Mwisho wa Miaka 6,000 ya Utawala wa Mwanadamu Wakaribia—Ni Mambo Gani Yametimizwa?
KWA kuwa mwaka mpya wa Kiyahudi wenye miezi mifupi ulianza Septemba mwaka wa 1975 sehemu ya maana sana katika historia ya kibinadamu ilifikiwa. Hiyo ni nini? Kulingana na hesabu ya Biblia ya wakati, wakati huo wanadamu walimaliza miaka 6,000 ya kuwako duniani. Naam, mwanadamu wa kwanza Adamu angalikuwa hai bado akiwa mwenye umri wa miaka 6,000 katika Septemba wa mwaka jana, kama angalichagua kuendelea kuwa mtii akiwa chini ya utawala wa Mungu.
Basi, je! hii yamaanisha kwamba sasa wanadamu wamemaliza miaka 6,000 ya kipindi cha miaka 7,000 ambacho Mungu ‘alibariki akakitakasa’ kuwa ‘siku yake kuu ya kustarehe’? Je! yamaanisha kwamba utawala wa Ufalme wa Kristo wa miaka elfu, ambao ndio utamalizia ‘siku hiyo ya kustarehe,’ umepaswa uhesabiwe kuanzia Septemba mwaka wa 1975?—Mwa. 1:27, 31; 2:2, 3; Ufu. 20:1-6.
Sivyo. Kwa sababu gani? Maandishi ya Biblia yanaonyesha kwamba Mungu hakuacha kuumba baada ya kumwumba Adamu “siku” iliyotangulia ile ‘siku ya kustarehe’ ya miaka 7,000. Yaonyesha muda fulani ulipita baada ya Adamu kuumbwa ndipo Hawa mkewe akaumbwa. Wakati huo, Mungu alimwagiza Adamu awape wanyama majina. Hatujui kama kipindi hicho kilikuwa cha juma mbili au miezi au miaka. Kwa hiyo hatujui barabara wakati ‘siku kuu ya kustarehe’ kwa Yehova ilipoanza, wala hatujui barabara itakapokwisha. Ndivyo ilivyo juu ya mwanzo wa utawala wa miaka elfu wa Kristo. Biblia haitupi njia ya kuweka tarehe yenyewe, na kwa hiyo haifai tufikiri-fikiri tarehe hiyo itakuwa wakati gani.—Mwa. 2:18-25; Mt. 24:42, 44.
Lakini, hesabu ya wakati wa Biblia inatuonyesha kwamba miaka 6,000 ya historia ya mwanadamu ilikwisha mwaka wa 1975. Mwanzoni mwa ‘siku ya kustarehe’ kwa Mungu Adamu alipata kuwa mwasi juu ya utawala wa Mungu. Hivyo, muda mwingi wa miaka 6,000 ya historia ya mwanadamu umekuwa wa utawala wa mwanadamu. Utawala wa kujitegemea wa mwanadamu ulitimiza nini miaka elfu sita hiyo, au katika vipindi sita vyenye miaka 1,000 kila kimoja? Acheni tuviangalie vipindi hivyo vya miaka elfu elfu, hatua kwa hatua.
Miaka Elfu ya Kwanza
Furaha ya mwanadamu katika paradiso ya Edeni ilikwisha kwa kuwa Adamu na Hawa waliiasi enzi kuu ya Muumba wao, Yehova Mungu. Kwa haki, Mungu alimfukuza mwanamume na mkewe katika bustani hiyo wakaingia katika dunia isiyolimwa, wakajitunze wenyewe wakiwa chini ya serikali ya kujitegemea waliyojichagulia. Pengine huo ulipata kuwa namna ya utawala wa mababu. Lakini miaka 900 iliyobaki kabla Adamu hajafa, wanadamu wenye dhambi walihusika zaidi na zaidi katika jeuri, uuaji, dini ya uongo na kufuata mambo yo yote waliyotaka na mwishowe wakafa.—Rum. 5:12; Mwa. 3:12, 16-19; 4:10, 11, 23, 26.
MIAKA ELFU YA PILI
Chini ya utawala wa mwanadamu, “maovu ya mwanadamu” yaliongezeka hata Mungu akaleta gharika ya dunia yote awaharibu waliokuwa ‘wameharibu’ dunia wakaijaza jeuri, baada ya kuwaonya kwa wakati wake. Ingawa Mungu alimhifadhi Nuhu hai na jamaa yake kwa sababu ya haki yao, wazao wao walihusika katika siasa za kibinadamu kwa kumdharau Yehova Mungu. Miaka inayopungua 200 baada ya Gharika, Nimrodi akawa mfalme mkatili mwenye kutumia nguvu. Akajikweza juu ya Mungu Aliye Juu Zaidi, hata kukawa na usemi uliosema, “Kama Nimrodi, hodari wa kuwinda wanyama mbele za [Yehova].” Uwindaji wake hodari bila shaka ulitia na kuua wanadamu, na vile-vile wanyama, hata akaendeleza uonezi juu ya wanadamu. Alipofikia upeo wa uasi kwa kujenga mji, Babeli, na “mnara, na kilele chake kifike mbinguni,” Yehova alifanya mwujiza wa kuvuruga lugha ya mwanadamu. Hii iliwalazimisha waache ujenzi wao, na kutawanyika duniani. Huo ndio uliokuwa utawala wa kwanza wa kibinadamu wenye kutumia nguvu kuvunjwavunjwa!—Mwa. 6:4, 5, 11; 10:8-12; 11:1-9.
