakobo alisema hivi: “Mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.” (Yakobo 1:5) Ongea na Yehova katika sala juu ya tatizo lako; yeye aweza kukuimarisha ili ukabiliane na majaribu au mitihani ya imani yako.
Mkristo mchanga aweza kufanya jambo gani jingine? Kitabu cha Mithali chasema hivi: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.” (Mithali 23:22) Mtume Paulo aliunga mkono shauri hilo, kwa maana alisema hivi: “Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Wakolosai 3:20) Wazazi Wakristo wanaweza kukusaidia uwe imara katika imani. Sikiliza madokezo yao. Kwa msaada wao, tafuta-tafuta Maandiko na vichapo vyenye msingi wa Biblia, tafuta mawazo, mashauri, na mambo yaliyoonwa. Wewe na wazazi wako pia mtaonea hilo shangwe, nalo litakusaidia ushinde haya au hofu.—2 Timotheo 1:7.
Faidika kikamili na maandalizi ambayo Yehova Mungu amefanya kupitia kundi la Kikristo. Jitayarishe vizuri kwa ajili ya mikutano. Ongea na wazee waliowekwa na wengine ambao wamepitia maono hayo hayo unayokabili sasa. Sulemani alisema hivi: “Mwenye hekima asikie [atasikiliza, NW] na kuongezewa elimu, na mwenye ufahamu ayafikie [hujipatia, NW] mashauri yenye njia. (Mithali 1:5) Kwa hiyo jifunze kutoka kwa hao wenye umri mkubwa zaidi. Unaweza kujifunza, pia, kutoka kwa vijana Wakristo wanaowezana na matatizo kama yako kwa kufanikiwa.
Uaminifu Unaleta Mibaraka
Kwa kusimama imara katika imani, utakuwa ukitumia shauri la Paulo kuwa ‘imara, bila kuondoleka, sikuzote ukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Wakorintho 15:58, NW) Yehova anajua na kufahamu matatizo unayokabili. Ameimarisha wengi ambao wamekabili magumu ayo hayo, naye atakuimarisha. Ukimtegemea Mungu, atakutegemeza, kwa maana mtunga zaburi alisema hivi: “Umtwike BWANA [Yehova, NW] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.”—Zaburi 55:22.
Petro aliandika hivi: “Mwe na dhamiri njema, ili katika neno lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale wautukanao mwenendo wenu mwema katika Kristo.” (1 Petro 3:16) Ukikataa kuridhiana kuhusu sheria na kanuni zenye uadilifu za Mungu, utakuwa na dhamiri njema, ambayo ni baraka ya halisi kutoka kwa Yehova. Tena, utawekea mfano mzuri vijana Wakristo ambao imani yao huenda ikawa dhaifu. (1 Timotheo 4:15, 16) Mwenendo wako huenda ukawatia moyo kufanya jitihada kuwa imara katika imani na hivyo kuweza kuvumilia majaribu.
Huenda hata ukasaidia wale ambao mwanzoni hupinga msimamo wako wa Kikristo. Kumbuka haya maneno yenye kuamsha tumaini: “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa, kama ni hii au hii, au kama zote zitafaa sawasawa.” (Mhubiri 11:6) Ni nani ajuaye ni matokeo gani mazuri yatakayotokana na kupanda kwako mbegu nzuri kupitia matendo yako yenye uaminifu?
Miongoni mwa mibaraka mikubwa utakayovuna ni msimamo wenye kukubalika pamoja na Yehova. Hatimaye, kuwa imara katika imani kutatokeza uhai wa milele. (Yohana 17:3; linganisha Yakobo 1:12.) Hakuna faida kupoteza zawadi hiyo kwa kuridhiana ili upate ondoleo la jaribu kwa muda tu.
Vipi juu ya yule kijana aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii? Alivumilia jaribu lake. Baada ya kusanyiko la shule kumalizika, alijaribu kueleza kwa busara msimamo wake kwa walimu. Ingawa hakukuwako itikio njema, alikuwa na uradhi wa kujua kwamba alikuwa amefanya moyo wa Yehova ushangilie. (Mithali 27:11) Aliendelea kutetea imani yake mpaka alipomaliza masomo yake. Kisha akawa painia. Uvumilivu wako wenye uaminifu na uwe wenye tokeo ilo hilo. Itakuwa hivyo ukithibitika kuwa imara katika imani.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mazungumzo juu ya hayo na kanuni nyingine za Biblia, ona kitabu Questions Young People Ask—Answers That Work, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Sanduku katika ukurasa wa 25]
MSAADA WAPATIKANA
◻ Sikiliza hekima ya wazazi wako wenye kumhofu Mungu.
◻ Faidika na maandalizi ya kiroho katika kundi la Kikristo.
◻ Sema na wazee waliowekwa na wengine ambao huenda wakawa na matatizo kama yako.
◻ Ongea na Wakristo wengine wachanga wanaokabiliana na vizuizi hivyo hivyo kwa kufanikiwa.