MIAKA ELFU YA TATU
Kulikuwa na vita kati ya wanadamu, kabila likipigana na kabila, serikali ya mji ikipigana na serikali ya mji na ufalme ukipigana na ufalme. Misri ndiyo ikawa mamlaka kuu ya ulimwengu, lakini iliadhibiwa na Mungu kwa sababu ilionea watu wake, Israeli. Watu wa mataifa walirudi nyuma nyuma hata wakaanza kuabudu sanamu za kipagani, hata wakaanza kutoa watoto kama dhabihu. Tawala zenye kutumia nguvu na uonezi zilitokea na watu wa kawaida wakatumiwa kama wazuzu na watawala.—Mwa. 14:1-16; Kut. 1:8-11; 6:1-6; 14:26-31; Kut. 18:9-12.
MIAKA ELFU YA NNE
Baada ya Misri, milki za ulimwengu zenye kutawaliwa na wafalme wenye kutaka makuu zilifuatana. Zilitokea wazi katika kipindi cha nne cha miaka elfu. Ashuru, Babeli, Umedi-Uajemi, Ugiriki na Rumi—kila mojawapo ilipigana ikiwa na majeshi yake hodari ikanyakua utawala wa ulimwengu. Ziliruhusiwa pia kulitawala taifa la Israeli. Unabii mbalimbali wa Danieli na Ufunuo unafananisha mamlaka hodari hizo za kisiasa na “wanyama.” Dini ya uongo ilitokeza sikuzote kuwa yenye kuunga mkono tawala hizo zenye kutumia ukatili na nguvu.—Dan. 7:2-8, 17; 8:3-8, 20-22; Ufu. 13:1, 2; 17:3-8, 11; Eze. 21:25-27.
MIAKA ELFU YA TANO
Sasa Milki ya Rumi ilitawala nchi nyingi. Yohana Mbatizaji alikatwa kichwa katika utawala wa Rumi, Yesu Kristo alitundikwa katika mti wa mateso katika Milki iyo hiyo, na katika Milki iyo hiyo majeshi yake yaliuharibu Yerusalemu na Wakristo wakateswa—na hayo yote yalitokea katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Katika karne ya nne C.E., Kaisari Konstantino asiyebatizwa alitayarisha Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) pamoja na viongozi wake wa kidini na serikali ya Rumi ya mwungano wa siasa na dini, nao Utawala wa Mapadre wa Kikatoliki ukatokeza kipindi kirefu kisichokuwa na uvumbuzi wa mambo yo yote, pamoja na uonezi wao wote wenye kuleta msiba kwa watu wa kawaida, na hasa kwa wale waliojaribu kumtumikia Mungu. Mwungano wa Kanisa na Serikali ulitukuzwa mwaka wa 800 C.E. wakati papa wa Kirumi alipomvika Charlemagne taji kama mtawala wa Milki Takatifu ya Kirumi.—Marko 6:25, 27; 15:25, 37; Luka 21:20-24; 2 The. 2:3.
MIAKA ELFU YA SITA
Milki ya Rumi iligawanyika katika serikali ndogo ndogo za Kizungu zenye mashindano na uonezi. Hizo zilipeleka manowari zao ng’ambo zikateke na kufanya maeneo yaliyoitwa ‘ya kipagani’ ya dunia ya kikoloni. Uingereza ikawa mamlaka kuu ya ulimwengu. Amerika ya kikoloni ikatangaza na kujipatia uhuru wa kutokuwa chini ya Uingereza, lakini wakaendelea kuwa na urafiki wa karibu wakiwa mwungano wa mamlaka ya ulimwengu ya Waingereza na Waamerika. Karne ya kumi na nane kulikuwa na mabadiliko makubwa yaliyosababishwa na uvumbuzi wa mashine mbali-mbali, nayo karne ya 20 ikawa mwanzo wa kipindi cha vita vya ulimwengu, ambavyo vilitia ndani karibu mataifa yote ya kisiasa, yakiungwa mkono na dini zilizo kubwa kubwa. Utawala wa “mfalme wa kusini” wa kidemokrasi ulipingwa na “ufalme wa kaskazini” wa Kijeremani, lakini sasa Ujeremani yenye kutumia nguvu imeshindwa na Wakomunisti hodari wakiwa “mfalme.” Hakuna yo yote kati ya namna hizo za serikali ya kisiasa imeletea raia zake furaha au usalama wa kweli. Na sasa kuna tisho la uharibifu wa wanadamu kwa sababu ya mataifa kushindania kupata wingi wa silaha za atomiki. Mapinduzi na uasi juu ya mamlaka, kutokeza kwa jamii yenye kufanya mambo itakavyo tu na kuongezeka kasi kasi kwa uvunjaji wa sheria na uchafuzi kumeongezea mwanadamu magumu.—Dan. 11:27-40; Ufu. 11:18.
UCHUNGUZI WA HATUA KWA HATUA
Mwanzoni mwa kipindi hiki cha miaka 6,000 ya kuwako mwanadamu paradiso ilipotezwa. Kuanzia wakati huo, wanadamu wenye kufadhaika wamejaribu serikali za namna nyingi wakijitahidi kupata tena angaa paradiso ya namna fulani ionekanayo. Lakini ni mambo gani yametimizwa? Ulimwengu umevurugika. Wanadamu wanaelekea uharibifu, kama vile Yesu alivyosema mapema kwa unabii juu ya siku zetu: “Katika nchi dhiki ya mataifa wakishangaa . . . watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu.” Lakini Neno la Mungu linatoa tumaini!—Luka 21:25, 26.